Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Waaminifu wa Zamani Waliongozwa na Roho ya Mungu

Waaminifu wa Zamani Waliongozwa na Roho ya Mungu

Waaminifu wa Zamani Waliongozwa na Roho ya Mungu

“Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova mwenyewe amenituma, ndiyo, roho yake.”—ISA. 48:16.

1, 2. Ni nini kinachohitajiwa ili kuonyesha imani, na tutatiwa moyo jinsi gani tukichunguza watumishi waaminifu wa kale?

INGAWA watu wengi wameonyesha imani tangu siku za Abeli, Biblia inasema kwamba “imani si mali ya watu wote.” (2 The. 3:2) Basi mtu anawezaje kuwa na imani, na ni nini kinachomwezesha kuwa mwaminifu? Kwa kadiri kubwa, imani inafuata mambo yanayosikiwa kutoka katika Neno la Mungu. (Rom. 10:17) Ni sehemu ya tunda la roho takatifu ya Mungu. (Gal. 5:22, 23) Kwa hiyo, ili tuwe na imani na kuionyesha kwa matendo tunahitaji roho takatifu.

2 Ni kosa kukata kauli kwamba wanaume na wanawake wenye imani wanazaliwa wakiwa na imani, yaani, ni sifa ya asili. Watumishi walioweka mfano mzuri ambao tunasoma kuwahusu katika Biblia walikuwa watu ‘wenye hisia kama zetu.’ (Yak. 5:17) Walikuwa na shaka, wasiwasi, na udhaifu mbalimbali lakini “wakafanywa kuwa wenye nguvu” na roho ya Mungu ili waweze kukabiliana na hali ngumu. (Ebr. 11:34) Tukichunguza jinsi roho ya Yehova ilivyowasaidia watumishi hao, tunaweza kutiwa moyo kuendelea kuwa waaminifu leo, kwa kuwa tunaishi wakati ambapo imani yetu inashambuliwa.

Roho ya Mungu Ilimtia Nguvu Musa

3-5. (a) Tunajuaje kwamba Musa alitimiza majukumu yake kwa msaada wa roho takatifu? (b) Mfano wa Musa unatufundisha nini kuhusu jinsi Yehova anavyotupatia roho yake?

3 Musa “alikuwa mpole zaidi” kuliko wanadamu wote waliokuwa hai katika mwaka wa 1513 K.W.K. (Hes. 12:3) Mtumishi huyo mwenye tabia-pole alikabidhiwa daraka zito sana katika taifa la Israeli. Roho ya Mungu ilimtia nguvu Musa ili atoe unabii, ahukumu, aandike, aongoze, na afanye miujiza. (Soma Isaya 63:11-14.) Hata hivyo, pindi moja, Musa alilalamika kwamba mzigo aliobeba ulikuwa mzito sana. (Hes. 11:14, 15) Hivyo, Yehova aliondoa “sehemu ya roho” iliyokuwa juu ya Musa na kuiweka juu ya watu wengine 70 ili wamsaidie kuubeba mzigo huo. (Hes. 11:16, 17) Ingawa mzigo wa Musa ulionekana kuwa mzito sana, kwa kweli, hakuwa akiubeba peke yake, na wale 70 pia waliowekwa rasmi ili wamsaidie hawangeubeba peke yao.

4 Musa alikuwa amepewa roho takatifu ya kutosha ili kutimiza kazi hiyo. Baada ya badiliko hilo, bado Musa alikuwa na roho yote aliyohitaji. Musa hakuwa na kiasi kidogo sana cha roho, na wale wanaume wazee 70 hawakuwa na roho nyingi sana. Yehova anatupatia kiasi tunachohitaji cha roho yake, kulingana na hali zetu. ‘Hatoi roho kwa kipimo’ lakini anatoa “kutokana na wingi alio nao.”—Yoh. 1:16; 3:34.

5 Je, unavumilia majaribu? Je, majukumu yako yanaongezeka na yanazidi kuchukua wakati wako mwingi zaidi? Je, unajitahidi kuiandalia familia yako mahitaji yake ya kiroho na ya kimwili huku ukikabiliana na gharama zinazozidi kuongezeka au mahangaiko kuhusu afya? Je, unabeba majukumu mazito katika kutaniko? Uwe na hakika kwamba kupitia roho yake, Mungu anaweza kukupa nguvu unazohitaji ili ukabiliane na hali yoyote.—Rom. 15:13.

