Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wasaidie Watu ‘Waamke Kutoka Katika Usingizi’

Wasaidie Watu ‘Waamke Kutoka Katika Usingizi’

Wasaidie Watu ‘Waamke Kutoka Katika Usingizi’

“Mnayajua majira, kwamba tayari ni saa ya ninyi kuamka kutoka katika usingizi.”—ROM. 13:11.

JE, UNAWEZA KUELEZA?

Kwa nini ni muhimu kwa Wakristo kuendelea kukesha kiroho?

Kwa nini tunapaswa kuwa macho na makini na kuwasikiliza watu katika huduma?

Kwa nini sifa ya fadhili na upole ni muhimu katika huduma yetu?

1, 2. Ni katika maana gani watu wengi wanahitaji kuamka?

KILA mwaka, maelfu ya watu wanakufa kwa sababu wanasinzia au hata kulala usingizi wanapoendesha gari. Wengine wanapoteza kazi zao kwa sababu wanachelewa kuamka ili kwenda kazini au kwa sababu wanalala wakiwa kazini. Lakini kusinzia kiroho kunaweza kuwa na matokeo mabaya hata zaidi. Ni katika muktadha huo muhimu kwamba Biblia inasema hivi: “Mwenye furaha ni yule anayekaa macho.”—Ufu. 16:14-16.

2 Wanadamu kwa ujumla wanalala usingizi wa kiroho kadiri siku kuu ya Yehova inavyokaribia. Hata viongozi fulani wa dini zinazodai kuwa za Kikristo wamewaita kondoo wao ‘walalaji wakubwa.’ Usingizi wa kiroho ni nini? Kwa nini ni muhimu Wakristo wa kweli waendelee kukesha? Tunawezaje kuwasaidia wengine waamke kutoka kwenye usingizi huo?

USINGIZI WA KIROHO NI NINI?

3. Unaweza kusema nini kuhusu mtu ambaye amelala kiroho?

3 Kwa kawaida watu wanaolala hawatendi. Kinyume na hilo, wale wanaolala kiroho wanaweza kuwa na shughuli nyingi sana, lakini si za kiroho. Wanaweza kujishughulisha sana na mahangaiko ya kila siku ya maisha au kutafuta raha, umaarufu, au utajiri. Pamoja na utendaji huo wote, hawajali mahitaji yao ya kiroho. Hata hivyo, watu ambao wako macho kiroho, wanatambua kwamba tunaishi “katika siku za mwisho,” hivyo wanakuwa wenye kutenda kadiri iwezekanavyo katika kufanya mapenzi ya Mungu.—2 Pet. 3:3, 4; Luka 21:34-36.

4. Shauri hili: “Na tusiendelee kulala usingizi kama wenginelinamaanisha nini?

4 Soma 1 Wathesalonike 5:4-8. Katika andiko hilo mtume Paulo anawahimiza waamini wenzake ‘wasiendelee kulala usingizi kama wengine.’ Alimaanisha nini? Tunaweza ‘kuendelea kulala’ ikiwa tunapuuza viwango vya maadili vya Yehova. Tunaweza pia, ‘kuendelea kulala usingizi’ ikiwa tunapuuza ukweli wa kwamba wakati wa Yehova wa kuwaharibu watu wasiomwogopa umekaribia. Ni lazima tuhakikishe kwamba watu hao wasiomwogopa Mungu hawatushawishi tuige njia na mitazamo yao.

5. Watu wanaolala kiroho wana mitazamo gani?

5 Watu fulani wanawaza kwamba hakuna Mungu ambaye atawahukumu. (Zab. 53:1) Wengine wanawaza kwamba Mungu hapendezwi na sisi wanadamu, kwa hiyo hatuna sababu ya kupendezwa naye. Na bado kuna wengine ambao wanahisi kwamba kuwa washiriki wa kanisa fulani kutawafanya wawe marafiki wa Mungu. Watu hao wote wanalala kiroho. Wanahitaji kuamka. Tunaweza kuwasaidiaje?

