Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Je, tabia ya Mkristo ya kutazama ponografia inaweza kuwa mbaya sana hivi kwamba anaweza kutengwa na ushirika wa kutaniko la Kikristo?

▪ Ndiyo, inawezekana. Hilo linakazia kwa nini ni muhimu kuepuka kabisa aina zote za ponografia, yaani, iwe katika maandishi au picha katika magazeti, sinema, video, na kwenye Intaneti.

Ponografia inapatikana kila mahali duniani. Intaneti inafanya habari za ponografia zipatikane kwa urahisi kuliko wakati mwingine wowote na imeongeza idadi ya watu wanaoathiriwa na zoea hilo baya. Watu fulani, wadogo kwa wakubwa, wamefungua vituo vya ponografia kwenye Intaneti bila kukusudia. Wengine wameingia kwenye vituo hivyo kimakusudi bila kuogopa kwa kuwa wanaweza kusoma au kutazama ponografia kwa siri nyumbani au kazini. Kwa nini Wakristo wanapaswa kuchukua kwa uzito jambo hilo?

Tunapata sababu kuu katika onyo hili ambalo Yesu alitoa: “Kila mtu ambaye anaendelea kumtazama mwanamke na kumtamani tayari amefanya uzinzi pamoja naye moyoni mwake.” (Mt. 5:28) Ni kweli kwamba mahusiano ya kawaida ya kingono kati ya mume na mke ni sawa na ni jambo linalowaletea furaha wenzi wa ndoa. (Met. 5:15-19; 1 Kor. 7:2-5) Lakini ponografia haikazii jambo hilo. Badala yake, inahusisha ngono haramu inayochochea mawazo mapotovu kiadili ambayo Yesu alituonya tujiepushe nayo. Ni wazi kwamba kusoma au kutazama ponografia ni kinyume kabisa na mwongozo huu wa Mungu: “Kwa hiyo, viueni viungo vya mwili wenu vilivyo duniani kwa habari ya uasherati, uchafu, hamu ya ngono, tamaa yenye madhara, na kutamani, ambako ni ibada ya sanamu.”—Kol. 3:5.

Namna gani ikiwa Mkristo alitazama ponografia katika pindi moja au mbili hivi? Kisa chake kinaweza kulinganishwa na hali hatari ambayo mtunga-zaburi Asafu alikabili wakati fulani: “Mimi nami karibu miguu yangu igeuke kando, hatua zangu zilikuwa karibu kuteleza.” Mkristo anawezaje kuwa na dhamiri safi na kuwa na amani pamoja na Mungu ikiwa atatazama picha za ponografia za wanawake walio uchi au watu wanaofanya uasherati? Asafu pia hakuwa na amani: “Nami nikapata mapigo mchana kutwa, na rekebisho langu ni la kila asubuhi.”—Zab. 73:2, 14.

Mkristo ambaye amekuwa na zoea la kutazama ponografia anapaswa kutambua kwamba hilo linaathiri uhusiano wake pamoja na Yehova na kwamba anahitaji msaada wa kiroho. Msaada huo unaweza kupatikana kutanikoni: “Hata mtu akijikwaa katika kosa fulani kabla ya yeye kulijua, ninyi mlio na sifa za kustahili kiroho jaribuni kumrekebisha upya mtu huyo katika roho ya upole, huku kila mmoja wenu akiendelea kujiangalia.” (Gal. 6:1) Mzee mmoja Mkristo au wawili wanaweza kumpa msaada anaohitaji, kutia ndani kumtolea ‘sala za imani ambazo zinaweza kumponya mtu huyo asiyejisikia vizuri, na dhambi yake inaweza kusamehewa.’ (Yak. 5:13-15) Wale ambao wametafuta msaada ili kuondoa doa hilo la ponografia wameona kwamba kumkaribia Mungu kumekuwa jambo jema kwao, kama ilivyokuwa kwa Asafu.—Zab. 73:28.

