Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Yehova Anajua Jinsi ya Kuwakomboa Watu Wake

Yehova Anajua Jinsi ya Kuwakomboa Watu Wake

Yehova Anajua Jinsi ya Kuwakomboa Watu Wake

“Yehova anajua jinsi ya kuwakomboa watu wenye ujitoaji-kimungu kutoka katika jaribu.”—2 PET. 2:9.

KWA NINI TUNAWEZA KUWA NA HAKIKA KWAMBA YEHOVA:

Anajua wakati wa kutimizwa kwa matukio fulani ili atimize kusudi lake?

Atatumia nguvu zake kuingilia kati ili kuwaokoa watu wake?

Anajua jinsi matukio ya mwisho yatakavyofikia upeo wake?

1. Hali zitakuwaje ulimwenguni wakati wa ile “dhiki kuu”?

KUTEKELEZWA kwa hukumu ya Mungu juu ya ulimwengu wa Shetani kutatukia kwa ghafula. (1 The. 5:2, 3) “Ile siku kuu ya Yehova” inapoanza, jamii ya wanadamu itakuwa katika machafuko makubwa. (Sef. 1:14-17) Hali ngumu na shida zitakuwa kila mahali. Huo utakuwa wakati wa taabu “ambayo haijapata kutukia tangu mwanzo wa ulimwengu mpaka sasa.”—Soma Mathayo 24:21, 22.

2, 3. (a) Watu wa Mungu watakabili nini wakati wa ile “dhiki kuu”? (b) Ni nini kinachoweza kutuimarisha kwa ajili ya mambo yatakayotukia wakati ujao?

2 “Dhiki kuu” inapoelekea upeo wake, watu wa Mungu watakuwa shabaha ya mashambulizi makali ya “Gogu wa nchi ya Magogu.” Wakati wa mashambulizi hayo, “jeshi kubwa sana” litakuja dhidi ya watu wa Mungu “kama mawingu ili kuifunika nchi.” (Eze. 38:2, 14-16) Hakuna tengenezo la kibinadamu litakalowalinda watu wa Yehova. Wokovu wao utategemea Mungu peke yake. Watu wa Mungu watatendaje maadui wao watakapojaribu kuwaangamiza?

3 Ikiwa wewe ni mtumishi wa Yehova, je, una imani kwamba Yehova anaweza na atawalinda watu wake ili waokoke ile dhiki kuu? Mtume Petro aliandika hivi: “Yehova anajua jinsi ya kuwakomboa watu wenye ujitoaji-kimungu kutoka katika jaribu, lakini kuwaweka akiba watu wasio waadilifu kwa ajili ya ile siku ya hukumu ili wakatiliwe mbali.” (2 Pet. 2:9) Kutafakari juu ya matendo ya Yehova ya ukombozi ya wakati uliopita kunaweza kutuimarisha kwa ajili ya mambo yatakayotukia wakati ujao. Acheni tuchunguze mifano mitatu ambayo itatuchochea kuwa na uhakika katika uwezo wa Yehova wa kuwakomboa watu wake.

KUOKOKA GHARIKA YA ULIMWENGUNI POTE

4. Kwa nini wakati ulikuwa jambo muhimu kuhusiana na Gharika?

4 Kwanza, tuchunguze simulizi la Gharika ya siku za Noa. Ili mapenzi ya Yehova yatimizwe, lilikuwa jambo la muhimu kuzingatia wakati. Kazi kubwa ya kujenga safina ilipaswa kukamilishwa na wanyama walipaswa kuingizwa mahali salama ndani ya safina kabla ya mvua kubwa kuanza kunyesha. Simulizi la kitabu cha Mwanzo halisemi kwamba Yehova alingojea mpaka ujenzi wa safina ukamilike ndipo aamue lini Gharika ingeanza. Badala yake, kabla ya kumwambia Noa jambo lolote kuhusu kujenga safina, Mungu aliamua ni wakati gani hususa ambao Gharika ingeanza. Tunajuaje hilo?

