Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Dumisha Moyo Kamili Kumwelekea Yehova

Dumisha Moyo Kamili Kumwelekea Yehova

Dumisha Moyo Kamili Kumwelekea Yehova

“Mwanangu, mjue Mungu wa baba yako, umtumikie kwa moyo kamili.”—1 NYA. 28:9.

TAFUTA MAJIBU YA MASWALI HAYA:

Moyo wa mfano ni nini?

Ni njia gani tunayoweza kutumia ili kuuchunguza moyo wetu?

Tunaweza kuendelea jinsi gani kuufanya moyo wetu uwe kamili kumwelekea Yehova?

1, 2. (a) Ni sehemu gani ya mwili ambayo inarejelewa mara nyingi kwa njia ya mfano katika Neno la Mungu kuliko sehemu nyingine yoyote? (b) Kwa nini ni muhimu tuelewe maana ya moyo wa mfano?

MARA nyingi, Neno la Mungu linazungumzia kwa njia ya mfano sehemu mbalimbali za mwili wa binadamu. Kwa mfano, mzee wa ukoo Ayubu alisema hivi: “Hakuna jeuri mikononi mwangu.” Mfalme Sulemani alisema: “Habari ambayo ni njema huifanya mifupa inone.” Yehova alimhakikishia Ezekieli hivi: ‘Nimelifanya paji la uso wako kuwa gumu kuliko jiwe gumu.’ Na mtume Paulo aliambiwa hivi: “Unaanzisha mambo yaliyo mageni masikioni mwetu.”—Ayu. 16:17; Met. 15:30; Eze. 3:9; Mdo. 17:20.

2 Hata hivyo, kuna sehemu fulani ya mwili wa binadamu ambayo inarejelewa kwa njia ya mfano katika Biblia mara nyingi zaidi kuliko sehemu nyingine yoyote ile. Ni ile inayotajwa katika sala ya mwaminifu Hana: “Moyo wangu unafurahi katika Yehova.” (1 Sam. 2:1) Kwa kweli, waandikaji wa Biblia wanataja moyo karibu mara elfu moja hivi, na karibu mara zote hizo ni katika maana ya mfano. Ni jambo la muhimu sana kuelewa moyo unafananisha nini kwa sababu Biblia inasema kwamba tunahitaji kuulinda.—Soma Methali 4:23.

MOYO WA MFANO NI NINI?

3. Tunawezaje kutambua maana ya neno “moyo” katika Biblia? Toa mfano.

3 Neno la Mungu linatusaidia kuelewa maana ya neno “moyo” ingawa halitumii maana inayotumiwa na kamusi kueleza maana ya neno hilo. Jinsi gani? Kwa mfano, fikiria picha maridadi sana iliyotengenezwa kwa maelfu ya mawe madogo-madogo yaliyounganishwa pamoja kwa ukaribu sana. Ili kuona jinsi mawe yote yalivyounganishwa, tunahitaji kuchunguza na kuitazama picha yote kwa ujumla. Vivyo hivyo, tunahitaji kutazama sehemu mbalimbali katika Biblia ambazo neno “moyo” linatumiwa ili tuelewe maana yake. Kwa hiyo, moyo wa mfano ni nini?

4. (a) Neno “moyo” linamaanisha nini? (b) Maneno ya Yesu katika Mathayo 22:37 yanamaanisha nini?

4 Waandikaji wa Biblia wanatumia neno “moyo” ili kueleza jinsi mtu alivyo kwa ndani kwa ujumla. Hilo linatia ndani tamaa zetu, mawazo, utu, mitazamo, uwezo wetu mbalimbali, nia, na malengo yetu. (Soma Kumbukumbu la Torati 15:7; Methali 16:9; Matendo 2:26.) Kama kitabu kimoja cha marejeo kinavyosema, moyo ni “jumla ya jinsi mtu alivyo kwa ndani.” Nyakati nyingine, neno “moyo” halimaanishi hivyo. Kwa mfano, Yesu alisema hivi: “Lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa akili yako yote.” (Mt. 22:37) Katika kisa hicho, neno “moyo” linamaanisha hisia, na tamaa za mtu wa ndani. Kwa kutaja moyo, nafsi, na akili, yaani, kila kiungo peke yake, Yesu alikazia wazo la kwamba ni lazima tuonyeshe upendo wetu kwa Mungu kwa hisia zetu na pia kwa jinsi tunavyoishi na kutumia akili zetu. (Yoh. 17:3; Efe. 6:6) Lakini neno “moyo” linapotajwa lenyewe tu, linamaanisha mtu kwa ujumla alivyo kwa ndani.