Hata hivyo, mtume Paulo alisema kwamba baadhi ya watu ambao walitenda dhambi hawakutubu “unajisi wao na uasherati na mwenendo mpotovu.” * (2 Kor. 12:21) Kuhusu neno la Kigiriki linalotafsiriwa hapa kuwa “unajisi,” Profesa Marvin R. Vincent aliandika kwamba neno hilo “linatoa wazo la matendo machafu sana.” Ni jambo linalohuzunisha kwamba baadhi ya ponografia ni mbaya zaidi kuliko picha za watu walio uchi au za mwanamume na mwanamke wanaofanya uasherati. Kuna ponografia chafu sana yenye kuchukiza inayotia ndani ngono kati ya watu wa jinsia moja, ngono za vikundi vya watu, ngono na wanyama, ponografia zinazohusisha watoto, kubakwa na genge la watu, kuwatendea wanawake kikatili, utumwa wa ngono, au kuwatesa watu kwa ukatili kingono. Watu fulani katika siku za Paulo ambao walikuwa “katika giza kiakili” walikuja ‘kuishiwa na ufahamu wote wa maadili na kujitoa wenyewe ili kuwa na mwenendo mpotovu na kufanya ukosefu wa usafi wa kila namna kwa pupa.’Efe. 4:18, 19.

Paulo pia alitaja kuhusu “uchafu” kwenye andiko la Wagalatia 5:19. Msomi fulani Mwingereza alisema hivi: “Neno hilo huenda [likamaanisha] hasa tamaa zote zisizo za asili.” Ni Mkristo yupi anayeweza kupinga kwamba mambo yenye kuchukiza yanayotajwa hapo juu, yaani, ponografia zinazotia ndani mambo mapotovu sana ya kingono ni “tamaa zisizo za asili” na ni chafu sana? Paulo alimalizia hivi kwenye Wagalatia 5:19-21: “Wale walio na mazoea” ya kufanya mambo machafu kama hayo “hawataurithi ufalme wa Mungu.” Kwa hiyo, ikiwa mtu amezoea kutazama ponografia zilizopotoka sana kingono na zenye kuchukiza, labda kwa kipindi kirefu cha wakati, na ikiwa hatubu na kugeuka, hawezi kubaki katika kutaniko la Kikristo. Anapaswa kutengwa na ushirika ili kulinda usafi na hali nzuri ya kiroho ya kutaniko.—1 Kor. 5:5, 11.

Ni vizuri kujua kwamba watu fulani ambao walianguka katika mtego wa kutazama ponografia zenye kuchukiza wamewafikia wazee ili kupata msaada wa kiroho unaohitajika kusudi wafanye mabadiliko makubwa. Yesu aliwasihi watu fulani katika kutaniko la kale la Sardi hivi: “Uyatie nguvu mambo yanayobaki yaliyokuwa tayari kufa, . . . endelea kukazia akilini jinsi ulivyopokea na jinsi ulivyosikia, nawe uendelee kulishika, na utubu. Hakika usipoamka, . . . hutajua hata kidogo saa nitakayokuja juu yako.” (Ufu. 3:2, 3) Inawezekana kutubu na hivyo kunyakuliwa kana kwamba kutoka katika moto.—Yuda 22, 23.

Hata hivyo, inafaa zaidi kila mmoja wetu aazimie kabisa kutokaribia kamwe hali hiyo hatari. Naam, tunapaswa kuazimia kabisa kuepuka aina zote za ponografia!

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 8 Kuhusu tofauti kati ya ‘unajisi na uasherati na mwenendo mpotovu,’ ona gazeti la Mnara wa Mlinzi la Julai 15, 2006, ukurasa wa 29-31.

[Blabu katika ukurasa wa 30]

Mkristo ambaye amekuwa na zoea la kutazama ponografia anapaswa kutambua kwamba hilo linaathiri uhusiano wake pamoja na Yehova na kwamba anahitaji msaada wa kiroho