Roho Takatifu Ilimfanya Bezaleli Astahili

6-8. (a) Roho ya Mungu iliwawezesha Bezaleli na Oholiabu kufanya nini? (b) Ni nini kinachoonyesha kwamba Bezaleli na Oholiabu waliongozwa na roho ya Mungu? (c) Kwa nini simulizi la Bezaleli linatia moyo sana?

6 Simulizi la Bezaleli aliyeishi siku za Musa linafunua mengi kuhusu jinsi roho ya Mungu inavyofanya kazi. (Soma Kutoka 35:30-35.) Bezaleli aliwekwa rasmi ili aongoze katika kutengeneza vifaa muhimu vya maskani. Je, alikuwa na ujuzi wa kazi ya ufundi kabla ya mradi huo mkubwa? Labda, lakini kuna uwezekano mkubwa sana kwamba kazi ya mwisho aliyofanya kabla ya mradi huo ilikuwa kazi ya kuwatengenezea Wamisri matofali. (Kut. 1:13, 14) Basi Bezaleli angetimizaje kazi yake ngumu? Yehova “akamjaza roho ya Mungu katika hekima, katika uelewaji na katika ujuzi na katika kila aina ya ufundi na kwa ajili ya kubuni vyombo . . . ili kufanya vifaa sanifu vya kila namna.” Roho takatifu ilizidisha kipawa chochote cha asili ambacho huenda Bezaleli alikuwa nacho. Ndivyo ilivyokuwa na Oholiabu. Ni wazi kwamba Bezaleli na Oholiabu walijifunza vyema kazi yao, kwa kuwa hawakutimiza tu kazi yao bali pia waliwafundisha wengine mambo ya kufanya. Ndiyo, Mungu alitia hekima moyoni mwao ili wawafundishe wengine.

7 Pia, tunajua kwamba Bezaleli na Oholiabu waliongozwa na roho ya Mungu kwa sababu vitu walivyotengeneza vilidumu kwa muda mrefu sana. Vitu walivyotengeneza bado vilikuwa vikitumiwa miaka 500 baadaye. (2 Nya. 1:2-6) Tofauti na watu wanaotengeneza bidhaa leo, Bezaleli na Oholiabu hawakuwa na nia ya kuandika jina lao juu ya vitu walivyotengeneza ili kujiletea sifa. Sifa zote zilimwendea Yehova kwa sababu ya kazi walizotimiza.—Kut. 36:1, 2.

8 Leo, huenda tukawa na kazi ngumu zinazohitaji ustadi wa pekee, kama vile kujenga, kuchapisha, kupanga makusanyiko ya wilaya, kutoa misaada wakati wa misiba, na kuwasiliana na madaktari na wafanyakazi wa hospitali kuhusiana na msimamo wetu wa Kimaandiko unaohusu matumizi ya damu. Nyakati nyingine, kazi hizo zinafanywa na wafanyakazi wenye ustadi, lakini mara nyingi zinafanywa na wajitoleaji ambao hawana uzoefu katika kazi hususa. Roho ya Mungu inafanya jitihada zao zifanikiwe. Je, unasitasita kukubali mgawo katika utumishi wa Yehova, na kuhisi kwamba wengine wanastahili zaidi kuliko wewe? Kumbuka kwamba roho ya Yehova inaweza kuongeza ujuzi na uwezo wako na kukusaidia kutimiza mgawo wowote ambao anakupa.

Yoshua Alifanikiwa kwa Msaada wa Roho ya Mungu

9. Waisraeli walijikuta katika hali gani baada ya kutoka Misri, na ni swali gani lililozuka?

9 Roho ya Mungu ilimwongoza pia mtu mwingine aliyeishi katika siku za Musa na Bezaleli. Muda mfupi baada ya Waisraeli kutoka Misri, Waamaleki waliwashambulia watu wa Mungu bila sababu yoyote. Wakati ulifika wa Waisraeli kukabiliana na tishio hilo. Ingawa Waisraeli hawakuwa wamezoea kamwe kupigana vita, walilazimika kushiriki katika pambano la kwanza la kijeshi wakiwa watu waliowekwa huru. (Kut. 13:17; 17:8) Mtu fulani alihitajiwa ili kuongoza jeshi hilo katika vita. Ni nani angewaongoza?

