Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Unatoa Mrudisho wa Utukufu wa Yehova?

Je, Unatoa Mrudisho wa Utukufu wa Yehova?

Je, Unatoa Mrudisho wa Utukufu wa Yehova?

‘Tunatoa kama vioo mrudisho wa utukufu wa Yehova.’—2 KOR. 3:18.

UNGEJIBUJE?

Licha ya hali yetu ya dhambi, tunawezaje kumtukuza Yehova?

Sala zetu na kuhudhuria mikutano ya Kikristo kunatusaidiaje kutoa mrudisho wa utukufu wa Mungu?

Ni nini kinachoweza kutusaidia kuendelea kumtukuza Yehova?

1, 2. Kwa nini inawezekana kwa wanadamu kuiga sifa za Yehova?

KATIKA njia moja au nyingine, sisi sote tunafanana na wazazi wetu. Kwa hiyo, haishangazi kumsikia mtu akimwambia mvulana fulani hivi, ‘Wewe ni kama tu baba yako.’ Msichana anaweza kuambiwa, ‘Unanikumbusha mama yako.’ Na mara nyingi watoto wanaiga yale wanayoona wazazi wao wakifanya. Lakini namna gani sisi? Je, tunaweza kumwiga Baba yetu wa mbinguni, Yehova? Licha ya kwamba hatujamwona, tunaweza kuona sifa zake bora kwa kujifunza Neno lake, kwa kuchunguza uumbaji wake, na kutafakari juu ya Maandiko na hasa maneno na matendo ya Mwana wa Mungu, Yesu Kristo. (Yoh. 1:18; Rom. 1:20) Tunaweza kutoa mrudisho wa utukufu wa Yehova.

2 Kabla ya kuumbwa kwa Adamu na Hawa, Mungu alikuwa na hakika kwamba wanadamu wangeweza kutimiza mapenzi yake, wangeiga sifa zake, na kumletea utukufu. (Soma Mwanzo 1:26, 27.) Ili kufuatia ujitoaji-kimungu, tunapaswa kuonyesha sifa za Yule aliyetuumba. Tunapofanya hivyo, tunakuwa na pendeleo kubwa la kutoa mrudisho wa utukufu wa Mungu, licha ya utamaduni, elimu, au kabila letu. Kwa nini? Kwa sababu “Mungu hana ubaguzi, bali katika kila taifa mtu ambaye anamwogopa na kutenda uadilifu anakubalika kwake.”—Mdo. 10:34, 35.

3. Wakristo wanahisije wanapomtumikia Yehova?

3 Wakristo watiwa-mafuta wanatoa mrudisho wa utukufu wa Yehova. Hivyo, mtume Paulo, ambaye alizaliwa kwa roho aliandika hivi: “Sisi sote, wakati tunapotoa kama vioo mrudisho wa utukufu wa Yehova tukiwa na nyuso zisizo na utaji, tunageuzwa na kuwa katika mfano uleule kutoka utukufu mpaka utukufu.” (2 Kor. 3:18) Nabii Musa aliposhuka kutoka kwenye Mlima Sinai akiwa amebeba mabamba yaliyokuwa na Amri Kumi, uso wake ulitoa miale kwa sababu Yehova alikuwa amezungumza naye. (Kut. 34:29, 30) Licha ya kwamba Wakristo hawajapitia jambo kama hilo maishani na nyuso zao hazitoi miale, nyuso zao zinang’aa kwa shangwe wanapowaambia wengine kumhusu Yehova, sifa zake, na kusudi lake zuri ajabu kwa ajili ya wanadamu. Kama vioo vya chuma vilivyong’aa katika nyakati za kale, watiwa-mafuta na waandamani wao duniani wanatoa mrudisho wa utukufu wa Yehova kupitia maisha yao na pia huduma yao. (2 Kor. 4:1) Je, wewe unatoa mrudisho wa utukufu wa Yehova kupitia mwenendo wako unaompendeza Mungu na kwa utendaji wako ukiwa mtangazaji wa kawaida wa Ufalme?

