Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Linda Roho Nzuri ya Kutaniko

Linda Roho Nzuri ya Kutaniko

Linda Roho Nzuri ya Kutaniko

“Fadhili zisizostahiliwa za Bwana Yesu Kristo ziwe pamoja na roho mnayoonyesha.” —FLP. 4:23.

TUNAWEZA KUCHOCHEAJE ROHO NZURI KUTANIKONI . . .

tunaposhirikiana na ndugu zetu?

tunaposhiriki katika huduma ya shambani kwa bidii?

tunaporipoti dhambi nzito?

1. Kwa nini makutaniko ya Filipi na Thiatira yalipongezwa?

WAKRISTO wa karne ya kwanza huko Filipi walikuwa maskini kimwili. Hata hivyo, walikuwa wakarimu na waliwaonyesha waamini wenzao upendo mwingi sana. (Flp. 1:3-5, 9; 4:15, 16) Hivyo, akimalizia barua yake iliyoongozwa na roho ya Mungu aliyowaandikia, mtume Paulo alisema hivi: “Fadhili zisizostahiliwa za Bwana Yesu Kristo ziwe pamoja na roho mnayoonyesha.” (Flp. 4:23) Kwa kuwa Wakristo huko Thiatira walionyesha roho kama hiyo, Yesu Kristo aliyetukuzwa aliwaambia hivi: ‘Mimi nayajua matendo yenu, na upendo wenu na imani na huduma na uvumilivu wenu, na kwamba matendo yenu ya hivi karibuni yanazidi yale ya zamani.’—Ufu. 2:19.

2. Tunawezaje kusitawisha roho ambayo kutaniko letu linaonyesha?

2 Vivyo hivyo leo, kila kutaniko la Mashahidi wa Yehova huonyesha roho au mtazamo fulani. Makutaniko fulani yanajulikana hasa kwa sababu yanaonyesha roho ya uchangamfu na upendo. Mengine yanajulikana kwa kuunga mkono kwa bidii kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme na kuthamini sana huduma ya wakati wote. Kila mmoja wetu anapojitahidi kusitawisha roho nzuri, tunachangia umoja wa kutaniko na kulisaidia kwa ujumla lizidi kufanya maendeleo ya kiroho. (1 Kor. 1:10) Kwa upande mwingine, tukiwa na roho isiyofaa tunaweza kuwafanya wengine katika kutaniko wasinzie kiroho, wawe na mtazamo wa kupuuza mambo ya kiroho, na hata kuachilia matendo mabaya kutanikoni. (1 Kor. 5:1; Ufu. 3:15, 16) Kutaniko lenu lina roho ya aina gani? Wewe binafsi unaweza kuendeleza jinsi gani roho nzuri ya kutaniko?

CHOCHEA ROHO NZURI

3, 4. Tunaweza jinsi gani ‘kumsifu Yehova katika kutaniko kubwa’?

3 Mtunga-zaburi aliimba hivi: “Nitakusifu [Yehova] katika kutaniko kubwa; nitakusifu kati ya kikundi cha watu wengi.” (Zab. 35:18) Mtunga-zaburi hakusita kumsifu Yehova akiwa miongoni mwa watumishi wengine wa Mungu. Mikutano ya kila juma ya kutaniko, kutia ndani Funzo la Mnara wa Mlinzi hutupatia fursa nzuri za kuonyesha bidii yetu ya kiroho tunapotoa maelezo mbalimbali kuhusu imani yetu. Ni vizuri sote tujiulize hivi: ‘Je, ninatumia kwa ukamili pendeleo la kushiriki katika mikutano? Je, ninajitayarisha vizuri kwa ajili ya mikutano na kutoa maelezo yenye kujenga? Nikiwa kichwa cha familia, je, ninawasaidia watoto wangu kutayarisha mapema maelezo na kuwafundisha kutoa maelezo hayo kwa maneno yao wenyewe?’

4 Mtunga-zaburi Daudi alihusianisha hali ya moyo wetu kuwa imara na uimbaji wetu. “Moyo wangu uko imara, Ee Mungu,” akasema, “moyo wangu uko imara. Nitaimba na kupiga muziki.” (Zab. 57:7) Nyimbo zinazotumiwa katika mikutano ya Kikristo zinatupatia fursa nzuri ya ‘kumwimbia na kumpigia Yehova muziki’ tukiwa na mioyo imara. Ikiwa hatujui baadhi ya nyimbo hizo, kwa nini tusitumie jioni ya Ibada ya Familia kujizoeza kuimba nyimbo hizo? Acheni tuazimie ‘kumwimbia Yehova katika maisha yetu yote na kumpigia Mungu wetu muziki maadamu tupo.’—Zab. 104:33.