NI LAZIMA SISI WENYEWE TUENDELEE KUKESHA

6. Kwa nini ni lazima Wakristo wajitahidi kuendelea kukesha kiroho?

6 Ili kuweza kuwaamsha wengine, ni lazima sisi wenyewe tuwe macho. Hilo linatia ndani nini? Neno la Mungu linahusianisha usingizi wa mfano na “matendo ya giza,” yaani, karamu za kupindukia, vipindi vya kulewa, ngono isiyo halali, mwenendo mpotovu, mizozo, na wivu. (Soma Waroma 13:11-14.) Inaweza kuwa vigumu kuepuka mwenendo kama huo. Ni muhimu sana tukae macho. Dereva wa gari anayepuuza hatari ya kulala usingizi anapoendesha gari huenda anahatarisha uhai wake. Ni muhimu kama nini kwa Mkristo kutambua kwamba usingizi wa kiroho unaweza kuwa hatari!

7. Kuwa na maoni yasiyofaa kuhusu watu katika eneo letu kunawezaje kutuathiri?

7 Kwa mfano Mkristo anaweza kuwazia kwamba watu wote katika eneo lake wamekataa kabisa habari njema. (Met. 6:10, 11) Huenda akafikiri, ‘Ikiwa hakuna mtu atakayekubali habari njema, kwa nini nijaribu kwa bidii kuwatafuta au kuwasaidia watu?’ Ni kweli kwamba huenda watu wengi sasa wanalala kiroho, lakini hali na mitazamo yao inaweza kubadilika. Wengine wanaamka kiroho na kukubali habari njema. Na tunaweza kuwasaidia ikiwa sisi wenyewe tunaendelea kukesha, kama vile kwa kujaribu kutumia njia mpya zenye kuvutia za kuhubiri ujumbe wa Ufalme. Ili kuendelea kukesha, tunahitaji kujikumbusha kwa nini huduma yetu ni muhimu sana.

NI NINI KINACHOFANYA HUDUMA YETU IWE MUHIMU SANA?

8. Kwa nini huduma yetu ya Kikristo ni muhimu sana?

8 Kumbuka kwamba hata ikiwa watu hawasikilizi, kazi yetu ya kuhubiri inamletea Yehova heshima na anaitumia ili kutimiza kusudi lake. Hivi karibuni, wale wasiotii habari njema watahukumiwa adhabu. Watu watahukumiwa kwa msingi wa jinsi wanavyoitikia kazi yetu ya kuhubiri. (2 The. 1:8, 9) Isitoshe, lingekuwa kosa kwa Mkristo kufikiri kwamba si lazima ahubiri kwa bidii sana kwa sababu “kutakuwa na ufufuo wa waadilifu na wasio waadilifu pia.” (Mdo. 24:15) Tunaelewa kutokana na Neno la Mungu kwamba wale wanaohukumiwa kuwa “mbuzi” “watakatiliwa mbali milele.” Kupitia kazi yetu ya kuhubiri, Mungu anawaonyesha watu rehema kwa kuwa anawapa fursa ya kubadilika na hivyo kupata “uzima wa milele.” (Mt. 25:32, 41, 46; Rom. 10:13-15) Ikiwa hatuhubiri, watu watapataje fursa ya kusikia ujumbe ambao unaweza kuokoa uhai wao?

9. Kuhubiri habari njema kumekufaidi wewe na wengine jinsi gani?

9 Sisi pia tunafaidika kwa kuhubiri habari njema. (Soma 1 Timotheo 4:16.) Je, hujaona kwamba kuzungumza kumhusu Yehova na tumaini la Ufalme kunaimarisha imani yako na upendo wako kumwelekea Mungu? Je, si ni kweli kwamba kumekusaidia kusitawisha sifa za Kikristo? Je, si kweli kwamba unapata furaha zaidi unapojitoa kabisa kwa Mungu kwa kushiriki katika huduma? Wengi ambao wamekuwa na pendeleo la kuwafundisha wengine kweli ya Biblia wamefurahi kuona roho ya Mungu ikiwasaidia watu hao kuboresha njia yao ya maisha.

UWE MAKINI

10, 11. (a) Yesu na Paulo walionyesha jinsi gani kwamba walikuwa macho na makini? (b) Toa mfano unaoonyesha jinsi kuwa macho na makini kunavyoweza kuboresha huduma yetu.

