Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Acha Yehova Akuongoze Kupata Uhuru wa Kweli

Acha Yehova Akuongoze Kupata Uhuru wa Kweli

Acha Yehova Akuongoze Kupata Uhuru wa Kweli

‘Chunguza ndani ya sheria kamilifu iliyo ya uhuru.’​—YAK. 1:25.

JE, UNAWEZA KUELEZA?

Ni sheria gani inayoongoza kwenye uhuru wa kweli, na ni nani wanaofaidika kutokana na sheria hiyo?

Ni nini siri ya kupata uhuru wa kweli?

Wote wanaoendelea kutembea kwenye njia ya uzima watapata uhuru gani?

1, 2. (a) Unaweza kusema nini kuhusu uhuru wa watu leo, na kwa nini hali iko hivyo? (b) Ni uhuru gani ambao watumishi wa Yehova watapata wakati ujao?

TUNAISHI wakati ambapo mambo kama vile pupa, uasi-sheria, na jeuri yanazidi kuongezeka. (2 Tim. 3:1-5) Ili kukabiliana na matatizo hayo, serikali zinatunga sheria zaidi, zinaimarisha vikosi vya polisi, na kutumia vifaa vya kielektroniki vya ulinzi. Katika nchi fulani, raia wanajaribu kuongeza usalama wao kwa kuweka ving’ora katika nyumba zao, na pia kufunga milango yao kwa makufuli mengi zaidi na hata kuweka nyua za umeme. Watu wengi hawatoki nje usiku au kuwaruhusu watoto wao wacheze nje peke yao iwe mchana au usiku. Ni wazi kwamba watu wanazidi kupoteza uhuru wao na inaelekea kwamba hali hiyo itazidi kuwa mbaya.

2 Katika bustani ya Edeni, Shetani alidai kwamba siri ya kupata uhuru wa kweli ni kutomtegemea Yehova. Dai hilo limethibitika kuwa la uwongo na la uovu kama nini! Kwa kweli, kadiri watu wanavyopuuza mipaka ya maadili na ya kiroho ambayo Mungu ameweka, ndivyo wanadamu kwa ujumla wanavyozidi kuteseka. Hali hiyo inayozidi kuwa mbaya inatuathiri sisi pia tukiwa watumishi wa Yehova. Hata hivyo, tunatumaini kuona wanadamu wakiwekwa huru kutoka katika utumwa wa dhambi na uharibifu na kufurahia ule ambao Biblia inauita “uhuru wenye utukufu wa watoto wa Mungu.” (Rom. 8:21) Kwa kweli, tayari Yehova ameanza kuwatayarisha watumishi wake ili wafurahie uhuru huo. Kwa njia gani?

3. Yehova amewapa wafuasi wa Kristo sheria gani, na ni maswali gani tutakayochunguza?

3 Jibu linategemea ile sheria ambayo mwandikaji wa Biblia, Yakobo, aliiita “sheria kamilifu iliyo ya uhuru.” (Soma Yakobo 1:25.) Tafsiri nyingine za Biblia zinatafsiri hivi maneno hayo, “sheria ambayo inatufanya tuwe huru” (The New English Bible) na “sheria kamilifu ya uhuru” (The New American Bible). Bila shaka, kwa kawaida watu wanaposikia neno “sheria” wanalihusianisha na vizuizi, bali si uhuru. Basi, ni nini “sheria kamilifu iliyo ya uhuru”? Na sheria hiyo inatuwekaje huru?

SHERIA INAYOTUWEKA HURU

4. “Sheria kamilifu iliyo ya uhuru” ni nini, na ni nani wanaofaidika nayo?

4 “Sheria kamilifu iliyo ya uhuru” si Sheria ya Musa, kwa sababu Sheria ya Musa ilifanya makosa yawe wazi na ilitimizwa na Kristo. (Mt. 5:17; Gal. 3:19) Hivyo basi, Yakobo alikuwa akizungumza kuhusu sheria gani? Alikuwa akizungumza kuhusu “sheria ya Kristo,” ambayo pia inaitwa “sheria ya imani” na “sheria ya watu huru.” (Gal. 6:2; Rom. 3:27; Yak. 2:12) Kwa hiyo, “sheria kamilifu” inatia ndani kila jambo ambalo Yehova anataka tufanye. Wakristo watiwa-mafuta na “kondoo wengine” wanafaidika na sheria hiyo.​—Yoh. 10:16.