10. Kwa nini Waisraeli walishinda vita chini ya uongozi wa Yoshua?

10 Yoshua alichaguliwa. Ikiwa angehitaji kutaja kazi ambayo alikuwa na uzoefu wa kufanya ili astahili kupata mgawo huo, angetaja kazi gani? Je, angesema kwamba amewahi kufanya kazi akiwa mtumwa? Kazi ya kuchanganya nyasi za kutengeneza matofali? Kukusanya mana? Ni kweli kwamba Elishama, babu ya Yoshua, alikuwa mkuu wa kabila la Efraimu na ni wazi kwamba aliongoza wanaume 108,100 waliokuwa katika mgawanyo mmoja kati ya migawanyo ya makabila matatu ya Israeli. (Hes. 2:18, 24; 1 Nya. 7:26, 27) Hata hivyo, Yehova aliagiza kupitia Musa kwamba Yoshua ndiye aliyepaswa kuongoza jeshi ambalo lingemwangamiza adui, hakumchagua Elishama au Nuni, mwana wake. Vita hivyo viliendelea kwa karibu siku nzima. Waisraeli walishinda kwa sababu Yoshua alitii kikamili na kuthamini kwa moyo wote mwongozo wa roho takatifu ya Mungu.—Kut. 17:9-13.

11. Tunaweza kufanikiwa jinsi gani katika utumishi mtakatifu kama Yoshua?

11 Baadaye, Yoshua, ‘akiwa amejaa roho ya hekima,’ alichukua mahali pa Musa. (Kum. 34:9) Roho takatifu haikumpa uwezo wa kutoa unabii au kufanya miujiza kama Musa, lakini ilimwezesha Yoshua kuwaongoza Waisraeli katika mapambano mengi ya kijeshi ambayo yaliwasaidia kushinda na kuichukua nchi ya Kanaani. Leo, huenda tukahisi kwamba hatuna uzoefu au hatustahili kutimiza migawo fulani katika utumishi wetu mtakatifu. Hata hivyo, kama Yoshua, tuna hakika kwamba tutafanikiwa ikiwa tutafuata kwa ukaribu maagizo kutoka kwa Mungu.—Yos. 1:7-9.

‘Roho ya Yehova Ilimfunika Gideoni’

12-14. (a) Ushindi wa wanaume 300 Waisraeli waliopigana na jeshi kubwa sana la Wamidiani unaonyesha nini? (b) Yehova alimpa Gideoni uhakikisho gani? (c) Mungu anatuhakikishia nini leo?

12 Baada ya kifo cha Yoshua, Yehova aliendelea kuonyesha jinsi nguvu zake zinavyoweza kuwaimarisha watu waaminifu. Kitabu cha Waamuzi kina masimulizi mengi kuhusu wanadamu ambao ‘kutoka hali ya udhaifu walifanywa kuwa wenye nguvu.’ (Ebr. 11:34) Kupitia roho takatifu, Mungu alimchochea Gideoni apigane kwa niaba ya watu Wake. (Amu. 6:34) Hata hivyo, jeshi ambalo Gideoni alikusanya lilikuwa dogo sana likilinganishwa na jeshi la Wamidiani. Kulikuwa na askari-jeshi wanne Wamidiani kwa kila askari-jeshi mmoja wa Israeli. Machoni pa Yehova, jeshi hilo dogo sana la Waisraeli lilikuwa kubwa sana. Mara mbili Yehova alimwagiza Gideoni apunguze jeshi lake kufikia askari-jeshi 1 Mwisraeli kwa askari-jeshi 450 wa adui. (Amu. 7:2-8; 8:10) Yehova alikubali idadi hiyo. Ikiwa wangepata ushindi mkubwa, ni nani angejigamba kwamba walishinda kwa sababu ya jitihada au hekima ya wanadamu?