10 Tunaweza kutumia njia mbalimbali ili kuwachochea watu wapendezwe na habari njema. Hivyo, wahudumu Wakristo wanapaswa kuwa macho. Yesu ni kielelezo chetu. Kwa kuwa alikuwa mkamilifu, Yesu aliweza kutambua hasira ya Farisayo mmoja hata bila mtu huyo kusema lolote, aliweza pia kutambua toba ya kweli ya mwanamke mmoja mtenda-dhambi, na pia mtazamo wa kujidhabihu wa mjane mmoja. (Luka 7:37-50; 21:1-4) Yesu angeweza kumtimizia kila mtu mahitaji yake ya kiroho. Hata hivyo, mtumishi wa Mungu hahitaji kuwa mkamilifu ili kutambua mahitaji ya wengine. Mtume Paulo aliweka mfano mzuri katika kufanya hivyo. Alibadili mazungumzo yake ili kuvutia vikundi mbalimbali vya watu na pia watu wenye mitazamo tofauti.—Mdo. 17:22, 23, 34; 1 Kor. 9:19-23.

11 Kwa kujitahidi kuwa macho na makini kama Yesu na Paulo, tunaweza kutambua njia nzuri ya kuchochea upendezi wa watu tunaokutana nao. Kwa mfano, unapowafikia watu, angalia ishara zinazoonyesha utamaduni wao, mapendezi yao, au hali yao ya familia. Labda unaweza kutambua kazi wanayofanya wakati huo na kusema jambo fulani zuri kuhusu kazi hiyo wakati unapoanzisha mazungumzo.

12. Tunaposhiriki katika huduma, kwa nini tunapaswa kuwa waangalifu kuhusu mazungumzo yetu?

12 Mhubiri aliye macho na makini anajitahidi kuepuka mambo yanayokengeusha fikira. Tunapokuwa katika huduma, mazungumzo yetu pamoja na mhubiri mwenzetu yanaweza kuwa yenye kujenga. Hata hivyo, tunapaswa kukumbuka kwamba kusudi letu la kushiriki katika huduma ya shambani ni kuwahubiria wengine. (Mhu. 3:1, 7) Hivyo, tunapaswa kuwa waangalifu ili mazungumzo yetu tunapoenda nyumba kwa nyumba yasivuruge huduma yetu. Kujadiliana kuhusu mawazo ambayo tungependa kuzungumza na watu wanaopendezwa ni njia nzuri ya kukazia akili kusudi letu. Pia, ingawa simu ya mkononi inaweza nyakati fulani kutusaidia kuwa wenye matokeo katika huduma yetu, tunapaswa kuhakikisha kwamba simu yetu haivurugi mazungumzo yetu pamoja na mwenye nyumba.

ONYESHA KWAMBA UNAPENDEZWA KIBINAFSI NA WATU

13, 14. (a) Tunawezaje kutambua mambo yanayompendeza mtu? (b) Ni nini kinachoweza kuwachochea watu wapendezwe na mambo ya kiroho?

13 Wahudumu walio macho na makini wanawasikiliza kwa uangalifu watu ambao wanakutana nao. Ni maswali gani unayoweza kuuliza ili mtu fulani katika eneo lenu aeleze hisia zake? Je, ana wasiwasi kuhusu idadi inayoongezeka ya dini, jeuri katika eneo, au kushindwa kwa serikali? Je, unaweza kuwachochea watu wapendezwe na mambo ya kiroho kwa kuzungumzia jinsi ambavyo vitu vilivyo hai vimeumbwa kwa njia ya ajabu au jinsi mashauri ya Biblia yalivyo yenye faida? Watu wa tamaduni karibu zote, hata watu fulani wanaoamini kwamba hakuna Mungu, wanapendezwa na sala. Wengi wanajiuliza ikiwa kuna yeyote anayesikia sala. Huenda wengine wakapendezwa na maswali kama haya: Je, Mungu anasikiliza sala zote? Ikiwa sivyo, tunapaswa kufanya nini ili Mungu atusikilize?

14 Inaelekea kwamba tunaweza kujifunza mengi kuhusu ustadi wa kuanzisha mazungumzo kwa kuchunguza kwa makini jinsi wahubiri wenye uzoefu wanavyofanya. Ona jinsi wanavyoepuka kumfanya mtu afikiri kwamba anahojiwa au mambo yake ya kibinafsi yanaingiliwa. Sauti na nyuso zao zinaonyeshaje kwamba wanajitahidi kuelewa maoni ya mwenye nyumba?—Met. 15:13.

