Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Simulizi la Maisha

Nilivutiwa na Watu Wazee Wenye Hekima

Nilivutiwa na Watu Wazee Wenye Hekima

Limesimuliwa na Elva Gjerde

Miaka 70 hivi iliyopita, mgeni fulani aliyetutembelea nyumbani alimpa baba yangu pendekezo ambalo lilibadili kabisa maisha yangu. Tangu siku hiyo muhimu, watu wengine wengi wamenisaidia sana maishani. Kwa msaada wa watu wote hao, nimepata rafiki mwenye thamani sana kuliko wengine wote. Acheni niwaeleze.

NILIZALIWA huko Sydney, Australia, mwaka wa 1932. Wazazi wangu walimwamini Mungu lakini hawakuwa wakienda kanisani. Mama yangu alinifundisha kwamba Mungu ananitazama daima na yuko tayari kuniadhibu nikiwa mtukutu. Hilo lilinifanya nimwogope Mungu. Hata hivyo, nilivutiwa sana na Biblia. Shangazi yangu alipotutembelea Jumamosi na Jumapili, alinisimulia hadithi nyingi za kupendeza kutoka katika Biblia. Sikuzote nilitazamia kwa hamu ziara zake.

Nilipokuwa tineja, baba yangu alisoma vitabu kadhaa ambavyo mama yangu alikuwa amepewa na mwanamke fulani mzee ambaye alikuwa Shahidi wa Yehova. Baba alivutiwa sana na mambo aliyosoma katika vitabu hivyo vya Kikristo hivi kwamba akakubali kujifunza Biblia na Mashahidi. Jioni moja alipokuwa akijifunza Biblia, baba alinikuta nikisikiliza mazungumzo yao kwa siri. Aliponiambia niende nikalale mgeni huyo alisema, “Kwa nini usimruhusu Elva ajiunge nasi?” Pendekezo hilo lilikuwa mwanzo wa maisha mapya na wa urafiki wangu pamoja na Mungu wa kweli, Yehova.

Muda mfupi baadaye, mimi na baba yangu tulianza kuhudhuria mikutano ya Kikristo. Mambo aliyojifunza yalimchochea kubadili maisha yake. Hata alianza kudhibiti hasira yake. Hilo lilimfanya mama na ndugu yangu mkubwa, Frank, waanze kuhudhuria mikutano. * Sote wanne tulifanya maendeleo na mwishowe tukabatizwa na kuwa Mashahidi wa Yehova. Tangu wakati huo, nimepata marafiki wengi wazee ambao wamenisaidia maishani.

NILIPOKUWA NIKICHAGUA KAZI YA KUFANYA MAISHANI

Nilipokuwa tineja, nilivutiwa na watu wazee katika kutaniko letu. Mmoja wao alikuwa Alice Place, dada mzee ambaye aliihubiria familia yetu mwanzoni. Alikuwa kama nyanya yangu. Alice alinizoeza katika huduma ya hadharani na kunitia moyo nibatizwe. Nikiwa na umri wa miaka 15, nilitimiza lengo au mradi huo.

Pia, nilisitawisha urafiki wa karibu na wenzi wa ndoa wazee, Percy na Madge [Margaret] Dunham. Kushirikiana nao kulinisaidia sana katika maisha yangu ya baadaye. Nilipenda hesabu sana, na niliazimia kuwa mwalimu wa hesabu. Percy na Madge walitumika wakiwa wamishonari huko Latvia katika miaka ya 1930. Vita vya Pili vya Ulimwengu vilipoanza huko Ulaya, walialikwa kutumikia katika Betheli ya Australia, katika viunga vya Sydney. Percy na Madge walipendezwa nami kikweli. Walisimulia mambo mengi yenye kusisimua ambayo walifurahia katika utumishi wao wa umishonari. Niliona waziwazi kwamba ningepata uradhi zaidi kwa kufundisha Biblia badala ya kufundisha hesabu. Kwa hiyo, niliamua kuwa mmishonari badala ya mwalimu.

Ndugu na Dada Dunham walinitia moyo nifanye upainia ili nijitayarishe kwa ajili ya utumishi wa umishonari. Hivyo, katika mwaka wa 1948, nikiwa na umri wa miaka 16, nilijiunga na vijana wengine kumi ambao walikuwa wakifurahia upainia katika kutaniko la nyumbani kwetu huko Hurstville, Sydney.

