Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wewe Hutoaje Shauri?

Wewe Hutoaje Shauri?

Wewe Hutoaje Shauri?

Je, umewahi kuombwa uwashauri wengine? Kwa mfano, je, umewahi kuulizwa maswali kama haya: ‘Nifanye nini? Je, niende kwenye tafrija hii? Je, nifuatie kazi hii maishani? Je, nianzishe urafiki na mtu huyu nikiwa na lengo la kufunga ndoa naye?’

Watu wanyoofu wanaweza kukuomba uwasaidie kufanya maamuzi ambayo yanaweza kuwa na uvutano juu ya uhusiano wao pamoja na marafiki, familia, au hata na Yehova. Jibu lako litategemea nini? Kwa kawaida unawashauri wengine jinsi gani? Iwe ni kuhusu jambo linaloonekana kuwa dogo au kubwa, andiko la Methali 15:28 linasema, “moyo wa mwadilifu hutafakari ili kujibu.” Fikiria jinsi kanuni tano zifuatazo za Biblia zinavyoweza kutusaidia kuhusiana na kutoa shauri.

1 Elewa Jinsi Hali Ilivyo Kikweli.

“Yeyote anapojibu jambo kabla ya kulisikia, huo ni upumbavu na aibu kwake.”MET. 18:13.

Ili kutoa shauri zuri, ni lazima tuelewe hali na maoni ya yule anayetafuta msaada. Kwa mfano: Ikiwa mtu angekupigia simu na kukuuliza kuhusu njia nzuri zaidi ya kufika nyumbani kwako, ungehitaji kujua nini ili umsaidie? Je, unaweza kumwelekeza kuhusu njia nzuri zaidi ya kufuata ikiwa kwanza hujui mahali alipo kwa sasa? Bila shaka huwezi! Vivyo hivyo, ili kutoa mwongozo unaofaa tunahitaji kuelewa “mahali” ambapo yule anayeomba mwongozo yupo, yaani, kuelewa hali na maoni yake. Je, huenda kukawa na hali fulani za kuzingatia ambazo zinaweza kuamua jinsi tutakavyomjibu? Bila kujua vizuri hali yake, huenda tukatoa shauri ambalo linamfanya mtu avurugike hata zaidi.—Luka 6:39.

Chunguza Amefanya Utafiti Mwingi Kadiri Gani. Huenda pia likawa jambo la hekima kumuuliza mtu anayeomba shauri maswali kama haya: “Unafikiri ni kanuni gani za Biblia zinazohusika?” “Maamuzi unayotaka kufanya yataleta faida au hasara gani?” “Tayari umefanya utafiti gani?” “Ni msaada gani ambao tayari umepata kutoka kwa wengine, kama vile wazee wa kutaniko, wazazi wako, au mwalimu wako wa Biblia?”

Majibu yake yanaweza kutusaidia kufahamu jitihada ambazo tayari mtu huyo amefanya ili kutafuta jibu. Pia, tunapotoa shauri tutazingatia mambo ambayo huenda wengine tayari wamesema. Huenda tukatambua pia ikiwa mtu huyo anataka hasa mshauri ambaye ‘atafurahisha masikio yake’ kwa kumpa shauri analotaka kusikia.—2 Tim. 4:3.

2 Epuka Kujibu Haraka-Haraka.

“Kila mtu lazima awe mwepesi kuhusu kusikia, si mwepesi wa kusema.”YAK. 1:19.

Huenda tukajibu haraka-haraka tukiwa na nia nzuri. Lakini kwa kawaida, je, kufanya hivyo ni jambo la hekima, hasa ikiwa tunazungumzia habari ambayo hatujafanyia utafiti kamili? Andiko la Methali 29:20 linasema: “Je, umemwona mtu mwenye haraka kwa maneno yake? Kuna tumaini zaidi kwa mjinga kuliko kwake.”

