Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Walitangaza Neno la Mungu kwa Uhodari!

Walitangaza Neno la Mungu kwa Uhodari!

Walitangaza Neno la Mungu kwa Uhodari!

Uhodari—au hata ujasiri—tunapokabili upinzani. Sifa hizo zinaonyeshwa na Wakristo wa kweli, kama inavyoelezwa katika vitabu “Kutoa Ushahidi Kamili” Kuhusu Ufalme wa Mungu na Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu. Kama ilivyokuwa kwa waabudu wenzetu wa karne ya kwanza, sisi husali kwa Yehova ili atupe roho yake na ili atusaidie kusema neno lake kwa ujasiri.—Mdo. 4:23-31.

Kuhusu kazi yetu ya kuhubiri wakati wa vita vya kwanza vya ulimwengu, ndugu mmoja aliandika hivi: “Kwa bidii watumishi wa Mungu walikuwa wakigawanya buku la saba la Studies in the Scriptures, lenye kichwa The Finished Mystery. Buku hilo liligawanywa kwa kiwango kikubwa sana. Trakti Habari za Ufalme Na. 1 ilitolewa mwaka 1918. Muda mfupi baadaye trakti Habari za Ufalme Na. 2 ilitolewa. Trakti hiyo ilieleza kwa nini wenye mamlaka walipiga marufuku kugawanywa kwa kitabu The Finished Mystery. Kisha, trakti Habari za Ufalme Na. 3 ikatolewa. Machapisho hayo yaligawanywa kwa kiwango kikubwa na jamii ya watiwa-mafuta waaminifu. Ilihitaji imani na uhodari ili kugawanya trakti Habari za Ufalme.”

Kwa kawaida leo wahubiri wapya wa Ufalme huzoezwa kushiriki katika huduma, lakini haikuwa hivyo nyakati zote. Akikumbuka jinsi alivyoshiriki kwa mara ya kwanza katika utumishi wa shambani mwaka wa 1922, ndugu mmoja Mpolandi huko Marekani aliandika hivi: “Nikiwa bila ujuzi wa jinsi ya kutoa machapisho na nikizungumza Kiingereza kibovu sana, nilisimama nikiwa peke yangu mlangoni pa daktari mmoja na kubisha mlango. Muuguzi akafungua mlango. Sitasahau kamwe jambo hilo, kwa kuwa nilisisimuka na kuwa na wasiwasi. Nilipokuwa nikifungua mkoba wangu, vitabu vyote vilianguka miguuni pa yule muuguzi. Sikumbuki nilisema nini, lakini nilimwachia kitabu. Kufikia wakati nilipokuwa nikiondoka, nilikuwa nimepata ujasiri na nilihisi kuwa nimebarikiwa na Yehova. Siku hiyo, niliwaachia watu wengi vijitabu katika eneo hilo la biashara.”

Dada mmoja alisema hivi: “Karibu mwaka 1933, ndugu wengi walikuwa wakitumia magari yenye vipaza-sauti kueneza ujumbe wa Ufalme.” Pindi moja, yeye pamoja na wenzi fulani wa ndoa Mashahidi walikuwa wakihubiri katika eneo lenye milima huko California, Marekani. Dada huyo anakumbuka hivi: “Ndugu aliendesha gari lenye vipaza-sauti hadi milimani, na mimi na mke wake tukabaki chini mjini. Alipocheza santuri ya ujumbe uliorekodiwa, ujumbe huo ulisikika kana kwamba unatoka mbinguni. Watu wa mji huo walijaribu tena na tena kumtafuta ndugu huyo lakini hawakumpata. Ujumbe huo uliorekodiwa ulipomalizika, tuliwatembelea watu na kuwahubiria. Nilitumika katika magari mengine mawili yenye vipaza-sauti na ninakuhakikishia kwamba watu wengi hawakupenda kusikiliza ujumbe wetu. Hata hivyo, hawakuwa na la kufanya isipokuwa kusikiliza hotuba hizo kwa kuwa zilisikika nyumbani mwao. Nyakati zote tuliweza kuona kwamba Yehova alielekeza mambo ili njia inayofaa itumike kwa wakati unaofaa. Tulihitaji kujipa ujasiri mkubwa ili kuitumia njia hiyo, lakini mara zote ilitimiza kusudi lake, na jina la Yehova lilitukuzwa.”