TUNATAMANI KUTOA MRUDISHO WA UTUKUFU WA YEHOVA

4, 5. (a) Kama Paulo, ni pambano gani tulilo nalo? (b) Dhambi imetuathirije?

4 Tukiwa watumishi wa Yehova, bila shaka tunataka kumheshimu na kumtukuza Muumba wetu katika kila jambo tunalofanya. Hata hivyo, mara nyingi hatufanyi yale tunayotamani kufanya. Paulo alipambana kibinafsi na tatizo hilo. (Soma Waroma 7:21-25.) Akieleza kwa nini tuna pambano kama hilo, Paulo aliandika hivi: “Wote wamefanya dhambi na kupungukiwa na utukufu wa Mungu.” (Rom. 3:23) Naam, kwa sababu ya dhambi waliyorithi kutoka kwa Adamu, wanadamu wote walikuja kuwa chini ya utumwa wenye ukatili wa ‘Mfalme Dhambi.’—Rom. 5:12; 6:12.

5 Dhambi ni nini? Ni jambo lolote lililo kinyume na utu wa Yehova, njia zake, viwango vyake, na mapenzi yake. Dhambi inaharibu uhusiano wa mtu pamoja na Mungu. Dhambi inatufanya tukose shabaha, kama vile mlenga-shabaha anavyoweza kukosa shabaha anapopiga mshale. Tunaweza kutenda dhambi bila kukusudia au kimakosa. (Hes. 15:27-31) Dhambi imetia mizizi ndani ya wanadamu nayo inawatenganisha na Muumba wao. (Zab. 51:5; Isa. 59:2; Kol. 1:21) Hivyo, wanadamu kwa ujumla wanaishi maisha ambayo hayapatani kabisa na njia za Yehova na wanakosa fursa yenye thamani ya kutoa mrudisho wa utukufu wa Mungu. Bila shaka, dhambi ni ulemavu mbaya sana unaowatesa wanadamu.

6. Tunawezaje kumtukuza Mungu licha ya hali yetu ya dhambi?

6 Licha ya hali yetu ya dhambi, Yehova amethibitika kuwa “Mungu anayetoa tumaini.” (Rom. 15:13) Ameandaa njia ya kukomesha dhambi, yaani, dhabihu ya fidia ya Yesu Kristo. Kwa kudhihirisha imani katika dhabihu hiyo, hatuwi tena “watumwa wa dhambi,” bali tunakuwa na nafasi ya kutoa mrudisho wa utukufu wa Yehova. (Rom. 5:19; 6:6; Yoh. 3: 16) Tukidumisha uhusiano huo mzuri pamoja na Mungu tuna hakika kwamba Yehova atatubariki sasa na wakati ujao, tutapata uzima wa milele tukiwa wakamilifu. Ingawa bado sisi ni wanadamu wenye dhambi, ni baraka kama nini kuonwa na Mungu kuwa watu ambao wanaweza kutoa mrudisho wa utukufu wake!

KUTOA MRUDISHO WA UTUKUFU WA MUNGU

7. Ni lazima tutambue nini kuhusu hali yetu ili tutoe mrudisho wa utukufu wa Mungu?

7 Ili kuwa katika hali nzuri ya kutoa mrudisho wa utukufu wa Mungu, ni lazima tutambue kwa unyoofu hali yetu ya dhambi. (2 Nya. 6:36) Tunahitaji kutambua mielekeo yetu ya dhambi na kujitahidi kuidhibiti ili tuweze kufanya maendeleo ili hatimaye tuweze kumtukuza Mungu kikweli. Kwa mfano, ikiwa tumetumbukia katika dhambi yenye kuaibisha ya kutazama ponografia, ni lazima tukubali ukweli wa kwamba tunahitaji msaada wa kiroho, na kwamba tunapaswa kuchukua hatua ya kuupata msaada huo. (Yak. 5:14, 15) Hiyo ni hatua ya kwanza tunayopaswa kuchukua ikiwa tunataka kuwa na maisha yanayomheshimu Mungu kikamili. Tukiwa waabudu wa Yehova, ni lazima tuendelee kujichunguza wenyewe ili kujua ikiwa tunatimiza viwango vyake vya uadilifu. (Met. 28:18; 1 Kor. 10:12) Hata tuwe na mielekeo gani ya dhambi, ni lazima tuendelee kupambana nayo ili tuweze kutoa mrudisho wa utukufu wa Mungu.