KWA NINI TUNAHITAJI KULINDA MOYO WETU?

5. Kwa nini tunataka kufanya yote tuwezayo ili kumtumikia Yehova kwa moyo kamili?

5 Kuhusiana na moyo, Mfalme Daudi alimkumbusha Sulemani hivi: “Mwanangu, mjue Mungu wa baba yako, umtumikie kwa moyo kamili na kwa nafsi yenye shangwe; kwa maana Yehova anaichunguza mioyo yote, naye anatambua kila mwelekeo wa fikira.” (1 Nya. 28:9) Kwa kweli, Yehova ni Mchunguzaji wa mioyo yote, kutia ndani mioyo yetu. (Met. 17:3; 21:2) Kile anachokiona mioyoni mwetu kinaamua uhusiano wetu pamoja naye sasa na wakati ujao. Kwa hiyo, tuna sababu ya kufuata shauri la Daudi lililoongozwa kwa roho ya Mungu kwa kufanya yote tuwezayo ili kumtumikia Yehova kwa moyo kamili.

6. Tunapaswa kutambua nini kuhusu azimio letu la kumtumikia Yehova?

6 Utendaji wetu mbalimbali wenye bidii tukiwa watu wa Yehova unaonyesha kwamba kwa kweli tuna tamaa ya ndani kabisa ya kumtumikia Mungu kwa moyo kamili. Wakati huohuo, tunatambua kwamba mikazo ya ulimwengu mwovu wa Shetani na mielekeo ya mwili wetu wenye dhambi inaweza kuwa na uvutano wenye nguvu ambao unadhoofisha azimio letu la kumtumikia Mungu kwa moyo wote. (Yer. 17:9; Efe. 2:2) Hivyo, ili kuchunguza kwamba azimio letu la kumtumikia Mungu halidhoofishwi, yaani, hatulegezi ulinzi wetu, tunapaswa kuuchunguza kwa ukawaida moyo wetu. Tunawezaje kufanya hivyo?

7. Ni nini kinachoonyesha hali ya moyo wetu?

7 Kwa kweli, hakuna mwanadamu anayeweza kuona jinsi tulivyo kwa ndani, kama vile tu hakuna mtu anayeweza kuona moyo au sehemu ya katikati kabisa ya mti. Hata hivyo, kama Yesu alivyosema katika Mahubiri yake ya Mlimani, kama vile tu matunda yanavyofunua hali ya mti, ndivyo matendo yetu yanavyoonyesha hali halisi ya moyo wetu. (Mt. 7:17-20) Acheni tuchunguze mojawapo ya matendo hayo.

NJIA NZURI YA KUUCHUNGUZA MOYO WETU

8. Maneno ya Yesu katika Mathayo 6:33 yanahusianaje na mambo yaliyo moyoni mwetu?

8 Mapema katika mahubiri hayohayo, Yesu aliwaambia wasikilizaji wake jambo ambalo wangepaswa kufanya ili kuonyesha tamaa yao ya ndani ya kumtumikia Yehova kwa moyo wao wote. Alisema hivi: “Basi, endeleeni kuutafuta kwanza ufalme na uadilifu wake, nanyi mtaongezewa hivi vitu vingine vyote.” (Mt. 6:33) Kwa kweli, kupitia mambo tunayotanguliza maishani, tunaonyesha wazi mambo tunayotamani, tunayofikiri, na tunayopanga ndani kabisa ya moyo wetu. Kuchunguza mambo tunayotanguliza katika maisha yetu ni njia moja iliyo wazi ya kuchunguza ikiwa tunamtumikia Mungu kwa moyo kamili.

9. Yesu aliwapa wanaume fulani mwaliko gani, na majibu yao yalifunua nini?

9 Muda mfupi tu baada ya Yesu kuwahimiza wafuasi wake ‘waendelee kuutafuta kwanza ufalme,’ jambo fulani lilitukia linaloonyesha jinsi hali ya moyo wa mwanadamu inavyojulikana kupitia mambo anayotanguliza maishani. Luka, mwandikaji wa Injili, anaanza kuzungumzia jambo hilo kwa kusema kwamba Yesu “aliukaza uso wake kwenda Yerusalemu,” ingawa alijua vizuri mambo ambayo hatimaye yangempata huko. Yeye na mitume wake “walipokuwa wakienda barabarani,” Yesu alikutana na wanaume fulani ambao aliwaalika kwa kusema: ‘Iweni wafuasi wangu.’ Wanaume hao walikuwa tayari kukubali mwaliko wa Yesu, lakini kwa masharti fulani. Mwanamume mmoja alijibu: “Niruhusu kwanza niondoke nikamzike baba yangu.” Mwingine alisema: “Nitakufuata, Bwana; lakini kwanza niruhusu niwaage watu wa nyumbani mwangu.” (Luka 9:51, 57-61) Bila shaka, tunaweza kuona tofauti kubwa kati ya azimio thabiti la Yesu la kufanya mapenzi ya Mungu kwa moyo wote na majibu hafifu na yenye masharti ya wale wanaume ambao Yesu aliwaalika. Kwa kutanguliza kwanza mahangaiko yao badala ya faida za Ufalme, walifunua kwamba mioyo yao haikuwa kamili kumwelekea Mungu.