5. Yehova alisema nini katika tangazo lililorekodiwa katika Mwanzo 6:3, na tangazo hilo lilitolewa wakati gani?

5 Biblia inatuambia kwamba Yehova alitoa tangazo mbinguni. Kulingana na Mwanzo 6:3, Yehova alisema hivi: “Roho yangu haitavumiliana sikuzote na mwanadamu kwa kuwa yeye pia ni mwili. Kwa hiyo siku zake zitakuwa miaka 120.” Yehova hakuwa akizungumza kuhusu urefu wa maisha ambao watu kwa ujumla wangeishi, badala yake, Yehova alikuwa akizungumza kuhusu wakati ambao angeondoa uovu wote duniani. * Kwa kuwa Gharika ilianza mwaka wa 2370 K.W.K., tunaweza kusema kwamba Mungu alitoa tangazo hilo katika mwaka wa 2490 K.W.K. Wakati huo, Noa alikuwa na umri wa miaka 480. (Mwa. 7:6) Miaka 20 hivi baadaye, katika mwaka wa 2470 K.W.K., Noa alianza kuzaa wana. (Mwa. 5:32) Miaka mia moja hivi ilikuwa imebaki kabla ya Gharika kuanza, lakini Yehova alikuwa hajamfunulia Noa daraka la pekee ambalo angetimiza ili kuhifadhi familia ya kibinadamu. Mungu angengojea muda gani kabla ya kumweleza Noa?

6. Ni lini Yehova alipomwamuru Noa ajenge safina?

6 Inaelekea Yehova alingojea makumi ya miaka kabla ya kumfunulia Noa yale ambayo Alikusudia kufanya. Tunafikia mkataa huo kwa msingi gani? Biblia inaonyesha kwamba wana wa Noa walikuwa tayari watu wazima na walikuwa wameoa Mungu alipomwamuru Noa ajenge safina. Yehova alimwambia Noa hivi: “Ninafanya agano langu pamoja nawe; nawe uingie ndani ya safina, wewe na wana wako na mke wako na wake za wana wako pamoja nawe.” (Mwa. 6:9-18) Kwa hiyo, inawezekana kwamba Noa alipopewa kazi ya kujenga safina, miaka 40 au 50 tu ilikuwa imebaki kabla ya Gharika.

7. (a) Noa na familia yake walionyeshaje imani? (b) Ni lini hatimaye Mungu alimwambia Noa wakati hususa ambao Gharika ingeanza?

7 Kazi ya kujenga safina ilipokuwa ikiendelea, huenda Noa na familia yake walikuwa wakijiuliza ni kwa jinsi gani Mungu angetimiza kusudi lake na ni lini Gharika ingeanza. Hata hivyo, kutojua kwao habari hizo hakukuwazuia kujenga safina. Maandiko yanasema hivi: “Noa akafanya kulingana na yote ambayo Mungu alikuwa amemwamuru. Alifanya vivyo hivyo.” (Mwa. 6:22) Siku saba kabla ya Gharika kuanza, muda ambao ungeweza kutosha kwa Noa na familia yake kuingiza wanyama ndani ya safina, hatimaye Yehova alimwambia Noa wakati hususa ambao Gharika ingeanza. Kwa hiyo, malango ya mbinguni yalipofunguliwa “katika mwaka wa mia sita wa maisha ya Noa, mwezi wa pili, siku ya kumi na saba ya mwezi,” kila kitu kilikuwa tayari.—Mwa. 7:1-5, 11.

8. Simulizi la Gharika linatusaidiaje kuwa na hakika kwamba Yehova anajua wakati wa kuwakomboa watu wake?

8 Simulizi hilo kuhusu Gharika linathibitisha uwezo wa Yehova wa kuwa si Mtunza-Wakati tu, bali pia Mkombozi. Tunapokaribia mwisho wa mfumo huu wa mambo, tunaweza kuwa na uhakika kwamba kila kitu ambacho Yehova amekusudia kitatimia kwa wakati uliowekwa, kwa ‘siku na saa’ aliyoamua.—Mt. 24:36; soma Habakuki 2:3.