8. Licha ya kwamba sisi si wakamilifu, tunapaswa kufanya nini?

8 Yesu alikuwa ndiye mwanadamu pekee aliyewahi kuishi na kufa bila kumkosea Mungu, na akatoa mrudisho wa utukufu wa Mungu. Ingawa sisi si wakamilifu kama Yesu alivyokuwa, tunaweza na tunapaswa kujitahidi kufuata mfano wake. (1 Pet. 2:21) Yehova anatambua jitihada zetu na maendeleo tunayofanya, naye anabariki jitihada zetu zenye bidii za kumletea utukufu.

9. Biblia inawasaidiaje Wakristo kutoa mrudisho wa utukufu wa Mungu kwa njia bora zaidi?

9 Neno la Yehova lililoandikwa linaweza kutusaidia kuboresha mapito yetu. Ni muhimu tujifunze Maandiko kwa kina na kutafakari juu ya yale tunayosoma katika Biblia. (Zab. 1:1-3) Kusoma Maandiko kila siku kutatusaidia kufanya maendeleo. (Soma Yakobo 1:22-25.) Ujuzi wa Biblia ndio msingi wa imani yetu na ndio njia ya kutia nguvu azimio letu la kuepuka dhambi nzito na kumpendeza Yehova.—Zab. 119:11, 47, 48.

10. Sala inaweza kutusaidiaje kumtumikia Yehova kikamili zaidi?

10 Ili kutoa mrudisho wa utukufu wa Mungu, tunahitaji pia ‘kudumu katika sala.’ (Rom. 12:12) Tunaweza na tunapaswa kusali ili Yehova atusaidie tumtumikie kwa njia anayokubali. Ili kufanya hivyo, tunaweza kumwomba roho yake takatifu, imani zaidi, nguvu za kushinda kishawishi, na uwezo wa ‘kulitumia sawasawa neno la kweli.’ (2 Tim. 2:15; Mt. 6:13; Luka 11:13; 17:5) Tunahitaji kumtegemea Baba yetu wa mbinguni, Yehova, kama mtoto anavyomtegemea baba yake. Tukimwomba atusaidie ili tumtumikie kikamili zaidi, tunaweza kuwa na hakika kwamba atatusaidia. Tusihisi kamwe kwamba tunamsumbua! Badala yake, acheni tumsifu, tumshukuru, tutafute mwongozo wake kupitia sala hasa tunapokabili jaribu, na tumwombe atusaidie ili tumtumikie katika njia zinazolitukuza jina lake.—Zab. 86:12; Yak. 1:5-7.

11. Mikutano ya kutaniko inatusaidiaje kutoa mrudisho wa utukufu wa Mungu?

11 Mungu amemkabidhi “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” jukumu la kuwatunza kondoo wake wenye thamani. (Mt. 24:45-47; Zab. 100:3) Jamii ya mtumwa inapendezwa sana kujua jinsi waamini wenzao wanavyotoa mrudisho wa utukufu wa Yehova. Mikutano yetu inatusaidia kufanya marekebisho katika maisha yetu na kuboresha sifa za Kikristo, kama vile tu mshonaji wa nguo anavyorekebisha nguo zetu ili tupendeze zaidi. (Ebr. 10:24, 25) Kwa hiyo, acheni tufike mapema kwenye mikutano, kwa sababu tukiwa na zoea la kufika tumechelewa, tunakosa mambo fulani ya kiroho tunayohitaji ili kuboresha hali yetu tukiwa watumishi wa Yehova.