Katika miaka ya 1930 na mwanzoni mwa miaka ya 1940, gramafoni na hotuba za Biblia zilizorekodiwa zilitumiwa katika huduma yetu. Mwanamke mmoja Mkristo anakumbuka hivi: “Dada mmoja kijana alikuwa akihubiri nyumba kwa nyumba akitumia gramafoni. Muda mfupi baada ya kuanza kucheza santuri kwenye nyumba moja, mwenye nyumba alikasirika sana hivi kwamba akaipiga teke gramafoni hivi kwamba ikaanguka kutoka kwenye varanda. Hakuna hata santuri moja iliyovunjika. Wanaume watatu waliokuwa wakila chakula chao cha mchana kwenye gari lililokuwa limeegeshwa waliona kilichotokea, wakamwomba dada huyo awachezee santuri hiyo, na wakachukua vitabu. Hilo lilimtuliza sana dada huyo.” Uhodari ulihitajiwa ili kuvumilia majaribu kama hayo.

Dada huyo aliongeza hivi: “Ninakumbuka tulipoanza kazi ya kuwaachia watu magazeti barabarani mwaka wa 1940. Mwanzoni, tulikuwa tukitembea barabarani ili kutangaza habari mbalimbali. Wakiwa wamejipanga mstari mmoja akina ndugu na dada wangetembea mjini kwenye njia za watu wanaotembea kwa miguu wakiwa wamebeba mabango yaliyokuwa na maandishi haya, ‘Dini Ni Mtego na Hila’ na ‘Mtumikie Mungu na Kristo Mfalme.’ Wakati huohuo, watu walipewa trakti bila malipo. Uhodari ulihitajiwa ili kushiriki katika mahubiri ya aina hii, hata hivyo, kazi hiyo ilitimiza kusudi la kutangaza jina la Yehova na watu wake mbele za watu.”

Dada mwingine alisema hivi: “Kuwaachia watu magazeti katika miji midogo ilikuwa kazi ngumu sana. Hali ilikuwa hivyo upinzani dhidi ya Mashahidi ulipokuwa mkali. . . . Ilihitaji uhodari kwelikweli kusimama mahali fulani barabarani ukiwa umeshika magazeti na kusema kwa sauti kubwa mapendekezo uliyopewa. Hata hivyo, ni Jumamosi chache sana ambazo hatukushiriki. Nyakati fulani watu wangekuwa wenye urafiki. Na nyakati nyingine vikundi vya watu wenye hasira vingetuzingira, na mara kwa mara tulihitaji kukimbia ili tusipigwe na umati.”

Licha ya mateso waliyopitia wakati wa Vita vya Pili vya Ulimwengu, Mashahidi wa Yehova waliendelea na huduma yao kwa uhodari. Katika kampeni ya siku 43 iliyofanywa kuanzia Desemba 1, 1940 hadi Januari 12, 1941, karibu wahubiri 50,000 nchini Marekani waligawanya vijitabu milioni nane hivi katika kipindi ambacho kiliitwa, Wakati wa Kutoa Ushahidi kwa “Uhodari.”

Wengi wenye umri mkubwa katika tengenezo la Mungu wanakumbuka vizuri jinsi walivyokabiliana na majaribu ambayo yaliwalazimu wajipe uhodari nyakati zilizopita. Wengine wanakumbuka kwamba kwa miaka mingi, roho yao ya uhodari ilionyeshwa katika msemo uliorudiwa mara nyingi, Endelea na pigano hadi mwisho! Hatujui tutatumia njia gani nyingine ya kuhubiri ujumbe tuliopewa na Mungu kabla ya mwisho wa mfumo huu mwovu. Hata hivyo, kwa msaada wa Mungu, tutaendelea kutangaza neno la Yehova kwa imani na uhodari.

[Blabu katika ukurasa wa 9]

Sikuzote uhodari umehitajika ili kushiriki katika kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme