Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wivu Sifa Mbaya Inayoweza Kutia Sumu Akili Zetu

Wivu Sifa Mbaya Inayoweza Kutia Sumu Akili Zetu

Wivu Sifa Mbaya Inayoweza Kutia Sumu Akili Zetu

Napoleon Bonaparte alikuwa nayo. Yulio Kaisari alikuwa nayo. Aleksanda Mkuu alikuwa nayo. Licha ya mamlaka na utukufu wao, mioyo ya wanaume hao ilikuwa na sifa mbaya ambayo inaweza kutia sumu akili ya mtu. Kila mmoja wa wanaume hao watatu alimwonea mtu fulani wivu.

Mwanafalsafa Mwingereza Bertrand Russell aliandika hivi: “Napoleon alimwonea wivu Kaisari, Kaisari alimwonea wivu Aleksanda [Mkuu], naye Aleksanda, ninathubutu kusema, alimwonea wivu Hercules, ambaye hata hakuwahi kuwapo.” Mtu yeyote hata awe tajiri kadiri gani, awe na kipaji, au hata awe amefanikiwa kadiri gani maishani, anaweza kuwa na wivu.

Wivu ni hisia ya kinyongo kuwaelekea wengine kwa sababu ya mali zao, ufanisi, faida, na vitu vingine walivyo navyo. Kitabu kimoja kinachozungumzia Biblia kinasema hivi: “Neno ‘wivu’ katika Biblia halimaanishi tu tamaa ya kufanikiwa kama mtu mwingine bali tamaa ya kumnyang’anya mtu mwingine kitu alicho nacho.” Mtu mwenye wivu hatamani tu vitu ambavyo wengine wanavyo bali pia anataka kuwanyang’anya vitu hivyo.

Ni jambo la hekima kwetu kuchunguza jinsi wivu unavyoweza kusitawi ndani yetu na matokeo yake. Tunahitaji hasa kujua hatua tunazoweza kuchukua ili kuzuia wivu usiongoze maisha yetu.

ROHO INAYOWEZA KUCHOCHEA MOTO WA WIVU

Ingawa wanadamu wasio wakamilifu wana “mwelekeo wa kuona wivu,” mambo mbalimbali yanaweza kuchochea na kuimarisha mwelekeo huo. (Yak. 4:5) Akifunua moja ya mambo hayo, mtume Paulo aliandika hivi: “Na tusiwe wenye kujisifu, wenye kuchochea mashindano juu ya mtu na mwenzake, tukioneana wivu.” (Gal. 5:26) Roho ya mashindano inaweza kufanya mwelekeo wetu usio mkamilifu wa kuwa na wivu uwe mbaya hata zaidi. Wakristo wawili wanaoitwa Cristina na José * waligundua kwamba jambo hilo ni la kweli.

Cristina, ambaye ni painia wa kawaida, anasema hivi: “Mara nyingi ninajikuta nikiwatazama wengine kwa wivu. Ninalinganisha vitu walivyo navyo na vitu ambavyo sina.” Pindi moja, Cristina alikuwa akila chakula pamoja na wenzi wa ndoa ambao walikuwa na pendeleo la kutumikia katika kazi ya kusafiri. Cristina alipotambua kwamba umri wake na wa mume wake, Eric, ulikaribiana na umri wa huyo mwangalizi anayesafiri pamoja na wa mke wake na pia wote walikuwa na migawo ileile zamani, Cristina alisema hivi: “Mume wangu pia ni mzee wa kutaniko! Inakuwaje kwamba ninyi mko katika kazi ya kusafiri na sisi ni bure tu?” Moto wa wivu, ukichochewa na roho ya mashindano, ulimpofusha dada huyo asione kazi nzuri ambayo yeye na mume wake walikuwa wakifanya na hilo lilimfanya akose kutosheka na maisha yao.

José alitamani kutumikia akiwa mtumishi wa huduma kutanikoni. Alipokosa kuwekwa rasmi huku wengine wakiwekwa rasmi, aliwaonea wivu na kumkasirikia mratibu wa baraza la wazee. José anakiri hivi: “Wivu ulinifanya nisitawishe chuki kuelekea ndugu huyo na kuwa na maoni yasiyofaa kuhusu nia yake. Wivu unapoongoza maisha yako, unaanza kujifikiria sana na huwezi kufikiri vizuri.”

