Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Yehova Hutulinda ili Kutuokoa

Yehova Hutulinda ili Kutuokoa

Yehova Hutulinda ili Kutuokoa

‘Mnalindwa kwa nguvu za Mungu kupitia imani kwa ajili ya wokovu ulio tayari kufunuliwa katika kipindi cha mwisho cha wakati.’—1 PET. 1:4, 5.

UNGEJIBUJE?

Yehova alituvuta jinsi gani kwenye ibada ya kweli?

Tunaweza kumruhusu Yehova jinsi gani atuongoze kupitia mashauri yake?

Yehova anatupatia kitia-moyo jinsi gani?

1, 2. (a) Ni uhakikisho gani tulionao kwamba Mungu atatusaidia tudumishe utimilifu wetu? (b) Yehova anamjua vizuri kila mmoja wetu jinsi gani?

“YULE ambaye atavumilia mpaka mwisho ndiye atakayeokolewa.” (Mt. 24:13) Kwa maneno hayo, Yesu alionyesha wazi kwamba ili tuokolewe wakati Mungu atakapotekeleza hukumu yake juu ya ulimwengu wa Shetani, ni lazima tudumishe utimilifu wetu hadi mwisho. Lakini hilo halimaanishi kwamba Yehova anatutazamia tuvumilie kwa hekima au nguvu zetu wenyewe. Biblia inatuhakikishia hivi: “Mungu ni mwaminifu, naye hatawaacha ninyi mjaribiwe kupita mnavyoweza kuhimili, bali pamoja na hilo jaribu ataifanya pia njia ya kutokea kusudi mweze kulivumilia.” (1 Kor. 10:13) Maneno hayo yanamaanisha nini?

2 Ili Yehova ahakikishe kwamba hatujaribiwi kupita tunavyoweza kuhimili, anahitaji kujua kila kitu kutuhusu, kutia ndani matatizo tunayokabili, hali yetu tukiwa mtu mmojammoja, na uwezo wetu wa kuvumilia majaribu. Je, kweli Mungu anatujua vizuri kadiri hiyo? Ndiyo. Maandiko yanafunua kwamba Yehova anamjua kila mmoja wetu kwa undani sana. Anajua tabia yetu na mambo tunayofanya kila siku. Anaweza kutambua hata mawazo na makusudi ya moyo wetu.—Soma Zaburi 139:1-6.

3, 4. (a) Ni kwa jinsi gani jambo lililompata Daudi linaonyesha kwamba Yehova anamkazia uangalifu mtu mmojammoja? (b) Yehova anatimiza kazi gani ya ajabu leo?

3 Je, kweli inawezekana kwamba Mungu anaweza kupendezwa kwa kiasi hicho na wanadamu wa hali ya chini? Mtunga-zaburi Daudi alitafakari kuhusu swali hilo alipomwambia Yehova hivi: “Ninapoziona mbingu zako, kazi za vidole vyako, mwezi na nyota ambazo umetayarisha, mwanadamu anayeweza kufa ni nini hivi kwamba umweke akilini?” (Zab. 8:3, 4) Huenda Daudi aliuliza swali hilo kutokana na jambo lililompata yeye mwenyewe. Yehova alipomtazama mwana mdogo wa Yese, alikuwa amempata “mtu anayekubalika kwa moyo wake” na akamchukua ili ‘aache kufuata kundi na awe kiongozi’ juu ya Israeli. (1 Sam. 13:14; 2 Sam. 7:8) Hebu wazia jinsi ambavyo Daudi alihisi alipogundua kwamba Muumba wa ulimwengu wote mzima alikuwa amekazia fikira kutafakari kwake, yaani, mawazo ya mvulana mchungaji!

4 Upendezi wa kibinafsi ambao Yehova anatuonyesha leo ni wenye kushangaza pia. Anavikusanya pamoja katika ibada ya kweli “vitu vyenye kutamanika vya mataifa yote,” na anawasaidia watumishi wake wadumishe utimilifu wao. (Hag. 2:7) Ili kuelewa vizuri jinsi ambavyo Yehova anatusaidia kudumisha utimilifu wetu, acheni kwanza tufikirie jinsi anavyowavuta watu katika ibada ya kweli.