10. (a) Wafuasi wa Kristo wameitikiaje mwaliko wa Yesu? (b) Yesu alitoa mfano gani mfupi?

10 Tofauti na wanaume hao ambao wangekuwa wanafunzi, sisi tumekubali kwa hekima mwaliko wa Yesu wa kuwa wafuasi wake na sasa tunamtumikia Yehova kila siku. Katika njia hiyo, tunaonyesha jinsi tunavyohisi ndani ya mioyo yetu kumhusu Yehova. Lakini, hata iwe sisi ni wahubiri wenye bidii kutanikoni, bado tunahitaji kutambua kwamba moyo wetu unaweza kuwa hatarini. Ni hatari gani hiyo? Katika mazungumzo yaleyale pamoja na wanaume wale ambao wangekuwa wanafunzi wake, Yesu alifunua hatari hiyo, kwa kusema hivi: “Hakuna mtu ambaye ameweka mkono wake kwenye jembe la ng’ombe na kutazama mambo yaliyo nyuma anayefaa kwa ajili ya ufalme wa Mungu.” (Luka 9:62) Ni somo gani tunaloweza kupata kutokana na mfano huo?

JE, ‘TUNASHIKAMANA NA YALIYO MEMA’?

11. Ni nini kilichotokea kuhusu kazi ya yule mtu anayetajwa katika mfano wa Yesu, na kwa nini?

11 Ili kuelewa vizuri zaidi somo linalotokana na mfano mfupi wa Yesu, acheni tuongeze maelezo zaidi kwenye mfano huo. Mtu anayefanya kibarua cha kulima shambani analima kwa bidii sana. Hata hivyo, anapoendelea kulima, anawaza kuhusu nyumbani kwake jinsi ambavyo angekuwa pamoja na familia yake, marafiki, na kufurahia chakula, muziki, kicheko, na kivuli. Anatamani sana vitu hivyo. Baada ya kulima kipande fulani cha shamba, tamaa ya mfanyakazi huyo kuhusu vitu hivyo vizuri maishani inakuwa kubwa sana hivi kwamba anageuka na kutazama “mambo yaliyo nyuma.” Ingawa bado kuna kazi nyingi ya kufanya kabla shamba halijapandwa mbegu, mfanyakazi huyo anakengeushwa na hafanyi kazi yake vizuri. Bila shaka, bwana wa mfanyakazi huyo anatamaushwa na ukosefu wa uvumilivu wa mfanyakazi wake.

12. Mkristo anawezaje leo kuwa katika hali inayofanana na ya mtu anayetajwa katika mfano wa Yesu?

12 Sasa ona jinsi hali kama hiyo inavyoweza kutokea leo. Yule mkulima anaweza kufananisha Mkristo yeyote ambaye anaonekana anafanya vizuri kiroho lakini kwa kweli yuko katika hatari. Kwa mfano, acheni tuwazie ndugu mwenye bidii katika huduma. Hata hivyo, ingawa anahudhuria mikutano na kushiriki katika utumishi wa shambani, anaendelea kufikiria vitu fulani vya ulimwengu huu ambavyo anapenda. Katika moyo wake, anavitamani sana vitu hivyo. Hatimaye, baada ya ndugu huyo kumtumikia Mungu kwa miaka mingi, tamaa yake kwa ajili ya baadhi ya vitu hivyo inakuwa kubwa sana hivi kwamba anatazama “mambo yaliyo nyuma.” Ingawa bado kuna mengi ya kufanya katika huduma, ndugu huyo haendelei “kulishika sana neno la uzima,” na hivyo hamtumikii Mungu kama alivyofanya zamani. (Flp. 2:16) Yehova, “Bwana wa mavuno,” anahuzunika wakati mmoja wa wafanyakazi wake anaposhindwa kuvumilia.—Luka 10:2.

