Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mtumikie Mungu wa Uhuru

Mtumikie Mungu wa Uhuru

Mtumikie Mungu wa Uhuru

“Kumpenda Mungu humaanisha hivi, kwamba tuzishike amri zake; na bado amri zake si mzigo mzito.”​—1 YOH. 5:3.

JE, UNAWEZA KUJIBU?

Shetani hujaribu jinsi gani kufanya sheria za Mungu zionekane kuwa mzigo mzito?

Kwa nini ni lazima tuwe waangalifu sana tunapochagua marafiki wetu?

Ni nini kitakachotusaidia kuendelea kuwa washikamanifu kwa Mungu wa uhuru?

1. Yehova ana maoni gani kuhusu uhuru, na alionyeshaje hivyo aliposhughulika na Adamu na Hawa?

YEHOVA peke yake ndiye aliye na uhuru kamili. Hata hivyo, hautumii vibaya kamwe uhuru huo; wala kuwanyima uhuru watumishi wake kwa kuingilia kila jambo wanalofanya. Badala yake, amewapa watumishi wake uhuru wa kuchagua, ambao unawaruhusu kutumia uwezo wao kutosheleza tamaa zao zote zinazofaa. Kwa mfano, Mungu aliwapa Adamu na Hawa amri moja tu iliyowakataza kula matunda ya “mti wa ujuzi wa mema na mabaya.” (Mwa. 2:17) Walikuwa na uhuru mwingi ajabu wa kutimiza mapenzi ya Muumba wao!

2. Kwa nini wazazi wetu wa kwanza walipoteza uhuru ambao Mungu aliwapa?

2 Kwa nini Mungu aliwapa wazazi wetu wa kwanza uhuru mwingi hivyo? Aliwaumba kwa mfano wake na kuwapa dhamiri, na hivyo alitarajia kwamba upendo wao kumwelekea akiwa Muumba wao ungewaongoza katika njia inayofaa. (Mwa. 1:27; Rom. 2:15) Inahuzunisha kwamba Adamu na Hawa hawakumthamini Muumba wao mzuri ajabu na hawakuthamini uhuru ambao alikuwa amewapa. Badala yake, walichagua uhuru usiofaa ambao Shetani aliwaahidi, yaani, uhuru wa kimaadili. Lakini badala ya kupata uhuru zaidi, wazazi wetu wa kwanza walijiuza wenyewe na wazao wao wa baadaye katika utumwa wa dhambi, na hivyo matokeo yakawa mabaya sana.​—Rom. 5:12.

3, 4. Shetani anajaribu kutudanganya jinsi gani kuhusiana na viwango vya Yehova?

3 Ikiwa Shetani alifaulu kuwashawishi wanadamu wawili wakamilifu, pamoja na viumbe wengi wa roho, wakatae enzi kuu ya Mungu, anaweza pia kutudanganya. Bado anatumia mbinu hiyohiyo leo. Anajaribu kutupotosha kwa kutufanya tufikiri kwamba viwango vya Mungu ni mzigo mzito, na vinatunyima raha na shangwe. (1 Yoh. 5:3) Kufikiri kwa njia hiyo kunaweza kuwa na uvutano mkubwa juu yetu ikiwa tutashirikiana kwa ukawaida na watu wanaofikiri kwa njia hiyo. Dada mmoja mwenye umri wa miaka 24 ambaye alifanya uasherati alisema hivi: “Marafiki wabaya walikuwa na uvutano mkubwa sana juu yangu, hasa kwa sababu niliogopa kuwa na maoni tofauti na vijana wenzangu.” Huenda wewe pia umekabili msongo kama huo wa marafiki.

4 Inahuzunisha kwamba nyakati nyingine kunaweza pia kuwa na uvutano wa marafiki wabaya katika kutaniko la Kikristo. Kijana mmoja Shahidi alisema hivi: “Ninajua vijana fulani ambao walikuwa na uhusiano wa kimahaba na watu ambao si waamini. Hata hivyo, mwishowe niligundua kwamba kadiri nilivyoshirikiana nao, ndivyo nilivyozidi kuwa kama wao. Hali yangu ya kiroho ikaanza kuharibika. Sikuwa nikifurahia chakula cha kiroho katika mikutano, na sikushiriki kwa ukawaida katika utumishi. Hapo ndipo nilipotambua kwamba nilihitaji kukatisha urafiki huo, na ndivyo nilivyofanya!” Je, unajua uvutano wenye nguvu ambao marafiki wako wanaweza kuwa nao juu yako? Fikiria mfano fulani katika Biblia ambao unatuhusu leo.​—Rom. 15:4.