Chukua wakati ili kuhakikisha kwamba jibu lako linapatana kabisa na hekima ya Mungu. Jiulize hivi: ‘Je, fikira na “roho ya ulimwengu” imeathiri njia yangu ya kufikiri?’ (1 Kor. 2:12, 13) Kumbuka kwamba huenda isitoshe kuwa tu na nia nzuri. Mtume Petro, baada ya kusikia kuhusu mgawo mgumu wa Yesu, alimshauri hivi: “Jitendee kwa fadhili, Bwana; wewe hutapatwa hata kidogo na jambo hili.” Tunaweza kujifunza nini kutokana na itikio la Petro? Tunajifunza kwamba hata mtu mnyoofu asipokuwa mwangalifu anaweza kueneza, “si fikira za Mungu, bali za wanadamu.” (Mt. 16:21-23) Ni muhimu kama nini kufikiri kabla ya kuongea! Si ni kweli kwamba uzoefu wetu ni mdogo sana ukilinganishwa na hekima ya Mungu?—Ayu. 38:1-4; Met. 11:2.

3 Tumia Neno la Mungu kwa Unyenyekevu.

“Sifanyi jambo lolote kwa uamuzi wangu mwenyewe; bali kama vile Baba alivyonifundisha, ndivyo ninavyosema mambo haya.”YOH. 8:28.

Je, utasema, “Kama ningekuwa wewe, ninge . . .”? Hata kama jibu la swali uliloulizwa linaonekana kuwa wazi, itakuwa vizuri kwako kujifunza kutokana na mfano wa unyenyekevu na kiasi ambao Yesu alituwekea. Alikuwa na uzoefu na hekima nyingi zaidi kuliko mwanadamu yeyote; hata hivyo, alisema hivi: “Sijasema kutokana na msukumo wangu mwenyewe, bali Baba mwenyewe . . . amenipa amri kuhusu jambo la kutangaza na la kusema.” (Yoh. 12:49, 50) Sikuzote mafundisho na mashauri ya Yesu yalitegemea mapenzi ya Baba yake.

Kwa mfano, katika Luka 22:49 tunasoma kwamba Yesu alipokuwa karibu kukamatwa wanafunzi wake walimuuliza ikiwa walipaswa kupigana. Mwanafunzi mmoja alitumia upanga. Angalia simulizi linalofanana na hilo katika Mathayo 26:52-54 linaonyesha kwamba hata chini ya hali hizo, Yesu alitumia wakati wake kumsaidia mwanafunzi huyo kuelewa mapenzi ya Yehova. Akitambua kanuni iliyo katika Mwanzo 9:6 na unabii wa Zaburi 22 na Isaya 53, Yesu aliweza kutoa mwongozo wenye hekima ambao bila shaka uliokoa uhai wa watu na kumpendeza Yehova.

4 Tumia Maktaba Yako ya Kitheokrasi.

“Ni nani kwa kweli mtumwa mwaminifu na mwenye busara ambaye bwana wake alimweka rasmi juu ya watumishi wake wa nyumbani, awape chakula chao kwa wakati unaofaa?”MT. 24:45.

Yesu ameweka rasmi jamii ya mtumwa inayotegemeka ambayo inatoa chakula muhimu cha kiroho. Unapotoa shauri na mwongozo kuhusu mambo muhimu, je, unatumia wakati kufanya utafiti kabisa katika machapisho yanayotegemea Biblia?

Vifaa kama vile Fahirisi na Watchtower Library * vinatusaidia kupata haraka habari nyingi sana zilizo wazi. Lingekuwa kosa kubwa kama nini kupuuza habari hizo nyingi muhimu! Vifaa hivyo vina maelfu ya vichwa vya habari, na makala nyingi za kumsaidia mtu anayetafuta shauri. Je, una ustadi wa kuwasaidia wengine kutumia vifaa hivyo kufanya utafiti kuhusu kanuni za Biblia na kufanya maamuzi wakitegemea Neno la Mungu? Kama vile tu ramani inavyoweza kumsaidia mtu kujua mahali alipo na kumsaidia kufika mahali anapoenda, ndivyo vifaa vya utafiti vinavyoweza kumsaidia mtu kujua njia anayofuata na kufanya maamuzi ambayo yatamsaidia kubaki kwenye njia ya uzima.

