Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutoka Katika Hifadhi ya Vitu Vyetu vya Kale

‘Kilifanya Nijulikane na Watu Wengi’

‘Kilifanya Nijulikane na Watu Wengi’

Wakati mhubiri wa wakati wote Charlotte White alipofika huko Louisville, Kentucky, Marekani, huku akisukuma sanduku lake lenye magurudumu, watu wengi walishangaa.

HUO ulikuwa mwaka wa 1908, na kwa kweli watu wengi katika mji huo walishangaa kumwona Dada White akisukuma kifaa kipya kilichotoka tu kugunduliwa, yaani, Kigari cha Dawn. Dada White alisema hivi: “Watu walisema mengi kuhusu kigari hicho, na hivyo kunifanya nijulikane na watu wengi.”

Wanafunzi wa Biblia, kama Mashahidi wa Yehova walivyokuwa wakiitwa wakati huo, waliona kuna uhitaji wa kuwaambia wengine kweli zenye thamani walizopata baada ya kujifunza Maandiko kwa bidii. Wengi walikuwa wamepata ujuzi wa Biblia kutoka katika mfululizo wa mabuku yaliyoitwa Millennial Dawn (baadaye yaliitwa Studies in the Scriptures). Wakristo hao ambao walikuwa tayari kusafiri na ambao walikuwa na uwezo wa kusafiri maeneo ya mbali, yaani, mijini, vijijini, na maeneo ya mashambani walitoa vitabu hivyo ambavyo viliitwa “Misaada ya Wanafunzi wa Biblia” kwa watu wenye hamu ya kusoma.

Mnamo 1908, Dada White na wahubiri wengine wenye bidii wa Ufalme waliwaachia watu mabuku hayo sita yaliyo na majalada yaliyofunikwa kwa vitambaa, kwa dola 1.65 za Marekani. Badala ya kumpa mwenye nyumba mabuku hayo papo hapo, wahubiri hao waliandika kwanza majina ya watu waliohitaji, kisha, wakarudi baadaye—mara nyingi katika siku ya mshahara ili kuwapelekea watu mabuku hayo na kuchukua mchango mdogo wa gharama za uchapishaji. Mwanamume mmoja mpinzani alilalamika kuhusu kiasi kidogo cha pesa ambacho watu walichanga walipokuwa wakipewa vitabu hivyo!

Malinda Keefer anakumbuka akiandika majina ya watu kati ya mia mbili na mia tatu kwa juma waliohitaji mabuku hayo. Hata hivyo, upendezi mkubwa ulioonyeshwa na watu kuelekea mabuku ya Dawn ulitokeza matatizo fulani. Buku la sita peke yake lilikuwa na kurasa 740! Gazeti la Mnara wa Mlinzi lilikiri hivi: “Vitabu hamsini vina uzito wa kilogramu 18, ambao ni uzito mkubwa sana,” hasa kwa akina dada kubeba.

Ili kutatua tatizo la kuwapelekea watu mabuku ya Dawn, Ndugu James Cole alibuni fremu ya kukunjwa yenye magurudumu mawili ambayo sanduku lingeweza kufungiliwa juu yake kwa skurubu. Kukiwa hakuna uhitaji wa kubeba tena makatoni mazito yaliyojaa vitabu, James Cole aliyebuni kigari hicho alisema hivi: “Sitaki tena kuvunja mabega yangu.” Kwenye kusanyiko la wilaya la Wanafunzi wa Biblia la mwaka 1908 huko Cincinnati, Ohio, Ndugu Cole aliwaonyesha wahudhuriaji wenye furaha kifaa hicho kipya. Kwenye sehemu ya juu ya kufungia kulikuwa na jina Kigari cha Dawn, kwa sababu kilitumiwa kubeba mabuku ya Millennial Dawn. Baada ya kukizoea kigari hicho, ilikuwa rahisi kusukuma kwa mkono mmoja sanduku lililojaa vitabu vingi. Urefu wa kigari hicho ungeweza kurekebishwa, na magurudumu yake yangeweza kutembea hata kwenye barabara za vumbi. Baada ya kushiriki katika huduma kwa siku nzima, mtu angeweza kukunja magurudumu ya mpira ya kigari hicho kando ya sanduku na kurudi nacho nyumbani kwa miguu au kwa gari.

Akina dada ambao walikuwa katika utumishi wa wakati wote wangeweza kupata Kigari cha Dawn bila malipo. Wengine wangeweza kukinunua kigari hicho kwa dola 2.50 za Marekani. Dada Keefer, ambaye picha yake imeonyeshwa hapa, alijua kutumia Kigari cha Dawn vizuri sana hivi kwamba angeweza kusukuma sanduku lililojaa vitabu kwa mkono mmoja na kubeba mfuko wenye vitabu kwa mkono mwingine. Akiwa amepata watu wengi wenye kupendezwa katika mji mmoja wenye migodi huko Pennsylvania, Marekani, katika siku ya kupeleka vitabu, kwa kawaida dada Keefer alifunga safari na kuvuka daraja mara tatu au nne.

Mwishoni mwa miaka ya 1980, rubani mmoja wa ndege alivumbua begi lenye magurudumu ambalo linatumiwa kwa kawaida na watu wanaosafiri kwa ndege au wanaotembea katika barabara za majiji zenye shughuli nyingi. Lakini miaka mia moja hivi iliyopita, yaelekea Wanafunzi wa Biblia wenye bidii walifurahia kutazamwa kwa mshangao na watu wengi wenye udadisi walipokuwa wakisukuma huku na huku Vigari vyao vya Dawn wakipanda mbegu zenye thamani za kweli ya Biblia.

[Blabu katika ukurasa wa 32]

Katika siku ya kupeleka vitabu, kwa kawaida Dada Keefer alifunga safari na kuvuka daraja mara tatu au nne

[Blabu katika ukurasa wa 32]

Kigari hiki kilisuluhisha tatizo la kubeba mabuku ya Dawn