Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Usitazame “Mambo Yaliyo Nyuma”

Usitazame “Mambo Yaliyo Nyuma”

Usitazame “Mambo Yaliyo Nyuma”

“Hakuna mtu ambaye ameweka mkono wake kwenye jembe la ng’ombe na kutazama mambo yaliyo nyuma anayefaa kwa ajili ya ufalme wa Mungu.”—LUKA 9:62.

UNGEJIBUJE?

Kwa nini tunapaswa ‘kumkumbuka mke wa Loti’?

Ni mambo gani matatu tunayopaswa kuepuka kukazia fikira?

Tutafanya nini ili tuendelee kusonga mbele pamoja na tengenezo la Yehova?

1. Yesu alitoa onyo gani, na ni swali gani linalotokea?

“MKUMBUKENI mke wa Loti.” (Luka 17:32) Onyo hilo ambalo Yesu Kristo alitoa miaka 2,000 hivi iliyopita ni muhimu sana sasa kuliko wakati mwingine wowote. Lakini Yesu alimaanisha nini alipotoa onyo hilo kali? Wayahudi ambao walikuwa wakimsikiliza hawakuhitaji maelezo zaidi kuhusu maneno hayo. Walijua jambo lililompata mke wa Loti. Mke wa Loti alipokuwa akikimbia kutoka Sodoma pamoja na familia yake, alikosa kutii kwa kutazama nyuma na hivyo akageuzwa kuwa nguzo ya chumvi.—Soma Mwanzo 19:17, 26.

2. Kwa nini huenda mke wa Loti alitazama nyuma, na alipoteza nini kwa sababu ya tendo lake la kutotii?

2 Lakini kwa nini mke wa Loti alitazama nyuma? Je, alitamani kuona mambo yaliyokuwa yakitukia? Je, alitazama nyuma kwa sababu alikuwa na shaka au alikosa imani? Au je, alitazama nyuma kwa sababu alitamani vitu vyote ambavyo alikuwa ameacha nyuma huko Sodoma? (Luka 17:31) Hata iwe alitazama nyuma kwa sababu gani, alipoteza uhai wake kwa sababu ya tendo lake la kutotii. Hebu fikiria jambo hili! Alikufa siku ileile pamoja na wakaaji wenye maadili mapotovu wa Sodoma na Gomora. Haishangazi kwamba Yesu alisema hivi: “Mkumbukeni mke wa Loti”!

3. Yesu alikaziaje kwamba hatupaswi kutazama nyuma kwa njia ya mfano?

3 Sisi pia tunaishi wakati ambao ni muhimu kutotazama nyuma kwa njia ya mfano. Yesu alikazia jambo hilo alipomjibu mtu fulani aliyeuliza ikiwa angerudi ili kuiaga familia yake kabla ya kuwa mwanafunzi wake. Yesu alisema hivi: “Hakuna mtu ambaye ameweka mkono wake kwenye jembe la ng’ombe na kutazama mambo yaliyo nyuma anayefaa kwa ajili ya ufalme wa Mungu.” (Luka 9:62) Je, Yesu alimjibu mtu huyo kwa ukali au bila ufikirio? Hapana, kwa sababu alijua kwamba ombi la mtu huyo lilikuwa tu kisingizio cha kuepuka daraka. Yesu alisema kwamba kuahirisha-ahirisha mambo kwa njia hiyo ni kutazama “mambo yaliyo nyuma.” Je, inategemea ikiwa mtu anayelima kwa jembe la ng’ombe anatazama mambo yaliyo nyuma kwa muda mfupi tu au ikiwa anaweka jembe hilo chini na kugeuka nyuma? Katika visa hivyo viwili, anakengeushwa kutokana na jambo analopaswa kufanya, na huenda kazi anayofanya ikaharibika.

4. Ni lazima tuhakikishe macho yetu yanakazia nini?

4 Badala ya kukazia macho mambo yaliyopita, ni lazima tuhakikishe kwamba macho yetu yanakazia mambo ya wakati ujao. Ona jinsi jambo hilo linavyoelezwa waziwazi katika andiko la Methali 4:25: “Macho yako yatazame mbele moja kwa moja, naam, macho yako yenye kung’aa yanapaswa kutazama mbele yako moja kwa moja.”