Katika muda wa miaka minne iliyofuata, nilifanya upainia katika miji mingine minne, yote iko New South Wales na Queensland. Betty Law (sasa anaitwa Remnant) alikuwa kati ya wanafunzi wangu wa kwanza wa Biblia. Betty, msichana mwenye kujali, alinizidi umri kwa miaka miwili. Baadaye tulifanya upainia pamoja katika mji wa Cowra, kilomita 230 hivi upande wa magharibi wa Sydney. Ingawa tulifanya upainia pamoja kwa muda mfupi tu, mimi na Betty tungali marafiki mpaka leo.

Baada ya kupokea mgawo wa kuwa painia wa pekee, nilihamia Narrandera, mji ulio umbali wa kilomita 220, upande wa kusini-magharibi wa mji wa Cowra. Mwenzi wangu mpya katika upainia aliitwa Joy Lennox (sasa anaitwa Hunter). Alikuwa painia mwenye bidii na yeye pia alinizidi umri kwa miaka miwili. Sisi peke yetu ndio tuliokuwa Mashahidi katika mji huo. Mimi na Joy tuliishi pamoja na Ray na Esther Irons, wenzi wa ndoa wenye ukarimu. Wenzi hao pamoja na mwana na mabinti wao watatu walipendezwa na kweli. Katikati ya juma, Ray na mwana wake walifanya kazi nje ya mji katika shamba la ngano ambamo pia kondoo walifugwa, huku Esther na mabinti wake wakitunza nyumba ya wageni katika mji huo. Kila Jumapili, mimi na Joy tulipika chakula kingi kwa ajili ya familia ya Irons na watu wengine 12 hivi walioishi katika nyumba ya wageni. Wanaume hao waliofanya kazi katika shirika la reli walikuwa wakila chakula kingi sana! Tulipunguziwa kodi ya nyumba kwa sababu ya kufanya kazi hiyo. Baada ya kusafisha vyombo, tuliiandalia familia ya Irons chakula cha kiroho chenye lishe, funzo la kila juma la Mnara wa Mlinzi. Ray, Esther, na watoto wao wanne walikubali kweli na kuwa washiriki wa kwanza wa Kutaniko la Narrandera.

Katika mwaka wa 1951, nilihudhuria kusanyiko la wilaya la Mashahidi wa Yehova huko Sydney. Katika kusanyiko hilo, nilihudhuria mkutano wa pekee wa mapainia ambao walipendezwa na kazi ya umishonari. Mapainia zaidi ya 300 walihudhuria mkutano huo ambao ulifanyiwa ndani ya hema kubwa. Nathan Knorr kutoka Betheli ya Brooklyn alihutubia kikundi hicho na kukazia kwamba kulikuwa na uhitaji wa haraka wa kuhubiri habari njema katika kila pembe ya dunia. Tulisikiliza kwa makini sana kila neno alilosema. Mapainia wengi waliohudhuria mkutano huo, baadaye walieneza kazi ya Ufalme katika Pasifiki ya Kusini na maeneo mengine. Nilisisimuka sana kuwa mmojawapo wa Waaustralia 17 walioalikwa kuhudhuria darasa la 19 la Shule ya Gileadi mwaka wa 1952. Nikiwa na umri wa miaka 20 tu, ndoto yangu ya kutumikia nikiwa mmishonari ilikuwa ikitimia!

NILIPOHITAJI KUFANYA MABADILIKO ZAIDI

Elimu niliyopata katika Shule ya Gileadi na pia ndugu na dada nilioshirikiana nao waliongeza ujuzi wangu wa Biblia na kuimarisha imani yangu, na pia walinisaidia kuboresha utu wangu. Nilikuwa kijana na nilikuwa na matumaini makubwa sana na nilitaka kila jambo nililofanya liwe kamilifu, na pia niliwatazamia wengine wawe wakamilifu. Nyakati nyingine nilikosa kabisa usawaziko. Kwa mfano, nilipomwona Ndugu Knorr akicheza mpira pamoja na kikundi cha vijana Wanabetheli, nilishtuka.

Bila shaka, walimu wa Gileadi ambao wote walikuwa wanaume wenye utambuzi na uzoefu wa miaka mingi waliona kwamba nilikuwa nikikabili hali ngumu kwa sababu ya utu wangu. Walipendezwa nami na kunisaidia kubadili njia yangu ya kufikiri. Hatua kwa hatua, nilianza kumwona Yehova kuwa Mungu mwenye upendo na uthamini, bali si Mungu mkali mwenye kudai mno. Baadhi ya wanafunzi wenzangu walinisaidia pia. Ninakumbuka mmoja wao akisema hivi: “Elva, huko mbinguni Yehova hatumii kiboko. Usijiwekee viwango vinavyopita kiasi!” Maneno yake manyoofu yaliugusa moyo wangu.

