Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mtegemee Yehova—Mungu wa “Nyakati Na Majira”

Mtegemee Yehova—Mungu wa “Nyakati Na Majira”

Mtegemee Yehova—Mungu wa “Nyakati Na Majira”

“Anabadili nyakati na majira, akiondoa wafalme na kuwasimamisha wafalme.”—DAN. 2:21.

UNGEJIBUJE?

Uumbaji na unabii uliotimia unaonyeshaje kwamba Yehova ni Mtunza-Wakati Mkuu?

Kuthamini kwamba Yehova ni Mungu wa “nyakati na majira” kunatuchochea kufanya nini?

Kwa nini ratiba ya Yehova haitegemei matukio ya ulimwengu na mipango ya wanadamu?

1, 2. Ni nini kinachoonyesha kwamba Yehova anaelewa kikamili maana ya wakati?

YEHOVA MUNGU aliandaa njia ya kupima wakati muda mrefu kabla ya kumuumba mwanadamu. Katika siku ya nne ya uumbaji, Mungu alisema hivi: “Kuwe na mianga katika anga la mbingu ili kutenganisha mchana na usiku; nayo iwe ishara na kwa ajili ya majira na kwa ajili ya siku na miaka.” (Mwa. 1:14, 19, 26) Kulingana na mapenzi ya Yehova, bila shaka, hivyo ndivyo ilivyokuwa.

2 Hata hivyo, kufikia sasa, wanasayansi wanajadiliana kuhusu maana ya wakati. Kitabu kimoja cha utafiti kinasema hivi: “Wakati ni mojawapo ya mafumbo yasiyoeleweka kamwe ulimwenguni. Hakuna mtu anayeweza kusema kwa usahihi wakati ni nini hasa.” Hata hivyo, Yehova anaelewa kikamili maana ya wakati. Kwa kweli, yeye ndiye “Muumba wa mbingu, . . . Mfanyizaji wa dunia na Mtengenezaji wake.” Pia, Yehova ‘ndiye Anayetangaza tangu mwanzo ule mwisho, na kutoka zamani za kale mambo ambayo hayajafanywa.’ (Isa. 45:18; 46:10) Hivyo, ili kuimarisha imani yetu katika Yehova na Neno lake, Biblia, acheni tuchunguze jinsi uumbaji na unabii uliotimia unavyoonyesha kwamba Yehova ni Mtunza-Wakati Mkuu.

UUMBAJI UNAIMARISHA IMANI YETU KATIKA MTUNZA-WAKATI MKUU

3. Taja baadhi ya vitu katika uumbaji ambavyo vinafuata wakati kwa usahihi kabisa.

3 Vitu vingi katika uumbaji, vidogo kwa vikubwa, vinafuata wakati kwa usahihi kabisa. Vitu vidogo zaidi vinavyoitwa atomu vinatetema kwa mwendo usiobadilika. Saa za ukutani ambazo zinatumia atomu zinazotetema kupima wakati, ni sahihi sana hivi kwamba haziwezi kuwa nyuma hata kwa sekunde moja katika muda wa miaka milioni 80. Pia, mwendo wa sayari na nyota angani umepimwa kwa usahihi kabisa. Kwa kuwa wanadamu wanaweza kujua mapema mahali ambapo sayari na nyota zitakuwa katika mzunguko, hilo linawasaidia kujua majira na kujua wanakoelekea wanaposafiri. Yehova, akiwa Mtengenezaji wa atomu, nyota, na sayari zinazotegemeka katika kufuata wakati, kwa kweli yeye ni “hodari katika nguvu” na anastahili kusifiwa na wanadamu.—Soma Isaya 40:26.