5. Tuna sababu gani ya kutotazama mambo yaliyo nyuma?

5 Tuna sababu nzuri ya kutotazama mambo yaliyo nyuma. Ni sababu gani hiyo? Hizi ni “siku za mwisho.” (2 Tim. 3:1) Hivi karibuni Mungu hataharibu tu majiji mawili maovu, bali ataharibu mfumo mzima wa mambo ulimwenguni. Ni nini kitakachotusaidia kuepuka hali kama ile iliyompata mke wa Loti? Kwanza, tunahitaji kujua mambo fulani yaliyo nyuma yetu ambayo huenda tukashawishiwa kutazama. (2 Kor. 2:11) Basi acheni tuchunguze mambo hayo na kuona jinsi tunavyoweza kuepuka kuyakazia fikira.

MAONI YA KWAMBA SIKU ZA ZAMANI ZILIKUWA BORA

6. Kwa nini huenda mambo ya zamani tunayokumbuka yasiwe jinsi yalivyokuwa kikweli?

6 Hatari moja kubwa ni kuwa na maoni yaliyopotoka ya kwamba siku za zamani zilikuwa bora. Huenda mambo ya zamani tunayokumbuka yasiwe jinsi yalivyokuwa kikweli. Bila kujua, huenda tukaanza kufikiri kwamba matatizo tuliyokabili zamani hayakuwa mabaya sana na wakati huohuo kutia chumvi kwamba tulikuwa na shangwe nyingi zaidi, na kufanya ionekane kwamba mambo yalikuwa mazuri zaidi kuliko jinsi yalivyokuwa kikweli. Kuwa na maoni hayo yaliyopotoka kuhusu mambo ya zamani kunaweza kutufanya tutamani siku bora za zamani. Lakini Biblia inatuonya hivi: “Usiseme: ‘Kwa nini siku za zamani zilikuwa bora kuliko hizi?’ kwa maana hukuuliza hilo kwa hekima.” (Mhu. 7:10) Kwa nini ni hatari kufikiri kwa njia hiyo?

7-9. (a) Waisraeli walipatwa na nini huko Misri? (b) Waisraeli walikuwa na sababu gani za kushangilia? (c) Waisraeli walianza kunung’unika na kulalamika kuhusu nini?

7 Waisraeli walipatwa na nini katika siku za Musa. Ingawa mwanzoni Waisraeli walionwa kuwa wageni katika nchi ya Misri, baada ya siku za Yosefu, Wamisri ‘waliweka juu ya Waisraeli wakuu wa kazi ya kulazimishwa kusudi wawakandamize katika kazi yao ya kubeba mizigo.’ (Kut. 1:11) Mwishowe watu wa Mungu walikabili hatari ya kuangamizwa kwa sababu Farao alijaribu kupunguza idadi yao. (Kut. 1:15, 16, 22) Basi haishangazi kwamba Yehova alimwambia Musa hivi: “Pasipo shaka nimeyaona mateso ya watu wangu walio Misri, nami nimesikia kilio chao kwa sababu ya wale wanaowalazimisha kufanya kazi; kwa sababu nayajua vizuri maumivu waliyo nayo.”—Kut. 3:7.

8 Je, unaweza kuwazia shangwe ambayo Waisraeli walikuwa nayo walipowekwa huru kutoka katika nchi ambamo walikuwa watumwa? Kwa njia ya kustaajabisha, walikuwa wameona nguvu za Yehova alipoleta Mapigo Kumi juu ya Farao mwenye kiburi na watu wake. (Soma Kutoka 6:1, 6, 7.) Kwa kweli, mwishowe Wamisri hawakuwaachilia huru tu Waisraeli bali pia waliwahimiza waondoke, nao wakawapa dhahabu na fedha nyingi sana hivi kwamba inaweza kusemwa kwamba watu wa Mungu ‘waliwaacha Wamisri bila chochote.’ (Kut. 12:33-36) Waisraeli walishangilia zaidi walipoona Farao na majeshi yake yakiangamizwa katika Bahari Nyekundu. (Kut. 14:30, 31) Imani yetu ingeimarishwa kama nini ikiwa tungeshuhudia matukio hayo yenye kusisimua!