UWE MWENYE FADHILI NA USTADI

15. Kwa nini tunapaswa kuwa wenye fadhili tunapokuwa katika kazi yetu ya kuhubiri?

15 Je, unafurahi mtu fulani anapokuamsha kutoka kwenye usingizi mzito? Watu wengi hawafurahi wanapoamshwa kwa ghafula. Wengi hufurahi wanapoamshwa taratibu. Hilo ni kweli pia kuhusu jitihada za kuwaamsha watu kiroho. Kwa mfano, utafanya nini ikiwa mtu atatenda au kufoka kwa hasira unapomtembelea, kwa kawaida ni jambo gani zuri la kufanya? Uwe mwenye fadhili, na uonyeshe kwamba unaheshimu hisia zake, mshukuru kwa unyoofu wake, kisha uondoke kwa utulivu. (Met. 15:1; 17:14; 2 Tim. 2:24) Huenda fadhili zako zikamchochea mtu huyo kuitikia vizuri zaidi Shahidi mwingine atakapomtembelea wakati ujao.

16, 17. Tunawezaje kutumia utambuzi katika huduma yetu?

16 Nyakati nyingine, huenda ukaendelea na mazungumzo hata mtu anaposema kwamba hapendezwi. Mtu anaweza kusema, “Hapana, asante. Nina dini yangu” au, “Sipendezwi na mambo hayo.” Anaweza kusema hivyo kwa sababu tu anaona hiyo kuwa njia rahisi zaidi ya kukomesha mazungumzo. Hata hivyo, kwa ustadi na fadhili, unaweza kuuliza swali la kuchochea fikira ambalo litamsaidia mwenye nyumba kupendezwa na mambo ya kiroho.—Soma Wakolosai 4:6.

17 Nyakati nyingine tunapokutana na watu ambao wanahisi kwamba wana shughuli nyingi sana wasiweze kutusikiliza, ni vizuri kuheshimu maoni yao na kuondoka. Hata hivyo, pindi nyingine huenda ukatambua kwamba unaweza kusema jambo fulani muhimu kwa ufupi. Ndugu fulani wanaweza kufungua Biblia, kusoma andiko fulani lenye kuvutia, na kumwachia mwenye nyumba swali, kwa muda unaopungua dakika moja. Nyakati nyingine, mazungumzo yao mafupi yanachochea sana upendezi hivi kwamba mwenye nyumba anahisi kuwa hana shughuli nyingi sana za kumzuia kuwa na mazungumzo mafupi. Kwa nini usijaribu kufanya hivyo hali inaporuhusu?

18. Tunaweza kufanya nini ili tuwe wenye matokeo zaidi katika mahubiri yasiyo rasmi?

18 Tunapokutana na watu katika shughuli zetu za kila siku, tunaweza kila mara kuwachochea watu kupendezwa na habari njema ikiwa tuko tayari kutoa ushahidi kwa njia isiyo rasmi. Ndugu na dada wengi wanabeba machapisho fulani ndani ya mifuko au mikoba yao. Huenda pia wakawa na andiko hususa la Biblia akilini ambalo wanaweza kuwasomea wengine nafasi inapopatikana. Unaweza kuzungumza na mwangalizi wa utumishi au mapainia katika kutaniko lenu kuhusu jinsi unavyoweza kujitayarisha kufanya hivyo.

TUWASAIDIE KWA FADHILI WATU WETU WA UKOO WAAMKE KIROHO

19. Kwa nini tunapaswa kuendelea kujaribu kuwasaidia watu wetu wa ukoo?

19 Kwa kawaida, tungependa kuwasaidia watu wetu wa ukoo kukubali habari njema. (Yos. 2:13; Mdo. 10:24, 48; 16:31, 32) Ikiwa walikataa tulipowahubiria mwanzoni, huenda tusiwe na shauku ya kujaribu tena. Huenda tukafikiri kwamba hakuna mengi tunayoweza kufanya au kusema ambayo yatabadili mtazamo wao. Hata hivyo, huenda mambo fulani yakatukia ambayo yanaweza kubadili maisha au maoni ya watu wako wa ukoo. Au huenda umeboresha uwezo wako wa kueleza kweli hivi kwamba unaweza sasa kupata matokeo tofauti.

