Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Miaka Sabini ya Kushikilia Upindo wa Nguo ya Mtu Aliye Myahudi

Miaka Sabini ya Kushikilia Upindo wa Nguo ya Mtu Aliye Myahudi

Simulizi la Maisha

Miaka Sabini ya Kushikilia Upindo wa Nguo ya Mtu Aliye Myahudi

Limesimuliwa na Leonard Smith

Nilipokuwa katika miaka ya mapema ya ujana, nilivutiwa na mistari miwili ya Biblia. Leo, zaidi ya miaka 70 baadaye, bado ninakumbuka wakati nilipoelewa maana ya andiko la Zekaria 8:23, ambalo linasema kuhusu “watu kumi” wataushika “upindo wa nguo ya mtu aliye Myahudi.” Watu hao wanamwambia hivi mtu huyo aliye Myahudi: “Tutakwenda pamoja nanyi, kwa maana tumesikia ya kuwa Mungu yupo pamoja nanyi.”

MTU huyo Myahudi anafananisha Wakristo watiwa-mafuta, na “watu kumi” wanawakilisha “kondoo wengine,” au “Wayonadabu,” kama walivyojulikana wakati huo. * (Yoh. 10:16) Nilipoelewa kweli hiyo, nilitambua jinsi kutimizwa kwa tumaini langu la kuishi milele duniani kunavyotegemea kuiunga mkono kwa ushikaminifu jamii ya watiwa-mafuta.

Pia, mfano wa Yesu kuhusu “kondoo” na “mbuzi,” unaopatikana katika andiko la Mathayo 25:31-46, ulinivutia sana. “Kondoo” wanafananisha wale wanaohukumiwa kuwa wanastahili kupata uzima wakati wa mwisho kwa kuwa wanawafanyia mambo mema ndugu za Kristo watiwa-mafuta ambao bado wako duniani. Nikiwa Myonadabu kijana, nilijiambia, ‘Len, ikiwa unataka kuonwa na Kristo kuwa kondoo, unapaswa kuwaunga mkono ndugu zake watiwa-mafuta, ukubali mwongozo wao kwa kuwa Mungu yupo pamoja nao.’ Uelewaji huo umeniongoza kwa kipindi cha zaidi ya miongo saba.

‘MIMI NINA SEHEMU GANI?’

Mama yangu alibatizwa mwaka wa 1925 kwenye ukumbi wa mikutano wa Betheli. Ukumbi huo uliitwa London Tabernacle, na ulitumiwa na akina ndugu katika eneo hilo. Nilizaliwa Oktoba 15, 1926. Mnamo Machi 1940, nilichukua hatua ya kubatizwa kwenye kusanyiko huko Dover kwenye pwani ya Uingereza. Nikaja kuipenda kweli ya Biblia. Kwa kuwa Mama alikuwa Mkristo mtiwa-mafuta, ‘upindo wa nguo ya mtu aliye Myahudi’ nilioshika kwanza ulikuwa ule wa mama yangu. Wakati huo, baba na dada yangu mkubwa hawakuwa wakimtumikia Yehova. Tulishirikiana na Kutaniko la Gillingham lililoko kusini-mashariki mwa Uingereza, ambalo wengi wa washiriki wake walikuwa Wakristo watiwa-mafuta. Mama aliweka mfano mzuri wa bidii katika kazi ya kuhubiri.

Mnamo Septemba 1941, kwenye kusanyiko lililofanywa katika mji wa Leicester, hotuba yenye kichwa “Utimilifu” ilizungumzia suala la utawala wa ulimwenguni pote. Hotuba hiyo ilinisaidia kuelewa kwa mara ya kwanza kuwa tunahusika katika suala lililopo kati ya Yehova na Shetani. Hivyo, tunahitaji kusimama upande wa Yehova na kudumisha utimilifu wetu kwake akiwa Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote.

Katika kusanyiko hilo, utumishi wa painia ulikaziwa sana, na vijana walitiwa moyo wawe na lengo la kuwa mapainia. Hotuba yenye kichwa “Sehemu ya Painia Katika Tengenezo” ilinifanya nijiulize, ‘Mimi nina sehemu gani?’ Nilisadikishwa katika kusanyiko hilo kwamba nikiwa Myonadabu jukumu langu ni kuisaidia jamii ya watiwa-mafuta katika kazi ya kuhubiri kwa kadiri ya uwezo wangu. Nilijaza fomu ya kuwa painia nikiwa palepale Leicester.

