Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Iga Mfano Ambao Yesu Aliweka Katika Kukesha

Iga Mfano Ambao Yesu Aliweka Katika Kukesha

Iga Mfano Ambao Yesu Aliweka Katika Kukesha

“Endeleeni kukesha na kusali.”—MT. 26:41.

UNGEJIBUJE?

Sala zetu zinaweza kuonyesha jinsi gani kwamba tunakesha?

Ni katika njia zipi tunaweza kuonyesha kwamba tunaendelea kukesha katika huduma yetu?

Kwa nini ni muhimu tuendelee kukesha tunapokuwa chini ya majaribu, na tunawezaje kufanya hivyo?

1, 2. (a) Ni maswali gani ambayo huenda mtu akajiuliza kuhusiana na mfano ambao Yesu aliweka katika kukesha? (b) Je, wanadamu wenye dhambi wanaweza kuiga mfano mkamilifu wa Yesu? Toa mfano.

HUENDA ukajiuliza hivi: ‘Kwa kuwa Yesu alikuwa mkamilifu, je, kweli tunaweza kuiga mfano wake katika kukesha? Isitoshe, nyakati nyingine Yesu alijua wazi mambo yatakayotukia wakati ujao, hata kwa maelfu ya miaka! Je, alihitaji kweli kukesha?’ (Mt. 24:37-39; Ebr. 4:15) Acheni basi tujibu kwanza maswali hayo ili tuone hasa jinsi habari hii ilivyo muhimu na yenye uharaka.

2 Je, wanadamu wenye dhambi wanaweza kuiga mfano wa mtu mkamilifu? Naam, wanaweza kwa sababu tunaweza kujifunza kutokana na mfano mzuri wa mwalimu bora. Kwa mfano, wazia mtu anayejifunza kupiga mshale kwa mara ya kwanza. Mwanzoni, hawezi kulenga shabaha, lakini anaendelea kujifunza zaidi na anaendelea kujaribu. Ili awe mlenga-shabaha stadi anachunguza kwa makini mfano wa mwalimu wake, ambaye ni bingwa wa kupiga mishale. Mwanafunzi huyo anaangalia kwa makini jinsi mwalimu wake anavyosimama, jinsi anavyoweka mikono yake, na jinsi anavyotumia vidole vyake kuvuta kamba ya upinde. Pole kwa pole, mwanafunzi huyo mpya mwenye bidii anajifunza anapaswa kuvuta kamba ya upinde kwa nguvu nyingi kadiri gani; anafikiria jinsi upepo unavyovuma, na anaendelea kujitahidi. Kwa kuiga yale ambayo anaona mwalimu wake akifanya, hatimaye anajifunza kulenga mishale yake karibu zaidi na shabaha. Vivyo hivyo, tunaendelea kujitahidi kufanya mabadiliko tukiwa Wakristo kwa kufuata maagizo ya Yesu na kuiga mfano wake mkamilifu.

3. (a) Yesu alionyeshaje kwamba alihitaji kukesha? (b) Tutachunguza nini katika makala hii?

3 Hata hivyo, namna gani kuhusu kukesha? Je, kwa kweli Yesu alihitaji kufanya hivyo? Naam, alihitaji. Kwa mfano, usiku wa mwisho wa maisha yake duniani, Yesu aliwahimiza mitume wake waaminifu hivi: “Mwendelee kukesha pamoja nami.” Akaongeza: “Endeleeni kukesha na kusali sikuzote, ili msiingie katika jaribu.” (Mt. 26:38, 41) Licha ya kwamba sikuzote alikesha, Yesu alitaka kuendelea kukesha na kuwa karibu iwezekanavyo na Baba yake wa mbinguni hasa katika saa hizo ngumu kabla ya kifo chake. Alijua kwamba wafuasi wake walihitaji pia kuendelea kukesha, si wakati huo tu bali pia wakati ujao. Hivyo, acheni tuchunguze kwa nini Yesu anataka tuendelee kukesha. Baadaye, tutachunguza njia tatu ambazo tunaweza kuiga katika maisha yetu ya kila siku, jinsi Yesu alivyokesha.

KWA NINI YESU ANATAKA TUENDELEE KUKESHA?

