Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Simulizi la Maisha

“Kuna Uzuri Upande wa Mkono Wako wa Kuume Milele”

“Kuna Uzuri Upande wa Mkono Wako wa Kuume Milele”

Limesimuliwa na Lois Didur

Ni mara ngapi katika maisha yako umesema, ‘Laiti singefanya uamuzi niliofanya’? Kwa kweli, baada ya kufanya utumishi wa wakati wote kwa miaka 50, sidhani kuna jambo lolote lisilopendeza lenye kudumu ambalo nimekabili kwa sababu ya kuwa upande wa mkono wa kuume wa Yehova. Acheni niwaambie sababu.

NILIZALIWA mwaka wa 1939 na nililelewa mashambani huko Saskatchewan, Kanada, pamoja na dada zangu wanne na ndugu yangu mmoja. Maisha ya mashambani yalifurahisha. Siku moja, Mashahidi wa Yehova walimtembelea baba yangu, na nikawauliza ikiwa Mungu ana jina. Walituonyesha jina Yehova katika Zaburi 83:18. Hilo lilinifanya nitake kujua mengi zaidi kumhusu Mungu na Neno lake.

Katika miaka hiyo, watoto wa mashambani walisomea katika shule za mashambani zilizokuwa na chumba kimoja ambacho kilitumiwa na darasa la kwanza mpaka darasa la nane. Walitumia farasi au walitembea kilomita nyingi ili kufika shuleni. Mahitaji ya mwalimu wa shule yaliandaliwa na familia zilizokuwa katika wilaya. Kwa muda wa mwaka mmoja, ilikuwa zamu ya wazazi wangu kuishi na mwalimu mpya, John Didur.

Sikujua kwamba mwanamume huyo kijana alipendezwa sana pia na Neno la Mungu. Pindi moja nilikuwa nikiusifu ukomunisti na ujamaa, mifumo ya kisiasa ambayo baba yangu alitetea wakati huo. John alijibu hivi kwa sauti ya chini: “Hakuna mtu aliye na haki ya kuwatawala watu wengine. Mungu peke yake ndiye aliye na haki hiyo.” Jibu lake lilifanya tuwe na mazungumzo mengi yenye kupendeza.

Kwa kuwa John alizaliwa mwaka wa 1931, alikuwa amesikia kuhusu matatizo yanayosababishwa na vita. Vita vya Korea vilipoanza kwa ghafula mwaka wa 1950, aliwauliza viongozi mbalimbali wa makanisa kwa nini walishiriki katika vita. Wote walisema kwamba ni jambo linalokubalika kwa Wakristo kushiriki katika vita. Baadaye, aliwauliza Mashahidi wa Yehova swali hilohilo. Walimwonyesha msimamo wa Kimaandiko kuhusu vita ambao Wakristo wa kwanza walichukua. John alibatizwa mwaka wa 1955. Mwaka uliofuata, mimi pia nikabatizwa. Sote wawili tulijua kwamba tulitaka kutumia maisha na nguvu zetu kumtumikia Yehova. (Zab. 37:3, 4) Mnamo Julai 1957, mimi na John tulifunga ndoa.

Kwa miaka mingi tarehe ya kukumbuka arusi yetu iliangukia siku ya kusanyiko letu la wilaya. Tulifurahia kuwa pamoja na maelfu ya watu wengine walioheshimu ndoa. Tulihudhuria kusanyiko letu la kwanza la kimataifa mwaka wa 1958. Tulisafiri watu watano kwa gari kutoka Saskatchewan hadi jiji la New York City. Kwa muda wa juma moja, tulisafiri wakati wa mchana, na kila usiku tulilala katika hema. Wazia jinsi tulivyoshangaa wakati ndugu tuliyekutana naye huko Bethlehem, Pennsylvania, alipotualika tukae na familia yake usiku huo! Kwa sababu ya fadhili zake ambazo hatukutarajia tuliweza kufika katika jiji la New York City tukiwa safi na nadhifu. Kusanyiko hilo kubwa lilitufanya tuthamini furaha kubwa tuliyo nayo ya kumtumikia Yehova! Kama mtunga-zaburi alivyoandika, ‘kuna uzuri upande wa mkono wa Yehova wa kuume milele.’—Zab. 16:11.

TWAFANYA UPAINIA

Mwaka mmoja baadaye, mnamo 1959, tulikuwa tukifanya upainia na kuishi kwenye mlima fulani huko Saskatchewan katika nyumba ndogo inayokokotwa na gari. Ungeweza kuona mbali sana, na baadhi ya sehemu hizo zilikuwa eneo letu.

