Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Nathani—Mteteaji Mshikamanifu wa Ibada Safi

Nathani—Mteteaji Mshikamanifu wa Ibada Safi

Nathani​—Mteteaji Mshikamanifu wa Ibada Safi

Si rahisi kumsadikisha mwanamume mwenye mamlaka kwamba yeye ni mpotovu na anahitaji kubadilika. Je, ungeweza kumfikia mtu kama huyo ikiwa ungejua kwamba alikuwa amemuua mtu ili kuepuka aibu?

Mfalme Daudi wa taifa la kale la Israeli alikuwa amefanya uzinzi na Bath-sheba, na Bath-sheba akapata mimba. Ili kuficha dhambi yao, Daudi alifanya mpango ili mume wa Bath-sheba auawe, kisha akamchukua Bath-sheba awe mke wake. Miezi ilipita huku Daudi akiishi maisha ya unafiki, bila shaka aliendelea kutimiza majukumu yake akiwa mfalme. Lakini Yehova hakuacha dhambi za mfalme huyo zibaki bila kujulikana. Alimtuma nabii wake Nathani ili amkabili Daudi.

Huo ulikuwa mgawo mgumu. Jiweke katika hali ya Nathani. Bila shaka, ushikamanifu kwa Yehova na pia kushikamana kwa uthabiti na viwango vya Mungu kulimchochea Nathani amkumbushe Daudi dhambi zake. Nabii huyo angewezaje kufanya hivyo na kumsadikisha Mfalme Daudi kwamba alihitaji kutubu?

MWALIMU MWENYE BUSARA

Kwa nini usitumie dakika chache kusoma 2 Samweli 12:1-25? Wazia kwamba wewe ni Nathani na unamwambia Daudi hadithi hii: “Palikuwa na wanaume wawili waliokuwa katika jiji moja, mmoja alikuwa tajiri na yule mwingine alikuwa maskini. Yule mwanamume tajiri alikuwa na kondoo na ng’ombe wengi sana; lakini yule mwanamume maskini hakuwa na chochote isipokuwa mwana-kondoo jike mmoja, aliye mdogo, ambaye alikuwa amenunua. Naye alikuwa akimhifadhi hai, na huyo kondoo alikuwa akikua pamoja naye na wanawe, wote pamoja. Kondoo huyo alikuwa akila tonge lake, na kunywa kutoka katika kikombe chake, naye alikuwa akilala kifuani pake, na kondoo huyo akawa kama binti kwake. Baada ya muda, mgeni akaja kwa yule mwanamume tajiri, lakini hakuchukua kutoka kati ya kondoo zake na ng’ombe zake ili kumwandalia yule msafiri aliyekuja kwake. Kwa hiyo akachukua yule mwana-kondoo jike wa yule mwanamume maskini, akamwandalia yule mtu aliyekuja kwake.”—2 Sam. 12:1-4.

Inaonekana kwamba Daudi ambaye pia aliwahi kuwa mchungaji aliamini kwamba jambo hilo lilitukia kihalisi. Msomi mmoja anafikiria hivi: “Labda, Nathani alizoea kumfikia Daudi ili kuwatetea watu walioumizwa ambao hawangeweza kutetewa na yeyote, na Daudi alifikiri Nathani alikuja kumwona kwa sababu hiyo.” Hata kama ndivyo ilivyokuwa, Nathani alihitaji kuonyesha ushikamanifu kwa Mungu na pia ujasiri ili kuzungumza na mfalme kama alivyofanya. Hadithi ya Nathani ilimkasirisha sana Daudi. Akasema hivi kwa hasira: “Kama Yehova anavyoishi, mtu huyo aliyefanya hivyo anastahili kufa!” Kisha Nathani akatoa tangazo hili la kumponda Daudi moyo: “Wewe mwenyewe ndiye yule mwanamume!”—2 Sam. 12:5-7.