4. Ukweli wa kwamba vitu vilivyo hai vinafuata wakati unadhihirishaje hekima ya Mungu?

4 Vitu vilivyo hai vinafuata wakati kwa usahihi kabisa. Mimea na wanyama wengi wanafuata saa za kisilika zilizo ndani yao. Ndege wengi wanajua kisilika wakati ambapo wanapaswa kuanza kuhama. (Yer. 8:7) Wanadamu pia wana saa kama hizo ndani yao ambazo zinawaongoza kwa saa 24 mchana na usiku. Baada ya mtu kusafiri kwa ndege kupitia maeneo ya dunia yanayotofautiana kwa wakati, huenda mwili wake ukahitaji siku chache ili kujipatanisha na saa hizo tofauti. Kwa kweli, vitu vingi katika uumbaji ambavyo vinafuata wakati vinadhihirisha nguvu na hekima ya Mungu wa “nyakati na majira.” (Soma Zaburi 104:24.) Naam, Mtunza-Wakati Mkuu ni mwenye hekima yote na mwenye nguvu zote. Hivyo, tunaweza kuamini kwamba anaweza kutimiza mapenzi yake!

UNABII MBALIMBALI ULIOTIMIA KWA WAKATI UNAIMARISHA IMANI

5. (a) Ni njia gani pekee inayoweza kutusaidia kujua wakati ujao wa wanadamu? (b) Kwa nini Yehova anaweza kutabiri matukio na wakati hususa yatakapotukia?

5 Uumbaji unatufundisha mengi kuhusu ‘sifa za Yehova ambazo hazionekani,’ lakini haujibu maswali muhimu kama vile, Wakati ujao wa wanadamu utakuwaje? (Rom. 1:20) Ili kupata jibu ni lazima tujifunze yale ambayo Mungu amefunua katika Neno lake, Biblia. Tunapolichunguza, tunapata unabii mbalimbali ambao ulitimia kwa wakati kamili! Yehova anaweza kufunua mambo ambayo bado hayajatukia kwa sababu anaweza kuona kimbele mambo ya wakati ujao kwa usahihi. Zaidi ya hayo, mambo ambayo Maandiko yanatabiri yanatukia kwa wakati kwa sababu Yehova Mungu anaweza kusababisha matukio yatukie kulingana na kusudi lake na ratiba yake.

6. Ni nini kinachoonyesha kwamba Yehova anataka tuelewe utimizo wa unabii mbalimbali wa Biblia?

6 Yehova anataka waabudu wake waelewe unabii mbalimbali wa Biblia na kufaidika nao. Ingawa Mungu haoni wakati kama sisi tunavyouona, tunaweza kuelewa maneno anayotumia anapotabiri kwamba tukio fulani litatukia kwa wakati hususa. (Soma Zaburi 90:4.) Kwa mfano, kitabu cha Ufunuo kinazungumza kuhusu “malaika wanne” ambao “wametayarishwa kwa ajili ya ile saa na siku na mwezi na mwaka,” vipimo vya wakati ambavyo tunaweza kuelewa. (Ufu. 9:14, 15) Tunapoona jinsi unabii mbalimbali ulivyotimia kwa wakati hususa, hilo linapaswa kuimarisha imani yetu katika Mungu wa “nyakati na majira” na katika Neno lake. Acheni tuchunguze mifano michache.

7. Kutimia kwa unabii wa Yeremia kuhusiana na Yerusalemu na Yuda kunaonyeshaje kwamba Yehova ni Mtunza-Wakati Mkuu?

7 Kwanza, acheni tuchunguze yale yaliyotukia katika karne ya saba K.W.K. “Katika mwaka wa nne wa Yehoyakimu mwana wa Yosia, mfalme wa Yuda,” neno la Mtunza-Wakati Mkuu ‘lilimjia Yeremia kuhusu watu wote wa Yuda.’ (Yer. 25:1) Yehova alitabiri kuhusu uharibifu wa Yerusalemu na kupelekwa uhamishoni kwa Wayahudi kutoka nchi ya Yuda hadi Babiloni. Wakiwa huko ‘wangemtumikia mfalme wa Babiloni miaka 70.’ Majeshi ya Babiloni yaliharibu Yerusalemu mwaka wa 607 K.W.K., na kwa kweli Wayahudi kutoka Yuda wakapelekwa uhamishoni Babiloni. Lakini ni nini ambacho kingetukia mwishoni mwa ile miaka 70? Yeremia alitabiri hivi: “Yehova amesema hivi, ‘Kupatana na kutimia kwa miaka 70 katika Babiloni nitawakazia ninyi fikira, nami nitawatimizia neno langu jema kwa kuwarudisha tena mahali hapa.’” (Yer. 25:11, 12; 29:10) Unabii huo ulitimia kwa wakati unaofaa kabisa, yaani, katika mwaka wa 537 K.W.K. baada ya Wamedi na Waajemi kuwaweka huru Wayahudi kutoka Babiloni.