5, 6. Tunawezaje kuwa wakaribishaji-wageni na wakarimu kuelekea wengine, na kufanya hivyo kutachangia nini kutanikoni?

5 Kuwaonyesha ndugu na dada zetu ukaribishaji-wageni ni njia nyingine ya kusitawisha roho ya upendo katika kutaniko. Katika sura ya mwisho ya barua yake kwa Waebrania, Paulo anatia ndani himizo hili: “Upendo wenu wa kindugu na uendelee. Msisahau ukaribishaji-wageni.” (Ebr. 13:1, 2) Kuwaandalia chakula waangalizi wanaosafiri na wake zao au watumishi wa wakati wote katika kutaniko ni njia bora ya kuonyesha ukaribishaji-wageni. Wafikirie pia wajane, familia za mzazi mmoja, au watu wengine ambao wanaweza kufaidika wakijiunga nasi mara kwa mara kwa ajili ya chakula au wakati wa ibada yetu ya familia.

6 Paulo alimwagiza Timotheo awahimize wengine “wafanye mema, wawe matajiri katika matendo mazuri, wawe wakarimu, tayari kushiriki, wakijiwekea wenyewe kwa usalama hazina ya msingi mzuri kwa ajili ya wakati ujao, ili waushike imara uzima ulio wa kweli.” (1 Tim. 6:17-19) Paulo alikuwa akipendekeza kwamba waabudu wenzake wasitawishe roho ya ukarimu. Hata wakati wa hali ngumu za kiuchumi tunaweza kuchochea roho ya ukarimu. Njia nzuri ya kufanya hivyo ni kwa kuandaa usafiri katika huduma ya shambani na kuwasaidia wale wanaohitaji kusafiri kwenda na kurudi kutoka mikutanoni. Lakini namna gani kuhusu wale wanaonufaika na matendo hayo ya fadhili zenye upendo? Watakuwa wanachochea roho nzuri kutanikoni ikiwa wataonyesha uthamini, labda kwa kutoa chochote wanachoweza ili kusaidia kulipia gharama za mafuta ya gari zinazozidi kuongezeka. Njia nyingine ya kuwafanya ndugu na dada zetu wa kiroho wahisi kuwa wanahitajika na kupendwa ni kupanga kutumia wakati mwingi hata zaidi pamoja nao. Tunapotenda mambo mengi mema ‘kuelekea wale ambao katika imani ni jamaa zetu,’ na kuwa tayari kutumia wakati na mali zetu pamoja nao, upendo wetu kuwaelekea utaongezeka, na pia tunachochea roho nzuri na yenye uchangamfu katika kutaniko.—Gal. 6:10.

7. Kutunza siri ya mambo ya kibinafsi ya wengine husaidiaje kulinda roho nzuri kutanikoni?

7 Fikiria pia mambo mengine ambayo yanaweza kuimarisha kifungo cha upendo kati yetu na waabudu wenzetu, yaani, urafiki na kutunza siri. (Soma Methali 18:24.) Marafiki wa kweli hutunza siri za mambo ya kibinafsi. Ndugu zetu wanapotueleza hisia zao na mambo yao ya siri wakiwa na hakika kwamba hatutawaambia watu wengine mambo hayo, kifungo cha upendo ambacho huenda kipo kitaimarika. Acheni tuchochee kutanikoni roho ya upendo kama ile iliyo katika familia kwa kuwa marafiki wenye kuaminika ambao wanaweza kutunza siri.—Met. 20:19.

UWE NA BIDII KATIKA HUDUMA

8. Walaodikia walipewa shauri gani, na kwa nini?

8 Katika ujumbe wake kwa kutaniko la Laodikia, Yesu alisema hivi: “Mimi nayajua matendo yako, kwamba wewe si baridi wala si moto. Laiti ungalikuwa baridi au moto. Kwa hiyo, kwa sababu wewe ni vuguvugu na si moto wala si baridi, nitakutapika kutoka kinywani mwangu.” (Ufu. 3:15, 16) Walaodikia hawakuwa na bidii katika huduma ya Kikristo. Inaelekea kwamba mtazamo huo uliathiri mahusiano yao ya kibinafsi pia. Hivyo, kwa upendo Yesu aliwashauri hivi: “Wale wote ninaowapenda, mimi huwakaripia na kuwatia nidhamu. Kwa hiyo uwe mwenye bidii na utubu.”—Ufu. 3:19.