Fikiria kwa nini Nathani alishughulikia tatizo hilo kwa njia hiyo. Si rahisi kwa mtu ambaye ana uhusiano wa kihisia na mwingine kufikiri kwa njia inayofaa kuhusu hali hiyo. Sote tuna mwelekeo wa kutoa visingizio ili kujaribu kujitetea wakati tunapotenda kwa njia isiyofaa. Lakini mfano ambao Nathani alitoa ulimchochea Daudi kushutumu matendo yake mwenyewe bila kujua. Mfalme huyo aliona wazi kwamba mwenendo uliofafanuliwa na Nathani ulikuwa wenye kusikitisha. Hata hivyo, baada tu ya Daudi mwenyewe kuushutumu mwenendo huo ndipo Nathani alipofunua kwamba mfano huo ulimhusu mfalme huyo. Sasa Daudi angeweza kuona uzito wa dhambi yake. Hilo lilimfanya awe na mtazamo unaofaa wa akili wa kukubali karipio. Alikiri kwamba kwa kweli ‘alimdharau’ Yehova kupitia mwenendo wake na Bath-sheba, naye Daudi akakubali karipio alilostahili.—2 Sam. 12:9-14; Zab. 51, maelezo ya utangulizi.

Tunaweza kujifunza nini kutokana na kisa hicho? Lengo la mwalimu wa Biblia ni kuwasaidia wasikilizaji wake wafikie uamuzi unaofaa. Nathani alimheshimu Daudi na hivyo akazungumza naye kwa busara. Nathani alijua kwamba Daudi alipenda uadilifu na haki kutoka moyoni. Kupitia mfano huo, nabii huyo aliugusa moyo wa Daudi aliyekuwa na sifa hizo zinazompendeza Mungu. Sisi pia tunaweza kuwasaidia watu wanyoofu kuelewa maoni ya Yehova. Jinsi gani? Kwa kuchochea uwezo wao wa kutambua mambo yanayofaa, bila sisi kujifanya kuwa na maadili bora zaidi au kuwa watu wa kiroho zaidi kuliko wao. Biblia ndio mamlaka tunayotumia kuamua mambo yanayofaa na yasiyofaa bali si maoni yetu wenyewe.

Zaidi ya mambo yote, ushikamanifu kwa Mungu ndio uliomwezesha Nathani kumkaripia mfalme huyo mwenye nguvu. (2 Sam. 12:1) Tukiwa na ushikamanifu kama huo tutakuwa na ujasiri wa kutetea kwa uthabiti kanuni za uadilifu za Yehova.

ALIENDELEZA IBADA SAFI

Inaonekana kwamba Daudi na Nathani walikuwa marafiki wa karibu, kwa kuwa Daudi alimpa mmoja wa wanawe jina Nathani. (1 Nya. 3:1, 5) Nathani anatajwa mara ya kwanza katika Biblia akiwa pamoja na Daudi. Wote wawili walimpenda Yehova. Inaonekana kwamba Mfalme Daudi aliamini uwezo wa Nathani wa kufanya maamuzi kwa sababu alimfunulia nabii huyo kwamba alitamani kumjengea Yehova hekalu. Daudi alisema hivi: “‘Tazama, mimi ninakaa katika nyumba ya mierezi, lakini sanduku la Mungu wa kweli linakaa katikati ya vitambaa vya mahema.’ Basi Nathani akamwambia mfalme: ‘Kila jambo lililo moyoni mwako—nenda, lifanye, kwa sababu Yehova yupo pamoja nawe.’”—2 Sam. 7:2, 3.

Akiwa mwabudu mwaminifu wa Yehova, Nathani aliunga mkono kwa msisimko mpango wa Daudi wa kujenga kituo cha kwanza cha kudumu cha ibada safi duniani. Hata hivyo, inaonekana kwamba pindi hiyo Nathani alieleza hisia zake mwenyewe badala ya kuzungumza katika jina la Yehova. Usiku huo, Mungu alimwagiza nabii wake ampelekee Mfalme Daudi ujumbe tofauti: Daudi hangejenga hekalu la Yehova. Yule ambaye angejenga hekalu hilo ni mmoja wa wana wa Daudi. Lakini Nathani akatangaza kwamba Mungu alikuwa akifanya agano na Daudi ili kiti chake cha ufalme ‘kifanywe imara mpaka wakati usio na kipimo.’—2 Sam. 7:4-16.