9 Hata hivyo, jambo lisilowazika ni kwamba muda mfupi tu baada ya kukombolewa kimuujiza, watu haohao walianza kunung’unika na kulalamika. Walinung’unika kuhusu nini? Kuhusu chakula! Hawakutosheka na maandalizi ya Yehova na hivyo wakalalamika hivi: “Jinsi tunavyokumbuka samaki tuliokuwa tukila bure huko Misri, matango na matikiti-maji na vitunguu vya majani na vitunguu na vitunguu saumu! Lakini sasa nafsi yetu imekauka. Macho yetu hayaoni chochote isipokuwa mana.” (Hes. 11:5, 6) Naam, maoni yao yalikuwa yamepotoka sana hivi kwamba hata walitaka kurudi katika nchi ambako walikuwa watumwa! (Hes. 14:2-4) Waisraeli walitazama mambo yaliyokuwa nyuma na hivyo wakapoteza kibali cha Yehova.—Hes. 11:10.

10. Mfano wa Waisraeli unatufundisha somo gani?

10 Tunajifunza somo gani leo? Tunapokabili matatizo na hali ngumu, acheni tusikazie fikira mambo ya zamani ambayo huenda yakaonekana yalikuwa mazuri, labda hata kabla ya hatujapata ujuzi wa kweli. Ingawa si vibaya kutafakari kuhusu masomo ambayo tumejifunza kutokana na mambo ya zamani au kukumbuka kwa furaha mambo mazuri ya zamani, tunahitaji kuendelea kuwa na maoni yanayofaa na yenye usawaziko kuhusu mambo hayo. Tusipofanya hivyo, tunaweza kukosa kutosheka na hali zetu za sasa na hivyo kushawishiwa kurudia maisha yetu ya zamani.—Soma 2 Petro 2:20-22.

MAMBO TULIYODHABIHU ZAMANI

11. Watu fulani wana maoni gani kuhusu mambo waliyodhabihu zamani?

11 Inahuzunisha kwamba watu fulani wanafikiria mambo waliyodhabihu zamani na kuhisi kwamba walipoteza nafasi za kufanikiwa kimwili. Labda ulikuwa na nafasi za kupata elimu ya juu, umashuhuri, au nafasi ya kupata pesa nyingi, lakini ukaamua kutofuatilia mambo hayo. Ndugu na dada zetu wengi wameacha nafasi nzuri za kupata ufanisi katika biashara, burudani, au michezo. Sasa wakati umepita, na bado mwisho haujafika. Je, unawazia-wazia jinsi ambavyo mambo yangekuwa ikiwa hungedhabihu mambo hayo?

12. Paulo alihisije kuhusu vitu vyote ambavyo alikuwa ameacha nyuma?

12 Mtume Paulo alidhabihu vitu vingi ili awe mfuasi wa Kristo. (Flp. 3:4-6) Alihisije kuhusu vitu alivyokuwa ameacha nyuma? Anatuambia hivi: “Vitu vilivyokuwa faida kwangu, hivyo nimeviona kuwa hasara kwa sababu ya Kristo.” Kwa nini? Anaendelea kusema hivi: “Kwa kweli naviona vitu vyote kuwa hasara kwa sababu ya thamani bora zaidi ya kumjua Kristo Yesu Bwana wangu. Kwa sababu yake nimekubali hasara ya vitu vyote nami naviona kuwa takataka nyingi, ili niweze kumpata Kristo.” * (Flp. 3:7, 8) Kama vile tu mtu anayetupa takataka, au uchafu, asivyorudi baadaye na kuomboleza kwamba amepata hasara, vivyo hivyo, Paulo hakujuta kwa sababu ya nafasi zozote za kufanikiwa kimwili ambazo alikuwa ameacha nyuma. Hakuhisi tena kwamba vitu hivyo vilikuwa na thamani yoyote.

13, 14. Tunaweza kuigaje mfano wa Paulo?