9. Mtazamo wetu kuelekea huduma ya shambani unachochea jinsi gani roho ya kutaniko?

9 Ili kuchochea roho nzuri katika kutaniko, tunapaswa kuwa wenye bidii katika utumishi wa shambani. Kutaniko limepangwa kwa kusudi la kuwatafuta watu wenye mfano wa kondoo katika eneo na kuwajenga kiroho. Hivyo, tunahitaji kushiriki kwa shauku katika kazi ya kufanya wanafunzi kama Yesu alivyofanya. (Mt. 28:19, 20; Luka 4:43) Kadiri tunavyokuwa wenye bidii zaidi katika huduma, ndivyo tutakavyokuwa na muungano zaidi tukiwa “wafanyakazi wenzi wa Mungu.” (1 Kor. 3:9) Tunapowaona wengine katika utumishi wa shambani wakitetea imani yao na kuonyesha uthamini kuelekea mambo ya kiroho, tunachochewa kuwapenda na kuwaheshimu zaidi. Pia, kutumikia “bega kwa bega” katika huduma huchochea roho ya muungano kutanikoni.—Soma Sefania 3:9.

10. Jitihada ya kuboresha utumishi wetu wa shambani inaweza kuchocheaje roho ya wengine kutanikoni?

10 Pia, jitihada zetu za kuboresha huduma yetu zina matokeo mazuri juu ya wengine. Kadiri tunavyoonyesha hangaiko kubwa kuelekea watu tunaokutana nao na kuboresha uwezo wetu wa kugusa mioyo ya watu wanaotusikiliza, ndivyo shangwe yetu katika huduma itakavyoongezeka. (Mt. 9:36, 37) Tukiwa wachangamfu, watu walio pamoja nasi watakuwa wachangamfu pia. Yesu aliwatuma wanafunzi wake wawili-wawili ili wahubiri badala ya kuwatuma wakiwa mtu mmojammoja. (Luka 10:1) Hilo halikuwatia moyo na kuwazoeza tu bali pia liliwachochea kuwa na bidii zaidi katika huduma. Je, hatuthamini kushirikiana na wahubiri wa Ufalme wenye bidii? Roho yao ya uchangamfu inatutia moyo na kutuchochea tuendelee katika kazi ya kuhubiri.—Rom. 1:12.

JIHADHARI DHIDI YA KUNUNG’UNIKA NA KUFICHA DHAMBI

11. Waisraeli katika siku za Musa walisitawisha roho gani, na roho hiyo ilikuwa na matokeo gani kwao?

11 Majuma machache tu baada ya kuwa taifa jipya, Waisraeli walisitawisha roho ya kutoridhika na kunung’unika. Hilo liliwafanya wamwasi Yehova na wawakilishi wake. (Kut. 16:1, 2) Ni idadi ndogo tu ya Waisraeli waliotoka Misri ndio walioiona Nchi ya Ahadi. Hata Musa hakuruhusiwa kuingia katika nchi hiyo kwa sababu ya jinsi alivyotenda Waisraeli walipoonyesha roho isiyofaa! (Kum. 32:48-52) Tunaweza kufanya nini leo ili tusiwe na roho hiyo isiyofaa?

12. Ni nini kinachoweza kutusaidia tusiwe na roho ya kunung’unika?

12 Ni lazima tujihadhari ili tusisitawishe roho ya kunung’unika. Ingawa kusitawisha unyenyekevu na kuheshimu mamlaka kutatusaidia, tunahitaji kuwa waangalifu kuhusu watu tunaoshirikiana nao. Ikiwa tutachagua burudani isiyofaa au kutumia muda mwingi kazini au shuleni kushirikiana na watu ambao hawaheshimu viwango vya uadilifu matokeo yatakuwa mabaya. Ni jambo la hekima kutoshirikiana sana na watu wenye mwelekeo wa kunung’unika au wanaochochea roho ya kujitegemea.—Met. 13:20.

13. Uvutano wenye madhara wa kunung’unika unaweza kuongoza kwenye tabia gani nyingine zenye kudhuru kiroho kutanikoni?

13 Uvutano wenye madhara wa kunung’unika unaweza kuongoza kwenye tabia nyingine zenye kudhuru kiroho. Kwa mfano, kunung’unika kunaweza kuvuruga amani na umoja wa kutaniko. Zaidi ya hayo, kulalamika kuhusu waamini wenzetu hakutawaumiza tu waamini wenzetu lakini pia kunaweza kutufanya tutende dhambi ya uchongezi na kuwatukana wengine. (Law. 19:16; 1 Kor. 5:11) Wanung’unikaji fulani katika kutaniko la karne ya kwanza walikuwa ‘wakipuuza mamlaka na kuwatukana watukufu.’ (Yuda 8, 16) Bila shaka, Mungu hakukubali tabia hiyo ya kunung’unika juu ya wanaume wenye mamlaka katika kutaniko.