WALIKOMBOLEWA KWENYE BAHARI NYEKUNDU

9, 10. Yehova aliwatumiaje watu wake kama chambo ili kuyanasa majeshi ya Misri katika mtego?

9 Kufikia hapa, tumeona kwamba Yehova anajua kikamili wakati wa kutimizwa kwa matukio fulani ili atimize kusudi lake. Mfano wa pili tutakaochunguza unakazia sababu nyingine inayoonyesha kwa nini tunaweza kuamini kwamba Yehova atawakomboa watu wake: Atatumia nguvu zake zisizo na mipaka ili kuhakikisha kwamba mapenzi yake yanatimia. Uwezo wa Yehova wa kuwakomboa watumishi wake ni hakika kwa kuwa nyakati nyingine amewatumia watumishi wake kama chambo ili kuwanasa maadui wake katika mtego. Hivyo ndivyo ilivyokuwa alipowaweka Waisraeli huru kutoka katika utumwa wa Wamisri.

10 Waisraeli walioondoka Misri huenda walikuwa watu milioni tatu hivi. Yehova alimwamuru Musa awaongoze Waisraeli katika njia ambayo ilimfanya Farao afikiri kwamba walikuwa wamepotea njia na kuvurugika. (Soma Kutoka 14:1-4.) Hivyo, akiwa na majeshi yake Farao aliwafuata na kuwanasa watumwa wake hao wa zamani kwenye Bahari Nyekundu. Ilionekana kana kwamba hapakuwa na njia ya kuponyokea. (Kut. 14:5-10) Hata hivyo, Waisraeli kwa kweli hawakuwa katika hatari yoyote. Kwa nini? Kwa sababu Yehova alikuwa karibu kuingilia kati ili kuwaokoa.

11, 12. (a) Yehova aliingilia kati jinsi gani ili kuwaokoa watu wake? (b) Kulikuwa na matokeo gani Mungu alipoingilia kati, na simulizi hilo linatufundisha nini kumhusu Yehova?

11 “Nguzo ya wingu” iliyokuwa ikiwaongoza Waisraeli ilirudi ikawa nyuma yao, ikayazuia majeshi ya Farao yasiwakaribie na kufanya majeshi hayo yawe katika giza. Hata hivyo, kwa upande wa Waisraeli, nguzo hiyo ilitoa nuru kimuujiza usiku. (Soma Kutoka 14:19, 20.) Kisha, Yehova akaigawa bahari mara mbili kwa kutumia upepo wenye nguvu wa mashariki, na hivyo “kuligeuza bonde la bahari liwe nchi kavu.” Bila shaka, jambo hilo lilichukua muda fulani, kwa sababu simulizi linasema hivi: “Mwishowe wana wa Israeli wakapita katikati ya bahari juu ya nchi kavu.” Waisraeli walikuwa wakitembea polepole wakilinganishwa na wanajeshi wa Farao waliokuwa ndani ya magari yao ya vita. Hata hivyo, hapakuwa na uwezekano wowote wa kwamba Wamisri wangewafikia kwa sababu Yehova alikuwa anawapigania Waisraeli. Yehova “akaivuruga kambi ya Wamisri. Naye akawa akiyaondoa magurudumu kutoka kwenye magari yao hivi kwamba wakawa wakiyaendesha kwa shida.”—Kut. 14:21-25.