Siku moja, tulipata barua yenye kufurahisha kutoka ofisi ya tawi. Nilienda haraka mahali ambapo John alikuwa akirekebisha trekta. Ilikuwa barua ya kutualika kuwa mapainia wa pekee huko Red Lake, Ontario. Kwa kuwa hatukujua eneo hilo, basi tulichukua haraka ramani na kutafuta eneo hilo.

Eneo hilo lilikuwa tofauti kama nini na nyanda pana zenye majani! Sasa tuliishi katika eneo lenye misitu mikubwa na miji midogo iliyojengwa karibu na machimbo ya dhahabu. Siku ya kwanza tulipokuwa tukitafuta mahali pa kulala, msichana mdogo alisikia tulipokuwa tukizungumza na jirani yao. Msichana huyo alikimbia nyumbani kumwambia mama yake tulikuwa tukitafuta mahali pa kulala. Mama huyo alitukaribisha kwa fadhili tulale kwao usiku huo. Kitanda tulicholalia kilikuwa katika nyumba ndogo ya udongo. Siku iliyofuata, tulipata mahali pa kuishi, nyumba yenye vyumba viwili iliyojengwa kwa magogo ambayo haikuwa na mabomba ya maji wala fanicha, ilikuwa tu na jiko la mabati lililotumia kuni. Tulipata vitu vingine vichache katika duka linalouza vitu vilivyotumiwa na punde si punde tulikuwa na vitu vingi tulivyohitaji.

Hakukuwa na kutaniko umbali wa kilomita 209. Wafanyakazi wengi katika machimbo ya dhahabu walitoka Ulaya, na walituuliza ikiwa tungeweza kuwapelekea Biblia katika lugha yao. Baada ya muda mfupi, tulikuwa na mafunzo 30 mazuri sana ya Biblia. Katika muda wa miezi sita, kutaniko dogo lilianzishwa.

Mume wa mwanamke fulani ambaye tulijifunza naye Biblia alimpigia kasisi wao simu na kumwambia aje kumrekebisha mke wake. Wakati wa makabiliano hayo, kasisi huyo alisema kwamba kati ya mambo mengine, tunapaswa kuwafundisha watu kuhusu Utatu. Mwanamke huyo alichukua Biblia yao ya Kikatoliki na kumwomba kasisi huyo athibitishe mambo aliyokuwa akisema. Kasisi huyo aliitupa kwa nguvu Biblia hiyo mezani, akisema kwamba hakuhitaji kuthibitisha jambo lolote. Alipokuwa akiondoka, kasisi huyo alisema katika Kiukrainia kwamba tunapaswa kufukuzwa kutoka katika nyumba hiyo na tusiruhusiwe kamwe kurudi. Hakujua kwamba John alielewa Kiukrainia!

Muda mfupi baadaye, tuliondoka eneo la Red Lake kwa sababu John alipaswa kuzoezwa kuwa mwangalizi wa mzunguko. Hata hivyo, baada ya mwaka mmoja hivi, John alipokuwa akitoa hotuba ya ubatizo katika kusanyiko la wilaya, mume huyo alikuwa kati ya watu ambao walikuwa tayari kubatizwa! Yale makabiliano na kasisi yalimfanya aanze kuichunguza Biblia yeye mwenyewe.

TULIKUWA NA SHUGHULI NYINGI KATIKA KAZI YA KUSAFIRI

Katika kazi ya mzunguko, tulikuwa na pendeleo la pekee la kukaa na familia mbalimbali. Tulikuwa na uhusiano wa karibu sana na wale ambao walitukaribisha ili tukae nao katika nyumba zao. Pindi moja wakati wa baridi kali, tulikaa katika chumba kilicho katika ghorofa ambacho hakikuwa na mfumo wa kupasha joto. Asubuhi na mapema, tulikuwa tukimsikia dada aliyezeeka akiingia kimya-kimya ndani ya chumba chetu ili kuwasha jiko dogo. Muda si muda, alirudi akiwa amebeba beseni na maji ya moto ili tujitayarishe kwa ajili ya shughuli za siku hiyo. Nilijifunza mengi kutokana na upole na wororo wa dada huyo.