Baada ya Gileadi, mimi na wanafunzi wenzangu wanne tulipewa mgawo wa kutumika nchini Namibia, Afrika. Muda si muda, tulikuwa tukiongoza jumla ya mafunzo 80 ya Biblia. Niliipenda nchi ya Namibia na maisha ya umishonari, lakini nilimpenda mwanafunzi mwenzangu wa Gileadi ambaye alipewa mgawo wa kutumika nchini Uswisi. Baada ya kukaa Namibia kwa mwaka mmoja, nilijiunga na mchumba wangu huko Uswisi. Baada ya kufunga ndoa, nilijiunga na mume wangu katika kazi yake akiwa mwangalizi wa mzunguko.

NILIPOKABILI MATATIZO

Baada ya kufurahia kazi ya mzunguko kwa miaka mitano, tulialikwa kutumika katika Betheli ya Uswisi. Nikiwa katika familia ya Betheli ya Uswisi, nilisisimuka kushirikiana na ndugu na dada wengi wazee walio wakomavu kiroho.

Muda mfupi baadaye, niligundua jambo lenye kushtua sana, kwamba mume wangu hakuwa mwaminifu kwangu wala kwa Yehova. Kisha akaniacha. Nilivurugika kabisa! Sidhani ningeweza kukabiliana na hali hiyo bila upendo na utegemezo wa marafiki wangu wapendwa wazee katika familia ya Betheli. Walinisikiliza nilipohitaji kuzungumza na waliniacha nipumzike nilipohitaji kupumzika. Maneno yao yenye kufariji na matendo yao ya fadhili yalinitegemeza nilipokuwa na maumivu makali sana na yalinisaidia kumkaribia Yehova hata zaidi.

Pia, nilikumbuka maneno yaliyosemwa miaka iliyopita na watu wazee wenye hekima ambao walikuwa wamejifunza mengi kupitia majaribu. Kwa mfano, maneno ya Madge Dunham, aliyeniambia hivi pindi moja: “Elva, utakabili majaribu mengi maishani unapomtumikia Yehova, lakini majaribu magumu zaidi huenda yakatokana na wale walio karibu nawe. Unapopata majaribu hayo, mkaribie Yehova. Kumbuka kwamba unamtumikia yeye, si wanadamu wasio wakamilifu!” Shauri la Madge lilinisaidia kuvumilia majaribu mengi magumu. Niliazimia kutoruhusu kamwe makosa ya mume wangu yanitenganishe na Yehova.

Baada ya muda, niliamua kurudi Australia kufanya upainia nikiwa karibu na familia yetu. Nilipokuwa nikisafiri kwa meli kurudi nyumbani, nilifurahia kwa ukawaida mazungumzo mazuri ya Biblia pamoja na kikundi cha wasafiri wenzangu. Mwanamume mnyamavu kutoka Norway anayeitwa Arne Gjerde alikuwa katika kikundi hicho. Alifurahia mambo aliyosikia. Baadaye, Arne alinitembelea pamoja na familia yetu huko Sydney. Alifanya maendeleo ya kiroho haraka na kuja katika kweli. Katika mwaka wa 1963, mimi na Arne tulifunga ndoa, na miaka miwili baadaye nilijifungua mwana wetu, Gary.

NILIPOKABILI JARIBU LINGINE

Mimi, Arne, na Gary tulikuwa na maisha ya familia yenye furaha. Baada ya muda Arne alipanua nyumba yetu ili tuishi pamoja na wazazi wangu waliozeeka. Hata hivyo, baada ya miaka sita ya ndoa, tulipata pigo lingine tofauti lenye kushtua. Arne aligunduliwa kuwa na kansa ya ubongo. Nilimtembelea hospitalini kila siku alipokuwa akipokea tiba ya miale kwa muda mrefu. Kwa muda fulani, ilionekana ni kwamba alikuwa anapata nafuu; kisha hali yake ikazorota na akapata ugonjwa wa kupooza. Niliambiwa kwamba angeishi kwa majuma machache tu. Hata hivyo, Arne hakufa. Mwishowe alirudi nyumbani, ambako niliendelea kumtunza hadi afya yake ilipoboreka. Baada ya muda, aliweza kutembea tena na kurudia utendaji wake akiwa mzee wa kutaniko. Mtazamo wake wa furaha na ucheshi wake ulimsaidia kupata nafuu na hivyo ikawa rahisi zaidi kwangu kuendelea kumtunza.