5. Kwa nini sheria ya uhuru si mzigo mzito?

5 Tofauti na sheria za nchi nyingi, “sheria kamilifu” si ngumu kueleweka wala si mzigo mzito bali inatia ndani amri rahisi na kanuni za msingi. (1 Yoh. 5:3) Yesu alisema hivi: “Nira yangu ni laini na mzigo wangu ni mwepesi.” (Mt. 11:29, 30) Zaidi ya hayo, “sheria kamilifu” haihitaji kuwa orodha ndefu ya vizuizi, au adhabu, kwa sababu inategemea upendo na imeandikwa katika akili na mioyo, si kwenye mabamba ya mawe.​—Soma Waebrania 8:6, 10.

JINSI “SHERIA KAMILIFU” INAVYOTUWEKA HURU

6, 7. Tunaweza kusema nini kuhusu viwango vya Yehova, na kwa nini sheria ya uhuru inatuweka huru?

6 Mipaka ambayo Yehova amewawekea viumbe wake wenye akili inawanufaisha na kuwalinda. Kwa mfano, fikiria sheria za kiasili ambazo zinadhibiti nishati na vitu mbalimbali. Watu hawalalamiki kwamba sheria hizo zinawakandamiza. Badala yake, wanazithamini, na kutambua kwamba sheria za kiasili ni muhimu kwa ajili ya hali yao njema. Vivyo hivyo, viwango vya Yehova vya maadili na vya kiroho, tunavyojifunza kupitia ile “sheria kamilifu” ya Kristo, vimewekwa kwa faida ya wanadamu.

7 Mbali na kwamba inatulinda, sheria ya uhuru inaturuhusu kutosheleza tamaa zetu zote zinazofaa bila kujiumiza au kuingilia uhuru na haki ya wengine. Basi siri ya kuwa huru kikweli, yaani, kuweza kufanya mambo tunayotamani, ni kusitawisha tamaa zinazofaa, ambazo zinapatana na utu wa Yehova na viwango vyake. Kwa maneno mengine, tunapaswa kujifunza kupenda mambo ambayo Yehova anapenda na kuchukia yale anayochukia, na sheria ya uhuru inatusaidia kufanya hivyo.—Amo. 5:15.

8, 9. Wale wanaoshikamana na sheria ya uhuru wanapata faida gani? Toa mfano.

8 Kwa sababu ya hali yetu ya kutokamilika, tunapambana na mwili wetu ili kushinda tamaa zisizofaa. Hata hivyo, tunapofuata kwa ushikamanifu sheria ya uhuru, tunafurahia kwa kadiri fulani uwezo wa sheria hiyo wa kutuweka huru hata sasa. Kwa mfano, mwanafunzi mpya wa Biblia anayeitwa Jay alizoea kuvuta tumbaku. Alipojifunza kwamba zoea hilo halimpendezi Mungu, alilazimika kufanya uamuzi. Je, angeendelea kuutii mwili wake au angejitiisha chini ya Yehova? Kwa hekima, alichagua kumtumikia Mungu, hata ingawa mwili wake ulitamani sana tumbaku. Alihisije baada ya kushinda zoea hilo? Baadaye alisema hivi: “Nilifurahi sana na kujihisi nikiwa huru kabisa.”

9 Jay alijifunza kupitia mambo aliyokabili kwamba uhuru wa ulimwengu, ambao unawaruhusu watu ‘kukaza akili juu ya mwili,’ kwa kweli unawafanya wawe watumwa, lakini uhuru wa Yehova, ambao unamaanisha “kukaza akili juu ya roho,” unawaweka watu huru na kuwawezesha kupata “uzima na amani.” (Rom. 8:5, 6) Jay alipata wapi nguvu za kushinda zoea lake ambalo lilimfanya awe mtumwa? Nguvu hizo zilitoka kwa Mungu; hazikuwa nguvu zake mwenyewe. Alisema hivi: “Nilijifunza Biblia kwa ukawaida, nilisali ili nipate roho takatifu, na kutafuta msaada wenye upendo ambao nilipewa kwa hiari na kutaniko la Kikristo.” Maandalizi hayohayo yanaweza kutusaidia sisi sote kupata uhuru wa kweli. Acheni tuone jinsi yanavyoweza kutusaidia.

