Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Uwe na Maoni Yanayofaa Kuhusu Ndoa Yenye Matatizo

Uwe na Maoni Yanayofaa Kuhusu Ndoa Yenye Matatizo

Uwe na Maoni Yanayofaa Kuhusu Ndoa Yenye Matatizo

“Kwa watu waliofunga ndoa natoa maagizo, lakini si mimi bali ni Bwana.”—1 KOR. 7:10.

JE, UNAWEZA KUELEZA?

Ni katika njia gani Mungu anawaunganisha wenzi wa ndoa?

Wazee wanaweza kuwasaidiaje Wakristo ambao wana matatizo ya ndoa?

Tunapaswa kuionaje ndoa?

1. Wakristo wanaionaje ndoa, na kwa nini?

WAKRISTO wanapofunga ndoa, wanaweka nadhiri mbele za Mungu. Hilo ni daraka ambalo halipaswi kuchukuliwa kivivi hivi. (Mhu. 5:4-6) Kwa kuwa Yehova ndiye Mwanzilishi wa mpango wa ndoa, ‘amewaunganisha’ wale waliofunga ndoa. (Marko 10:9) Mungu anatambua muungano au kifungo hicho bila kujali sheria zilizotumiwa kuihalalisha ndoa hiyo. Watumishi wa Yehova wanapaswa kuiona ndoa kuwa mpango wa kudumu iwe walikuwa au hawakuwa waabudu wake wakati walipofunga ndoa.

2. Ni maswali gani yatakayozungumziwa katika makala hii?

2 Ndoa yenye mafanikio inaweza kuleta furaha nyingi. Lakini ni nini kinachoweza kufanywa ikiwa ndoa ina matatizo? Je, ndoa iliyodhoofika inaweza kuimarishwa? Kuna msaada gani kwa ajili ya wale ambao hawana amani katika ndoa yao?

JE, UTAPATA SHANGWE AU MAUMIVU YA MOYO?

3, 4. Ni nini kinachoweza kutokea ikiwa mtu anafanya uamuzi usio wa hekima anapomchagua mwenzi wa ndoa?

3 Ndoa ya Mkristo inapofanikiwa, humpa shangwe na humletea Yehova heshima. Ndoa hiyo ikivunjika inasababisha tu maumivu ya moyo. Mkristo mseja ambaye anafikiria kufunga ndoa anaweza kuweka msingi mzuri wa ndoa kwa kufuata mwongozo wa Mungu. Kwa upande mwingine, mtu anayefanya uamuzi usio wa hekima anapomchagua mume au mke anaweza kuvunjika moyo na kuhuzunika. Kwa mfano, baadhi ya vijana wanaanzisha urafiki wa kimapenzi na mtu wa jinsia tofauti wakati ambapo hawako tayari kutimiza madaraka ya maisha ya ndoa. Watu fulani wanapata mchumba kupitia Intaneti na kisha wanakimbilia kufunga ndoa isiyo na furaha hata kidogo. Wengine wanatenda dhambi nzito wakati wa uchumba, hata hivyo wanafunga ndoa, lakini huenda wakaanza maisha yao ya ndoa bila kuheshimiana.

4 Baadhi ya Wakristo hawaoi au kuolewa “katika Bwana tu” na hivyo wanateseka sana kwa sababu ya kuwa katika familia iliyogawanyika kidini. (1 Kor. 7:39) Ikiwa unapitia hali hiyo, sali ili Mungu akusamehe na kukusaidia. Mungu haondoi madhara yanayosababishwa na makosa ambayo mtu alifanya zamani, lakini anawasaidia wale wanaotubu kuvumilia majaribu. (Zab. 130:1-4) Jitahidi kwa moyo wote kumpendeza sasa na milele, na ‘shangwe ya Yehova itakuwa ngome yako.’—Neh. 8:10.

KIFUNGO CHA NDOA KINAPOKUWA HATARINI

5. Watu walio katika ndoa isiyo na furaha wanapaswa kuepuka mawazo gani?

5 Wale wanaoumia moyoni kwa sababu ya uhusiano wao wa ndoa labda wanajiuliza hivi: ‘Je, ndoa yangu isiyo na furaha inastahili kweli kuokolewa? Laiti ningeweza kuanza maisha mapya na mwenzi mwingine wa ndoa!’ Huenda wakaanza kufikiria kuvunja kifungo chao cha ndoa wakijiambia hivi: ‘Ooh, ninataka kuwa huru tena! Kwa nini nisimtaliki? Hata kama siwezi kupata talaka ya Kimaandiko, mbona tusitengane ili nifurahie maisha tena?’ Badala ya kufikiri kwa njia hiyo au kuwazia jinsi ambavyo mambo yangekuwa, Wakristo wanapaswa kujitahidi kuboresha hali yao ya sasa kwa kutafuta mwongozo wa Mungu na kuufuata.