8, 9. Unabii wa Danieli kuhusu kuja kwa Masihi na kusimamishwa kwa Ufalme wa mbinguni, unaonyeshaje kwamba Yehova ni Mungu wa “nyakati na majira”?

8 Ona unabii mwingine ambao unawahusu watu wa Mungu wa nyakati za kale. Miaka miwili hivi kabla ya Wayahudi kutoka Babiloni, Mungu alitabiri kupitia nabii Danieli kwamba Masihi angetokea miaka 483 baada ya kutolewa kwa amri ya kujenga upya Yerusalemu. Mfalme wa Umedi na Uajemi alitoa amri hiyo mwaka wa 455 K.W.K. Miaka 483 kamili baadaye, mnamo mwaka wa 29 W.K., Yesu wa Nazareti alitiwa mafuta kwa roho takatifu alipobatizwa na hivyo akawa yule Masihi. *Neh. 2:1, 5-8; Dan. 9:24, 25; Luka 3:1, 2, 21, 22.

9 Sasa ona yale ambayo Maandiko yalitabiri kuhusu Ufalme. Unabii wa Biblia ulionyesha kwamba Ufalme wa Kimasihi ungesimamishwa huko mbinguni mwaka wa 1914. Kwa sehemu, Biblia inataja “ishara” ya kuwapo kwa Yesu, ikionyesha wakati ambao Shetani angetupwa kutoka mbinguni, jambo ambalo lingesababisha ole kubwa duniani. (Mt. 24:3-14; Ufu. 12:9, 12) Zaidi ya hayo, unabii wa Biblia ulionyesha wakati hususa, yaani, mwaka wa 1914, pindi ambayo ‘nyakati zilizowekwa za mataifa zingetimia’ na Ufalme huo ungeanza kutawala huko mbinguni.—Luka 21:24; Dan. 4:10-17. *

10. Ni matukio gani ya wakati ujao ambayo bila shaka yatatukia kwa wakati uliowekwa?

10 Hivi karibuni kutakuwa na “dhiki kuu” iliyotabiriwa na Yesu. Itafuatwa na Utawala wake wa Miaka Elfu Moja. Hapana shaka kwamba mambo yote hayo yatatukia kwa wakati hususa uliowekwa. Yesu alipokuwa duniani, tayari Yehova alikuwa ameweka ‘siku na saa’ ya matukio hayo.—Mt. 24:21, 36; Ufu. 20:6.

‘JINUNULIE WAKATI UNAOFAA’

11. Kujua kwamba tunaishi katika wakati wa mwisho kunapaswa kutuchocheaje?

11 Kutambua kwamba Ufalme umeanza kutawala na kwamba tunaishi katika “wakati wa mwisho” kunapaswa kutuchocheaje? (Dan. 12:4) Watu wengi wanaona jinsi hali za ulimwengu zinavyozidi kuwa mbaya, hata hivyo hawatambui kwamba hali hizo zinatimiza unabii wa Biblia kuhusu siku za mwisho. Huenda wakatarajia kuwa mfumo huu utaporomoka siku moja au huenda wakaamini kwamba kwa njia fulani jitihada za wanadamu zitafanikiwa kuleta “amani na usalama.” (1 The. 5:3) Vipi sisi? Ikiwa tunatambua kwamba tunaishi katika upeo wa siku za mwisho za ulimwengu wa Shetani, je, hatupaswi kujitahidi kuutumia wakati uliobaki kumtumikia yule Mungu wa “nyakati na majira” na kuwasaidia wengine wapate kumjua? (2 Tim. 3:1) Ni lazima tufanye maamuzi ya hekima kuhusu jinsi tunavyoutumia wakati wetu.—Soma Waefeso 5:15-17.