13. Kumtumikia Yehova kwa moyo kamili kunatia ndani nini?

13 Somo liko wazi. Ni jambo linalostahili pongezi ikiwa tunashiriki kwa ukawaida katika utendaji huo mzuri na wenye kuridhisha kama vile kuhudhuria mikutano ya kutaniko na kushiriki katika utumishi wa shambani. Lakini kumtumikia Yehova kwa moyo kamili kunatia ndani mengi zaidi. (2 Nya. 25:1, 2, 27) Ikiwa ndani kabisa ya moyo wake Mkristo anaendelea kupenda “mambo yaliyo nyuma,” yaani, vitu fulani ambavyo ni sehemu ya njia ya maisha ya ulimwengu huu, Mkristo huyo yuko katika hatari ya kupoteza uhusiano wake pamoja na Mungu. (Luka 17:32) Hivyo, ili kumtumikia Mungu kwa moyo kamili, ni lazima ‘tuchukie maovu na kushikamana na yaliyo mema,’ tukifanya hivyo tutakuwa wenye ‘kufaa kwa ajili ya ufalme wa Mungu.’ (Rom. 12:9; Luka 9:62) Kwa hiyo, sisi sote, tunapaswa kuhakikisha kwamba hakuna kitu chochote kile katika ulimwengu huu wa Shetani kinachoweza kutuzuia kufuatia masilahi ya Ufalme kwa moyo wetu wote, hata kionekane kuwa chenye manufaa au chenye kupendeza kadiri gani.—2 Kor. 11:14; soma Wafilipi 3:13, 14.

TUENDELEE KUWA MACHO!

14, 15. (a) Shetani anajaribu jinsi gani kuharibu hali ya moyo wetu? (b) Toa mfano unaoonyesha jinsi mbinu ya Shetani ilivyo hatari sana.

14 Kumpenda Yehova kulituchochea kujiweka wakfu kwake. Tangu wakati huo, wengi wetu wamethibitisha kwa muda wa miaka mingi kwamba wameazimia kuendelea kumtumikia Yehova kwa moyo kamili. Hata hivyo, Shetani hajachoka kujaribu kutushawishi. Bado anaulenga moyo wetu. (Efe. 6:12) Bila shaka, huenda Shetani akatambua kwamba hatutamwacha Yehova mara moja. Kwa hiyo, Shetani anatumia kwa werevu “mfumo huu wa mambo” ili kujaribu kudhoofisha hatua kwa hatua bidii yetu ya kutoka moyoni kwa ajili ya Mungu. (Soma Marko 4:18, 19.) Kwa nini mbinu hiyo ya Shetani imefanikiwa sana?

15 Ili kujibu swali hilo, wazia unasoma kitabu kwa kutumia taa ya umeme yenye uwezo wa wati 100, lakini baadaye taa hiyo inazimika. Kwa kuwa unabaki gizani, papo hapo unatambua kwamba unapaswa kuwasha tena taa yako. Chumba chako kinajaa nuru tena. Jioni inayofuata, unasoma kwa kutumia taa hiyohiyo. Hata hivyo, bila wewe kujua, mtu fulani alibadili taa hiyo ya wati 100 na kuweka taa nyingine yenye uwezo mdogo ya wati 95. Je, utatambua tofauti? Huenda usitambue. Na namna gani ikiwa siku inayofuata mtu fulani anaweka taa yenye uwezo wa wati 90? Inaelekea, bado hungetambua hilo. Kwa nini? Nuru ya taa inapungua hatua kwa hatua hivi kwamba hutambui jambo hilo. Vivyo hivyo, uvutano wa ulimwengu wa Shetani unaweza kupunguza bidii yetu pole kwa pole. Ikiwa jambo hilo linatokea itakuwa ni kana kwamba Shetani amefaulu kupunguza bidii yetu ya kumtumikia Yehova kwa moyo wote na sasa tunamtumikia kwa kiwango kidogo. Asipokuwa macho, Mkristo hawezi kutambua jinsi anavyobadilika hatua kwa hatua.—Mt. 24:42; 1 Pet. 5:8.

SALA NI MUHIMU SANA

16. Tunawezaje kujilinda wenyewe dhidi ya mbinu za Shetani?

16 Tunawezaje kujilinda wenyewe dhidi ya mbinu hizo za Shetani na hivyo kudumisha moyo kamili kumwelekea Yehova? (2 Kor. 2:11) Sala ni muhimu sana. Paulo aliwatia moyo waamini wenzake ‘wasimame imara ili kupinga hila za Ibilisi.’ Kisha akawahimiza hivi: “Kwa kila namna ya sala na dua mkiendeleza sala kila wakati.”—Efe. 6:11, 18; 1 Pet. 4:7.