UTUMISHI WA PAINIA WAKATI WA VITA

Niliwekwa rasmi kuwa painia wa pekee nikiwa na umri wa miaka 15, mnamo Desemba 1, 1941. Mama alikuwa mwandamani wangu wa kwanza katika utumishi wa upainia, lakini baada ya karibu mwaka mmoja hivi, alihitaji kuacha utumishi wake wa upainia kwa sababu ya matatizo ya afya. Kisha, ofisi ya tawi ya London ikanipa mwandamani mwingine, Ron Parkin, ambaye sasa anatumikia katika Halmashauri ya Tawi ya Puerto Riko.

Tulitumwa kwenye miji ya pwani ya Broadstairs na Ramsgate katika jimbo la Kent, ambako tulikodi chumba. Wakati huo rudishio la kila mwezi la painia wa pekee lilikuwa shilingi 40 (sawa na dola 8 za Marekani wakati huo). Hivyo, mara baada ya kulipa kodi ya chumba, tungebaki na kiasi kidogo cha pesa, na hivyo wakati mwingine hatungejua siku iliyofuata tungekula nini. Hata hivyo, kwa njia moja au nyingine, mara zote Yehova alituandalia mahitaji yetu.

Tulitumia sana baiskeli, tukijitahidi kuziendesha zikiwa na mizigo mikubwa dhidi ya upepo wenye nguvu uliokuwa ukitoka Bahari ya Kaskazini. Pia, tulihitaji kukabiliana na mashambulizi ya angani na makombora ya V-1 ya Ujerumani yaliyokuwa yakirushwa chinichini juu ya mji wa Kent ili kupiga jiji la London. Pindi mmoja nililazimika kuruka kutoka kwenye baiskeli na kujitupa ndani ya mtaro wakati bomu lilipopita juu ya kichwa changu na kulipuka kwenye shamba lililokuwa karibu. Hata hivyo, tulifurahia sana miaka tuliyotumia kwa ajili ya upainia huko Kent.

NINAKUWA “KIJANA WA BETHELI”

Mara nyingi mama yangu alizungumza kwa msisimko kuhusu Betheli. Alikuwa akisema hivi: “Sina jambo lingine bora zaidi ninalotamani kuliko wewe kuwa kijana wa Betheli.” Hivyo, wazia shangwe na mshangao wangu wakati nilipopokea mwaliko wa kutumikia Betheli huko London ili kusaidia kazi kwa majuma matatu mnamo Januari 1946. Mwishoni mwa majuma hayo, Pryce Hughes, mtumishi wa ofisi ya tawi, aliniomba nibaki Betheli. Mazoezi niliyopata Betheli yamenisaidia katika maisha yangu yote.

Wakati huo kulikuwa na washiriki 30 hivi katika Betheli ya London, wengi wakiwa ndugu waseja lakini pia ndugu kadhaa watiwa-mafuta, kutia ndani Pryce Hughes, Edgar Clay, na Jack Barr, ambaye baadaye alikuja kuwa mshiriki wa Baraza Linaloongoza. Lilikuwa pendeleo kubwa kama nini kuwasaidia ndugu za Kristo kwa kufanya kazi nikiwa kijana chini ya mwelekezo wa kiroho wa “nguzo” hizo!—Gal. 2:9.

Siku moja nikiwa Betheli, ndugu fulani aliniambia kuwa kuna dada kwenye mlango wa mbele ambaye alitaka kuniona. Nilishangaa nilipomwona mama yangu akiwa na mzigo mkononi mwake. Mama alisema kwamba hangeweza kuingia ndani ili asivuruge kazi yangu, lakini akanipa mzigo na kuondoka. Ndani ya mzigo huo kulikuwa na koti la majira ya baridi. Kitendo hicho cha upendo kilinikumbusha jinsi Hana alivyokuwa akimpelekea koti mwana wake mdogo Samweli alipokuwa akitumikia kwenye maskani.—1 Sam. 2:18, 19.

GILEADI—JAMBO AMBALO SITASAHAU

Mwaka wa 1947, ndugu na dada watano tuliokuwa tukifanya kazi Betheli tulipata mwaliko wa kuhudhuria Shule ya Gileadi huko Marekani, na mwaka uliofuata tulihudhuria darasa la 11. Tulipowasili, kulikuwa na baridi kali sana katika eneo la kaskazini ya New York, mahali ambapo shule hiyo ilikuwa. Jinsi nilivyofurahi kuwa na lile koti ambalo mama yangu alinipatia!