Kazi ya kusafiri ilinisaidia kumkaribia zaidi Yehova. Mzunguko fulani huko Alberta ulitia ndani mji wenye machimbo upande wa Mbali wa Kaskazini, ambako dada mmoja aliishi. Tengenezo la Yehova lilimwonaje dada huyo aliyekuwa peke yake? Kila miezi sita, tulienda huko kwa ndege na kushiriki naye katika utumishi na kufanya mikutano pamoja naye, kama tu tulivyofanya katika kutaniko kubwa la mjini. Jambo hilo lenye kutia moyo lilitukumbusha jinsi Yehova anavyomtunza kwa upendo kila mtumishi wake ambaye ni kama kondoo mdogo.

Tuliendelea kuwasiliana na wengi ambao walitupatia mahali pa kulala. Hilo linanikumbusha moja kati ya zawadi za kwanza ambazo John alinipa, sanduku maridadi lililojaa karatasi za kuandikia. Tulifurahia sana kuwasiliana na marafiki kupitia barua, ambazo tuliandika kwa kutumia karatasi hizo. Bado ninathamini sana sanduku hilo la barua.

Tulipokuwa katika mzunguko fulani huko Toronto, ndugu mmoja kutoka Betheli ya Kanada alitupigia simu na kutuuliza ikiwa tungeweza kwenda Betheli. Alitaka tumpe jibu lini? “Kesho ikiwezekana!” Tulikubali mgawo huo siku iliyofuata.

UTUMISHI WA BETHELI

Kila mgawo mpya tuliopewa ulitusaidia kuona uzuri mbalimbali unaopatikana upande wa mkono wa Yehova. Tuliendelea kuona uzuri huo tulipoingia Betheli mwaka wa 1977. Kushirikiana na baadhi ya watiwa-mafuta kulituwezesha kuona nyutu zao mbalimbali na pia kuona jinsi wanavyothamini sana Neno la Mungu.

Tulifurahia kufuata utaratibu mpya wa maisha ya Betheli. Kwa mfano, sasa tuliweka mavazi yetu katika kabati badala ya sanduku, na tulishirikiana na kutaniko moja. Zaidi ya mgawo wangu, sikuzote nilifurahia sana kutembeza vikundi vya wageni Betheli. Nilikuwa nikiwaeleza wageni kuhusu kazi inayofanywa Betheli, nilisikia maelezo yao, na kujibu maswali yao.

Miaka ilipita haraka, na katika mwaka wa 1997, John alialikwa kuhudhuria Shule ya Washiriki wa Halmashauri ya Tawi huko Patterson, New York. Baada ya hapo, tuliulizwa ikiwa tungeweza kuhamia Ukrainia. Tulitiwa moyo tufikirie kwa uangalifu na kusali kuhusu jambo hilo. Kufikia jioni hiyo, tulijua kwamba jibu letu lilikuwa ndiyo.

BADILIKO LINGINE LA KWENDA UKRAINIA

Tulikuwa tumehudhuria kusanyiko kubwa la kimataifa huko St. Petersburg, Urusi, mwaka wa 1992, na kisha kusanyiko lililokuwa huko Kiev, Ukrainia, mwaka wa 1993. Makusanyiko hayo yalituchochea kuwapenda ndugu zetu wa Ulaya Mashariki. Makao yetu mapya huko Lviv, Ukrainia, yalikuwa kwenye ghorofa ya pili ya nyumba fulani ya zamani. Madirisha yalielekeana na uwanja wenye bustani ndogo, kulikuwa pia na jogoo mkubwa mwekundu, na vifaranga wa kuku. Tulihisi ni kana kwamba tulikuwa mashambani huko Saskatchewan. Tuliishi katika nyumba hiyo watu 12. Kila siku asubuhi tulivuka jiji ili kufanya kazi Betheli.

Tulihisije kuhusu kuwa Ukrainia? Lilikuwa jambo lenye kunyenyekeza kuwa pamoja na ndugu wengi ambao walikuwa wamepata majaribu, marufuku, na kufungwa gerezani. Hata hivyo, waliendelea kuwa na imani yenye nguvu. Tulipowapongeza walisema hivi: “Tulivumilia kwa sababu tunampenda Yehova.” Hawakuhisi kamwe kwamba waliachwa peke yao. Hata sasa, ukimshukuru mtu anayekutendea kwa fadhili, huenda akajibu hivi: “Mshukuru Yehova,” akionyesha kwamba Yehova ndiye Chanzo cha vitu vyote vyema.