13 Gideoni na askari-jeshi wake walikuwa tayari. Kama ungekuwa katika jeshi hilo dogo, je, ungejihisi salama kujua kwamba wale ambao waliogopa au wale ambao hawakuwa macho kuona hatari waliambiwa warudi nyumbani? Au ungeogopa ikiwa ungefikiria matokeo ya vita hivyo? Tuna hakika kwamba Gideoni alimtegemea Mungu. Alifanya mambo aliyoambiwa afanye! (Soma Waamuzi 7:9-14.) Yehova hakumshutumu Gideoni alipoomba ishara ya kuthibitisha kwamba Mungu angekuwa pamoja naye. (Amu. 6:36-40) Badala yake, Mungu aliimarisha imani ya Gideoni.

14 Nguvu za Yehova za kuokoa hazina mipaka. Anaweza kuwakomboa watu wake kutoka katika hali yoyote ngumu, hata anaweza kuwakomboa akitumia watu ambao wanaonekana kuwa dhaifu au wasio na uwezo. Huenda nyakati nyingine tukahisi kwamba maadui wetu ni wengi mno au tunakabili hali ngumu sana. Hatutazamii Mungu atuonyeshe ishara za kimuujiza kama alizomwonyesha Gideoni, lakini tunaweza kupata mwongozo na uhakikisho mwingi kutoka katika Neno la Mungu na kupitia kutaniko lake ambalo linaongozwa na roho yake. (Rom. 8:31, 32) Ahadi za Yehova zenye upendo zinaimarisha imani yetu na kutusadikisha kwamba kwa kweli yeye ni Msaidiaji wetu!

“Sasa Roho ya Yehova Ikaja Juu ya Yeftha”

15, 16. Kwa nini binti ya Yeftha alikuwa na mtazamo mzuri, na hilo linawatiaje moyo wazazi?

15 Fikiria mfano mwingine. Waisraeli walipolazimika kupigana na Waamoni, roho ya Yehova ‘ilikuja juu ya Yeftha.’ Akiwa na hamu kubwa ya kushinda vita hivyo na kumletea Yehova sifa, Yeftha aliweka nadhiri ambayo ilimgharimu sana. Yeftha aliweka nadhiri kwamba ikiwa Mungu angewatia Waamoni mikononi mwake, mtu ambaye angetoka kwanza nje ya mlango na kumpokea anaporudi nyumbani, angekuwa wa Yehova. Yeftha aliporudi baada ya kuwashinda Waamoni, binti yake alikuja mbio kumlaki. (Amu. 11:29-31, 34) Je, Yeftha alishangazwa na jambo hilo? Inaelekea kwamba halikumshangaza kwa sababu alikuwa na mtoto mmoja tu. Alitimiza nadhiri yake kwa kumtoa binti yake kwa ajili ya utumishi wa pekee katika patakatifu pa Yehova huko Shilo. Akiwa mwabudu mshikamanifu wa Yehova, binti ya Yeftha alisadiki kwamba nadhiri ya baba yake ilipaswa kutimizwa. (Soma Waamuzi 11:36.) Roho ya Yehova iliwapa wote wawili nguvu walizohitaji.

16 Binti ya Yeftha alisitawishaje roho hiyo ya kujidhabihu? Hapana shaka kwamba imani yake ilijengwa alipoona bidii ya baba yake ya kujitoa kwa Mungu. Wazazi, watoto wenu wanaona mfano wenu. Maamuzi yenu yanaonyesha kwamba mnaamini mambo mnayosema. Watoto wenu wanasikiliza sala zenu za unyoofu, wanasikiliza kwa makini mafundisho yenu, na kuona jitihada zenu zote za kumtumikia Yehova kwa moyo kamili. Watoto wenu wanapofanya hivyo, inaelekea kwamba watasitawisha tamaa yenye nguvu ya kujitoa ili wamtumikie Yehova. Jambo hilo litawaletea shangwe.