12. Tunaweza kujifunza nini kutokana na maneno ya Yesu kuhusu siku za Noa?

12 Katika ulimwengu huu uliojaa mambo yanayokengeusha fikira, si rahisi ‘kujinunulia wakati unaofaa.’ Yesu alionya hivi: “Kama vile siku za Noa zilivyokuwa, ndivyo kuwapo kwa Mwana wa binadamu kutakavyokuwa.” Siku za Noa zilikuwaje? Ilikuwa imetabiriwa kwamba ulimwengu wa wakati huo ungekoma. Wakati huo, wanadamu waovu wangekufa kwa maji ya gharika ya ulimwenguni pote. Akiwa “mhubiri wa uadilifu,” Noa aliwatangazia kwa uaminifu watu wa siku zake ujumbe wa Mungu. (Mt. 24:37; 2 Pet. 2:5) Lakini walikuwa “wakila na kunywa, wanaume wakioa na wanawake wakiolewa, . . . nao hawakujali mpaka gharika ikaja na kuwafagilia mbali wote.” Kwa hiyo, Yesu aliwaonya wafuasi wake hivi: “Iweni tayari, kwa sababu Mwana wa binadamu atakuja katika saa msiyofikiria.” (Mt. 24:38, 39, 44) Tunapaswa kuwa kama Noa, bali si kama watu wa siku zake. Ni nini kitakachotusaidia kuwa tayari?

13, 14. Kukumbuka nini kumhusu Yehova kutatusaidia kumtumikia kwa uaminifu huku tukingojea kuja kwa Mwana wa binadamu?

13 Ingawa Mwana wa binadamu anakuja katika saa ambayo hatufikirii, tunahitaji kukumbuka kwamba Yehova ni Mtunza-Wakati Mkuu. Ratiba yake haitegemei matukio ya ulimwengu au mipango ya wanadamu. Yehova anaongoza wakati na jinsi mambo yanavyotukia ili yatimize mapenzi yake. (Soma Danieli 2:21.) Kwa kweli, andiko la Methali 21:1 linatueleza hivi: “Moyo wa mfalme ni kama vijito vya maji mkononi mwa Yehova. Huugeuza kuelekea popote anapopenda.”

14 Yehova anaweza kuongoza matukio ili yatimize kusudi lake na kulitimiza kwa wakati unaofaa. Mengi ya mabadiliko muhimu ulimwenguni yamekuwa yakitimiza unabii, hasa unabii kuhusu kuhubiriwa kwa habari njema ya Ufalme wa Mungu ulimwenguni pote. Fikiria kuhusu kuporomoka kwa Muungano wa Sovieti na matokeo yake. Ni watu wachache waliotarajia kwamba mabadiliko hayo makubwa ya kisiasa yangetokea haraka hivyo. Hata hivyo, kwa sababu ya mabadiliko hayo, habari njema inahubiriwa sasa katika nchi nyingi ambako kazi yetu ilikuwa imepigwa marufuku hapo awali. Hivyo basi, kwa vyovyote vile acheni tujinunulie wakati unaofaa ili kumtumikia kwa uaminifu Mungu wa “nyakati na majira.”

UWE NA IMANI KWAMBA YEHOVA ATATENDA KWA WAKATI WAKE

15. Tunawezaje kuonyesha imani kuhusiana na marekebisho yanayofanywa na tengenezo?

15 Ili kuendelea kuhubiri habari njema ya Ufalme katika siku hizi za mwisho, mtu anahitaji kuwa na imani kwamba Yehova atatenda kwa wakati wake. Hali za ulimwengu zinazobadilika zinaweza kutulazimu kubadili njia fulani tunazotumia kutimiza kazi yetu ya kufanya wanafunzi. Pindi kwa pindi, huenda tengenezo likafanya marekebisho ili kushughulikia mahitaji ya kazi yetu tukiwa watangazaji wa Ufalme. Tunaonyesha imani yetu katika Mungu wa “nyakati na majira” kwa kuunga mkono kabisa marekebisho hayo tunapoendelea kutumikia kwa ushikamanifu chini ya Mwana wake, aliye “kichwa cha kutaniko.”—Efe. 5:23.