6. Eleza maana ya maneno ya Yesu katika Mathayo 19:9.

6 Ikiwa Mkristo atapata talaka, huenda awe au asiwe huru kuoa au kuolewa tena kwa msingi wa Kimaandiko. Yesu alisema hivi: “Mtu yeyote anayemtaliki mke wake na kumwoa mwingine, ila kwa sababu ya uasherati, anafanya uzinzi.” (Mt. 19:9) Katika andiko hilo, neno “uasherati” linatia ndani uzinzi na dhambi nyingine nzito zinazohusiana na ngono. Ni muhimu Mkristo asali na kutafakari kwa uzito ikiwa anafikiria kumtaliki mwenzi wake wakati ambapo hakuna yeyote kati yao aliye na hatia ya kufanya uasherati.

7. Ndoa ya Mkristo ikivunjika huenda watazamaji wakafikiri nini?

7 Ndoa inapovunjika inaweza kuonyesha kwamba hali ya kiroho ya mtu imedhoofika. Mtume Paulo aliuliza swali hili zito: “Kwa kweli ikiwa mtu yeyote hajui jinsi ya kuisimamia nyumba yake mwenyewe, atalitunzaje kutaniko la Mungu?” (1 Tim. 3:5) Kwa kweli, wenzi wote wawili wanapodai kuwa Wakristo na bado ndoa yao inavunjika, huenda watazamaji wakafikiri kwamba kwa kweli watu hao hawatendi kupatana na mambo wanayohubiri.—Rom. 2:21-24.

8. Wenzi wa ndoa Wakristo wakiamua kuachana ni lazima kuwe na tatizo gani?

8 Wenzi wa ndoa waliobatizwa wanapopanga kutengana au kutalikiana kwa msingi usio wa Kimaandiko, bila shaka wana tatizo la kiroho katika maisha yao. Ni wazi kwamba mmoja wao au labda wote wawili hawafuati kanuni za Kimaandiko. Ikiwa kweli walikuwa ‘wakimtegemea Yehova kwa moyo wao wote,’ hakungekuwa na sababu yoyote ya kuamini kwamba wangeshindwa kuizuia ndoa yao isivunjike.—Soma Methali 3:5, 6.

9. Baadhi ya Wakristo ambao wamejitahidi kwa subira kufanikisha ndoa yao wamethawabishwaje?

9 Ndoa nyingi ambazo zilikuwa zinaelekea kuvunjika, baada ya muda zimefanikiwa sana. Wakristo ambao wanaazimia kutovunja haraka-haraka ndoa yenye matatizo mara nyingi wanapata thawabu kubwa. Fikiria jambo linaloweza kutokea katika familia iliyogawanyika kidini. Mtume Petro aliandika hivi: “Ninyi wake, jitiisheni kwa waume zenu wenyewe, ili, ikiwa wowote si watiifu kwa lile neno, wavutwe bila neno kupitia mwenendo wa wake zao, kwa sababu wamekwisha kushuhudia kwa macho mwenendo wenu ulio safi kiadili pamoja na heshima kubwa.” (1 Pet. 3:1, 2) Naam, mwenzi ambaye si mwamini anaweza kukubali kweli kwa sababu ya mwenendo mzuri wa mwenzi wake mwamini! Ndoa hiyo ambayo imeokolewa inamletea Mungu heshima na inaweza kumletea baraka nyingi mume, mke, na watoto ambao huenda wakawa nao.

10, 11. Ni matatizo gani yanayoweza kutokea kwa ghafla katika ndoa, lakini Mkristo anaweza kuwa na uhakika gani?

10 Wakristo wengi waseja wanachagua waamini wenzao waliojiweka wakfu kuwa wenzi wa ndoa kwa sababu wanatamani kumpendeza Yehova. Hata hivyo, hali zinaweza kubadilika kwa ghafla. Kwa mfano, katika visa fulani, huenda mwenzi wa ndoa akapata matatizo makubwa ya kihisia. Au muda mfupi baada ya arusi, huenda mwenzi wa ndoa akawa mhubiri asiyetenda. Kwa mfano, Linda, * Mkristo mwenye bidii na mama mwenye upendo, alitazama bila kujua afanye nini mume wake aliyebatizwa alipoanza kujiendesha kwa njia isiyopatana na Maandiko bila kutubu, na hivyo akatengwa na ushirika. Mkristo anapaswa kufanya nini ikiwa inaonekana kwamba ndoa yake imeharibika kwa sababu kama hiyo na hakuna matumaini yoyote?