Sitasahau ile miezi sita ambayo niliitumia nikiwa Gileadi. Kuchangamana na wanafunzi wenzangu waliotoka katika nchi tofauti-tofauti 16 kulipanua mtazamo wangu. Zaidi ya manufaa ya kiroho niliyopata kutokana na mambo niliyojifunza Gileadi, nilifaidika na ushirika wa Wakristo wakomavu. Mmoja wa Wakristo hao alikuwa mwanafunzi mwenzangu Lloyd Barry; na pia mmoja wa walimu, Albert Schroeder; na vilevile John Booth, mwangalizi wa Shamba la Ufalme (mahali ambako Shule ya Gileadi ilikuwa) baadaye wote hao walikuja kuwa washiriki wa Baraza Linaloongoza. Ninathamini sana shauri lenye upendo ambalo ndugu hao walinipa na kielelezo chao kizuri cha ushikamanifu kwa Yehova na tengenezo lake.

KAZI YA MZUNGUKO NA KURUDI TENA BETHELI

Baada tu ya kumaliza Shule ya Gileadi, nilipewa mgawo wa kuwa mwangalizi wa mzunguko katika jimbo la Ohio, Marekani. Nilikuwa na miaka 21 tu, lakini akina ndugu walikubali kwa uchangamfu shauku yangu ya ujana. Katika mzunguko huo, nilijifunza mengi kutoka kwa ndugu wenye umri mkubwa na uzoefu mwingi.

Baada ya miezi michache, niliombwa nirudi Betheli ya Brooklyn kwa ajili ya mazoezi zaidi. Wakati huo nilikuja kufahamiana na nguzo kama vile Milton Henschel, Karl Klein, Nathan Knorr, T. J. (Bud) Sullivan, na Lyman Swingle, wote hao walitumika pindi fulani katika Baraza Linaloongoza. Lilikuwa jambo lenye kujenga sana kuwaona akina ndugu hao wakifanya kazi na kuona jinsi walivyoshughulikia mambo kwa njia ya Kikristo. Uhakika wangu kuelekea tengenezo la Yehova uliimarika sana. Kisha nikatumwa tena Ulaya kuendelea na utumishi wangu huko.

Mama yangu alikufa Februari 1950. Baada ya mazishi, niliongea waziwazi na baba na dada yangu, Dora. Niliwauliza kwa kuwa sasa Mama amekufa na mimi nimeondoka nyumbani wamekusudia kufanya nini kuhusu kweli? Walimjua na kumheshimu ndugu fulani mzee mtiwa-mafuta, Harry Browning, na wakakubali kuzungumza naye kuhusu kweli. Baada ya mwaka mmoja hivi, Baba na Dora wakabatizwa. Baadaye, Baba aliwekwa rasmi kuwa mtumishi wa Kutaniko la Gillingham. Baada ya kifo cha Baba, Dora alifunga ndoa na mzee mwaminifu, Roy Moreton, na akamtumikia Yehova kwa ushikamanifu hadi alipokufa mwaka wa 2010.

KUSAIDIA KAZI HUKO UFARANSA

Nikiwa shuleni, nilijifunza Kifaransa, Kijerumani, na Kilatini, na kati ya lugha hizo tatu, Kifaransa ndiyo iliyokuwa lugha ngumu zaidi kwangu. Hivyo, nilichanganyikiwa nilipoombwa niende kusaidia kazi Betheli ya Paris nchini Ufaransa. Nikiwa huko, nilipata pendeleo la kufanya kazi na mtumishi wa tawi Henri Geiger, ndugu mzee mtiwa-mafuta. Mgawo wangu haukuwa rahisi nyakati zote, na bila shaka nilifanya makosa mengi, lakini nilijifunza mengi kuhusu jinsi ya kushirikiana na wengine.

Zaidi ya hayo, kusanyiko la kwanza la kimataifa baada ya vita lilipangwa kufanyika huko Paris mwaka wa 1951, na nilishiriki katika kuliandaa. Léopold Jontès, ndugu kijana aliyekuwa mwangalizi anayesafiri, alikuja Betheli ili kunisaidia. Baadaye, Léopold aliwekwa rasmi kuwa mwangalizi wa tawi. Kusanyiko hilo lilifanyika Palais des sports, karibu na Mnara wa Eiffel. Wajumbe walitoka katika nchi 28. Siku ya mwisho ya kusanyiko, Mashahidi 6,000 wa Ufaransa walishangilia kuona hudhurio la watu 10,456!

Nilipofika Ufaransa kwa mara ya kwanza, sikujua vizuri Kifaransa. Jambo baya hata zaidi nililofanya lilikuwa kuzungumza lugha hiyo wakati tu nilipokuwa na uhakika kwamba Kifaransa changu ni sahihi. Lakini ikiwa hukosei, hutarekebishwa na hutafanya maendeleo.