“Roho ya Yehova Ikaanza Kutenda Kazi Juu” ya Samsoni

17. Samsoni alifanya nini kupitia roho ya Mungu?

17 Fikiria mfano mwingine. Waisraeli walipotekwa nyara na Wafilisti, ‘baada ya muda roho ya Yehova ilianza kumchochea’ Samsoni ili awakomboe Waisraeli. (Amu. 13:24, 25) Samsoni alipewa nguvu za kutenda mambo ya kustaajabisha na yaliyohitaji uwezo usio na kifani. Wafilisti walipowashawishi Waisraeli wengine wamkamate Samsoni, “roho ya Yehova ikaanza kutenda kazi juu yake, na zile kamba zilizokuwa kwenye mikono yake zikawa kama nyuzi za kitani ambazo zimeunguzwa kwa moto, nazo pingu zake zikayeyuka kutoka kwenye mikono yake.” (Amu. 15:14) Hata katika hali ya udhaifu iliyosababishwa na uamuzi wake mbaya, Samsoni alifanywa kuwa mwenye nguvu “kupitia imani.” (Ebr. 11:32-34; Amu. 16:18-21, 28-30) Roho ya Yehova ilitenda kazi juu ya Samsoni kwa njia ya pekee kwa sababu ya hali zisizo za kawaida. Hata hivyo, matukio hayo ya kihistoria yanatutia moyo sana. Jinsi gani?

18, 19. (a) Kisa cha Samsoni kinatuhakikishia nini? (b) Umefaidikaje kwa kuchunguza mifano ya watu waaminifu ambao wamezungumziwa katika makala hii?

18 Tunategemea roho takatifu ileile ambayo Samsoni alitegemea. Tunafanya hivyo tunapotimiza kazi ambayo Yesu aliwapa wafuasi wake, yaani, ‘kuwahubiria watu na kutoa ushahidi kamili.’ (Mdo. 10:42) Mgawo huo unahitaji ustadi ambao huenda hatukuzaliwa nao. Tunashukuru kama nini kwamba Yehova anatumia roho yake kutuwezesha kutimiza kazi mbalimbali ambazo tumekabidhiwa! Hivyo, tunapotimiza mgawo wetu, tunaweza kusema hivi kama nabii Isaya: “Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova mwenyewe amenituma, ndiyo, roho yake.” (Isa. 48:16) Naam, ni roho ya Mungu ambayo imetutuma! Tunatimiza kazi hiyo kwa moyo wetu wote tukiwa na hakika kwamba Yehova atatufanya tustahili zaidi kama Musa, Bezaleli, na Yoshua. Tunauchukua “upanga wa roho, yaani, neno la Mungu,” tukiwa na hakika kwamba atatutia nguvu kama alivyomtia nguvu Gideoni, Yeftha, na Samsoni. (Efe. 6:17, 18) Tukimtegemea Yehova ili atusaidie kushinda vizuizi, tunaweza kuwa na nguvu nyingi za kiroho kama Samsoni alivyokuwa na nguvu nyingi za kimwili.

19 Ni wazi kwamba Yehova anawabariki wale ambao wanaunga mkono kwa ujasiri ibada ya kweli. Tunapofuata mwongozo wa roho takatifu ya Mungu, imani yetu inaongezeka. Kwa hiyo, tutafurahi pia kuchunguza baadhi ya matukio yenye kusisimua yaliyoandikwa katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Kufanya hivyo kutafunua jinsi roho ya Yehova ilivyotenda kazi juu ya watumishi wake waaminifu katika karne ya kwanza, kabla na baada ya Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K. Masimulizi hayo yatazungumziwa katika makala inayofuata.

Kwa nini unatiwa moyo kujua jinsi roho ya Mungu ilivyotenda kazi juu ya . . .

• Musa?

• Bezaleli?

• Yoshua?

• Gideoni?

• Yeftha?

• Samsoni?

[Maswali ya Funzo]

[Blabu katika ukurasa wa 22]

Roho ya Mungu inaweza kutufanya tuwe na nguvu nyingi za kiroho kama Samsoni alivyokuwa na nguvu nyingi za kimwili

[Picha katika ukurasa wa 21]

Wazazi, watoto wenu wanaiga mfano wenu mnapoonyesha bidii