TUNAYOJIFUNZA KUTOKANA NA MIFANO YA KIMAANDIKO

Biblia ina mifano mingi yenye kuonya. (1 Kor. 10:11) Baadhi ya mifano hiyo inaonyesha jinsi wivu unavyositawi na vilevile jinsi unavyotia sumu wale ambao wanauruhusu uwatawale.

Kwa mfano, Kaini, mwana wa kwanza wa Adamu na Hawa, alikasirika Yehova alipokubali dhabihu ya Abeli lakini si dhabihu yake. Kaini angeweza kushinda tatizo hilo, lakini alipofushwa sana na wivu hivi kwamba akamuua ndugu yake. (Mwa. 4:4-8) Si ajabu kwamba Biblia inasema Kaini ‘alitokana na yule mwovu,’ Shetani!—1 Yoh. 3:12.

Ndugu kumi wa Yosefu walimwonea wivu kwa sababu ya uhusiano wa pekee ambao Yosefu alikuwa nao pamoja na baba yao. Chuki yao kumwelekea Yosefu iliongezeka alipowaeleza kuhusu ndoto zake za kinabii. Hata walitaka kumuua. Mwishowe, wakamuuza kama mtumwa nao wakamtendea baba yao kwa ukatili kwa kumfanya aamini kwamba Yosefu alikuwa amekufa. (Mwa. 37:4-11, 23-28, 31-33) Miaka mingi baadaye, walikiri dhambi yao, wakisemezana hivi: “Bila shaka tuna hatia kuhusiana na ndugu yetu, kwa sababu tuliona nafsi yake ikitaabika alipotuomba kwa bidii tumwonee huruma, lakini sisi hatukusikiliza.”—Mwa. 42:21; 50:15-19.

Kora, Dathani, na Abiramu, walisitawisha wivu walipolinganisha mapendeleo yao na mapendeleo ya Musa na Haruni. Walidai kwamba Musa alikuwa ‘akijifanya mkuu juu yao’ na kwamba alikuwa akijiinua mwenyewe juu ya wengine. (Hes. 16:13) Shtaka hilo lilikuwa la uwongo. (Hes. 11:14, 15) Yehova mwenyewe alikuwa amemweka rasmi Musa kuwa mkuu. Lakini waasi hao walimwonea wivu Musa kwa sababu ya cheo chake. Hatimaye, Yehova aliwaangamiza kwa sababu ya wivu wao.—Zab. 106:16, 17.

Mfalme Sulemani alishuhudia matokeo mabaya yanayoweza kusababishwa na wivu. Mwanamke fulani ambaye mtoto wake mchanga alikuwa amekufa alijaribu kumdanganya mwanamke mwenzake kwa kumfanya afikiri kwamba mtoto wake ndiye aliyekufa. Kesi ilipofanywa, yule mwanamke mwongo hata alikubali wazo la kumuua mtoto aliyekuwa hai. Hata hivyo, Sulemani alihakikisha kwamba yule mtoto amekabidhiwa kwa mama yake halisi.—1 Fal. 3:16-27.

Wivu unaweza kusababisha madhara makubwa sana. Mifano ya Kimaandiko iliyotajwa inaonyesha kwamba wivu unaweza kuongoza kwenye chuki, ukosefu wa haki, na uuaji. Zaidi ya hayo, katika kila kisa, yule aliyetendewa vibaya hakuwa amefanya lolote ili astahili kuteswa hivyo. Je, kuna jambo lolote tunaloweza kufanya ili kuhakikisha kwamba wivu hauongozi maisha yetu? Ni hatua gani tunazoweza kuchukua ili kukabiliana na wivu?

NJIA BORA ZA KUKABILIANA NA WIVU!