Baada ya miaka mingi, mwaka wa 1986, afya ya Arne ilizorota tena. Tayari wazazi wangu walikuwa wamekufa, kwa hiyo tukahamia kwenye Milima ya Blue nje ya jiji la Sydney, karibu zaidi na marafiki wetu. Baadaye, Gary alimwoa Karin, dada mzuri sana wa kiroho, na wakapendekeza kwamba sote wanne tuishi katika nyumba moja. Baada ya miezi michache, sote tulihamia katika nyumba iliyokuwa karibu sana na mahali ambapo mimi na Arne tulikuwa tukiishi zamani.

Kwa muda wa miezi 18 ya mwisho ya maisha yake, Arne hakutoka kitandani na alihitaji kutunzwa daima. Kwa kuwa nilikaa nyumbani kwa muda mrefu wakati huo, nilitumia saa mbili kila siku kujifunza Biblia na machapisho ya Biblia. Katika vipindi hivyo vya kujifunza, nilipata mashauri mengi ya hekima kuhusu jinsi ya kukabiliana na hali yangu. Pia, nilionyeshwa upendo kwa kutembelewa na waliozeeka katika kutaniko letu, baadhi yao walikuwa wamevumilia majaribu kama yangu. Ziara zao zilinitia moyo kwelikweli! Arne alikufa mnamo Aprili 2003 akiwa na tumaini hakika la ufufuo.

YULE AMBAYE AMENITEGEMEZA ZAIDI

Nilipokuwa kijana, nilikuwa na matarajio makubwa sana. Lakini niligundua kwamba kwa kawaida mambo hayawi kama tunavyotarajia maishani. Nimefurahia baraka nyingi sana na pia nimevumilia misiba miwili mikubwa—mwenzi wangu mmoja aliniacha kwa sababu ya kutokuwa mwaminifu na mwingine alikufa kutokana na ugonjwa. Katika maisha yangu, nimepata mwongozo na faraja kutoka vyanzo mbalimbali. Yule ambaye angali ananitegemeza zaidi ni “Mzee wa Siku,” Yehova Mungu. (Dan. 7:9) Mashauri yake yamefinyanga utu wangu na kuniwezesha kupata mambo yenye kuthawabisha katika kazi ya umishonari. Matatizo yalipotokea, ‘fadhili zenye upendo za Yehova zilinitegemeza na faraja zake ziliikumbatia nafsi yangu.’ (Zab. 94:18, 19) Nimefurahia pia upendo na utegemezo wa familia yangu na wa ‘marafiki wa kweli waliozaliwa kwa ajili ya wakati wa taabu.’ (Met. 17:17) Wengi wao walikuwa watu wazee wenye hekima.

Mzee wa ukoo, Ayubu, aliuliza hivi: “Je, hekima haimo katikati ya wazee na uelewaji katika wingi wa siku?” (Ayu. 12:12) Nikifikiria miaka iliyopita ya maisha yangu, ninaweza kusema kwamba jibu ni ndiyo. Mashauri ya watu wazee wenye hekima yamenisaidia, faraja yao imenitegemeza, na urafiki wao umeboresha maisha yangu. Ninashukuru kwamba nilivutiwa nao.

Sasa nina umri wa miaka 80, mimi pia nimezeeka. Kwa sababu ya mambo niliyopitia maishani, niko tayari kuwasaidia wazee wenzangu. Bado ninapenda kuwatembelea na kuwasaidia. Lakini ninafurahia pia kuwa pamoja na vijana. Nguvu zao zinanichochea, na shauku yao inanitia moyo. Ninapoona vijana wakija kuniomba mwongozo au utegemezo, ninahisi kwamba ni pendeleo kuwasaidia.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 7 Baadaye, Frank Lambert, ndugu ya Elva, alikuwa painia mwenye bidii katika maeneo ya mashambani ya Australia. Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova cha 1983 cha Kiingereza kinaeleza kwenye ukurasa wa 110-112, mojawapo ya safari zake nyingi za kuhubiri zenye kusisimua.

[Picha katika ukurasa wa 14]

Nikifanya upainia pamoja na Joy Lennox huko Narrandera

[Picha katika ukurasa wa 15]

Elva akiwa na washiriki wa Betheli ya Uswisi mwaka wa 1960

[Picha katika ukurasa wa 16]

Nikimtunza Arne alipokuwa mgonjwa