ACHENI TUMWIGE MUNGU

12. Tunawezaje kumwiga Mungu?

12 Ili tutoe mrudisho wa utukufu wa Yehova, ni lazima ‘tuwe waigaji wa Mungu.’ (Efe. 5:1) Njia moja ya kumwiga Yehova ni kujifunza kuona mambo jinsi anavyoyaona. Kujaribu kuishi kulingana na njia zetu wenyewe kunamvunjia Yehova heshima na kutatudhuru. Kwa kuwa ulimwengu unaotuzunguka uko chini ya uvutano wa yule mwovu, Shetani Ibilisi, ni lazima tufanye bidii ili tuchukie mambo ambayo Yehova anachukia na kupenda kwa kina yale ambayo anapenda. (Zab. 97:10; 1 Yoh. 5:19) Tunahitaji kusadiki kutoka moyoni kwamba njia pekee inayofaa ya kumtumikia Mungu ni kufanya mambo yote kwa utukufu wake.—Soma 1 Wakorintho 10:31.

13. Kwa nini ni lazima tuchukie dhambi, na ni nini ambacho kitatuchochea kufanya hivyo?

13 Yehova anachukia dhambi, na sisi pia tunapaswa kuichukia. Kwa kweli, tunapaswa kukimbia mbali iwezekanavyo kutoka kwa jambo lolote ambalo linaweza kutufanya tutende dhambi na tusijaribu kuona tunaweza kuikaribia dhambi kwa kadiri gani bila kuanguka. Kwa mfano, tunahitaji kujilinda ili tusishawishiwe na uasi-imani, dhambi ambayo itatufanya tusistahili kumtukuza Mungu. (Kum. 13:6-9) Kwa hiyo, acheni tuwaepuke waasi-imani au mtu yeyote anayedai kuwa ndugu lakini ambaye anamvunjia Mungu heshima. Tunapaswa kufanya hivyo hata ikiwa mtu huyo ni mshiriki wa familia. (1 Kor. 5:11) Hatupati faida yoyote kwa kujaribu kukanusha hoja za waasi-imani au za wale wanaolichambua-chambua tengenezo la Yehova. Kwa kweli, watu hao ni hatari kiroho na hatupaswi kusoma habari zao, iwe zimechapishwa au zinapatikana kwenye Intaneti.—Soma Isaya 5:20; Mathayo 7:6.

14. Tunapojitahidi kutoa mrudisho wa utukufu wa Mungu, ni sifa gani tunayopaswa kusitawisha, na kwa nini?

14 Kuonyesha upendo ni njia bora zaidi ya kumwiga Baba yetu wa mbinguni. Naam, tunapaswa kuwa wenye upendo kama Baba yetu. (1 Yoh. 4:16-19) Kwa kweli, upendo ulio miongoni mwetu unatutambulisha kuwa wanafunzi wa Yesu na watumishi wa Yehova. (Yoh. 13:34, 35) Ingawa nyakati nyingine inaweza kuwa vigumu kuonyesha upendo kwa sababu ya dhambi tuliyorithi, ni lazima tupambane na hali hiyo na kujitahidi kuonyesha upendo nyakati zote. Kusitawisha upendo na sifa nyingine zinazompendeza Mungu kutatuzuia kufanya dhambi na mambo yasiyo yenye fadhili.—2 Pet. 1:5-7.

15. Upendo una uvutano gani juu ya uhusiano wetu pamoja na wengine?

15 Upendo unatufanya tutake kuwatendea watu wengine mambo mema. (Rom. 13:8-10) Kwa mfano, kumpenda mwenzi wetu wa ndoa kutafanya kitanda cha ndoa kiwe bila unajisi. Kuwapenda wazee wa kutaniko na kuheshimu kazi yao, kutatusaidia kuwa watiifu na kujitiisha chini ya uongozi wao. Watoto wanaowapenda wazazi wao huwatii, huwaheshimu, na hawasemi mambo mabaya kuwahusu. Ikiwa tunawapenda wanadamu wenzetu, hatutawaona kuwa watu wa hali ya chini au kuongea nao kwa njia isiyo ya heshima. (Yak. 3:9) Na wazee wanaowapenda kondoo wa Mungu watawatendea kwa wororo.—Mdo. 20:28, 29.