Wazee wengi wamewazoeza wahubiri kutafuta makala mbalimbali kwa kutumia Fahirisi au Watchtower Library, na hivyo wamewasaidia ndugu na dada zao kujifunza na kulinganisha Maandiko wanapofanya maamuzi. Msaada huo unawasaidia wahubiri kushughulikia matatizo yao ya sasa na zaidi ya hayo kusitawisha mazoea ya kufanya utafiti na kutegemea maandalizi ya kiroho kutoka kwa Yehova. Kwa kufanya hivyo, ‘nguvu zao za ufahamu zinazoezwa kutofautisha yaliyo sawa na yaliyo makosa pia.’—Ebr. 5:14.

5 Epuka Kujaribu Kuwafanyia Wengine Maamuzi.

“Kila mmoja ataubeba mzigo wake mwenyewe.”GAL. 6:5.

Mwishowe, kila mtu anahitaji kujichagulia mwenyewe shauri ambalo atafuata. Yehova ametupatia sote uhuru wa kuchagua ikiwa tutaongozwa na kanuni zake au la. (Kum. 30:19, 20) Hali fulani zinahusisha kanuni kadhaa za Biblia, lakini hatimaye, mtu anayetafuta shauri ni lazima afanye uamuzi wake mwenyewe. Ikitegemea suala linalohusika au umri wa yule anayetuomba shauri, huenda tukahitaji pia kujiuliza hivi: ‘Je, kweli nina mamlaka ya kushughulikia jambo hili?’ Ni vyema zaidi mambo fulani yapelekwe kwa wazee wa kutaniko au, ikiwa mtu anayeomba msaada ni kijana ni vyema azungumze na wazazi wake.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 20 CD-ROM ya Watchtower Library inapatikana sasa katika lugha 39. Fahirisi inapatikana sasa katika lugha zaidi ya 45.

[Sanduku/​Picha katika ukurasa wa 8]

Mradi wa Ibada ya Familia

Kwa nini usiwe na mradi wa kujifunza wa kufanya utafiti na kutafuta majibu ya maswali ambayo umeulizwa hivi karibuni? Ni makala na kanuni gani za Biblia ambazo unaweza kutumia kumsaidia mtu anayeuliza maswali kama hayo? Kwa mfano, tuseme ndugu au dada anakuuliza kuhusu kumchumbia mtu fulani akiwa na kusudi la kufunga ndoa naye. Mnapotumia Fahirisi au Watchtower Library, tafuteni kwanza kichwa kinachohusiana moja kwa moja na habari hiyo. Kwa mfano, katika Fahirisi mnaweza kutafuta neno “Uchumba” au “Ndoa.” Kisha chunguzeni vichwa vidogo ili kupata makala zinazofaa. Mnapotazama kichwa kikuu, angalieni ikiwa kuna vichwa vingine vyenye maneno “Ona pia,” ambavyo vinaweza kuwaelekeza kwenye kichwa kingine kinachohusiana moja kwa moja na habari mnayotafuta.

[Sanduku katika ukurasa wa 9]

Kwa sababu ya maandalizi ambayo Yehova anatupatia kupitia tengenezo lake, tunaweza kutoa na kupokea mashauri yaliyo bora kabisa. Andiko la Mhubiri 12:11 linasema hivi: “Maneno ya wenye hekima ni kama michokoo ya kuongoza ng’ombe, na kama tu misumari iliyopigiliwa ndani, ndivyo walivyo wale wanaoshughulika mno kukusanya maneno; wametolewa kutoka kwa mchungaji mmoja.” Kama tu “michokoo ya kuongoza ng’ombe,” yaani, vijiti vilivyochongoka vinavyotumiwa kuongoza wanyama wavutao mizigo, ndivyo mashauri mazuri na yenye upendo yanavyowaongoza watu wanyoofu upande unaofaa. “Misumari iliyopigiliwa ndani” inafanya majengo yawe imara. Vivyo hivyo, kutoa mashauri mazuri kunaweza kuwaimarisha wengine. Watu wenye hekima ‘wanashughulika mno,’ au wanafurahia sana ‘kukusanya maneno’ ambayo yanategemea hekima ya ‘mchungaji wao mmoja,’ Yehova.

Mwige Mchungaji huyo unapotoa shauri. Ni pendeleo kubwa kama nini kwetu kusikiliza kwa makini na pia kutoa shauri lenye faida inapowezekana! Shauri letu linapotegemea kikweli kanuni za Biblia, litakuwa zuri na linaweza kumnufaisha milele msikilizaji.