KUVUTWA NA MUNGU

5. Yehova anawavutaje watu kwa Mwana wake? Toa mfano.

5 Yesu alisema hivi: “Hakuna mtu anayeweza kuja kwangu isipokuwa Baba, aliyenituma, amvute.” (Yoh. 6:44) Maneno hayo yanadokeza kwamba ili tuwe mwanafunzi wa Kristo, tunahitaji msaada wa Mungu. Yehova anawavutaje watu wenye mfano wa kondoo kwa Mwana wake? Ni kupitia kuhubiriwa kwa habari njema na utendaji wa roho takatifu. Kwa mfano, wakati Paulo na wamishonari wenzake walipokuwa huko Filipi, walikutana na mwanamke anayeitwa Lidia na wakaanza kumhubiria habari njema. Maandiko yaliyoongozwa na roho ya Mungu yanasema hivi: “Yehova akafungua wazi moyo wake asikilize kwa makini mambo yaliyokuwa yakisemwa na Paulo.” Naam, Mungu alitoa roho yake ili kumsaidia Lidia aelewe maana ya ujumbe, matokeo ni kwamba yeye pamoja na nyumba yake wakabatizwa.—Mdo. 16:13-15.

6. Sote tulivutwa na Mungu kwenye ibada ya kweli jinsi gani?

6 Je, jambo hilo lilitokea katika kisa cha Lidia tu? Bila shaka, la. Ikiwa wewe ni Mkristo uliyejiweka wakfu, wewe pia ulivutwa na Mungu kwenye ibada ya kweli. Kama vile tu Baba yetu wa mbinguni alivyoona kitu fulani chenye thamani katika moyo wa Lidia, ndivyo alivyoona pia kitu fulani kizuri ndani yako. Ulipoanza kusikiliza habari njema, Yehova alikusaidia kuielewa kwa kukupa roho yake takatifu. (1 Kor. 2:11, 12) Ulipokuwa ukijitahidi kutumia yale uliyojifunza, alibariki jitihada zako za kufanya mapenzi yake. Ulipoweka maisha yako wakfu kwake, moyo wake ulishangilia. Kwa kweli, tangu ulipoanza kutembea kwenye njia hii inayoelekea kwenye uzima, Yehova amekuwa pamoja nawe katika kila hatua unayopiga.

7. Tunajuaje kwamba Mungu atatusaidia tubaki tukiwa waaminifu?

7 Kwa kuwa Yehova alitusaidia kuanza kutembea pamoja naye, hivyo tunaweza kuwa na uhakika kwamba ataendelea kutusaidia kubaki tukiwa waaminifu. Anajua kwamba kama vile ambavyo hatukuja katika kweli kwa nguvu zetu wenyewe, ndivyo tusivyoweza kuendelea kubaki katika kweli kwa nguvu zetu wenyewe. Akiwaandikia Wakristo watiwa-mafuta, mtume Petro alisema hivi: ‘Mnalindwa kwa nguvu za Mungu kupitia imani kwa ajili ya wokovu ulio tayari kufunuliwa katika kipindi cha mwisho cha wakati.’ (1 Pet. 1:4, 5) Kanuni ya maneno hayo inaweza kutumiwa kuwahusu Wakristo wote na inapaswa kutupendeza sote leo. Kwa nini? Kwa sababu, sote tunahitaji msaada wa Mungu ili tubaki tukiwa waaminifu kwake.

TUNALINDWA DHIDI YA KUCHUKUA HATUA ISIYOFAA

8. Kwa nini tunahitaji kuwa macho ili tusichukue hatua isiyofaa?

8 Mikazo ya maisha na hali yetu ya kutokamilika inaweza kutufanya tupoteze hali yetu ya kiroho na kutufanya tuchukue hatua isiyofaa bila hata sisi wenyewe kujua. (Soma Wagalatia 6:1.) Hilo linaonyeshwa na jambo lililompata Daudi katika maisha yake.

9, 10. Yehova alimzuiaje Daudi ili asichukue hatua isiyofaa, Naye anafanya nini kwa ajili yetu leo?