Mapenzi ya Mungu hayakupatana na uamuzi wa Nathani kuhusu ujenzi wa hekalu. Hata hivyo, bila kulalamika, nabii huyo mnyenyekevu alijitiisha chini ya kusudi la Yehova na kuliunga mkono. Alituwekea mfano mzuri kama nini wa kuiga wakati tunaporekebishwa na Mungu kwa njia fulani! Mambo ambayo Nathani alitenda baadaye akiwa nabii yanaonyesha kwamba hakupoteza kibali cha Mungu. Kwa kweli, inaonekana kwamba Yehova alimwongoza Nathani kwa roho takatifu, pamoja na Gadi yule mwonaji, ili wamwelekeze Daudi katika kupanga wanamuziki 4,000 katika utumishi wa hekalu.—1 Nya. 23:1-5; 2 Nya. 29:25.

MTETEAJI WA UFALME

Nathani alijua kwamba Sulemani alipaswa kuwa mfalme baada ya Daudi aliyezeeka. Hivyo, Nathani alitenda kwa haraka Adoniya alipojaribu kunyakua kiti cha ufalme katika miaka ya mwisho ya Daudi. Kwa mara nyingine tena, Nathani alitenda kwa busara na kwa ushikamanifu. Kwanza alimhimiza Bath-sheba amkumbushe Daudi kuhusu ahadi yake ya kumfanya mwana wao Sulemani kuwa mfalme. Kisha Nathani mwenyewe akaenda mbele ya mfalme ili kuuliza ikiwa Daudi alikuwa amemchagua Adoniya kuwa mfalme anayefuata. Akitambua uzito wa hali hiyo, mfalme huyo aliyezeeka alimwagiza Nathani na watumishi wengine washikamanifu wamtie mafuta Sulemani na kumtangaza kuwa mfalme. Mpango wa Adoniya wa kunyakua ufalme ukakomeshwa.—1 Fal. 1:5-53.

MWANAHISTORIA MNYENYEKEVU

Kwa ujumla Nathani na Gadi wanaonwa kuwa waandikaji wa kitabu cha 1 Samweli sura ya 25 hadi sura ya 31 na pia kitabu chote cha 2 Samweli. Kuhusu masimulizi ya kihistoria yaliyoongozwa na roho takatifu yaliyoandikwa katika vitabu hivyo, inasemwa hivi: “Na mambo ya Daudi mfalme, ya kwanza na ya mwisho, yameandikwa katika maneno ya Samweli mwonaji na katika maneno ya nabii Nathani na katika maneno ya Gadi mwonaji.” (1 Nya. 29:29) Nathani pia anatajwa kuwa mwandikaji wa simulizi linalohusu ‘mambo ya Sulemani.’ (2 Nya. 9:29) Hilo linamaanisha kwamba huenda Nathani aliendelea kutumika katika makao ya mfalme baada ya kifo cha Daudi.

Mambo mengi tunayojua kumhusu Nathani huenda yaliandikwa na nabii huyo mwenyewe. Hata hivyo, mambo fulani ambayo hasemi yanatusaidia kujua mengi kumhusu. Inaonekana kwamba Nathani alikuwa mwanahistoria mnyenyekevu. Hakuwa na kimbelembele, akitaka kujijengea jina mashuhuri. Kamusi moja ya Biblia inasema kwamba Biblia “haisemi lolote kumhusu wala kuhusu familia yake.” Hatujui jambo lolote kuhusu maisha ya kibinafsi ya Nathani au mababu zake.

ALICHOCHEWA NA USHIKAMANIFU KWA YEHOVA

Kutokana na mambo machache ambayo tumeelezwa katika Maandiko kumhusu Nathani, ni wazi kwamba alikuwa mteteaji mnyenyekevu lakini mwenye bidii wa mipango ya Mungu. Yehova Mungu alimpa madaraka mazito. Tafakari kuhusu sifa za Nathani, kama vile ushikamanifu kwa Mungu na uthamini wake mkubwa kwa matakwa ya Mungu. Jitahidi kuiga sifa kama hizo.

Inaelekea kwamba hutapewa mgawo wa kuwakaripia wafalme wazinzi au kuwazuia watu kunyakua ufalme. Hata hivyo, kwa msaada wa Mungu unaweza kuwa mshikamanifu kwa Mungu na kutetea viwango vyake vya uadilifu. Unaweza pia kuwa mwalimu jasiri, lakini mwenye busara, wa kweli na mteteaji wa ibada safi.

[Picha katika ukurasa wa 25]

Akiwa mteteaji wa ufalme, Nathani alizungumza kwa busara na Bath-sheba