16. Kwa nini tunaweza kuwa na imani kwamba Yehova atatusaidia kwa wakati unaofaa?

16 Yehova anataka tujihisi huru kusali kwake tukiwa na hakika kabisa kwamba atatupatia “msaada kwa wakati unaofaa” tunapouhitaji. (Ebr. 4:16) Je, hilo halionyeshi kwamba anatupenda na kutujali tukiwa mtu mmoja-mmoja? (Mt. 6:8; 10:29-31) Tunaonyesha imani yetu katika Yehova Mungu kwa kusali kwa ukawaida na kuomba msaada wake na kisha kutenda kupatana na sala zetu na mwongozo wake. Zaidi ya hayo, tunakumbuka kusali kwa ajili ya waamini wenzetu.

17, 18. (a) Ni hatua gani ambayo Yehova atachukua hivi karibuni dhidi ya maadui wake? (b) Ni lazima tuepuke mtego gani?

17 Huu si wakati wa ‘kusitasita kwa ukosefu wa imani’; ni wakati wa kuwa na nguvu katika imani. (Rom. 4:20) Maadui wa Mungu, yaani, Shetani na wale walio chini ya uvutano wake, wanajaribu kusimamisha kazi ambayo Yesu aliwapa wafuasi Wake, kutia ndani nasi. (Mt. 28:19, 20) Licha ya mashambulizi ya Ibilisi, tunajua kwamba Yehova ni “Mungu aliye hai, ambaye ni Mwokozi wa watu wa namna zote, hasa wa watu waaminifu.” Yeye “anajua jinsi ya kuwakomboa watu wenye ujitoaji-kimungu kutoka katika jaribu.”—1 Tim. 4:10; 2 Pet. 2:9.

18 Hivi karibuni, Yehova ataleta mwisho wa mfumo huu mwovu wa mambo. Hata ingawa hatujapewa maelezo yote na wakati kamili ambao mwisho huo utakuja, tunajua kwamba kwa wakati unaofaa kabisa, Kristo atawaangamiza maadui wa Mungu, na enzi kuu ya Yehova itatetewa. Hivyo basi, lingekuwa kosa kama nini kushindwa kutambua “nyakati na majira” tunamoishi sasa! Acheni tusinaswe kamwe na mtego wa kufikiri kwamba “mambo yote yanaendelea sawasawa kama tangu mwanzo wa uumbaji.”—1 The. 5:1; 2 Pet. 3:3, 4.

‘ONYESHA MTAZAMO WA KUNGOJEA’

19, 20. Kwa nini tunapaswa kuonyesha mtazamo wa kumngojea Yehova?

19 Kusudi la Yehova Mungu tangu mwanzo lilikuwa kwamba wanadamu waishi milele ili waendelee kujifunza kumhusu na kuhusu uumbaji wake maridadi. Andiko la Mhubiri 3:11 linasema hivi: “[Yehova] amefanya kila kitu kiwe chenye kupendeza kwa wakati wake. Tena wakati usio na kipimo ameuweka ndani ya moyo wao, ili mwanadamu asiweze kugundua kazi ambazo Mungu wa kweli amefanya tangu mwanzo mpaka mwisho.”

20 Tunafurahi kama nini kwamba Yehova hajabadili kamwe kusudi lake kwa ajili ya mwanadamu! (Mal. 3:6) Mungu “habadiliki, kama kugeuka kwa kivuli.” (Yak. 1:17) Ratiba yake haitegemei njia za wanadamu za kupima wakati, kama vile mzunguko wa dunia. Yehova ni “Mfalme wa umilele.” (1 Tim. 1:17) Kwa hiyo, acheni ‘tuonyeshe mtazamo wa kumngojea Mungu wa wokovu wetu.’ (Mika 7:7) Hivyo basi, “iweni hodari, nayo mioyo yenu na iwe na nguvu, ninyi nyote mnaomngojea Yehova.”—Zab. 31:24.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 8 Tazama kitabu Sikiliza Unabii wa Danieli! ukurasa wa 186-195.

^ fu. 9 Tazama kitabu Sikiliza Unabii wa Danieli! ukurasa wa 94-97.

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 19]

Danieli alikuwa na imani katika utimizo wa unabii uliotolewa na Mungu

[Picha katika ukurasa wa 21]

Je, unautumia vizuri wakati wako kufanya mapenzi ya Yehova?