ALIIBA MIOYO YAO

5, 6. Absalomu aliwadanganya wengine jinsi gani, na je, njama yake ilifanikiwa?

5 Biblia ina mifano mingi ya watu ambao walikuwa na uvutano mbaya juu ya wengine. Mfano mmoja mbaya ni Absalomu, mwana wa Mfalme Daudi. Absalomu alikuwa mwanamume mwenye sura nzuri sana. Hata hivyo, baada ya muda, aliruhusu pupa ya mambo makuu ijae katika moyo wake, kama Shetani, kwa kuwa alianza kutamani kiti cha ufalme cha baba yake, ambacho hakuwa na haki ya kuchukua. * Ili kujaribu kuchukua ufalme kwa hila, Absalomu alijifanya kwamba anawajali sana Waisraeli wenzake huku akionyesha kwa ujanja kwamba mfalme hakuwajali. Naam, kama tu Ibilisi alivyofanya katika bustani ya Edeni, Absalomu alijifanya kwamba anawasaidia, na wakati huohuo alikuwa akieneza uwongo mbaya kuhusu baba yake mwenyewe.​—2 Sam. 15:1-5.

6 Je, njama ya werevu ya Absalomu ilifanikiwa? Naam, ilifanikiwa kwa kadiri fulani kwa sababu simulizi la Biblia linasema hivi: “Absalomu akaendelea kuiba mioyo ya watu wa Israeli.” (2 Sam. 15:6) Hata hivyo, mwishowe Absalomu alishindwa kwa sababu ya kiburi chake. Na inasikitisha kwamba jambo hilo lilisababisha kifo chake na vifo vya maelfu ya watu ambao aliwashawishi kumfuata.​—2 Sam. 18:7, 14-17.

7. Ni mambo gani tunayoweza kujifunza kutokana na simulizi kumhusu Absalomu? (Tazama picha kwenye ukurasa wa 14.)

7 Kwa nini Waisraeli hao walidanganywa kwa urahisi sana? Labda walitamani vitu ambavyo Absalomu aliwaahidi. Au huenda walidanganywa na sura yake nzuri. Kwa vyovyote vile, tunaweza kuwa na hakika kuhusu jambo hili: Walikosa kuwa washikamanifu kwa Yehova na kwa mfalme aliyemweka rasmi. Leo, Shetani anaendelea kuwatumia “akina Absalomu wa mfano” ili kujaribu kuiba mioyo ya watumishi wa Yehova. Huenda watu hao wakasema, ‘viwango vya Yehova vinatubana sana. Hebu watazame watu wote ambao hawamtumikii Yehova. Wanaponda raha kabisa!’ Je, utatambua kwamba madai hayo ni uwongo wenye kuchukiza na hivyo kuendelea kuwa mshikamanifu kwa Mungu? Je, utatambua kwamba “sheria kamilifu” ya Yehova, yaani, sheria ya Kristo, ndiyo tu inayoweza kukuongoza kupata uhuru wa kweli? (Yak. 1:25) Ikiwa ndivyo, thamini sheria hiyo, na usijaribu kamwe kuutumia vibaya uhuru wako wa Kikristo.​—Soma 1 Petro 2:16.