12 Mara tu Waisraeli wote walipokuwa salama upande ule mwingine wa bahari, Yehova alimwambia Musa: “Unyooshe mkono wako juu ya bahari, ili maji yarudi juu ya Wamisri, magari yao ya vita na askari wao wapanda-farasi.” Wanajeshi wa Misri walipokuwa wakijaribu kukimbia maji yaliyokuwa yakirudi haraka juu yao, “Yehova akawakung’uta Wamisri katikati ya bahari.” Haikuwezekana kwa Wamisri kuponyoka. “Hakuna hata mmoja kati yao aliyebaki.” (Kut. 14:26-28) Hivyo, Yehova alionyesha kwamba ana nguvu za kuwakomboa watu wake katika hali yoyote ile.

KUPONYOKA UHARIBIFU WA YERUSALEMU

13. Yesu alitoa maagizo gani, na huenda wafuasi wake walijiuliza nini?

13 Yehova anajua ni namna gani hasa matukio yatakavyoanza ili kutimiza kusudi lake. Umuhimu wa jambo hilo unakaziwa katika mfano wa tatu ambao tutachunguza: kuzingirwa kwa Yerusalemu katika karne ya kwanza. Kupitia Mwana wake, Yehova aliandaa maagizo ya jinsi ya kuokoka kwa ajili ya Wakristo waliokuwa wakiishi Yerusalemu na Yudea kabla ya uharibifu wa jiji hilo katika mwaka wa 70 W.K. Yesu alisema hivi: “Mtakapoona lile chukizo linalosababisha ukiwa, kama vile lilivyosemwa kupitia nabii Danieli, likiwa limesimama katika mahali patakatifu,  . . . ndipo wale walio katika Yudea waanze kukimbilia milimani.” (Mt. 24:15, 16) Lakini wafuasi wa Yesu wangetambuaje wakati ambao unabii huo ungetimia?

14. Ni mambo gani yaliyotukia ambayo yalifanya maana ya maagizo ya Yesu yawe wazi zaidi?

14 Matukio yalipoanza, maana ya maneno ya Yesu yalianza kuwa wazi. Katika mwaka wa 66 W.K., majeshi ya Roma yakiongozwa na Sesho Galo yalifika Yerusalemu ili kuzima uasi wa Wayahudi. Wakati waasi Wayahudi, walioitwa Wazeloti, walipokimbilia ndani ya ngome ya hekalu, wanajeshi wa Roma walianza kubomoa ukuta wa hekalu. Wakristo waliokuwa macho walielewa kikamili maana ya mambo yote hayo: Jeshi la kipagani lililobeba sanamu zake (“lile chukizo”) liliukaribia ukuta wa hekalu (“mahali patakatifu”). Huo ulikuwa wakati kwa wafuasi wa Yesu ‘kuanza kukimbilia milimani.’ Lakini wangeondokaje katika jiji ambalo lilikuwa limezingirwa? Mambo fulani yasiyotazamiwa yalikuwa karibu kutukia.

15, 16. (a) Ni maagizo gani hususa ambayo Yesu alitoa, na kwa nini ilikuwa muhimu kwa wafuasi wake kuyatii? (b) Ukombozi wetu utategemea nini?

15 Inashangaza kwamba bila sababu yoyote ile, Sesho Galo na vikosi vyake waliondoka Yerusalemu na kuanza kurudi Roma. Wazeloti waliwafuata na kuwakimbiza. Sasa kwa kuwa Waroma na Wayahudi waasi walikuwa wametoka jijini, kwa ghafula wafuasi wa Yesu walikuwa na fursa ya kukimbia. Yesu alikuwa amewaagiza waziwazi wafuasi wake kutoka bila kukawia na kuacha vitu vyao vya kimwili. (Soma Mathayo 24:17, 18.) Je, kwa kweli ilikuwa lazima kutenda kwa haraka hivyo? Punde si punde, jibu lilikuwa wazi. Baada ya siku kadhaa, Wazeloti walirudi na kuanza kuwalazimisha wakaaji wa Yerusalemu na Yudea wajiunge nao katika uasi. Hali iliharibika haraka jijini wakati vikundi vya Wayahudi wenye kupingana vilianza kupambana ili kudhibiti jiji. Haikuwa rahisi kukimbia. Waroma waliporudi mwaka wa 70 W.K., haikuwezekana kukimbia kutoka Yerusalemu. (Luka 19:43) Mtu yeyote ambaye alisita-sita kutoka jijini alinaswa! Kuhusu Wakristo waliokimbilia milimani, kutii maagizo ya Yesu kuliokoa maisha yao. Walijionea wenyewe kwamba Yehova anajua jinsi ya kuwakomboa watu wake. Ni somo gani tunaloweza kujifunza kutokana na simulizi hilo?