CHUNGUZA NENO LA MUNGU

10. “Kuchunguza” ndani ya sheria ya Mungu kunamaanisha nini?

10 Andiko la Yakobo 1:25 linasema hivi kwa sehemu: “Yeye anayechunguza ndani ya sheria kamilifu iliyo ya uhuru na ambaye hudumu katika hiyo . . . atakuwa mwenye furaha katika kuitenda.” Neno la awali la Kigiriki ambalo linatafsiriwa kuwa “anayechunguza” linamaanisha “kuinama ili kuangalia kwa makini,” na linatoa wazo la kujitahidi kwa bidii. Naam, ikiwa tunataka sheria ya uhuru iguse akili na moyo wetu, ni lazima tutimize sehemu yetu kwa kujifunza Biblia kwa bidii, kusali, na kutafakari kuhusu yale tunayosoma.​—1 Tim. 4:15.

11, 12. (a) Yesu alikaziaje uhitaji wa kufanya kweli iwe njia yetu ya maisha? (b) Kulingana na mfano ulio katika fungu, ni hatari gani ambayo vijana hasa wanapaswa kuepuka?

11 Wakati huohuo, ni lazima ‘tudumu,’ au tuendelee, kufuata Neno la Mungu, na hivyo kufanya kweli iwe njia yetu ya maisha. Yesu alitoa wazo hilohilo alipowaambia hivi watu fulani waliomwamini: “Mkikaa katika neno langu, ninyi kwa kweli ni wanafunzi wangu, nanyi mtaijua kweli, nayo kweli itawaweka ninyi huru.” (Yoh. 8:31, 32) Kitabu kimoja kinasema kwamba neno “kujua,” katika andiko hilo linamaanisha pia kuthamini kwa sababu “jambo ‘linalojulikana’ ni lenye thamani au ni muhimu kwa yule anayelijua.” Kwa hiyo, ‘tunajua’ kweli katika maana kamili tunapoifanya kweli hiyo iwe njia yetu ya maisha. Hapo ndipo tunapoweza kwa kufaa kusema kwamba “neno la Mungu” “linafanya kazi” ndani yetu, likifinyanga utu wetu ili tumwige kwa ukaribu zaidi Baba yetu wa mbinguni.​—1 The. 2:13.

12 Jiulize hivi: ‘Je, kwa hakika ninaijua kweli? Je, nimeifanya iwe njia yangu ya maisha? Au bado ninatamani “uhuru” wa ulimwengu?’ Akifikiria miaka yake ya utineja, dada mmoja ambaye alilelewa na wazazi Wakristo aliandika hivi: “Unapolelewa katika familia inayofuata kweli, ni kana kwamba Yehova yuko daima katika familia yenu. Lakini mimi kwa kweli sikumjua kamwe. Sikujifunza kamwe kuchukia mambo anayochukia. Sikuamini kamwe kwamba alijali mambo niliyofanya. Na sikujifunza kamwe kuzungumza naye katika sala nilipokuwa na matatizo. Nilitegemea uelewaji wangu mwenyewe, lakini sasa ninajua kwamba lilikuwa jambo la upumbavu kutegemea uelewaji wangu kwa sababu sikujua chochote.” Inafurahisha kwamba baadaye dada huyo alitambua kwamba alifikiri kwa njia isiyofaa kabisa, na hivyo akafanya mabadiliko makubwa. Hata alianza kutumikia akiwa painia wa kawaida.