4. Kuna uhusiano gani kati ya mambo ambayo hatujui kuhusu wakati ujao na uhitaji wetu wa kuendelea kukesha?

4 Kwa ufupi, Yesu anataka tuendelea kukesha kwa sababu ya mambo ambayo hatujui na yale ambayo tunajua. Yesu alipokuwa mwanadamu duniani, je, alijua mambo yote ambayo yangetukia wakati ujao? Hapana, kwa sababu alikiri hivi kwa unyenyekevu: “Kuhusu siku ile na saa ile hakuna mtu anayejua, wala malaika wa mbinguni wala Mwana, ila Baba tu.” (Mt. 24:36) Wakati huo, Yesu, yaani, “Mwana,” hakujua ni lini hasa mwisho wa ulimwengu huu mwovu ungekuja. Namna gani sisi leo? Je, tunajua kila kitu kuhusu wakati ujao? Bila shaka hapana! Hatujui ni lini hasa Yehova atamtuma Mwana wake ili kuukomesha mfumo huu mwovu wa mambo. Kama tungejua, je, tungehitaji kwa kweli kuendelea kukesha? Kama Yesu alivyoeleza, mwisho utakuja kwa ghafula, bila kutarajiwa; hivyo tunahitaji kuendelea kukesha kuliko wakati mwingine wowote ule.—Soma Mathayo 24:43.

5, 6. (a) Ujuzi wetu kuhusu wakati ujao na makusudi ya Mungu unatusaidiaje kuendelea kukesha? (b) Kwa nini mambo tunayojua kumhusu Shetani yanapaswa kutufanya tuazimie zaidi kuendelea kukesha?

5 Kwa upande mwingine, Yesu alijua mambo mengi mazuri ajabu kuhusu wakati ujao, kweli ambazo watu wengi wa siku zake hawakuzijua kamwe. Hatujui mambo mengi hivyo kama Yesu, lakini kupitia mafundisho yake, tunajua mambo mengi kuhusu Ufalme wa Mungu na yale ambayo utatimiza hivi karibuni. Tunapowatazama watu wanaotuzunguka, shuleni, kazini, au katika eneo tunalohubiri, je, hatuoni kwamba wengi wao wanaishi katika giza zito la kiroho kwa sababu ya kutojua kweli hizo nzuri ajabu? Hiyo ni sababu nyingine inayotufanya tuendelee kukesha. Kama Yesu, tunahitaji kuwa macho sikuzote, kwa kutumia fursa zote tunazopata ili kuwaambia wengine mambo tunayojua kuhusu Ufalme wa Mungu. Kila fursa tunayopata ni yenye thamani, na hatutaki kupoteza fursa yoyote ile. Uhai wa watu uko hatarini!—1 Tim. 4:16.

6 Yesu alijua jambo lingine ambalo lilimfanya aendelee kukesha. Alijua kwamba Shetani alikuwa ameazimia kumjaribu, kumtesa, na kuvunja utimilifu wake. Adui huyo mwovu alikuwa sikuzote akitafuta “wakati mwingine unaofaa” ili kumjaribu Yesu. (Luka 4:13) Yesu hakuacha kamwe kukesha. Alitaka kuwa tayari kwa ajili ya jaribu lolote, iwe ni upinzani, kishawishi, au mateso. Je, inaweza kusemwa hivyo kutuhusu? Tunajua kwamba Shetani bado ni “kama simba anayenguruma, akitafuta kummeza mtu.” Ndiyo sababu Neno la Mungu linawahimiza Wakristo wote hivi: “Tunzeni akili zenu, iweni wenye kulinda.” (1 Pet. 5:8) Hata hivyo, tunawezaje kufanya hivyo?

JINSI YA KUENDELEA KUKESHA KATIKA SALA

7, 8. Yesu alitoa shauri gani kuhusu sala, na alituwekea mfano gani?

7 Biblia inaonyesha kwamba kuna uhusiano mkubwa kati ya kuwa macho kiroho au kukesha, na sala. (Kol. 4:2; 1 Pet. 4:7) Muda mfupi tu baada ya kuwaomba wafuasi wake waendelee kukesha pamoja naye, Yesu alisema hivi: “Endeleeni kukesha na kusali sikuzote, ili msiingie katika jaribu.” (Mt. 26:41) Je, alimaanisha kwamba wafuasi wake walipaswa kutii shauri hilo wakati huo tu walipokuwa wakikabiliana na hali ngumu sana? Hapana, shauri lake ni kanuni ambayo tunapaswa kufuata kila siku.