13 Ni nini kitakachotusaidia tukijikuta tukianza kukisia-kisia kuhusu zile zinazoonwa kuwa nafasi tulizopoteza za kufanikiwa kimwili? Iga mfano wa Paulo. Jinsi gani? Fikiria thamani ya vitu ulivyo navyo sasa. Umepata uhusiano wenye thamani sana pamoja na Yehova na umejijengea jina zuri pamoja naye kwa sababu ya kuwa mwaminifu. (Ebr. 6:10) Ulimwengu unaweza kukupa faida gani za kimwili ambazo zinaweza kulinganishwa hata kidogo na baraka za kiroho ambazo tunafurahia sasa na ambazo tutafurahia wakati ujao?—Soma Marko 10:28-30.

14 Kisha Paulo anataja jambo ambalo litatusaidia kuendelea kuwa waaminifu. Anasema kwamba alikuwa ‘anayasahau mambo ya nyuma na kujinyoosha kwenda mbele kuelekea mambo yaliyo mbele.’ (Flp. 3:13) Ona kwamba Paulo anakazia hatua mbili, na zote mbili ni muhimu. Kwanza, ni lazima tusahau mambo tuliyoacha nyuma, na kuepuka kupoteza nguvu na wakati wenye thamani kuhangaikia mambo hayo kupita kiasi. Pili, kama mkimbiaji anayekaribia kumaliza shindano la mbio, tunahitaji kujinyoosha mbele, tukikazia macho mambo yaliyo mbele.

15. Tunapata faida gani tunapotafakari kuhusu mifano ya watumishi waaminifu wa Mungu?

15 Tunapotafakari kuhusu mifano ya watumishi waaminifu wa Mungu, iwe waliishi zamani au wanaishi sasa, tunaweza kuchochewa zaidi kuendelea kusonga mbele badala ya kutazama mambo yaliyo nyuma. Kwa mfano, ikiwa Abrahamu na Sara wangeendelea kukumbuka Uru, “wangepata nafasi ya kurudi.” (Ebr. 11:13-15) Lakini hawakurudi huko. Mwanzoni Musa aliacha mambo mengi sana nchini Misri kuliko Mwisraeli mwingine yeyote aliyeishi baadaye. Hata hivyo, hatusomi popote kwamba Musa alitamani mambo hayo. Badala yake, simulizi la Biblia linatuambia kwamba “aliona shutuma ya Kristo kuwa ni utajiri mkubwa kuliko hazina za Misri; kwa maana alikaza macho kwenye malipo ya thawabu.”—Ebr. 11:26.

MAMBO YASIYOFAA YA ZAMANI

16. Mambo tuliyokabili zamani yanaweza kutuathirije?

16 Hata hivyo, si mambo yote ya zamani yanayoweza kuonekana kuwa mazuri. Labda tunashuka moyo tunapokumbuka dhambi au makosa tuliyofanya zamani. (Zab. 51:3) Huenda bado tukaumia sana moyoni kwa sababu ya shauri kali tulilopewa. (Ebr. 12:11) Huenda bado tukafikiria sana kuhusu ukosefu wa haki tuliotendewa au tunaohisi kwamba tulitendewa. (Zab. 55:2) Tunaweza kufanya nini ili kuhakikisha kwamba haturuhusu mambo kama hayo yatufanye tukazie fikira mambo yaliyo nyuma? Fikiria mifano hii mitatu.

17. (a) Kwa nini Paulo alisema kwamba yeye ni “mtu mdogo kuliko aliye mdogo zaidi kati ya watakatifu wote”? (b) Ni nini kilichomsaidia Paulo kutolemewa na maoni yasiyofaa?

