Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutoka Katika Hifadhi ya Vitu Vyetu vya Kale

Kuhifadhi Vitu Vyetu Vyenye Thamani vya Wakati Uliopita

Kuhifadhi Vitu Vyetu Vyenye Thamani vya Wakati Uliopita

WATU wa Yehova wana historia ndefu yenye thamani sana ya urithi wa kiroho. Historia yenye kuvutia ya urithi huo tunaweza kuipata si tu kupitia machapisho yetu tu, bali pia kupitia picha, barua, masimulizi ya maisha, na vifaa vya zamani vilivyohusiana na ibada, kazi yetu ya kuhubiri, na historia yetu. Hata hivyo, kuna faida gani ya kuhifadhi habari hizo na kuchunguza kwa undani wakati wetu uliopita? Katika taifa la Israeli la kale vichwa vya familia walipaswa kuwafundisha wana wao sheria na matendo ya ajabu ya Yehova ili kwamba wana hao “watie uhakika wao katika Mungu.”​—Zab. 78:1-7.

Kwa muda mrefu kuchunguza vitu vya kale kumechangia pakubwa katika kutimizwa kwa kusudi la Yehova. Kwa mfano, wapinzani walipojaribu kuzuia kazi ya ujenzi wa hekalu huko Yerusalemu, uchunguzi rasmi wa maandishi uliofanywa kwenye hifadhi ya vitu vya kale katika mji mkuu wa Umedi, Ekibatana, ulisaidia kupatikana kwa hati iliyotolewa na Mfalme Koreshi ikiidhinisha ujenzi huo. (Ezra 6:1-4, 12) Hivyo, hekalu likajengwa upya kupatana na mapenzi ya Mungu. Maandishi ya kale yalitumiwa pia na mwandikaji wa Injili Luka, ambaye ‘alifuata kwa uangalifu mambo yote tangu mwanzo kwa usahihi.’​—Luka 1:1-4.

Baraza Linaloongoza linapendezwa sana na historia yetu ya kitheokrasi. Akizungumzia kuhusu umuhimu wa kutunza hati, na kupitisha urithi wetu wa kiroho, mshiriki mmoja wa Baraza Linaloongoza alisema hivi: “Ili kujua tunaenda wapi, tunapaswa kujua tumetoka wapi.” Basi, hivi karibuni Idara ya Kuhifadhi Vitu Vyetu vya Kale ilianzishwa kwenye makao makuu ya ulimwenguni pote huko Brooklyn, New York na Idara hiyo iko chini ya Halmashauri ya Uandikaji.

‘KITABU CHA PICHA’ NA ‘VITU VYA URITHI WA FAMILIA YETU’

Kadiri wakati unavyopita, ndivyo mambo ya zamani yanavyosahaulika na inaelekea wengi wetu wangetamani kuwa na rekodi kamili ya familia. Katika Idara ya Kuhifadhi Vitu Vyetu vya Kale, kazi kubwa inafanywa sasa ili kuhifadhi na kutunza urithi wetu mkubwa unaoendelea kuongezeka. Picha ambazo zimetunzwa kwa uangalifu katika Hifadhi ya Vitu Vyetu vya Kale zitakuwa sehemu ya ‘kitabu cha picha za familia yetu.’ Machapisho yetu ya mapema, masimulizi ya maisha ya watu binafsi yenye kusisimua, na vitu fulani vya kumbukumbu, pia ni miongoni mwa vito vyenye thamani vilivyowekwa katika Hifadhi hiyo. Vitu hivyo ni kama ‘vitu vya urithi vya familia yetu’ ambavyo vinatuelimisha kuhusu urithi wetu wa kitheokrasi na kutusaidia kuutazamia wakati ujao wa familia yetu ya kiroho tukiwa na uhakika.

Tunakualika uichunguze Idara ya Kuhifadhi Vitu Vyetu vya Kale kupitia makala mpya yenye kichwa, “Kutoka Katika Hifadhi ya Vitu Vyetu vya Kale.” Itakuwa ikichapishwa mara kwa mara katika toleo la funzo la Mnara wa Mlinzi. Kwa mfano, katika toleo lijalo tuna mpango wa kuchapisha habari iliyokusudiwa kujibu maswali haya: Kigari cha Mabuku ya Dawn kilikuwa nini? Kilitumiwa na akina nani? Kilitumiwa wakati gani na kwa kusudi gani?

Kama vile kitabu cha picha za kumbukumbu ya familia kinavyoonyesha, mkusanyo wa vitu vyetu mbalimbali vya kale unatueleza mengi kutuhusu na kuhusu ndugu zetu wa kiroho waliotutangulia—kuhusu imani na ujasiri wa wale waliotutangulia, kuhusu shangwe na hali ngumu walizokabili walipokuwa wakimtumikia Baba yetu wa mbinguni mwenye upendo, kuhusu mwongozo wa Mungu na msaada wenye kutegemeka wa watu wake. (Kum. 33:27) Tuna hakika kwamba Yehova atabariki jitihada zinazoendelea za kuhifadhi historia yetu ya kiroho ili tuendelee kuwa na umoja zaidi na hivyo kuimarishwa ili tuendelee kufanya mapenzi yake.

[Sanduku/​Picha katika ukurasa wa 31]

Kuchunguza kwa Makini Zaidi

Wakati wa kuandaa machapisho ya Kikristo, DVD, na machapisho mengine yanayotegemea Biblia, waandikaji wetu, wachoraji, watafiti, na wengine hutumia habari zilizo katika hifadhi za vitu vya kale. Hivyo, Idara ya Kuhifadhi Vitu Vyetu vya Kale huchukua hatua muhimu ili kukusanya na kutunza kwa uangalifu sana habari nyingi za kihistoria kutoka vyanzo kama vile ofisi za tawi, idara za Betheli, makutaniko, watu binafsi, na taasisi za umma. Ona kwa ufupi mambo yanayohusika katika kazi hiyo:

Kupata na Kuchanganua: Vitu vya peke vinaendelea kukusanywa na kuongezwa katika Hifadhi ya Vitu Vyetu vya Kale. Vingi kati ya vitu hivyo vinatolewa kama mchango au mkopo na watu ambao familia zao zimemtumikia Yehova kwa uaminifu kwa miongo mingi. Kuchanganua na kulinganisha habari au vitu hivyo hutusaidia kuongeza uelewaji wa historia yetu na ya watu walioishi katika kipindi hicho.

Kuorodhesha Vitu vya Kale: Vitu vilivyokusanywa katika Idara ya Kuhifadhi Vitu Vyetu vya Kale vinatia ndani maelfu ya vifaa mbalimbali, na baadhi ya vifaa hivyo vimedumu kwa miaka zaidi ya 100. Vitu vinavyotumwa vina maumbo, ukubwa, na ni vya aina mbalimbali na ni lazima viorodheshwe kwa utaratibu kulingana na aina yake ili orodha hiyo iweze kutumiwa wakati ujao.

Kurekebishwa na Kuhifadhiwa: Vitabu na vifaa vingine ambavyo ni vikuu-kuu hurekebishwa na kuhifadhiwa kwa kutumia njia za kisasa. Hati, picha, madondoo ya magazeti, filamu, na kaseti zilizorekodiwa zinahifadhiwa kielektroniki. Hivyo, mtu anaweza kuvipata vitu hivyo kwa njia ya elektroniki ili asiharibu hati au vitu vya kale vyenye thamani ya kihistoria.

Kuweka na Kupata Habari Kuvihusu: Vitu vya kale vinawekwa kwa utaratibu na kutunzwa vizuri ili visiharibike na kuvilinda ili visiharibiwe na mwanga na unyevunyevu. Programu ya kompyuta inatayarishwa ili kusaidia kufanya utafiti na kupata habari kuhusu vitu hivyo vya kale vyenye thamani.

[Picha katika ukurasa wa 32]

1. Bango la sinema ya “Photo-Drama of Creation.” 2. Orodha ya uandikishaji wa magazeti. 3. Gari lenye vipaza-sauti. 4. Jalada la gazeti Mnara wa Mlinzi la Aprili 15, 1912. 5. Hati ya kumfunga gerezani J. F. Rutherford. 6. Kikuza-sauti cha kituo cha redio cha WBBR. 7. Gramafoni. 8. Sanduku la kubebea vitabu. 9. Maandishi ya kibinafsi. 10. Telegramu iliyotumwa kwa J. F. Rutherford.2