8 Yesu aliweka mfano mzuri sana kuhusiana na sala. Huenda unakumbuka kwamba wakati mmoja alisali kwa Baba yake usiku kucha. Acheni basi tujaribu kufikiria hali hiyo. (Soma Luka 6:12, 13.) Ni wakati wa majira ya kuchipua na inaelekea Yesu yuko karibu na mji wa wavuvi wa Kapernaumu, eneo la nyumbani ambapo Yesu anapiga kambi yake. Jioni inapofika, Yesu anapanda mlima mmoja ulio karibu na Bahari ya Galilaya. Anapoangalia eneo la chini wakati giza linapoingia, labda anaona mwangaza wa taa nyingi ndogo-ndogo za mafuta katika mji wa Kapernaumu na vijiji vya karibu. Hata hivyo, hakuna jambo lolote linalomkengeusha anapozungumza na Yehova katika sala. Dakika zinapita, na hatimaye saa. Hakazii sana fikira mwangaza wa taa ndogo-ndogo zilizo mbali na ambazo zinazimika moja baada ya nyingine au hakazii fikira mwezi unaosonga angani au sauti za wanyama wanaolia usiku porini. Inaelekea anasali kuhusu uamuzi mkubwa ambao uko mbele yake, yaani, uamuzi wa kuchagua mitume wake 12. Tunaweza kuwazia Yesu akisali kwa moyo wote kwa Baba yake akimwambia mawazo na mahangaiko yake yote kuhusu kila mwanafunzi wake anapomwomba kwa bidii mwongozo na hekima.

9. Tunaweza kujifunza nini kutokana na mfano wa Yesu wa kusali usiku kucha?

9 Tunaweza kujifunza nini kutokana na mfano wa Yesu? Je, mfano huo unatufundisha kwamba ni lazima tusali kwa muda wa saa nyingi? Hapana, kwa sababu Yesu alikiri hivi kwa unyoofu kuhusu wafuasi wake: “Bila shaka, roho inataka, lakini mwili ni dhaifu.” (Mt. 26:41) Hata hivyo, tunaweza kumwiga Yesu. Kwa mfano, je, tunazungumza na Baba yetu wa mbinguni kabla ya kufanya uamuzi wowote ambao huenda ukatuathiri sisi kiroho, familia yetu, au waamini wenzetu? Je, sala zetu zinatia ndani mahangaiko kuhusu ndugu na dada zetu katika imani? Je, tunasali kutoka moyoni badala ya kurudia-rudia maneno yaleyale? Ona pia kwamba Yesu alithamini kuzungumza kibinafsi, faraghani pamoja na Baba yake. Katika ulimwengu wa leo wenye shughuli nyingi, ni rahisi sana kusahau mambo yaliyo ya maana zaidi. Tukitenga wakati wa kutosha kwa ajili ya sala nzito, ya faraghani, tutakuwa macho zaidi kiroho. (Mt. 6:6, 7) Tutamkaribia zaidi Yehova, tukiwa na hamu zaidi ya kuimarisha uhusiano wetu pamoja naye na kuepuka kufanya jambo lolote ambalo linaweza kudhoofisha uhusiano huo.—Zab. 25:14.

JINSI YA KUENDELEA KUKESHA KATIKA KAZI YA KUHUBIRI

10. Ni mfano gani unaotuonyesha kwamba Yesu alikuwa macho kutumia fursa alizopata ili kutoa ushahidi?

10 Yesu aliendelea kukesha katika kazi aliyopewa na Yehova afanye. Huenda kukawa na kazi fulani ambazo zinaweza kuruhusu akili ya mfanyakazi kutanga-tanga bila madhara yoyote. Hata hivyo, kazi nyingi zinahitaji mtu kuwa makini na kubaki macho, na bila shaka huduma ya Kikristo inahitaji hivyo. Yesu alikuwa macho sikuzote katika kazi yake, akitafuta fursa mbalimbali ili kuhubiri habari njema. Kwa mfano, wakati yeye na wanafunzi wake walipofika katika mji wa Sikari baada ya kutembea asubuhi yote, wanafunzi walienda kununua chakula. Yesu alibaki kando ya kisima cha mji ili kupumzika, lakini alikuwa macho na aliona fursa ya kutoa ushahidi. Mwanamke Msamaria alikuja kuchota maji. Yesu angeamua kulala kidogo au angefikiria sababu nyingine za kutozungumza na mwanamke huyo. Hata hivyo, alianzisha mazungumzo na mwanamke huyo, na akamtolea ushahidi wenye nguvu ambao ulisaidia watu wengi katika jiji hilo. (Yoh. 4:4-26, 39-42) Je, tunaweza kuiga kwa ukaribu zaidi mfano wa Yesu katika kukesha, labda kwa kujitahidi kuwa macho zaidi ili kutumia fursa tunazopata kuwahubiria habari njema watu tunaokutana nao kila siku?