Nchini Ukrainia, wengi wanatembea kwenda mikutanoni, hivyo wana wakati wa kuzungumza na kutiana moyo. Wanatembea kwa muda wa saa moja au zaidi. Kuna makutaniko zaidi ya 50 huko Lviv, na makutaniko 21 kati yake yanatumia jengo kubwa lenye Majumba kadhaa ya Ufalme. Kila Jumapili, inavutia sana kuona ndugu wengi wakimiminika mikutanoni.

Baada ya muda mfupi, tuliwazoea ndugu na dada hao, ambao ni wapole na wako tayari kuwatunza wengine. Ninapokuwa na tatizo la kuelewa lugha, na hata sasa bado nina tatizo hilo, wanakuwa wenye subira sana. Kwa kawaida wanazungumza kwa hisia sana na macho yao yanaonyesha hisia hizo.

Kwa mfano, tuliona kwamba ndugu zetu wanaaminiana kikweli katika kusanyiko la kimataifa la 2003 huko Kiev. Tulikuwa tumefika tu kwenye kituo chenye shughuli nyingi cha magari-moshi ya chini ya ardhi wakati msichana mdogo alipotufikia na kusema hivi kwa sauti ya chini: “Nimepotea. Simwoni nyanya yangu.” Msichana huyo alikuwa ameona beji zetu na alijua kwamba sisi ni Mashahidi. Alikuwa na ujasiri sana na hakulia. Mke wa mwangalizi wa mzunguko ambaye alikuwa pamoja nasi alimchukua kwa fadhili msichana huyo na kumpeleka kwenye Idara ya Vilivyopotea na Kupatikana katika uwanja wa kusanyiko. Punde si punde, msichana huyo aliungana tena na nyanya yake. Niliguswa moyo sana kuona jinsi msichana huyo mdogo alivyotuamini kwa njia ya kustaajabisha, hata katikati ya umati wa maelfu ya watu.

Ndugu kutoka katika nchi nyingi walikuja Ukrainia mnamo Mei 2001 kwa ajili ya kuwekwa wakfu kwa ofisi yetu mpya ya tawi. Baada ya hotuba ya pekee iliyotolewa katika uwanja fulani Jumapili asubuhi, umati mkubwa wa ndugu na dada ulimiminika barabarani ili kutembelea Betheli mpya. Hatuwezi kamwe kusahau jambo hilo! Niliguswa moyo sana kuona ndugu hao, ambao walikuwa kimya na wenye utaratibu sana. Jambo hilo lilinifanya nithamini zaidi uzuri wa kumtumikia Mungu.

BADILIKO KUBWA KABISA

Jambo la kuhuzunisha ni kwamba mwaka wa 2004 John alipatikana kuwa na ugonjwa wa kansa. Tulienda Kanada ili apate matibabu. Matibabu ya kwanza ya kemikali yaliudhoofisha sana mwili wake, na alilazwa katika chumba cha wagonjwa mahututi kwa majuma kadhaa. Jambo zuri ni kwamba alirudiwa na fahamu. Ingawa hangeweza kuongea, macho yake yalionyesha daima kwamba aliwathamini wote waliomtembelea.

Lakini hakuweza kupona, na alikufa mnamo Novemba 27, 2004. Nilihisi kwamba sehemu kubwa sana ya mwili wangu haikuwapo. Mimi na John tulifurahia sana kumtumikia Yehova pamoja. Ningefanya nini? Niliamua kurudi Ukrainia. Nimethamini sana upendo mchangamfu wa familia ya Betheli na wa kutaniko langu nchini Ukrainia.

Hatujawahi kamwe kujuta kwa sababu ya maamuzi tuliyofanya maishani. Tumekuwa na maisha mazuri, na ushirika bora kabisa. Ninajua kwamba bado kuna mengi ya kujifunza kuhusu wema wa Yehova, na ninatumaini kwamba nitaendelea kumtumikia milele kwa sababu kwa kweli nimepata ‘uzuri upande wa mkono wa kuume wa Yehova.’

[Blabu katika ukurasa wa 6]

“Hatujawahi kamwe kujuta kwa sababu ya maamuzi tuliyofanya maishani”

[Picha katika ukurasa wa 3]

Nilipofunga ndoa na John

[Picha katika ukurasa wa 4]

Nilipokuwa painia wa pekee huko Red Lake, Ontario

[Picha katika ukurasa wa 5]

Nikiwa na John huko Ukrainia, mwaka wa 2002