8. Ni mifano gani ya watu halisi inayoonyesha kwamba kupuuza viwango vya Yehova hakuleti furaha?

8 Shetani anawalenga hasa vijana. Ndugu ambaye sasa ana umri wa miaka 30 na kitu alisema hivi kuhusu miaka yake ya utineja: “Niliona kwamba viwango vya Yehova vya maadili vinanibana sana, wala si ulinzi.” Kwa sababu hiyo, akafanya uasherati. Lakini hakupata furaha kwa kufanya hivyo. Alisema hivi: “Kwa miaka mingi nilisumbuliwa sana na hisia nyingi za hatia na majuto.” Dada mmoja aliandika hivi kuhusu miaka yake ya utineja: “Baada ya kufanya uasherati, unahuzunika sana na kujiona hufai. Hata sasa baada ya miaka 19 kupita, bado ninaumia ninapokumbuka jambo hilo.” Dada mwingine alisema hivi: “Nilipofikiria jinsi mwenendo wangu ulivyowavunja moyo watu ninaowapenda sana nilivurugika sana kiakili, kiroho, na kihisia. Ni jambo baya sana kuishi bila kibali cha Yehova.” Shetani hataki ufikirie matokeo hayo mabaya ya dhambi.

9. (a) Ni maswali gani yanayoweza kutusaidia kuchunguza maoni yetu kumhusu Yehova, sheria na kanuni zake? (b) Kwa nini ni muhimu kumjua Mungu vizuri?

9 Inahuzunisha kama nini kwamba vijana wengi katika kweli, hata watu wenye umri mkubwa, wamelazimika kujifunza kwa majonzi kwamba mara nyingi kufurahia dhambi kunasababisha madhara makubwa sana! (Gal. 6:7, 8) Kwa hiyo, jiulize hivi: ‘Je, ninatambua kwamba kwa kweli mbinu za Shetani ni za udanganyifu na zenye kuumiza? Je, ninamwona Yehova kuwa Rafiki yangu wa karibu zaidi, ambaye sikuzote ananiambia ukweli na anataka niwe na maisha mazuri? Je, ninasadiki kabisa kwamba Yehova hawezi kamwe kuninyima jambo ambalo kwa kweli ni zuri na litakaloniletea furaha kubwa zaidi?’ (Soma Isaya 48:17, 18.) Ili ujibu ndiyo kutoka moyoni, unahitaji kufanya mengi zaidi ya kuwa tu na ujuzi wa kijuu-juu kumhusu Yehova. Unahitaji kumjua kwa undani na kutambua kwamba sheria na kanuni za Biblia zinaonyesha kwamba anakupenda, na si kwamba anataka kukunyima uhuru.​—Zab. 25:14.

SALI ILI UWE NA MOYO WENYE HEKIMA NA MTIIFU

10. Kwa nini tunapaswa kujitahidi kumwiga Mfalme Sulemani alipokuwa kijana?

10  Alipokuwa angali kijana, Sulemani alisali hivi kwa unyenyekevu: ‘Mimi ni mvulana mdogo tu. Sijui jinsi ya kutoka na jinsi ya kuingia.’ Kisha akasali ili apewe moyo wenye hekima na mtiifu. (1 Fal. 3:7-9, 12) Yehova alijibu ombi hilo la unyoofu, na atajibu ombi lako pia, iwe wewe ni kijana au mzee. Bila shaka, Yehova hatakupa ufahamu na hekima kimuujiza. Lakini atakufanya uwe mwenye hekima ukijifunza kwa bidii Neno lake, ukisali ili akupe roho takatifu, na kunufaika kikamili na maandalizi ya kiroho ambayo anatoa kupitia kutaniko la Kikristo. (Yak. 1:5) Kwa kweli, Yehova anatumia njia hizo kuwafanya hata watumishi wake vijana wawe na hekima zaidi kuliko wale wote wanaopuuza mashauri yake, hata wale wanaoitwa eti “wenye hekima na walio na akili” katika ulimwengu huu.​—Luka 10:21; soma Zaburi 119:98-100.

11-13. (a) Ni mambo gani muhimu tunayoweza kujifunza kutokana na Zaburi 26:4, Methali 13:20, na 1 Wakorintho 15:33? (b) Unaweza kutumiaje kanuni hizo za Kimaandiko?

11 Kwa mfano, ili uone umuhimu wa kujifunza Biblia na kutafakari kuhusu mambo tunayosoma ili tumjue Yehova kwa undani, fikiria maandiko yafuatayo. Kila andiko lina kanuni muhimu kuhusu marafiki tunaochagua: “Sikuketi na watu wasiosema kweli; wala siingii pamoja na wale wanaoficha jinsi walivyo.” (Zab. 26:4) “Anayetembea na watu wenye hekima atakuwa na hekima, lakini anayeshirikiana na wajinga atapatwa na mabaya.” (Met. 13:20) “Mashirika mabaya huharibu tabia nzuri.”​—1 Kor. 15:33.