ROHO TAKATIFU INAWEZA KUKUSAIDIA UWE HURU

13. Roho takatifu ya Mungu inatusaidiaje kuwa huru?

13 Katika andiko la 2 Wakorintho 3:17, tunasoma hivi: “Mahali palipo na roho ya Yehova, pana uhuru.” Roho takatifu inatusaidiaje kuwa huru? Kati ya mambo mengine, inasitawisha ndani yetu sifa muhimu ambazo zinatuwezesha kuwa huru—“upendo, shangwe, amani, ustahimilivu, fadhili, wema, imani, upole, kujizuia.” (Gal. 5:22, 23) Bila sifa hizo, hasa upendo, watu hawawezi kuwa huru kikweli, na jambo hilo linaonekana wazi ulimwenguni leo. Inapendeza kujua kwamba baada ya kutaja sifa za tunda la roho, mtume Paulo aliongezea hivi: “Hakuna sheria juu ya mambo hayo.” Alimaanisha nini? Hakuna sheria yoyote inayoweza kulizuia tunda la roho ya Mungu lisiendelee kukua. (Gal. 5:18) Kwa wazi, sheria ya aina hiyo ingekuwa na faida gani? Ni mapenzi ya Yehova kwamba tusitawishe sifa kama za Kristo milele na kuonyesha sifa hizo bila kuzuiwa.

14. Ni katika njia gani roho ya ulimwengu inawafanya watu wanaojitiisha chini yake kuwa watumwa?

14 Wale ambao ni watumwa wa roho ya ulimwengu na ambao wanatosheleza tamaa zao za kimwili bila kujali huenda wakafikiri kwamba wako huru. (Soma 2 Petro 2:18, 19.) Hata hivyo, ukweli ni kwamba wao ni watumwa. Ni lazima maagizo na sheria nyingi sana zitungwe ili kudhibiti tamaa na tabia zao zenye kudhuru. Paulo anasema kwamba “sheria huwekwa, si kwa ajili ya mtu mwadilifu, bali kwa ajili ya watu wenye kuasi sheria na watundu.” (1 Tim. 1:9, 10) Watu hao pia ni watumwa wa dhambi, wanachochewa kufanya “mambo yanayopendwa na mwili,” mwili ambao ni bwana mkatili. (Efe. 2:1-3) Kwa njia fulani, watu hao ni kama wadudu wanaotambaa na kuingia ndani ya bakuli la asali. Wanasukumwa na tamaa yao, na kwa ghafula wanajikuta wamenaswa.​—Yak. 1:14, 15.

KUWEKWA HURU KATIKA KUTANIKO LA KIKRISTO

15, 16. Ushirika wetu katika kutaniko ni muhimu kadiri gani, na tunafurahia uhuru gani?

15 Ulipoanza kushirikiana na kutaniko la Kikristo, hukujiunga na kutaniko kana kwamba unajiunga na chama cha kijamii. Badala yake, uliingia katika kutaniko kwa sababu Yehova alikuvuta. (Yoh. 6:44) Ni nini kilichomchochea Yehova akuvute? Je, ni kwa sababu aliona wewe ni mtu mwadilifu anayemwogopa Mungu? Huenda ukajibu, “La, hasha!” Basi, Mungu aliona nini? Aliona kwamba una moyo ambao utakubali sheria yake inayowaweka watu huru, moyo ambao utajitiisha chini ya mwongozo wake wenye fadhili. Katika kutaniko, Yehova ameujenga moyo wako kwa kukulisha kiroho, kukuweka huru kutokana na uwongo wa kidini, ushirikina, na kukufundisha kusitawisha utu kama wa Kristo. (Soma Waefeso 4:22-24.) Matokeo ni kwamba umepata pendeleo la kuwa kati ya watu pekee ulimwenguni ambao wanaweza kwa kufaa kuitwa “watu huru.”​—Yak. 2:12.

16 Fikiria jambo hili: Je, unaogopa unapokuwa pamoja na watu wanaompenda Yehova kwa moyo wao wote? Je, unajikuta kila mara ukitazama huku na huku kwa wasiwasi? Unapoongea na ndugu na dada zako katika Jumba la Ufalme, je, unaogopa kwamba huenda wakaiba vitu vyako? Huogopi kamwe! Unatulia na kuhisi ukiwa huru. Je, ungehisi hivyo katika mkutano wa kilimwengu? Inaelekea kwamba hungehisi hivyo! Zaidi ya hayo, uhuru ambao unafurahia miongoni mwa watu wa Mungu ni kionjo tu cha uhuru ambao utafurahia wakati ujao.

