Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Ni jinsi gani kifo cha washikamanifu wa Mungu ni “chenye thamani machoni pa Yehova”?

▪ Mtunga-zaburi aliyeongozwa na roho ya Mungu aliimba hivi: “Ni chenye thamani machoni pa Yehova kifo cha washikamanifu wake.” (Zab. 116:15) Uhai wa kila mwabudu wa kweli wa Yehova ni wenye thamani sana machoni pake. Hata hivyo, maneno hayo ya Zaburi 116 hayamaanishi tu kifo cha mwabudu mmoja-mmoja wa Yehova.

Katika hotuba ya ukumbusho wa kifo cha Mkristo, isingefaa kutumia andiko la Zaburi 116:15 kumhusu Mkristo huyo aliyekufa, hata ingawa alikufa akiwa mtumishi mshikamanifu wa Yehova. Kwa nini? Kwa sababu maneno hayo ya mtunga-zaburi yana maana pana. Yanamaanisha kwamba Mungu anaona kifo cha washikamanifu wake wakiwa kikundi kuwa gharama kubwa sana kwake hivi kwamba hawezi kuwaruhusu wafe wote kwa ujumla.—Tazama Zaburi 72:14; 116:8.

Andiko la Zaburi 116:15 linatuhakikishia kwamba Yehova hataruhusu watumishi wake washikamanifu waondolewe kabisa duniani wakiwa kikundi. Kwa kweli, historia yetu ya kisasa inaonyesha kwamba tayari tumevumilia majaribu na mateso makali, na hilo linathibitisha waziwazi kwamba Mungu hataruhusu kamwe tuangamizwe sote tukiwa kikundi.

Kwa sababu Yehova ana nguvu zisizo na mipaka na kusudi lake haliwezi kukosa kutimia, hataruhusu tufutiliwe mbali kabisa tukiwa kama kikundi. Ikiwa Mungu angeruhusu jambo hilo litokee, ingeonekana kwamba maadui wake wana nguvu zaidi yake, na hilo ni jambo lisilowezekana! Kusudi la Yehova la kwamba dunia hii ikaliwe na watu ambao ni washikamanifu kwake halingetimia, na jambo hilo haliwezekani. (Isa. 45:18; 55:10, 11) Kwa kweli kumtolea Yehova utumishi mtakatifu kungekoma duniani ikiwa hakungekuwa na watu ambao wangebaki ili kumwabudu katika nyua za kidunia za hekalu lake kuu la kiroho! Hakungekuwa na msingi wa “dunia mpya,” yaani, jamii ya wanadamu waadilifu ambao wataishi katika dunia yetu chini ya “mbingu mpya.” (Ufu. 21:1) Vilevile, Utawala wa Miaka Elfu Moja wa Kristo haungekuwa halisi ikiwa hakungekuwa na raia wowote duniani.—Ufu. 20:4, 5.

Sifa na cheo cha Mungu kingetiliwa shaka ikiwa angewaruhusu maadui wake wawafagilie mbali watu wake kutoka duniani, wakiwa kikundi. Tukio hilo lingefanya cheo cha Yehova akiwa Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Mzima kitiliwe shaka. Zaidi ya hayo, Yehova hataruhusu washikamanifu wake wauawe wote wakiwa kikundi kwa sababu anajiheshimu na kuliheshimu jina lake takatifu. Hebu fikiria jambo hili: Kwa kuwa Mungu “hana ukosefu wowote wa haki,” hatakosa kamwe kulinda kikundi cha wanadamu ambao wamekuwa wakimtumikia kwa ushikamanifu. (Kum. 32:4; Mwa. 18:25) Isitoshe, kuwaruhusu watumishi wake waangamizwe wote wakiwa kikundi kungekuwa kinyume cha Neno la Mungu, linalosema: “Yehova hatawaacha watu wake kwa ajili ya jina lake kuu.” (1 Sam. 12:22) Kwa hakika, “Yehova hatawaacha watu wake, wala hatauacha urithi wake mwenyewe.”—Zab. 94:14.

Inafariji kama nini kujua kwamba watu wa Yehova hawataangamia kamwe kutoka duniani! Basi acheni tufanye yote tuwezayo kuendelea kuwa washikamanifu kwa Mungu, tukitumaini ahadi hii yake: “Silaha yoyote itakayofanywa juu yako haitafanikiwa, na ulimi wowote utakaoinuka juu yako katika hukumu wewe utauhukumu. Hilo ndilo fungu la urithi la watumishi wa Yehova, na uadilifu wao ni kutoka kwangu.”—Isa. 54:17.

[Blabu katika ukurasa wa 22]

Mungu hatawaruhusu kamwe watu wake waangamizwe wote wakiwa kikundi