14, 15. (a) Matokeo yatakuwa nini kwa kutaniko zima ikiwa dhambi nzito haishughulikiwi? (b) Tunapaswa kufanya nini ikiwa tunajua kwamba mtu fulani ametenda dhambi kisiri?

14 Namna gani ikiwa tutajua kwamba mtu fulani ametenda dhambi kisiri, labda amekunywa pombe kupita kiasi, ametazama ponografia, au anaishi maisha mapotovu kiadili? (Efe. 5:11, 12) Ikiwa hatutafunua dhambi nzito, tunaweza kuizuia roho takatifu ya Yehova isitende kazi kwa uhuru na hivyo kuhatarisha amani ya kutaniko zima. (Gal. 5:19-23) Kama ilivyokuwa kwa Wakristo wa karne ya kwanza huko Korintho ambao walipaswa kuondoa uovu, ndivyo ilivyo leo pia, uvutano wowote wenye kudhuru unapaswa kuondolewa katika kutaniko ili kulinda roho nzuri ya kutaniko. Unaweza kufanya nini ili kuchangia amani ya kutaniko?

15 Kama ilivyoelezwa mwanzoni, ni muhimu kutunza siri katika mambo fulani, hasa wengine wanapotuambia hisia na siri zao. Ni vibaya na inaumiza kama nini kueneza habari za siri kumhusu mtu mwingine! Hata hivyo, ikiwa dhambi nzito imefanywa, wale walio na jukumu la Kimaandiko la kushughulikia jambo hilo, yaani, wazee wa kutaniko, wanapaswa kujulishwa. (Soma Mambo ya Walawi 5:1.) Hivyo, ikiwa tunajua kwamba ndugu au dada fulani ameanguka katika dhambi ya aina hiyo, tunapaswa kumtia moyo awafikie wazee na kuomba msaada wao. (Yak. 5:13-15) Hata hivyo, ikiwa ndugu au dada huyo hafanyi hivyo katika kipindi fulani cha wakati, tunapaswa kuripoti dhambi hiyo.

16. Tunaporipoti dhambi nzito tunasaidiaje kulinda roho ya kutaniko?

16 Kutaniko la Kikristo ni mahali salama pa kiroho, na tunapaswa kulilinda kwa kuripoti dhambi nzito. Ikiwa wazee wanamsaidia mkosaji aelewe uzito wa dhambi yake, atubu, na kukubali kurekebishwa, hawezi kuhatarisha roho ya kutaniko. Lakini vipi ikiwa mtu aliyezoea kutenda dhambi nzito hatubu na hakubali shauri lenye upendo kutoka kwa wazee? Mtu huyo anapotengwa na ushirika, uvutano wenye madhara ‘unaangamizwa,’ au kuondolewa miongoni mwetu, na roho ya kutaniko inalindwa. (Soma 1 Wakorintho 5:5.) Naam, ili kulinda roho ya kutaniko kila mmoja wetu anahitaji kuchukua hatua zinazofaa, kushirikiana na baraza la wazee, na kulinda hali nzuri ya waamini wenzetu.

CHOCHEA “UMOJA WA ROHO”

17, 18. Ni nini kitakachotusaidia “kuushika umoja wa roho”?

17 Kwa “kujitoa wenyewe kwa fundisho la mitume,” wafuasi wa mapema wa Yesu walisaidia kusitawisha roho ya umoja ndani ya kutaniko. (Mdo. 2:42) Walithamini shauri na mwongozo wa Kimaandiko waliopata kutoka kwa wanaume wazee. Kwa kuwa leo wazee wanashirikiana na jamii ya mtumwa mwaminifu na mwenye busara, wote katika kutaniko wanatiwa moyo na kusaidiwa kubaki wakiwa na umoja. (1 Kor. 1:10) Tunapotii maagizo yanayotegemea Biblia kutoka kwa tengenezo la Yehova na kufuata mwongozo wa wazee, tunathibitisha kwamba ‘tunajitahidi sana kuushika umoja wa roho katika kifungo chenye kuunganisha cha amani.’—Efe. 4:3.

18 Basi, acheni tufanye yote tunayoweza ili kulinda roho nzuri ya kutaniko. Tukifanya hivyo, tunahakikishiwa kwamba ‘fadhili zisizostahiliwa za Bwana Yesu Kristo zitakuwa pamoja na roho tunayoonyesha.’—Flp. 4:23.

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 19]

Je, unachangia roho nzuri kwa kutayarisha maelezo yenye kujenga?

[Picha katika ukurasa wa 20]

Changia roho nzuri kwa kujifunza nyimbo zetu