16. Kuonyesha upendo kutatusaidiaje katika huduma yetu?

16 Sifa ya upendo inapaswa pia kuonekana wazi katika huduma yetu. Kwa sababu tunampenda sana Yehova, hatutajiruhusu tuvunjwe moyo na ubaridi au kutoitikia vizuri kwa baadhi ya wenye nyumba. Badala yake, tutaendelea kuhubiri habari njema. Upendo utatuchochea kujitayarisha vizuri na kujitahidi kuwa wenye matokeo katika huduma. Ikiwa kwa kweli tunampenda Mungu na majirani wetu, hatutahubiri kuhusu Ufalme ili tu kutimiza wajibu. Badala yake, tutaiona kazi hiyo kuwa pendeleo kubwa nasi tutaifanya kwa shangwe.—Mt. 10:7.

ENDELEA KUMTUKUZA YEHOVA

17. Tunafaidika jinsi gani tunapotambua kwamba hatuwezi kutoa mrudisho wa utukufu wa Mungu kwa ukamili?

17 Ulimwengu kwa ujumla hautambui uzito wa dhambi, lakini sisi tunatambua. Jambo hilo linatufanya tutambue uhitaji wa kupambana na mielekeo yetu ya dhambi. Kutambua hali yetu ya dhambi kunatuwezesha kuizoeza dhamiri yetu hivi kwamba itatuchochea kutenda kwa njia inayofaa wakati tamaa ya kutenda dhambi inapoanza kusitawi akilini na moyoni mwetu. (Rom. 7:22, 23) Ni kweli kwamba huenda tukawa dhaifu, lakini Mungu anaweza kutuimarisha ili tufanye yaliyo sawa katika hali yoyote ile.—2 Kor. 12:10.

18, 19. (a) Ni nini kinachotuwezesha kufanikiwa katika pambano letu na majeshi ya roho waovu? (b) Tunapaswa kuazimia kufanya nini?

18 Ikiwa tunataka kumtukuza Yehova, ni lazima pia tupambane na majeshi ya roho waovu. Silaha zetu za kiroho tulizopewa na Mungu zinatuwezesha kupambana kwa mafanikio. (Efe. 6:11-13) Shetani anajitahidi juu chini kunyakua utukufu wa Yehova ambao ni Yehova peke yake anastahili. Pia, Ibilisi anaendelea kujitahidi kwa kila njia kuharibu uhusiano wetu pamoja na Yehova. Lakini ni pigo kama nini kwa Shetani wakati sisi na mamilioni ya wanaume, wanawake, na watoto wasio wakamilifu tunapodumisha utimilifu na kumtukuza Mungu! Kwa hiyo, acheni tuendelee kumsifu Yehova kama viumbe wa mbinguni wanaopaaza sauti hivi: “Unastahili, Ee Yehova, naam, Mungu wetu, kupokea utukufu na heshima na nguvu, kwa sababu uliumba vitu vyote, na kwa sababu ya mapenzi yako vilikuwako navyo vikaumbwa.”—Ufu. 4:11.

19 Acheni basi tuazimie kuendelea kumtukuza Yehova chini ya hali yoyote ile. Bila shaka, Yehova anashangilia kuona kwamba watu wengi washikamanifu wanafanya yote wawezayo ili kumwiga na kutoa mrudisho wa utukufu wake. (Met. 27:11) Acheni tuhisi kama Daudi, aliyeimba hivi: “Ninakusifu, Ee Yehova Mungu wangu, kwa moyo wangu wote, nami nitalitukuza jina lako mpaka wakati usio na kipimo.” (Zab. 86:12) Tunatamani kama nini siku tutakapotoa mrudisho wa utukufu wa Yehova kwa ukamili na kuweza kumsifu milele! Wanadamu watiifu watashangilia kuona mambo hayo yakitimia. Je, wewe unatoa mrudisho wa utukufu wa Yehova Mungu sasa, ukitarajia kufanya hivyo kwa umilele wote?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 27]

Je, unatoa mrudisho wa utukufu wa Yehova katika njia hizi?