12 Ni mambo gani muhimu tunayoweza kujifunza kutokana na maandiko hayo? (1) Yehova anataka tuchague marafiki wetu kwa uangalifu. Anataka kutulinda kimaadili na kiroho. (2) Watu tunaoshirikiana nao wanaweza kuwa na uvutano mzuri au mbaya juu yetu; hilo ni jambo la hakika maishani. Maandiko hayo yameandikwa kwa njia inayoonyesha kwamba Yehova anajaribu kugusa mioyo yetu. Jinsi gani? Ona kwamba hakuna andiko lolote kati ya maandiko hayo ambalo linaweka sheria, kwa kusema “hupaswi . . .” Badala yake, maandiko hayo yameandikwa kwa njia rahisi inayoonyesha ukweli. Ni kana kwamba Yehova anatuambia hivi: ‘Huu ndio ukweli wa mambo. Utaitikiaje? Ni nini kilicho moyoni mwako?’

13 Mwishowe, kwa sababu maandiko hayo matatu yametolewa yakiwa kweli za msingi, yanatumika hata sasa na yanaweza kutumika katika hali nyingi mbalimbali. Kwa mfano, jiulize maswali kama vile: Ninaweza kuepuka jinsi gani kushirikiana na watu “wanaoficha jinsi walivyo”? Ninaweza kukutana na watu wa aina hiyo katika hali gani? (Met. 3:32; 6:12) “Watu wenye hekima” ambao Yehova anataka nishirikiane nao ni nani? “Wajinga” ambao anataka niwaepuke ni nani? (Zab. 111:10; 112:1; Met. 1:7) Ni ‘tabia gani nzuri’ ambazo nitaharibu nikichagua marafiki wabaya? Je, ninaweza kupata marafiki wabaya katika ulimwengu tu? (2 Pet. 2:1-3) Ungejibuje maswali hayo?

14. Mnawezaje kuboresha jioni yenu ya Ibada ya Familia?

14 Baada ya kuchanganua Maandiko hayo, kwa nini usichunguze maandiko mengine ya Biblia ambayo yanafunua maoni ya Mungu kuhusu mambo ambayo yanakuhusu wewe au familia yako? * Wazazi, pangeni kuzungumzia mambo hayo wakati wa jioni ya Ibada yenu ya Familia. Mnapofanya hivyo, kumbukeni kwamba mradi wenu ni kumsaidia kila mshiriki wa familia kuthamini kikamili zaidi kina cha upendo wa Mungu kutuelekea kama unavyofunuliwa katika sheria na kanuni zake. (Zab. 119:72) Kwa kweli, funzo kama hilo linapaswa kuwasaidia wote katika familia wamkaribie Yehova na kuwa na uhusiano wa karibu kati yao.

15. Utajuaje ikiwa unasitawisha moyo wenye hekima na mtiifu?

15 Utajuaje ikiwa unasitawisha moyo wenye hekima na mtiifu? Njia moja ni kulinganisha njia yako ya kufikiri na ile ya watu waaminifu walioishi zamani, kama vile Mfalme Daudi, aliyeandika hivi: “Ee Mungu wangu, nimependezwa na kufanya mapenzi yako, na sheria yako imo ndani yangu.” (Zab. 40:8) Pia, mwandikaji wa Zaburi 119 alisema hivi: “Jinsi ninavyoipenda sheria yako! Ndiyo ninayoihangaikia mchana kutwa.” (Zab. 119:97) Upendo wa aina hiyo haukui kwenye udongo usio na kina. Badala yake, unatokana na kujifunza kwa undani, kusali, kutafakari, na uzoefu, yaani, kuhesabu baraka nyingi sana ambazo umepata maishani kwa sababu ya kushikamana na viwango vya Mungu.​—Zab. 34:8.

PIGANIA UHURU WAKO WA KIKRISTO!

