Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Je, Unaweza Tafadhali Kutupiga Picha?”

“Je, Unaweza Tafadhali Kutupiga Picha?”

“Je, Unaweza Tafadhali Kutupiga Picha?”

Baada ya siku ya pili ya kusanyiko la wilaya, Josué, Mwanabetheli huko Mexico, alikuwa akitembelea jiji la Querétaro. Wenzi wa ndoa, Javier na Maru, watalii kutoka nchini Kolombia, walimwomba Josué awapige picha. Kwa kuwa Josué na rafiki zake ambao ni Mashahidi walikuwa nadhifu huku wakiwa wamevaa beji zao za kusanyiko, wenzi hao wa ndoa wakawauliza ikiwa walikuwa wametoka kuhudhuria sherehe fulani ya kuhitimu au tukio lingine la pekee. Josué aliwaeleza kwamba walikuwa wakihudhuria kusanyiko la Mashahidi wa Yehova na akawakaribisha wenzi hao wahudhurie programu ya siku ya Jumapili.

Wenzi hao walihisi kwamba wangeaibika sana ikiwa wangehudhuria kwa kuwa hawakuwa na mavazi mazuri kwa ajili ya programu kama hiyo. Hata hivyo, Josué akawapa jina lake na namba ya simu ya ofisi ya tawi aliyokuwa akitumikia.

Josué alishangaa miezi minne baadaye, alipopata ujumbe kutoka kwa Javier. Wenzi hao wa ndoa walikuwa wamehudhuria kusanyiko na walitaka Mashahidi wa Yehova wawatembelee huko Mexico City, walikokuwa wakiishi wakati huo. Punde si punde, Javier na Maru wakaanza kujifunza Biblia, na mara moja wakaanza kuhudhuria mikutano. Miezi kumi baadaye, wakawa wahubiri. Ingawa wenzi hao wa ndoa walihamia Toronto, Kanada, waliendelea kufanya maendeleo ya kiroho na wakabatizwa.

Baadaye, Josué alipokea barua kutoka kwa Javier akieleza nini kilichomchochea akubali kweli. “Kabla ya kuhudhuria kusanyiko, mimi na mke wangu tulizungumza kuhusu uhitaji wa kupata mwongozo wa kiroho. Tulipoona jinsi mlivyokuwa nadhifu tulifikiri kwamba ni lazima mlikuwa katika mkutano fulani wa pekee sana. Katika kusanyiko, tulivutiwa na jinsi tulivyosaidiwa kwa upendo kupata mahali pa kukaa, kuonyeshwa maandiko katika Biblia, na mwenendo wa wahudhuriaji. Inaonekana hakuna aliyejali kutuona tukiwa tumevaa kama watalii.”

Jinsi maneno ya Mfalme Sulemani yalivyothibitika kuwa ya kweli kumhusu Josué! Sulemani aliandika hivi: “Asubuhi panda mbegu zako na mpaka jioni usiache mkono wako upumzike; kwa maana hujui ni wapi hii itafanikiwa, hapa au pale, au ikiwa zote mbili zitakuwa njema.” (Mhu. 11:6) Je, unaweza kupanda mbegu kwa kutumia fursa unazopata kuwaambia watu wengine kuhusu hotuba ya watu wote au kusanyiko lijalo? Huenda Yehova akakutumia kuwavuta wale wenye njaa na kiu ya kupata mwongozo wa kiroho, kama Javier na Maru walivyokuwa.—Isa. 55:1.

[Picha katika ukurasa wa 32]

Kushoto kwenda kulia: Alejandro Voeguelin, Maru Pineda, Alejandro Pineda, Javier Pineda, na Josué Ramírez wakiwa katika ofisi ya tawi ya Mexico