Niliamua kurekebisha hali hiyo kwa kujiandikisha katika shule ambayo ilifundisha Kifaransa kwa wageni. Nilihudhuria masomo pindi za jioni wakati ambao hakukuwa na mikutano. Nilianza kupenda lugha ya Kifaransa, na tangu wakati huo nimezidi kuipenda lugha hiyo. Hilo limethibitika kuwa msaada mkubwa kwani nimeweza kusaidia tawi la Ufaransa katika kazi ya kutafsiri. Baadaye, nikawa mtafsiri, nikitafsiri kutoka Kiingereza kwenda Kifaransa. Lilikuwa pendeleo kuwatafsiria ndugu wanaozungumza Kifaransa duniani pote chakula bora cha kiroho kinachoandaliwa na jamii ya mtumwa.—Mt. 24:45-47.

NDOA NA MAPENDELEO ZAIDI

Mwaka wa 1956, nilifunga ndoa na Esther, painia Mswisi ambaye nilikutana naye miaka kadhaa mapema. Tulifunga ndoa kwenye Jumba la Ufalme lililo karibu na Betheli ya London (London Tabernacle ya zamani, mahali ambapo mama yangu alibatizwa). Ndugu Hughes alitoa hotuba ya ndoa. Mama ya Esther alikuwepo, yeye pia alikuwa na tumaini la kwenda mbinguni. Si kwamba ndoa yangu ilinipa mwenzi mpendwa na mshikamanifu tu, bali pia imenipa wakati mwingi wa ushirika wenye thamani pamoja na mama mkwe wangu mwenye mtazamo wa kiroho hadi alipomaliza mwendo wake wa kidunia mwaka wa 2000.

Baada ya harusi yetu, mimi na Esther tuliishi nje ya Betheli. Niliendelea kutafsiri kwa ajili ya Betheli na Esther alitumikia akiwa painia wa pekee kwenye viunga vya jiji la Paris. Aliweza kuwasaidia watu kadhaa wawe watumishi wa Yehova. Mwaka wa 1964 tulialikwa Betheli. Kisha mwaka wa 1976, wakati mpango wa Halmashauri za Tawi ulipoanzishwa, niliwekwa rasmi kuwa mshiriki wa Halmashauri ya Tawi. Kwa miaka mingi, Esther ameniunga mkono kwa upendo.

“HAMTAKUWA PAMOJA NAMI SIKUZOTE”

Nimekuwa na pendeleo la kurudi mara kadhaa kwenye makao makuu huko New York. Wakati wa ziara hizo, nimepokea mashauri mazuri kutoka kwa washiriki mbalimbali wa Baraza Linaloongoza. Kwa mfano, wakati mmoja nilipoeleza wasiwasi wangu kuhusu kutimiza kazi fulani kwa wakati, Ndugu Knorr alitabasamu na kusema: “Usijali. Fanya kazi!” Tangu wakati huo, kazi zinaporundamana, badala ya kuhangaika, mimi hufanya kazi moja baada ya nyingine na kuzikamilisha, mara nyingi kwa wakati.

Muda mfupi kabla ya kifo chake, Yesu aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Hamtakuwa pamoja nami sikuzote.” (Mt. 26:11) Sisi washiriki wa kondoo wengine pia tunajua kwamba hatutakuwa na ndugu watiwa-mafuta wa Kristo pamoja nasi siku zote hapa duniani. Hivyo, naliona kuwa pendeleo kubwa kushirikiana kwa zaidi ya miaka 70 na wengi wa watiwa-mafuta—nikishikilia kwa uthamini upindo wa nguo ya mtu aliye Myahudi.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 5 Kwa ufafanuzi wa jina “Yonadabu,” ona kitabu Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu, ukurasa wa 83, 165, 166.

[Blabu katika ukurasa wa 21]

Ndugu Knorr alitabasamu na kusema: “Usijali. Fanya kazi!”

[Picha katika ukurasa wa 19]

(Kushoto) Mama na baba yangu

(Kulia) Nikiwa Shule ya Gileadi mwaka 1948, nimevaa koti la majira ya baridi ambalo Mama alinipa

[Picha katika ukurasa wa 20]

Nikitafsiri hotuba ya Ndugu Lloyd Barry wakati wa kuwekwa wakfu kwa ofisi ya tawi ya Ufaransa, 1997

[Picha katika ukurasa wa 21]

(Kushoto) Nikiwa na Esther siku tuliyofunga ndoa

(Kulia) Tukiwa pamoja katika kazi ya kuhubiri