16 Matukio yatakapoanza wakati wa dhiki kuu, Wakristo watahitaji kutii maagizo kutoka katika Neno la Mungu na tengenezo. Kwa mfano, amri ya Yesu ya ‘kuanza kukimbilia milimani’ ina maana katika siku zetu. Hadi sasa haijulikani jinsi hasa tutakavyokimbia. * Hata hivyo, tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova atafunua wazi maana ya maagizo hayo wakati utakapofika ili tuweze kuyafuata. Kwa kuwa ukombozi wetu utategemea utii wetu, ni vizuri tujiulize: ‘Je, ninatii maagizo ambayo Yehova anatoa kwa watu wake sasa? Je, ninatii mara moja au ninasita-sita?’—Yak. 3:17.

TUNAIMARISHWA KWA AJILI YA MAMBO YATAKAYOTUKIA WAKATI UJAO

17. Unabii wa Habakuki unafunua nini kuhusu mashambulizi yanayokuja dhidi ya watu wa Mungu?

17 Acheni sasa tuzungumze kuhusu mashambulizi ya Gogu yaliyotajwa mwanzoni mwa habari hii. Katika unabii unaofanana na huo, Habakuki alisema hivi: “Nilisikia, tumbo langu likaanza kutetemeka; midomo yangu ilitetemeka kwa sababu ya ule mvumo; kuoza kukaanza kuingia katika mifupa yangu; na katika hali yangu nikafadhaika, kwamba ningojee kimya siku ya taabu, kuja [kwa majeshi yenye kutisha ya Mungu] kwa watu, apate kuwavamia.” (Hab. 3:16) Kusikia tu ripoti juu ya mashambulizi yanayokuja dhidi ya watu wa Mungu kulifanya tumbo la nabii huyo kuanza kusukasuka, midomo yake kutetemeka, na mwili wake kudhoofika. Woga wa Habakuki unaonyesha jinsi hali yetu itakavyoonekana kuwa ngumu wakati majeshi ya Gogu yatakapotushambulia. Hata hivyo, nabii huyo alikuwa tayari kungoja kwa utulivu siku kuu ya Yehova, akiwa na uhakika kwamba Yehova angewakomboa watu wake. Tunaweza kuwa na uhakika kama huo.—Hab. 3:18, 19.

18. (a) Kwa nini hatuna sababu ya kuogopa mashambulizi yanayokuja? (b) Tutachunguza nini katika makala inayofuata?

18 Mifano mitatu ambayo tumechunguza inaonyesha bila shaka kwamba Yehova anajua jinsi ya kuwakomboa watu wake. Kusudi lake haliwezi kukosa kutimia; ushindi ni hakika. Hata hivyo, ili tushiriki katika ushindi huo, ni lazima tubaki waaminifu hadi mwisho. Yehova anatusaidiaje leo kudumisha utimilifu wetu? Tutachunguza habari hiyo katika makala inayofuata.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 5 Ona gazeti la Mnara wa Mlinzi la Desemba 15, 2010, ukurasa wa 30-31.

^ fu. 16 Ona gazeti la Mnara wa Mlinzi la Mei 1, 1999, ukurasa wa 19.

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 24]

Je, Waisraeli walikuwa katika hatari yoyote ile kutokana na majeshi ya Farao?