“UHURU WENYE UTUKUFU WA WATOTO WA MUNGU”

17. Uhuru wa wanadamu unahusianaje na “kufunuliwa kwa wana wa Mungu”?

17 Paulo alipokuwa akizungumza kuhusu uhuru ambao Yehova atawapa watumishi wake duniani, aliandika hivi: “Uumbaji unangojea na kutazamia kwa hamu kufunuliwa kwa wana wa Mungu.” Kisha akaongezea hivi: “Uumbaji wenyewe pia utawekwa huru kutoka katika utumwa wa uharibifu na kuwa na uhuru wenye utukufu wa watoto wa Mungu.” (Rom. 8:19-21) “Uumbaji” unarejelea wanadamu ambao wana tumaini la kuishi milele duniani, wale ambao watafaidika wakati wa “kufunuliwa” kwa wana wa Mungu waliotiwa mafuta kwa roho. Kufunuliwa huko kutaanza wakati “wana” hao, ambao watakuwa wamefufuliwa na kuingia katika makao ya roho, watakaposhirikiana na Kristo katika kuondoa kabisa uovu duniani na kuokoa “umati mkubwa” ili uingie katika mfumo mpya wa mambo.​—Ufu. 7:9, 14.

18. Uhuru utaongezekaje kwa wanadamu watiifu, na ni uhuru gani ambao watafurahia mwishowe?

18 Wakati huo, wanadamu waliokombolewa watapata uhuru mpya kabisa, uhuru kutokana na uvutano wa Shetani na roho waovu. (Ufu. 20:1-3) Jambo hilo litaleta kitulizo kama nini! Kisha, wale 144,000 ambao watakuwa wafalme na makuhani pamoja na Kristo wataendelea kutumia faida za dhabihu ya fidia kuwaweka wanadamu huru hatua kwa hatua mpaka dhambi na hali ya kutokamilika iliyosababishwa na Adamu itakapokuwa imeondolewa kabisa. (Ufu. 5:9, 10) Baada ya kubaki waaminifu hata chini ya jaribu, wanadamu watakuwa wamepata uhuru kamili ambao Yehova alikusudia wawe nao, “uhuru wenye utukufu wa watoto wa Mungu.” Hebu fikiria jambo hilo! Hutahitaji tena kupambana na mwili wako ili kufanya mambo yanayofaa machoni pa Mungu kwa sababu mwili wako wote utakuwa mkamilifu na utu wako utakuwa umebadilika kabisa kulingana na utu wa Mungu.

19. Ni lazima tuendelee kufanya nini leo ili tupate uhuru wa kweli wakati ujao?

19 Je, unatamani kupata “uhuru wenye utukufu wa watoto wa Mungu”? Ikiwa ndivyo, acha akili na moyo wako uendelee kuongozwa na “sheria kamilifu iliyo ya uhuru.” Naam, jifunze Maandiko kwa bidii. Ishi kupatana na kweli, na uifanye iwe mali yako. Sali ili upate roho takatifu. Nufaika kikamili kwa kushirikiana na kutaniko la Kikristo na kula chakula cha kiroho ambacho Yehova anaandaa. Usimruhusu Shetani akudanganye, kama alivyomdanganya Hawa, kufikiri kwamba matakwa ya Mungu yanatubana sana. Kwa kweli, Ibilisi ni mjanja sana. Lakini kama tutakavyoona katika makala inayofuata, hakuna sababu ya ‘Shetani kutushinda akili, kwa maana tunazijua mbinu zake.’​—2 Kor. 2:11.

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 9]

Je, bado ninatamani sana kupata “uhuru” fulani katika ulimwengu huu?

[Picha katika ukurasa wa 9]

Je, nimefanya kweli iwe njia yangu ya maisha?