16. Ni lazima tutambue nini ikiwa tunataka kushinda vita vyetu vya kupata uhuru wa kweli?

16 Katika historia yote, mataifa yamepigana vita vya kikatili yakitafuta uhuru. Basi, ni muhimu hata zaidi kwako kuwa tayari kupigana kiroho kwa ajili ya uhuru wako wa Kikristo! Tambua kwamba maadui wako si Shetani tu, ulimwengu, na roho yake yenye sumu. Ni lazima pia upigane na hali yako ya kutokamilika, kutia ndani moyo wenye hila. (Yer. 17:9; Efe. 2:3) Hata hivyo, kwa msaada wa Yehova, unaweza kushinda vita hivyo. Isitoshe, kila mara unaposhinda, iwe ni katika jambo dogo au kubwa, kuna angalau faida mbili. Kwanza, utaufanya moyo wa Yehova ushangilie. (Met. 27:11) Pili, unapoona jinsi “sheria kamilifu iliyo ya uhuru” ilivyo na nguvu za kuweka huru, utaazimia hata zaidi kuendelea kutembea katika ‘barabara nyembamba’ inayoongoza kwenye uzima wa milele. Baadaye, utafurahia uhuru mwingi zaidi ambao washikamanifu wa Yehova watapata wakati ujao.​—Yak. 1:25; Mt. 7:13, 14.

17. Kwa nini hatupaswi kuvunjika moyo kwa sababu ya hali yetu ya kutokamilika, na Yehova anatusaidiaje?

17 Bila shaka, nyakati nyingine sote tunakosea. (Mhu. 7:20) Unapokosea, usivunjike moyo kupita kiasi au kuhisi kwamba hufai. Ukijikwaa, kwa njia ya mfano, simama na usonge mbele, hata ikiwa hilo linamaanisha kuwaomba msaada wazee wa kwenu. ‘Sala yao ya imani,’ akaandika Yakobo, ‘itamponya mtu asiyejisikia vizuri, na Yehova atamwinua. Pia, ikiwa amefanya dhambi, atasamehewa.’ (Yak. 5:15) Naam, usisahau kamwe kwamba Mungu ni mwenye rehema kwelikweli na kwamba alikuvuta katika kutaniko kwa sababu aliona sifa zako nzuri. (Soma Zaburi 103:8, 9.) Kwa hiyo, maadamu unaendelea kumtumikia Yehova kwa moyo kamili, hatakutupa kamwe.​—1 Nya. 28:9.

18. Tunaweza kutendaje kupatana na sala ya Yesu katika Yohana 17:15?

18 Alipokuwa akisali usiku wake wa mwisho pamoja na mitume wake waaminifu 11, Yesu alisema maneno haya yasiyosahaulika kwa niaba yao: “Uwalinde kwa sababu ya yule mwovu.” (Yoh. 17:15) Yesu hakuwahangaikia tu mitume wake, bali pia wafuasi wake wote. Kwa hiyo, tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova atajibu sala ya Yesu kwa kutulinda katika nyakati hizi za hatari. “[Yehova] ni ngao kwa wale wanaotembea kwa utimilifu . . . Atailinda njia ya washikamanifu wake.” (Met. 2:7, 8) Naam, njia ya utimilifu ina matatizo yake, lakini ndiyo njia pekee inayoongoza kwenye uzima wa milele na uhuru wa kweli. (Rom. 8:21) Usimruhusu mtu yeyote akushawishi uiache njia hiyo!

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 5 Ilikuwa baada ya kuzaliwa kwa Absalomu, ndipo Mungu alipompa Daudi ahadi kuhusu “uzao” ambao ungetokea wakati ujao na kurithi kiti chake cha ufalme. Kwa hiyo, bila shaka Absalomu alijua kwamba Yehova hakuwa amemchagua yeye kurithi kiti cha ufalme cha Daudi.​—2 Sam. 3:3; 7:12.

^ fu. 14 Mifano mizuri ya maandiko mnayoweza kutumia ni 1 Wakorintho 13:4-8, ambamo Paulo anafafanua upendo, na Zaburi 19:7-11, ambayo inataja baraka nyingi tunazopata tunapotii sheria za Yehova.

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 14]

Tunaweza kuwatambuaje akina Absalomu wa mfano leo na kujihadhari nao?