9 Alipokuwa akitafutwa na Mfalme Sauli, Daudi alionyesha uwezo wa ajabu wa kujizuia ili asilipize kisasi dhidi ya mtawala huyo mwenye wivu. (1 Sam. 24:2-7) Lakini muda mfupi baada ya hapo, Daudi alishindwa kujidhibiti. Alikuwa na uhitaji wa chakula kwa ajili ya wanaume waliokuwa pamoja naye na kwa heshima akamwomba Mwisraeli mwenzake aitwaye Nabali amsaidie. Wakati Nabali alipomjibu kwa matusi, Daudi alikasirika sana na akaamua kujilipizia kisasi kwa kuwaua wanaume wote katika nyumba ya Nabali, bila kutambua kwamba kuua watu wasio na hatia kungemfanya awe na hatia ya damu mbele za Mungu. Ni mara tu baada ya mke wa Nabali, Abigaili, kuingilia kati kwa wakati unaofaa ndipo Daudi alipoepushwa asifanye kosa hilo baya. Akitambua mwongozo wa Yehova katika jambo hilo, Daudi alisema hivi: “Abarikiwe Yehova Mungu wa Israeli, aliyekutuma leo unipokee! Busara yako na ibarikiwe, nawe ubarikiwe, ambaye umenizuia leo nisiingie katika hatia ya damu na kuacha mkono wangu mwenyewe uniokoe.”—1 Sam. 25:9-13, 21, 22, 32, 33.

10 Ni somo gani tunaloweza kujifunza kutokana na simulizi hilo? Yehova alimtumia Abigaili kumzuia Daudi asichukue hatua isiyofaa. Anafanya vivyo hivyo kwetu leo. Bila shaka, hatupaswi kutarajia Mungu amtume mtu fulani aingilie kati kila tunapokuwa karibu kukosea; wala hatujui kwa hakika jinsi ambavyo Mungu atatenda katika hali yoyote ile au kile atakachoruhusu kitupate ili kutimiza mapenzi yake. (Mhu. 11:5) Hata hivyo, tunaweza kuwa na uhakika kwamba mara zote Yehova anaelewa hali yetu na atatusaidia tubaki tukiwa waaminifu kwake. Anatuhakikishia hivi: “Nitakufanya uwe na ufahamu na kukufundisha katika njia unayopaswa kuiendea. Nitakupa shauri jicho langu likiwa linakutazama.” (Zab. 32:8) Yehova anatupa shauri jinsi gani? Shauri hilo linaweza kutunufaishaje? Na kwa nini tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova anawaongoza watu wake leo? Ona jinsi ambavyo maswali hayo yanajibiwa katika kitabu cha Ufunuo.

SHAURI HUTULINDA

11. Ni kwa kadiri gani Yehova anajua yale yanayotokea katika makutaniko ya watu wake?

11 Katika maono yaliyorekodiwa kwenye kitabu cha Ufunuo sura ya 2 na ya 3, Yesu Kristo aliyetukuzwa anayakagua makutaniko saba yaliyokuwa huko Asia Ndogo. Maono hayo yanafunua kwamba Kristo haoni mambo kwa ujumla tu bali anaona hali fulani hususa. Katika pindi nyingine, anawataja hata watu fulani, na katika kila kisa, anatoa pongezi zinazostahili au shauri. Hilo linaonyesha nini? Katika utimizo wa maono hayo, makutaniko saba yanawakilisha Wakristo watiwa-mafuta baada ya mwaka 1914, na shauri linalotolewa kwa makutaniko saba linayahusu pia makutaniko yote ya watu wa Mungu duniani pote leo. Hivyo, ni jambo la busara kukata maneno kwamba Yehova anawaongoza watu wake kwa bidii kupitia Mwana wake. Tunawezaje kunufaika kutokana na mwongozo huo?

