Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutoka Katika Hifadhi ya Vitu Vyetu vya Kale

“Ninaendelea Kujifunza Kuipenda Zaidi Kazi ya Ukolpota Kila Siku”

“Ninaendelea Kujifunza Kuipenda Zaidi Kazi ya Ukolpota Kila Siku”

MWAKA wa 1886, nakala mia moja za Buku la Kwanza la kitabu Millennial Dawn, zilisafirishwa kutoka katika Bible House (Nyumba ya Biblia) huko Allegheny, Pennsylvania, Marekani, na kupelekwa Chicago, Illinois. Charles Taze Russell alitumaini kusambaza buku hilo jipya katika maduka yote ya vitabu. Mojawapo ya kampuni kubwa zaidi zinazosambaza vitabu vya kidini nchini Marekani ilikubali kusafirisha mabuku ya Millennial Dawn. Lakini baada ya majuma mawili, mabuku hayo yote yalirudishwa katika Bible House.

Inaripotiwa kwamba mwinjilisti aliyejulikana sana alikasirika alipoona mabuku ya Millennial Dawn yakiwa dukani pamoja na vitabu vyake. Mwinjilisti huyo alisema kwa hasira kwamba ikiwa vitabu hivyo havingeondolewa dukani, basi yeye na marafiki wake wainjilisti waliokuwa mashuhuri wangepeleka vitabu vyao na biashara yao kwingineko. Muuzaji wa vitabu aliyarudisha mabuku ya Dawn kwa shingo upande. Isitoshe, matangazo kuhusu mabuku hayo yalikuwa yamewekwa katika magazeti. Lakini wapinzani walihakikisha kwamba mkataba wa matangazo hayo umefutwa. Hivyo basi, kitabu hicho kipya kingewafikiaje watu waliokuwa wakitafuta kweli?

Makolpota, kama walivyoitwa wakati huo, walitatua tatizo hilo. * Mwaka wa 1881, gazeti la Zion’s Watch Tower lilitoa mwito wa kwamba wahubiri 1,000 wajitolee kusambaza machapisho ya Biblia kwa wakati wote. Ingawa makolpota hao walikuwa wachache sana, walitawanya mbegu za kweli kotekote kupitia machapisho hayo. Kufikia mwaka wa 1897, mabuku karibu milioni moja ya Dawn yalikuwa yamesambazwa, hasa na makolpota. Wengi wao waliishi kwa kutegemea kiasi kidogo cha pesa walichopokea kutokana na malipo ya Mnara wa Mlinzi au ya vitabu ambavyo watu walichukua.

Makolpota hao wenye ujasiri walikuwa akina nani? Baadhi yao walianza wakiwa matineja, na wengine walianza wakiwa na umri mkubwa. Wengi wao walikuwa waseja au wenzi wa ndoa wasio na watoto, lakini kulikuwa na familia nyingi zilizoshiriki katika kazi ya ukolpota. Makolpota wa kawaida walihubiri kwa siku nzima, na makolpota wasaidizi walihubiri kwa saa moja au mbili kila siku. Si kila mtu alikuwa na afya nzuri au hali zilizomwezesha kufanya kazi ya ukolpota. Lakini kwenye kusanyiko la wilaya la mwaka wa 1906, wale ambao wangeweza kufanya ukolpota waliambiwa kwamba hawakuhitaji “kuwa wasomi sana, au kuwa na kipawa cha pekee, au kuwa na ulimi wa malaika.”

Katika karibu kila bara, watu wa kawaida walitimiza kazi kubwa ajabu. Ndugu mmoja alikadiria kwamba katika muda wa miaka saba aliwaachia watu vitabu 15,000. Hata hivyo, alisema, “Sikuanza kazi ya ukolpota ili niwe muuzaji wa vitabu, badala yake, nilikusudia kutoa ushahidi kumhusu Yehova na kweli yake.” Mahali popote ambapo makolpota walienda, mbegu za kweli zilitia mizizi na vikundi vya Wanafunzi wa Biblia vikaanza kuongezeka.