11 Huenda ukajiuliza hivi: ‘Je, ni lazima niendelee kujaribu kuiokoa ndoa yangu hata hali ziweje?’ Hakuna mtu anayeweza au anayepaswa kukufanyia uamuzi huo. Hata hivyo, kuna sababu nzuri za kuendelea kuimarisha kifungo cha ndoa kinachodhoofika bila kukata tamaa. Mungu anamthamini sana mwanamume au mwanamke anayemwogopa ambaye anavumilia majaribu katika ndoa yenye matatizo kwa sababu ya dhamiri yake. (Soma 1 Petro 2:19, 20.) Kupitia Neno lake na roho yake, Yehova atamsaidia Mkristo ambaye anajitahidi kabisa kuiimarisha ndoa yake yenye matatizo.

WAKO TAYARI KUSAIDIA

12. Wazee watatuonaje tukiwaomba msaada?

12 Ukikabili matatizo ya ndoa, usisite kutafuta msaada wa kiroho kutoka kwa Wakristo wakomavu. Wazee wanatumika wakiwa wachungaji wa kundi na watafurahi kukuonyesha mashauri yaliyoongozwa na roho takatifu ambayo yanapatikana katika Maandiko. (Mdo. 20:28; Yak. 5:14, 15) Usikate kauli kwamba wewe na mwenzi wako wa ndoa hamtaheshimiwa na wazee mkiwaomba msaada wa kiroho na kuzungumza nao kuhusu tatizo lenu zito la ndoa. Watawapenda na kuwaheshimu hata zaidi wanapoona kwamba mnatamani kabisa kumpendeza Mungu.

13. Ni shauri gani linalopatikana katika 1 Wakorintho 7:10-16?

13 Wazee wanapoombwa wawasaidie Wakristo wanaoishi katika familia iliyogawanyika kidini, wanarejelea shauri kama la Paulo, aliyeandika hivi: “Kwa watu waliofunga ndoa natoa maagizo, lakini si mimi bali ni Bwana, kwamba mke hapaswi kuondoka kwa mume wake; lakini kwa kweli akiondoka, na akae mseja kama sivyo apatane tena na mume wake; na mume hapaswi kumwacha mke wake. . . . Kwa maana, wewe mke, unajuaje kama utamwokoa mume wako? Au, wewe mume, unajuaje kama utamwokoa mke wako?” (1 Kor. 7:10-16) Inakuwa baraka kama nini wakati mwenzi wa ndoa ambaye si mwamini anapovutiwa  na kujiunga na ibada ya kweli!

14, 15. Ni wakati gani kwa kweli mwenzi wa ndoa Mkristo anaweza kufikiria kuondoka, lakini kwa nini ni muhimu asali kuhusu jambo hilo na kulifikiria kwa unyoofu?

14 Ni katika hali gani mke Mkristo anaweza ‘kwa kweli kuondoka’? Wengine wameamua kutengana kwa sababu mwenzi wao anakataa kimakusudi kuandaa mahitaji ya familia. Wengine wametengana kwa sababu mwenzi wao anawatesa sana kimwili au anahatarisha kabisa hali yao ya kiroho wakiwa Wakristo.

15 Kutengana au kutotengana na mwenzi wa ndoa ni uamuzi wa mtu binafsi. Hata hivyo, mwenzi aliyebatizwa anapaswa kusali kuhusu jambo hilo na kulifikiria kwa unyoofu. Kwa mfano, je, mwenzi ambaye si mwamini ndiye ambaye amehatarisha kabisa hali ya kiroho ya mwenzi Mkristo, au je, Mkristo mwenyewe amekuwa akipuuza funzo la Biblia, amekuwa hahudhurii mikutano kwa ukawaida, na hashiriki kwa ukawaida katika huduma?

16. Ni nini kinachopaswa kuwazuia Wakristo kuamua haraka-haraka kutalikiana?

16 Uhakika wa kwamba tunathamini uhusiano wetu pamoja na Mungu na kuthamini zawadi yake ya ndoa unapaswa kutuzuia kuamua haraka-haraka kutalikiana. Tukiwa watumishi wa Yehova, tunahangaikia kutakaswa kwa jina lake takatifu. Basi, bila shaka hatungetaka kamwe kupanga njama ya kumwacha mwenzi wetu wa ndoa huku tukipanga moyoni kuoa au kuolewa na mtu mwingine.—Yer. 17:9; Mal. 2:13-16.