12. Tunaweza kumruhusu Yehova aongoze hatua zetu jinsi gani?

12 Njia moja ambayo tunaweza kufaidika na mwongozo wenye upendo wa Yehova ni kupitia funzo la kibinafsi. Kupitia machapisho yanayotayarishwa na jamii ya mtumwa mwaminifu na mwenye busara, Yehova anatoa mashauri mengi yanayotegemea Maandiko. (Mt. 24:45) Hata hivyo, ili tufaidike, ni lazima tutenge wakati wa kujifunza na pia kutumia mambo hayo tunayojifunza. Funzo la kibinafsi ni njia mojawapo ambayo Yehova anaweza ‘kutulinda ili tusijikwae.’ (Yuda 24) Je, umewahi kujifunza jambo lolote kwenye machapisho yetu ambalo unaona kuwa liliandikwa kwa ajili yako? Kubali rekebisho hilo na kuliona kuwa linatoka kwa Yehova. Kama vile rafiki anayekushika bega ili kukueleza jambo fulani, Yehova anaweza kutumia roho yake kukusaidia kuelewa kwamba kuna jambo katika mwenendo au utu wako na bila shaka, utu na mwenendo wa wengine wengi kama wewe, unaohitaji marekebisho. Tunapokubali kuelekezwa na roho takatifu, tunamruhusu Yehova aongoze hatua zetu. (Soma Zaburi 139:23, 24.) Hivyo, ni jambo zuri kuchunguza mazoea yetu ya kujifunza.

13. Kwa nini ni jambo la busara kwetu kuchunguza mazoea yetu ya kujifunza?

13 Ikiwa tutatumia muda mrefu kwa ajili ya burudani, hatutakuwa na muda wa kutosha kwa ajili ya funzo la kibinafsi. Ndugu mmoja anasema hivi: “Ni rahisi sana kuacha wakati wa funzo la kibinafsi upite. Kuna burudani nyingi leo kuliko wakati mwingine wowote, na gharama yake ni ndogo kuliko wakati mwingine wowote. Burudani hiyo inapatikana kwenye televisheni, kwenye kompyuta na kwenye simu. Tunazungukwa na burudani.” Ikiwa hatutakuwa waangalifu tunaweza kuanza kutumia wakati mwingi zaidi katika burudani na hivyo hatua kwa hatua wakati tunaotumia kwa ajili ya funzo la kibinafsi lenye kina upungue na hatimaye ukosekane kabisa. (Efe. 5:15-17) Ni vizuri kila mmoja wetu akijiuliza hivi: ‘Ni mara ngapi mimi hutumia muda mwingi kusoma mambo yenye kina ya Neno la Mungu? Je, ni wakati tu ninapokuwa na hotuba au sehemu ya kutayarisha katika mikutano?’ Ikiwa ndivyo, labda tunaweza kutumia jioni zilizotengwa kwa ajili ya ibada ya familia au funzo la kibinafsi kuthamini hekima ya kiroho ambayo Yehova hutoa ili kutuokoa.—Met. 2:1-5.

TUNAIMARISHWA NA MAMBO YENYE KUTIA MOYO

14. Maandiko yanaonyeshaje kwamba Yehova anakazia fikira hisia zetu?

14 Daudi alikabili mambo mengi yenye kuvunja moyo katika maisha yake. (1 Sam. 30:3-6) Maneno ya Daudi yaliyoongozwa na roho ya Mungu yanaonyesha kuwa Yehova alijua hisia zake. (Soma Zaburi 34:18; 56:8.) Mungu anajua hisia zetu pia. Tunapokuwa ‘tumevunjika moyo’ au ‘kupondwa rohoni,’ yeye hutukaribia. Jambo hilo linaweza kutufariji kama lilivyomfariji Daudi, ambaye aliimba hivi: “Nitakuwa na shangwe na kushangilia katika fadhili zako zenye upendo, kwa kuwa umeona mateso yangu; umejua juu ya taabu za nafsi yangu.” (Zab. 31:7) Lakini Yehova hufanya mengi zaidi ya kuona tu hangaiko letu. Yeye hutuimarisha kwa kututia moyo na kutupa faraja. Njia moja anayofanya hivyo ni kupitia mikutano ya Kikristo.

