Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Ndoto Yangu Imetimia”

“Ndoto Yangu Imetimia”

“Ndoto Yangu Imetimia”

Miaka kumi na mitano iliyopita, Emilia alikuwa akitumikia kama painia wa kawaida. Hata hivyo, alilazimika kuuacha utumishi wa wakati wote. Katika miaka ya hivi karibuni, mara nyingi amekuwa akikumbuka wakati huo wenye shangwe zaidi katika maisha yake, na alitaka tena kuongeza utendaji wake katika huduma.

Hata hivyo, kazi ya kimwili ya Emilia ilichukua wakati wake mwingi, na hali hiyo ilimfanya akose shangwe. Pindi moja, akiwa pamoja na wafanyakazi wenzake alilalamika hivi: “Laiti ningefanya kazi kwa saa chache zaidi!” Mkubwa wake wa kazi alisikia jambo hilo, naye akamuuliza ikiwa alichosema ni kweli. Emilia alimhakikishia kwamba ni kweli. Hata hivyo, ili ombi lake likubaliwe, ilikuwa lazima mkurugenzi wa kampuni alikubali kwa kuwa sheria za kampuni zilitaka wafanyakazi wote wawajibike kabisa. Dada yetu alijitayarisha kukutana na mkurugenzi huyo naye akasali ili Yehova ampe utulivu na ujasiri.

Katika mkutano huo, Emilia aliomba kwa busara lakini kwa ujasiri apunguziwe saa za kufanya kazi. Alieleza kwamba yeye hutumia muda wake wa mapumziko kuwasaidia wengine: “Mimi ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova, na ninawasaidia watu kiroho. Siku hizi viwango vya maadili vya watu wengi vimeshuka. Wanahitaji viwango na kanuni zilizo wazi, na hekima ninayowaonyesha kutoka katika Biblia ni yenye thamani sana kwao. Sitaki shughuli ninazofanya baada ya saa za kazi ziharibu ubora wa kazi yangu hapa, lakini ningependa kuwa na wakati zaidi wa kuwasaidia watu. Ndiyo sababu ninahitaji saa zangu za kufanya kazi zipunguzwe.”

Mkurugenzi alisikiliza kwa makini na kusema kwamba wakati fulani yeye pia alifikiria kufanya kazi ya kuwasaidia wengine. Kisha akasema: “Kwa sababu ambazo umeeleza, ninahisi kwamba ni lazima nikubali ombi lako. Lakini, je, unatambua kwamba utakuwa ukipata kiasi kidogo zaidi cha pesa?” Emilia alisema kwamba anatambua hilo na ikiwa ni lazima, atarahisisha maisha yake. Akaongeza: “Lengo langu muhimu zaidi ni kufanya jambo ambalo litawanufaisha kabisa watu.” Mkurugenzi akamwambia: “Ninavutiwa na wale ambao wanatumia wakati wao bila ubinafsi kuwasaidia wengine.”

Hakuna hata mfanyakazi mmoja wa kampuni hiyo aliyewahi kupata pendeleo kama hilo. Sasa Emilia anaruhusiwa kufanya kazi siku nne tu katika juma. Na alishangaa sana alipoongezewa mshahara, na sasa analipwa kiasi kikubwa kuliko zamani! Anasema hivi: “Ndoto yangu imetimia, na sasa ninaweza kufanya upainia wa kawaida tena!”

Je, umefikiria kurekebisha hali zako ili uanze au kurudia tena utumishi wa upainia?

[Blabu katika ukurasa wa 32]

Mkurugenzi akamwambia: “Ninavutiwa na wale ambao wanatumia wakati wao bila ubinafsi kuwasaidia wengine”