17. Sala za Yesu zinatufunza somo gani?

17 Ili kumpinga Shetani kwa uthabiti, ni jambo la hekima tuige mtazamo wa Yesu wa kusali kwa bidii, mtazamo ambao ulionyesha tamaa yake ya ndani kabisa ya kudumisha moyo kamili kumwelekea Yehova. Kwa mfano, ona yale ambayo Luka aliandika kuhusu jinsi Yesu alivyosali usiku kabla ya kifo chake: “Akaingia katika maumivu makali, akaendelea kusali kwa bidii zaidi.” (Luka 22:44) Yesu alisali kwa bidii zaidi kabla ya hapo, lakini katika pindi hii, alipokuwa akikabili jaribu kali zaidi katika maisha yake hapa duniani, alisali kwa “bidii zaidi,” na sala yake ilijibiwa. Mfano wa Yesu unaonyesha kwamba sala fulani zinaweza kuwa zenye bidii zaidi kuliko nyingine. Kwa hiyo, kadiri majaribu yetu yanavyozidi kuwa makali na mbinu za Shetani kuwa za ujanja zaidi, ndivyo tunavyopaswa kusali kwa “bidii zaidi” ili kuomba ulinzi wa Yehova.

18. (a) Tunapaswa kujiuliza nini kuhusu sala, na kwa nini? (b) Ni mambo gani yanayoathiri moyo wetu, na kwa njia zipi? (Ona  sanduku kwenye ukurasa wa  16.)

18 Sala kama hizo zitatusaidiaje? Paulo alisema hivi: “Katika kila jambo kwa sala na dua pamoja na kutoa shukrani maombi yenu na yajulishwe Mungu; na amani ya Mungu yenye ubora unaozidi fikira zote itailinda mioyo yenu.” (Flp. 4:6, 7) Naam, tunapaswa kusali kwa bidii na kwa ukawaida ili tudumishe moyo kamili kumwelekea Yehova. (Luka 6:12) Kwa hiyo, jiulize hivi: ‘Ninasali kwa bidii na kwa ukawaida kadiri gani?’ (Mt. 7:7; Rom. 12:12) Jibu lako linafunua mengi kuhusu kina cha tamaa yako ya kutoka moyoni ya kumtumikia Mungu.

19. Utafanya nini ili kudumisha moyo kamili kumwelekea Yehova?

19 Kama tulivyochunguza, mambo tunayotanguliza maishani yanaweza kutuambia mengi kuhusu hali ya moyo wetu. Tunataka kuhakikisha kwamba si mambo tuliyoacha nyuma wala mbinu zenye hila za Shetani zitakazoweza kudhoofisha azimio letu la kumtumikia Yehova kwa moyo kamili. (Soma Luka 21:19, 34-36.) Hivyo, kama Daudi, tunaendelea kutoa dua kwa Yehova: “Unganisha moyo wangu.”—Zab. 86:11.

[Maswali ya Funzo]

[Sanduku katika ukurasa wa 16]

 MAMBO MATATU YANAYOATHIRI MOYO WETU

Kama vile tu tunavyoweza kuchukua hatua ili kulinda hali ya moyo wetu halisi, vivyo hivyo tunaweza kuchukua hatua za kutusaidia kudumisha hali nzuri ya moyo wetu wa mfano. Chunguza mambo haya matatu muhimu:

1 Chakula Bora: Moyo wetu halisi unahitaji chakula cha kutosha kilicho bora. Vivyo hivyo, tunapaswa kuhakikisha kwamba tunakula chakula cha kiroho cha kutosha kilicho bora kupitia funzo la kibinafsi la kawaida, kutafakari, na kuhudhuria mikutano. —Zab. 1:1, 2; Met. 15:28; Ebr. 10:24, 25.

2 Mazoezi: Ili kuwa na afya nzuri, moyo wetu halisi, nyakati nyingine, unahitaji kusukuma damu mwilini kwa nguvu. Vivyo hivyo, kushiriki kwa bidii katika huduma, labda kwa kujitahidi sana kutimiza utendaji wetu mbalimbali, kunafanya moyo wetu wa mfano uendelee kuwa katika hali nzuri.—Luka 13:24; Flp. 3:12.

3 Mazingira: Kufanya kazi na kuishi katika mazingira ya watu wasiomwogopa Mungu kunaweza kufanya moyo wetu halisi na wa mfano kuwa chini ya mkazo wenye nguvu sana. Hata hivyo, tunaweza kupunguza mkazo kama huo kwa kushirikiana kwa ukawaida kadiri iwezekanavyo na waamini wenzetu, ambao wanatujali kikweli na ambao mioyo yao ni kamili kumwelekea Mungu.—Zab. 119:63; Met. 13:20.