11, 12. (a) Yesu aliwaambia nini wale waliojaribu kumkengeusha asifanye kazi yake? (b) Yesu alionyesha usawaziko gani kuhusiana na kazi yake?

11 Nyakati nyingine, watu wenye nia nzuri walijaribu kumkengeusha Yesu asifanye kazi yake. Huko Kapernaumu, umati ulivutiwa sana na miujiza ya Yesu ya kuponya wagonjwa na hivyo ukataka kumzuia asiondoke. Inaeleweka kwa nini walitaka kufanya hivyo. Hata hivyo, kazi ya Yesu ilikuwa kuwahubiria ‘kondoo wote waliopotea wa nyumba ya Israeli,’ na si watu wa jiji moja tu. (Mt. 15:24) Hivyo, aliwaambia watu hao hivi: “Ni lazima nitangaze habari njema ya ufalme wa Mungu kwenye majiji mengine pia, kwa sababu nilitumwa kufanya hivyo.” (Luka 4:40-44) Kwa wazi, jambo muhimu zaidi katika maisha ya Yesu lilikuwa huduma yake. Hakuruhusu jambo lolote limkengeushe.

12 Je, Yesu alijishughulisha sana na kazi yake na hivyo akakosa usawaziko au kutokuwa na wakati wa kufurahia vitu vingine maishani? Je, alijishughulisha sana na huduma yake hivi kwamba alipuuza mahitaji ya watu? Hapana, Yesu aliweka mfano mkamilifu katika kuwa na usawaziko. Alifurahia maisha, pia alifurahia pindi za kuwa pamoja na marafiki wake. Alithamini familia mbalimbali, akaonyesha kwamba anaelewa mahitaji na matatizo yao, na akawaonyesha watoto upendo wa kutoka moyoni.—Soma Marko 10:13-16.

13. Tunawezaje kuiga mfano wa Yesu katika kukesha na kuwa na usawaziko inapohusu kazi yetu ya kuhubiri kuhusu Ufalme?

13 Tunapoiga mfano wa Yesu katika kukesha, tunawezaje kujitahidi kuwa na usawaziko kama wake? Haturuhusu ulimwengu huu utukengeushe kutoka katika kazi yetu. Hata marafiki na watu wa ukoo wenye nia nzuri wanaweza kutuhimiza tupunguze bidii yetu katika huduma au kutuhimiza tufuatie yale ambayo wanayaona kuwa maisha ya kawaida. Hata hivyo, ikiwa tunamwiga Yesu, tutaona huduma yetu kuwa muhimu kama chakula. (Yoh. 4:34) Huduma yetu inatuimarisha kiroho na pia inatuletea shangwe. Lakini hatutaki kamwe kukosa usawaziko, kwa kujiona kuwa waadilifu au kujizuia kufurahia vitu vingine. Kama Yesu, tunataka kuwa wenye shangwe, watumishi wa “Mungu mwenye furaha” ambao wana usawaziko.—1 Tim. 1:11.

JINSI YA KUENDELEA KUKESHA KATIKA NYAKATI ZA MAJARIBU

14. Wakati wa majaribu, tunahitaji kupinga mwelekeo gani, na kwa nini?

14 Kama ambavyo tumeona, Yesu alitoa baadhi ya mashauri mazito zaidi kuhusu kuendelea kukesha alipokuwa chini ya jaribu kali. (Soma Marko 14:37.) Tunapokabiliana na hali ngumu, tunahitaji kuiga mfano wake kuliko wakati mwingine wowote ule. Wanapokuwa chini ya jaribu, watu wengi wana mwelekeo wa kusahau kweli moja muhimu, kweli muhimu ambayo inatajwa mara mbili na kitabu cha Methali: “Kuna njia ambayo imenyooka mbele ya mwanadamu, lakini njia za kifo ndizo mwisho wake baadaye.” (Met. 14:12; 16:25) Tukitegemea akili zetu wenyewe, hasa wakati tunapokabili matatizo makubwa, inaelekea tutajihatarisha wenyewe na pia wale tunaowapenda.