Sitawisha upendo wa kindugu. Mtume Petro aliwahimiza Wakristo hivi: “Sasa kwa kuwa mmezitakasa nafsi zenu kwa kuwa watiifu kwa ile kweli tokeo likiwa ni upendo wa kindugu usio na unafiki, pendaneni sana kutoka moyoni.” (1 Pet. 1:22) Na upendo ni nini? Mtume Paulo aliandika hivi: “Upendo ni wenye ustahimilivu na wenye fadhili. Upendo hauna wivu, haujigambi, haujivuni, haujiendeshi bila adabu, hautafuti faida zake wenyewe.” (1 Kor. 13:4, 5) Je, kusitawisha upendo kama huo katika moyo wetu kuwaelekea wengine hakutaondoa mwelekeo usiofaa wa kuwaonea wivu? (1 Pet. 2:1) Badala ya kumwonea wivu Daudi, Yonathani ‘alimpenda kama nafsi yake mwenyewe.’—1 Sam. 18:1.

Shirikiana na watu wanaomwogopa Mungu. Mtungaji wa Zaburi ya 73 aliwaonea wivu watu waovu ambao walifurahia maisha ya anasa yasiyo na matatizo yoyote. Hata hivyo, alishinda hisia zake za wivu kwa ‘kuingia katika patakatifu pakuu pa Mungu.’ (Zab. 73:3-5, 17) Kushirikiana na waabudu wenzake kulimsaidia mtunga-zaburi huyo kutambua baraka ambazo alipata kwa “kumkaribia Mungu.” (Zab. 73:28) Kushirikiana kwa ukawaida na waamini wenzetu katika mikutano ya Kikristo kunaweza kutusaidia vivyo hivyo.

Jitahidi kutenda mema. Baada ya kuona kwamba wivu na chuki ilikuwa imesitawi ndani ya moyo wa Kaini, Mungu alimwambia hivi: ‘Geuka utende mema.’ (Mwa. 4:7) ‘Kutenda mema’ kunahusisha nini kwa Wakristo? Yesu alisema kwamba ‘lazima tumpende Yehova Mungu wetu kwa moyo wetu wote na kwa nafsi yetu yote na kwa akili yetu yote na lazima tumpende jirani yetu kama sisi mwenyewe.’ (Mt. 22:37-39) Tunapotanguliza utumishi wa Yehova katika maisha yetu na kuwasaidia wengine tunapata uradhi. Uradhi huo unatusaidia sana kushinda hisia za wivu. Kushiriki kwa bidii katika kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme na kazi ya kufanya wanafunzi ni njia bora ya kumtumikia Mungu na jirani yetu na inatuletea “baraka ya Yehova.”— Met. 10:22.

‘Shangilia na watu wanaoshangilia.’ (Rom. 12:15) Yesu alishangilia aliposikia kuhusu mafanikio ya wanafunzi wake, naye akasema kwamba wangetimiza mengi zaidi katika kazi ya kuhubiri hata kuliko yale aliyotimiza. (Luka 10:17, 21; Yoh. 14:12) Tumeungana tukiwa watumishi wa Yehova; hivyo, mafanikio ambayo yeyote kati yetu anapata ni baraka kwa wote. (1 Kor. 12:25, 26) Basi, je, hatupaswi kushangilia badala kuona wivu wengine wanapopokea mapendeleo makubwa zaidi?

SI PAMBANO RAHISI!

Pambano la kushinda wivu linaweza kuwa la muda mrefu. Cristina anakiri hivi: “Bado nina mwelekeo wenye nguvu wa kuona wivu. Hata ingawa ninachukia kuhisi hivyo, bado nina hisia hiyo, na ni lazima nipambane daima na hisia hiyo.” José amekuwa na pambano kama hilo. Anasema hivi: “Yehova amenisaidia kuthamini sifa nzuri za mratibu wa baraza la wazee. Kuwa na uhusiano mzuri pamoja na Mungu kumenisaidia sana.”

Wivu ni kati ya “matendo ya mwili,” ambayo kila Mkristo anapaswa kupambana nayo. (Gal. 5:19-21) Kwa kutoruhusu wivu utuongoze, tunafanya maisha yetu yawe yenye furaha zaidi na tunaweza kumpendeza Baba yetu wa mbinguni, Yehova.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 7 Majina yamebadilishwa.

[Blabu katika ukurasa wa 17]

‘Shangilia na watu wanaoshangilia’