17. Ni katika hali gani inaweza kusemwa kwamba Mungu amewaita Wakristo waliofunga ndoa kwenye amani?

17 Mkristo ambaye ameoa au kuolewa na mtu ambaye si mwamini anapaswa kujitahidi kabisa kuendelea kudumisha kifungo cha ndoa. Hata hivyo, Mkristo hahitaji kujiona kuwa na hatia ikiwa amejitahidi kwa unyoofu kudumisha kifungo cha ndoa lakini mwenzi wake wa ndoa ambaye si mwamini anakataa kuendelea kuishi naye. Paulo aliandika hivi: “Yule asiyeamini akiondoka, acha aondoke; ndugu au dada hayumo katika utumwa chini ya hali za namna hiyo, lakini Mungu amewaita ninyi kwenye amani.”—1 Kor. 7:15. *

MTUMAINI YEHOVA

18. Hata ikiwa ndoa haiwezi kuokolewa, jitihada za kujaribu kuiokoa zinaweza kuwa na matokeo gani mazuri?

18 Unaposhughulikia tatizo lolote la ndoa, mtegemee Yehova ili akupe uhodari na umtumaini sikuzote. (Soma Zaburi 27:14.) Mfikirie Linda, ambaye alitajwa mwanzoni mwa makala hii. Mwishowe, ndoa yake iliishia katika talaka ingawa alijitahidi na kujaribu kwa miaka mingi kuiokoa. Je, anahisi kwamba alipoteza wakati wake? Anasema hivi: “Sihisi hivyo hata kidogo. Jitihada zangu ziliwatolea ushahidi mzuri watazamaji. Nina dhamiri safi. Jambo bora zaidi ni kwamba miaka hiyo ilimsaidia binti yetu kubaki akiwa imara katika kweli. Baadaye alijiweka wakfu kwa Yehova na kuwa Shahidi mwenye bidii.”

19. Ni nini kinachoweza kutokea mtu akijitahidi kuiokoa ndoa yake?

19 Mwanamke Mkristo anayeitwa Marilyn anafurahi kwamba alimtegemea Mungu na kujitahidi sana kuiokoa ndoa yake. Anasema hivi: “Nilianza kufikiria kutengana na mume wangu kwa sababu hakunitegemeza kifedha na alihatarisha hali yangu ya kiroho. Hata hivyo, mume wangu alitumikia akiwa mzee kabla ya kujihusisha na biashara fulani zisizofaa. Alianza kukosa mikutano, na tukaacha kuwasiliana. Shambulizi la kigaidi katika jiji letu liliniogopesha sana hivi kwamba nilijitenga na wengine. Kisha nikatambua kwamba mimi pia nilikosea. Tulianza kuwasiliana tena, tukaanzisha tena funzo letu la familia, na kuhudhuria tena mikutano kwa ukawaida. Wazee walikuwa wenye fadhili na walitusaidia sana. Ndoa yetu ikaanza tena kusitawi. Baada ya muda, mume wangu alistahili tena kupata mapendeleo kutanikoni. Tulijifunza kupitia hali ngumu lakini matokeo yalikuwa yenye kufurahisha.”

20, 21. Tunapaswa kuazimia kufanya nini kuhusiana na ndoa?

20 Iwe sisi ni waseja au tumefunga ndoa, acheni sikuzote tutende kwa uhodari na kumtumaini Yehova. Ikiwa ndoa yetu ina matatizo, tunapaswa kujitahidi kabisa kuyatatua, huku tukikumbuka kwamba wale ambao wameunganishwa katika ndoa ‘si wawili tena, bali ni mwili mmoja.’ (Mt. 19:6) Na acheni tukumbuke kwamba licha ya matatizo, tukivumilia katika familia iliyogawanyika kidini, huenda tukapata shangwe ya kumsaidia mwenzi wetu wa ndoa ajiunge na ibada ya kweli.

21 Katika hali yoyote ile tunayokabili, na tuazimie kujiendesha kwa busara ili tuwatolee ushuhuda mzuri wale wanaotutazama ambao si Mashahidi wa Yehova. Ikiwa ndoa yetu iko hatarini, acheni tusali kwa bidii, tuchanganue nia yetu kwa unyoofu, na kuchunguza Maandiko kwa uangalifu, na kuwaomba wazee watusaidie kiroho. Zaidi ya yote, acheni tuazimie kumpendeza Yehova Mungu katika mambo yote na kuthamini kikweli ndoa kwa kuwa ni zawadi nzuri ajabu kutoka kwake.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 10 Majina yamebadilishwa.

^ fu. 17 Tazama kitabu “Jitunzeni Katika Upendo wa Mungu,” ukurasa wa 219-221; gazeti Mnara wa Mlinzi la Novemba 1, 1988, ukurasa wa 26-27; Juni 1, 1977, ukurasa wa 262.

[Maswali ya Funzo]

[Blabu katika ukurasa wa 10]

Mara nyingi Wakristo ambao hawaamui haraka-haraka kuivunja ndoa yenye matatizo wanapata thawabu kubwa

[Blabu katika ukurasa wa 12]

Sikuzote mtumaini Yehova na umtegemee ili akupe uhodari

[Picha katika ukurasa wa 9]

Yehova anawabariki wenzi wa ndoa Wakristo ambao wanajitahidi kuimarisha ndoa yenye matatizo

[Picha katika ukurasa wa 11]

Kutaniko la Kikristo linaweza kuandaa faraja na msaada wa kiroho