15. Ni jaribu gani ambalo huenda kichwa cha familia akakabili wakati wa hali ngumu za kiuchumi?

15 Kwa mfano, huenda kichwa cha familia akakabili mkazo mkali anapojitahidi kutosheleza mahitaji ya kimwili ya “wale walio washiriki wa nyumba yake.” (1 Tim. 5:8) Huenda akashawishiwa kutafuta kazi ambayo mara kwa mara inamfanya akose mikutano ya Kikristo, akose kuongoza ibada ya familia, au kushiriki katika huduma. Ikiwa anategemea tu akili yake ya kibinadamu, anaweza kuanza kujitetea na hata kuona kazi hiyo kuwa sawa. Hata hivyo, anaweza kuwa mgonjwa kiroho au kufa kiroho. Ingekuwa vyema zaidi kufuata shauri la Methali 3:5, 6! Sulemani alisema hivi: “Mtegemee Yehova kwa moyo wako wote wala usitegemee uelewaji wako mwenyewe. Mtambue yeye katika njia zako zote, naye atanyoosha mapito yako.”

16. (a) Yesu alituwekea mfano gani katika kuitegemea hekima ya Yehova badala ya kuitegemea hekima yake mwenyewe? (b) Wengi ambao ni vichwa vya familia wanaigaje mfano wa Yesu wa kumtegemea Yehova katika nyakati ngumu?

16 Yesu alipokuwa chini ya jaribu, hakukubali kamwe kutegemea uelewaji wake mwenyewe. Fikiria hili! Mtu mwenye hekima zaidi kuwahi kuishi duniani alichagua kutotegemea hekima yake mwenyewe. Kwa mfano, Shetani alipomjaribu, Yesu alijibu tena na tena kwa kusema hivi: “Imeandikwa.” (Mt. 4:4, 7, 10) Alitegemea hekima ya Baba yake ili kushinda jaribu, huku akionyesha unyenyekevu, sifa ambayo Shetani anadharau na ambayo hana. Je, tunafanya vivyo hivyo? Kichwa cha familia anayeiga kukesha kwa Yesu anaacha Neno la Mungu limwongoze, hasa katika nyakati ngumu. Ulimwenguni pote, maelfu ya vichwa vya familia wanafanya vivyo hivyo. Wanatanguliza kwa uthabiti ibada safi na Ufalme wa Mungu maishani mwao badala ya mahitaji ya kimwili. Katika njia hiyo, wanazitunza vizuri familia zao. Yehova anabariki jitihada zao za kuandalia familia zao mahitaji ya kimwili, kama vile tu Neno lake linavyoahidi.—Mt. 6:33.

17. Ni nini kinachokuchochea kuiga mfano wa Yesu katika kukesha?

17 Bila shaka yoyote, Yesu aliweka mfano mzuri iwezekanavyo katika kukesha. Mfano wake unasaidia, ni wenye manufaa, na hata unaokoa uhai. Kumbuka kwamba Shetani anajaribu sana kukubembeleza ili ulale kiroho, imani yako idhoofike, upoteze bidii yako ya kumwabudu Yehova, na kulegeza utimilifu wako. (1 The. 5:6) Usimwache akushinde! Endelea kukesha kama Yesu alivyofanya, yaani, endelea kukesha katika sala, katika huduma yako, na katika kupambana na majaribu. Ukifanya hivyo, utakuwa na maisha yenye kusudi, yenye furaha, na yenye kuridhisha hata sasa katika siku za mwisho za mfumo huu unaoangamia. Pia, ukiendelea kukesha utakuwa na uhakika kwamba Bwana Mkubwa wako atakapokuja kuleta mwisho wa mfumo huu, atakukuta ukiwa macho na mwenye kutenda, huku ukifanya mapenzi ya Baba yake. Yehova atafurahi kama nini kukuthawabisha kwa sababu ya uaminifu wako!—Ufu. 16:15.

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 6]

Yesu alimhubiria mwanamke huyo kwenye kisima. Unatumia fursa gani kuhubiri kila siku?

[Picha katika ukurasa wa 7]

Unaonyesha kwamba unaendelea kukesha kwa kutunza hali njema ya kiroho ya familia yako