17 Makosa ya zamani. Mtume Paulo alisema kwamba yeye ni “mtu mdogo kuliko aliye mdogo zaidi kati ya watakatifu wote.” (Efe. 3:8) Kwa nini alihisi hivyo? Anasema hivi: “Kwa sababu nililitesa kutaniko la Mungu.” (1 Kor. 15:9) Je, unaweza kuwazia jinsi Paulo alivyohisi alipokutana na baadhi ya watu ambao aliwatesa zamani? Hata hivyo, badala ya kuruhusu maoni hayo yasiyofaa yamlemee, Paulo alikazia fikira fadhili zisizostahiliwa ambazo alikuwa ameonyeshwa. (1 Tim. 1:12-16) Kuthamini fadhili hizo zisizostahiliwa kulimchochea kuendelea na huduma yake. Mambo ambayo Paulo aliazimia kusahau yalitia ndani mwenendo wake wa zamani wenye dhambi. Sisi pia tukikazia fikira rehema ambayo Yehova ametuonyesha, tutaepuka kudhoofishwa na mahangaiko yasiyo ya lazima kuhusu mambo yaliyotokea zamani ambayo hatuwezi kubadili. Tunaweza kutumia nguvu zetu kufanya kazi tuliyo nayo sasa.

18. (a) Ni nini kinachoweza kutokea ikiwa tutakuwa na maoni mabaya kuhusu shauri tulilopewa wakati uliopita? (b) Tunaweza kutii jinsi gani maneno ya Sulemani kuhusu kukubali shauri?

18 Shauri lenye kuumiza. Namna gani tukishawishiwa kukazia fikira shauri fulani tulilopewa wakati uliopita na kuwa na kinyongo moyoni? Kufanya hivyo hakutatuumiza tu bali pia kutatuvunja moyo na kutufanya ‘tuzimie.’ (Ebr. 12:5) Iwe ‘tunapuuza’ shauri kwa sababu tumekataa shauri hilo au tunalikubali na kisha ‘tunazimia’ baadaye, matokeo ni yaleyale, haturuhusu shauri hilo litunufaishe na kutufanya tuwe bora. Ni vizuri zaidi kutii maneno haya ya Sulemani: “Shika nidhamu; usiiache. Ilinde, kwa maana hiyo ndiyo uzima wako.” (Met. 4:13) Kama dereva anayetii ishara za barabarani, acheni tukubali shauri, tulitumie maishani, na kusonga mbele.—Met. 4:26, 27; soma Waebrania 12:12, 13.

19. Tunaweza kuigaje imani ya Habakuki na ya Yeremia?

19 Tunapotendewa isivyo haki au tunapohisi kwamba tumetendewa isivyo haki. Nyakati nyingine huenda tukahisi kama nabii Habakuki, ambaye alimlilia Yehova ili atekeleze haki, lakini hakuelewa kwa nini Yehova alikuwa ameruhusu mambo fulani yasiyo ya haki yatukie. (Hab. 1:2, 3) Ni muhimu kama nini tuige imani ya nabii huyo, ambaye alisema hivi: “Lakini mimi, nitafurahi katika Yehova mwenyewe; nitakuwa na shangwe katika Mungu wa wokovu wangu.” (Hab. 3:18) Kama Yeremia aliyeishi zamani, tukiendelea kuwa na “mtazamo wa kungojea” na kuwa na imani kamili katika Yehova, ambaye ni Mungu wa haki, tunaweza kuwa na hakika kwamba mambo yote yatarekebishwa kwa wakati unaofaa.—Omb. 3:19-24.

20. Tunaweza kuonyeshaje kwamba ‘tunamkumbuka mke wa Loti’?

20 Tunaishi katika nyakati zenye kusisimua. Matukio mazuri ajabu yanatukia sasa na mengi zaidi yatatukia hivi karibuni. Kila mmoja wetu na aendelee kusonga mbele pamoja na tengenezo la Yehova. Acheni tutii shauri la Kimaandiko kwa kutazama mbele na kuepuka kutazama mambo yaliyo nyuma. Tukifanya hivyo, tutaonyesha kwamba ‘tunamkumbuka mke wa Loti’!

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 12 Neno la lugha ya awali ambalo limetafsiriwa hapa kuwa “takataka” lilimaanisha pia “vitu ambavyo vinatupiwa mbwa,” “mavi ya ng’ombe,” “kinyesi.” Msomi mmoja wa Biblia anasema kwamba Paulo alitumia neno hilo kumaanisha “azimio la kuacha kabisa kitu fulani kisicho na thamani na chenye kuchukiza na ambacho mtu hataki kamwe kukiona tena.”

[Maswali ya Funzo]