20. Kwa nini sifa ya busara ni muhimu tunapozungumza na watu wetu wa ukoo?

20 Tunapaswa kuheshimu hisia za watu wetu wa ukoo. (Rom. 2:4) Je, hatupaswi kuzungumza nao kwa fadhili kama vile tu tunavyozungumza na watu tunaokutana nao katika kazi ya kuhubiri? Zungumza kwa upole na heshima. Si lazima uwahubirie kila mara watu wako wa ukoo, waonyeshe kwa matendo yako jinsi ambavyo kweli imekusaidia. (Efe. 4:23, 24) Fanya iwe rahisi kwao kuona jinsi ambavyo Yehova amebariki maisha yako, na ‘kukufundisha ili ujifaidi mwenyewe.’ (Isa. 48:17) Acha watu wako wa ukoo waone kupitia mfano wako jinsi Mkristo anavyopaswa kuishi.

21, 22. Simulia jambo lililoonwa ambalo linaonyesha umuhimu wa kuendelea kujitahidi kuwasaidia kiroho watu wetu wa ukoo.

21 Hivi karibuni, dada mmoja aliandika hivi: “Sikuzote nimejaribu kuwahubiria ndugu na dada zangu 13 kwa maneno na mwenendo. Siachi kamwe mwaka upite bila kumwandikia barua kila mmoja wao. Hata hivyo, kwa miaka 30, nimekuwa Shahidi peke yangu katika familia yetu.”

22 Dada huyo aliendelea kusema hivi: “Siku moja, nilimpigia simu mmoja wa dada zangu anayeishi mbali sana. Aliniambia kwamba aliomba mhubiri wa kanisa lao ajifunze Biblia pamoja naye, lakini mhubiri huyo hakufanya hivyo. Niliposema kwamba ningefurahi kumsaidia, alisema: ‘Vizuri, lakini ninakuambia sasa: Sitakuwa kamwe Shahidi wa Yehova.’ Baada ya kumtumia kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa?, nilimpigia simu kila baada ya siku chache. Lakini bado hakuwa amefungua kitabu hicho. Hatimaye, nilimwomba achukue kitabu chake, na kwa angalau dakika 15 akiwa kwenye simu, tulisoma na kuzungumzia baadhi ya maandiko yaliyonukuliwa. Baada ya kuzungumza naye mara kadhaa kwenye simu, alitaka kujifunza kwa zaidi ya dakika 15. Kisha, alianza kunipigia simu ili nijifunze naye, nyakati nyingine hata asubuhi kabla sijaamka na nyakati nyingine alipiga mara mbili kwa siku. Mwaka uliofuata, alibatizwa, na baada ya mwaka huo, alianza utumishi wa painia.”

23. Kwa nini hatupaswi kuchoka kujaribu kuwaamsha watu kutoka katika usingizi wa kiroho?

23 Kuwasaidia watu ili waamke kutoka katika usingizi wa kiroho ni ustadi ambao unahitaji jitihada zenye kuendelea. Hata hivyo, watu wapole bado wanaitikia jitihada zetu za kuwaamsha kiroho. Kwa wastani, watu zaidi ya 20,000 wanabatizwa kila mwezi na kuwa Mashahidi wa Yehova. Hivyo, acheni tuchukue kwa uzito shauri la Paulo kwa ndugu yetu Arkipo aliyeishi katika karne ya kwanza: “Endelea kuangalia huduma ambayo uliikubali katika Bwana, ili uitimize.” (Kol. 4:17) Makala inayofuata itatusaidia sote kuelewa maana ya kuhubiri tukiwa na hisi ya uharaka.

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 13]

JINSI UNAVYOWEZA KUENDELEA KUKESHA

▪ Endelea kuwa na mengi ya kufanya katika kutimiza mapenzi ya Mungu

▪ Epuka matendo ya giza

▪ Jihadhari na hatari ya usingizi wa kiroho

▪ Endelea kuwa na maoni yanayofaa kuhusu watu katika eneo lenu

▪ Jaribu njia mpya za kuwahubiria wengine

▪ Kumbuka umuhimu wa huduma yako