15. Tunaweza kujifunza somo gani kutokana na jambo lililompata Asafu?

15 Jambo ambalo mtunga-zaburi Asafu alijionea linatusaidia kuelewa umuhimu wa kuhudhuria mikutano. Kuendelea kufikiria kuhusu ukosefu wa haki kulimfanya Asafu ashuku faida za kumtumikia Mungu. Asafu alivunjika sana moyo. Anaelezea hisia zake hivi: “Moyo wangu ulikuwa umetiwa uchungu nami nilikuwa na maumivu makali kwenye figo zangu.” Matokeo yake alikuwa karibu aache kumtumikia Yehova. Ni nini kilichomsaidia Asafu asimame imara tena? Anasema hivi: ‘Nikaingia katika patakatifu pakuu pa Mungu.’ Huko, akiwa miongoni mwa watu wa Yehova, aliweza kuwa na maoni mazuri tena. Alielewa kuwa mafanikio ya waovu yalikuwa ya muda tu, na kwamba bila kukawia Yehova atarekebisha mambo. (Zab. 73:2, 13-22) Ndivyo ilivyo kwetu pia. Mkazo wa kushughulika na ukosefu wa haki katika ulimwengu wa Shetani unaweza kutuvunja moyo. Kukutana na ndugu zetu kunatuburudisha na kutusaidia kupata tena shangwe tunapoendelea kumtumikia Yehova.

16. Mfano wa Hana unaweza kutunufaisha jinsi gani?

16 Vipi ikiwa hali katika kutaniko inafanya iwe vigumu kwako kuhudhuria mikutano? Labda ulihitaji kuacha mapendeleo fulani ya utumishi na ukaaibika, au ulikuwa na maoni tofauti na ndugu au dada fulani. Ikiwa ndivyo ilivyo, unaweza kuona mfano wa Hana kuwa wenye kusaidia. (Soma 1 Samweli 1:4-8.) Kumbuka kwamba mke mwenzake, aliyeitwa Penina, alimsumbua sana. Hali ilizidi kuwa ngumu kwa Hana wakati familia ilipoenda kutoa dhabihu kwa Yehova huko Shilo kila mwaka. Katika pindi hizo hali ilikuwa ngumu sana kwa Hana hivi kwamba ‘alikuwa akilia na kukataa kula.’ Hata hivyo, Hana hakuruhusu hilo limzuie kwenda mahali ambapo angeweza kumwabudu Yehova. Yehova aliona uaminifu wake na akambariki.—1 Sam. 1:11, 20.

17, 18. (a) Ni katika njia zipi tunatiwa moyo katika mikutano ya kutaniko? (b) Unahisije kuhusu jinsi Yehova anavyotutunza kwa upendo ili kutusaidia kupata wokovu?

17 Leo, Wakristo wana sababu nzuri za kuiga mfano wa Hana. Tunahitaji kuhudhuria mikutano kwa uaminifu. Kama vile ambavyo sote tumeona, mikutano inatupa kitia-moyo tunachohitaji. (Ebr. 10:24, 25) Kushirikiana na ndugu na dada zetu Wakristo kunatuletea faraja. Jambo fulani tunalolisikia katika hotuba au kwenye maelezo linaweza kutugusa moyo. Katika mazungumzo kabla na baada ya mkutano, mwamini mwenzetu anaweza kutusikiliza au anaweza kutufariji kwa maneno yake. (Met. 15:23; 17:17) Na tunapomsifu Yehova kwa kumwimbia pamoja na wengine, tunahisi tumechochewa na kutiwa moyo. Hasa tunapokuwa tumeshuka moyo kwa sababu ya ‘fikira zinazofadhaisha,’ tunahitaji kitia-moyo tunachopata katika mikutano, mahali ambapo Yehova anatutegemeza kupitia ‘faraja zake mwenyewe’ na kutuimarisha katika azimio letu la kubaki waaminifu.—Zab. 94:18, 19.

18 Utunzaji wenye upendo wa Mungu wetu hutufanya tujihisi salama kama mtunga-zaburi Asafu aliyemwimbia Yehova hivi: “Umeushika mkono wangu wa kuume. Utaniongoza kwa shauri lako.” (Zab. 73:23, 24) Tunathamini kama nini kwamba Yehova hutulinda ili atuokoe!

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 28]

Wewe pia umevutwa na Yehova

[Picha katika ukurasa wa 30]

Tunalindwa kwa kutumia mashauri ya Mungu

[Picha katika ukurasa wa 31]

Tunaimarishwa kupitia kitia-moyo tunachopata