Makasisi waliwadhihaki makolpota, wakiwaita wachuuzi wa vitabu. Gazeti la Mnara wa Mlinzi la 1892 lilisema hivi: “Ni watu wachache [wanaowaona] kuwa wawakilishi wa Bwana, au wanaotambua kwamba Bwana anawaheshimu sana kwa sababu ya unyenyekevu na kujidhabihu kwao.” Kwa kweli, maisha ya makolpota hayakuwa “maisha ya raha mustarehe,” kama kolpota mmoja alivyosema. Walivaa viatu vigumu na walisafiri hasa kwa baiskeli. Ikiwa mwenye nyumba hakuwa na pesa, makolpota walimwachia vitabu na kuchukua vyakula kama malipo. Baada ya kuhubiri kwa siku nzima, licha ya uchovu, wahubiri hao wenye furaha walirudi katika mahema yao na vyumba walivyokodi. Baadaye walibuni Magari ya Makolpota (Colporteur Wagon). Magari hayo yaliyotumiwa kama nyumba yaliokoa pesa nyingi na wakati. *

Kuanzia mwaka wa 1893, katika Kusanyiko la Wilaya la Chicago, programu za makusanyiko zilitia ndani sehemu za pekee za makolpota. Sehemu hizo zilikuwa na masimulizi yenye kusisimua sana ya mambo yaliyoonwa, mapendekezo kuhusu mbinu za kuhubiri, na mashauri yalitolewa. Wakati mmoja, Ndugu Russell aliwahimiza wahubiri wenye bidii waanze siku kwa kiamsha-kinywa chenye afya, wanywe bilauri au gilasi ya maziwa baadaye asubuhi, na soda ya aiskrimu siku yenye joto.

Makolpota waliokuwa wakimtafuta mfanyakazi mwenzi, au mtu wa kuhubiri naye, walivalia utepe wa rangi ya manjano. Makolpota wapya walihubiri pamoja na makolpota wenye uzoefu zaidi. Mazoezi hayo yalihitajika kwa sababu kolpota mmoja mpya alipokuwa akimwonyesha mwenye nyumba kitabu alimwambia hivi huku akiwa na wasiwasi: “Hutaki vitabu hivi, sivyo?” Jambo la kufurahisha ni kwamba mwenye nyumba huyo alivikubali vitabu hivyo, na baadaye akawa dada.

Ndugu mmoja aliuliza, ‘Je, niendelee na kazi yangu ya mshahara mnono na kutoa mchango wa dola 1,000 za Marekani kwa mwaka kwa ajili ya kazi ya ukolpota, au niwe kolpota?’ Aliambiwa kwamba Bwana angethamini jambo lolote kati ya mambo hayo mawili, lakini angepata baraka nyingi zaidi ikiwa angetumia wakati wake kumtumikia Bwana moja kwa moja. Mary Hinds aliona kazi ya ukolpota kuwa “njia bora ya kuwasaidia watu wengi zaidi.” Naye Alberta Crosby aliyekuwa mwoga alisema, “Ninaendelea kujifunza kuipenda zaidi kazi ya ukolpota kila siku.”

Leo, watoto wengi wa kimwili na wa kiroho wa makolpota hao wenye bidii bado wanaendelea kushikilia urithi wao wa kiroho. Ikiwa hamjawahi kuwa na kolpota au hamna painia katika familia yenu, kwa nini usijitahidi kuanzisha urithi wa familia yenu? Wewe pia utajifunza kila siku kuipenda zaidi kazi ya kuhubiri wakati wote.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 5 Baada ya mwaka wa 1931, neno “painia” lilianza kutumiwa badala ya neno “kolpota.”

^ fu. 8 Habari zaidi kuhusu magari yaliyotumiwa kama nyumba zitachapishwa katika toleo la wakati ujao.

[Blabu katika ukurasa wa 32]

Hawakuhitaji “kuwa wasomi sana, au kuwa na kipawa cha pekee, au kuwa na ulimi wa malaika”

[Picha katika ukurasa wa 31]

Kolpota A. W. Osei nchini Ghana, karibu mwaka wa 1930

[Picha katika ukurasa wa 32]

Juu: Kolpota Edith Keen na Gertrude Morris nchini Uingereza, karibu mwaka wa 1918; chini: Stanley Cossaboom na Henry Nonkes nchini Marekani, wakiwa na makatoni matupu baada ya kuwaachia watu vitabu vyote