Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Simulizi la Maisha

Yehova Alinifundisha Kufanya Mapenzi Yake

Yehova Alinifundisha Kufanya Mapenzi Yake

Limesimuliwa na Max Lloyd

Usiku mmoja wa manane katika mwaka 1955, mimi na mmishonari mwenzangu tulikuwa katika mgawo wetu huko Paraguai, Amerika ya Kusini. Nyumba tuliyokuwamo ilizingirwa na umati wenye hasira uliokuwa ukipaaza sauti hivi: “Mungu wetu ni mungu mwenye kiu ya damu, naye anataka damu ya gringos.” Sisi gringos (wageni) tulifikaje katika eneo hilo?

MAISHA yangu yalianza miaka mingi iliyopita huko Australia, mahali nilipolelewa na ambako Yehova alianza kunifundisha kufanya mapenzi yake. Baba yangu alikubali kitabu Enemies alichopewa na Shahidi mmoja mwaka wa 1938. Tayari yeye na Mama hawakuridhishwa na kasisi wao ambaye mara nyingi alisema kwamba sehemu fulani za Biblia ni hekaya. Baada ya mwaka mmoja hivi, wazazi wangu walibatizwa ili kuonyesha wakfu wao kwa Yehova. Tangu wakati huo na kuendelea, kufanya mapenzi ya Yehova kulikuwa sehemu muhimu zaidi katika maisha ya familia yetu. Dada yangu, Lesley, aliyenizidi umri kwa miaka mitano, ndiye aliyebatizwa baada ya wazazi wangu, nami nikabatizwa mwaka 1940 nikiwa na umri wa miaka tisa.

Punde tu baada ya Vita vya Pili vya Ulimwengu kuanza, kazi ya kuchapa na kusambaza machapisho ya Mashahidi wa Yehova yanayozungumzia Biblia, ikapigwa marufuku nchini Australia. Kwa hiyo, nikiwa mtoto, nilijifunza jinsi ya kueleza msingi wa imani yangu kwa kutumia Biblia tu. Nilizoea kwenda na Biblia yangu shuleni ili kuonyesha kwa nini sikuisalimu bendera au kuunga mkono mataifa yaliyokuwa vitani.​—Kut. 20:4, 5; Mt. 4:10; Yoh. 17:16; 1 Yoh. 5:21.

Wengi shuleni hawakushirikiana nami kwa sababu walisema kwamba mimi ni “mpelelezi wa Ujerumani.” Wakati huo, sinema zilionyeshwa shuleni. Kabla ya sinema kuanza, kila mtu alipaswa kusimama na kuimba wimbo wa taifa. Nilipoendelea kuketi, wavulana wawili au watatu walijaribu kuniinua kwa lazima kutoka katika kiti kwa kuvuta nywele zangu. Hatimaye nilifukuzwa shuleni kwa sababu ya kushikilia imani yangu inayotegemea Biblia. Hata hivyo, nikiwa nyumbani niliendelea na masomo kupitia barua.

HATIMAYE NILITIMIZA MRADI WANGU

Nilikuwa nimejiwekea lengo au mradi wa kuanza utumishi wa wakati wote kama painia nikiwa na umri wa miaka 14. Nilivunjika moyo sana wazazi wangu waliposema kwamba ni lazima kwanza nitafute na kufanya kazi. Walisisitiza kwamba nilipe kodi ya chumba changu cha nyumbani, lakini waliahidi kwamba wakati ningefikisha umri wa miaka 18, ningeweza kuanza upainia. Hilo lilifanya tuzungumzie kwa ukawaida kuhusu pesa ambazo nilikuwa nikipata. Niliwaambia kwamba nilitaka kuhifadhi pesa hizo ili nifanye upainia, lakini walikuwa wakizichukua.

Wakati ulipofika wa kuanza upainia, wazazi wangu waliniketisha na kuniambia kwamba walikuwa wakihifadhi katika akaunti ya benki pesa ambazo nilikuwa nikiwapa. Kisha wakanirudishia pesa hizo zote ili ninunue nguo na vitu vingine nilivyohitaji kwa ajili ya upainia. Walikuwa wakinifundisha kujitegemea badala ya kutazamia wengine wanitegemeze. Ninapofikiria mazoezi hayo, ninaona kwamba yalikuwa yenye thamani sana.

Mimi na Lesley tulipokuwa tukiendelea kukua, mara nyingi mapainia walikaa katika nyumba yetu, na tulifurahia kushiriki nao katika huduma. Kila Jumamosi na Jumapili, tulihubiri nyumba kwa nyumba, barabarani, na kuongoza mafunzo ya Biblia. Miaka hiyo, mhubiri wa kutaniko alipaswa kuhubiri saa 60 kwa mwezi. Mama alitimiza takwa hilo la saa karibu kila mwezi, naye alituwekea mfano mzuri sana mimi na Lesley.

KUFANYA UPAINIA HUKO TASMANIA

Mgawo wangu wa kwanza wa upainia ulikuwa kwenye kisiwa cha Tasmania, huko Australia, ambako nilijiunga na dada yangu na mume wake. Lakini, waliondoka muda mfupi baadaye ili kuhudhuria darasa la 15 la Shule ya Gileadi. Nilikuwa mwenye haya sana, na kabla ya wakati huo, sikuwa nimeishi mbali na nyumbani. Wengine walikisia kwamba ningekaa Tasmania kwa miezi mitatu tu. Hata hivyo, katika muda wa mwaka mmoja tu, yaani, mwaka wa 1950, niliwekwa rasmi kutumikia nikiwa mtumishi wa kampuni, sasa anaitwa mratibu wa baraza la wazee. Baadaye, niliwekwa rasmi kuwa painia wa pekee, na ndugu mwingine kijana akajiunga nami.

Mgawo wetu ulikuwa katika mji mmoja wa mbali wenye migodi ya shaba, ambako hakukuwa na Shahidi yeyote. Tulisafiri kwa basi na kufika huko alasiri. Tulilala katika hoteli moja ya zamani usiku wa kwanza. Siku iliyofuata tulipokuwa tukihubiri nyumba kwa nyumba, tuliwauliza wenye nyumba ikiwa walijua mahali ambapo tungepata chumba kisichokuwa na mtu. Jioni hiyo, mtu fulani alitueleza kwamba katika nyumba ya mhudumu mmoja wa kanisa la Presbiteri tunaweza kupata nyumba isiyokuwa na mtu naye akatuambia tuzungumze na kasisi wa kanisa hilo. Alikuwa mwenye urafiki na akaturuhusu tuishi katika nyumba hiyo. Lilikuwa jambo lisilo la kawaida kwetu kutoka kila siku katika nyumba ya kasisi na kwenda kuhubiri.

Eneo hilo lilikuwa lenye matokeo mazuri sana. Tulikuwa na mazungumzo mazuri na watu na tulianzisha mafunzo mengi ya Biblia. Wasimamizi wa kanisa hilo katika mji mkuu walipopata habari hizo na kusikia kwamba Mashahidi wa Yehova walikuwa wakiishi katika nyumba ya kasisi, walimwamuru kasisi huyo atufukuze mara moja. Kwa mara nyingine tena hatukuwa na mahali pa kuishi!

Siku iliyofuata tulihubiri mpaka saa tisa hivi ya mchana, kisha tukatafuta mahali pa kulala usiku. Hatukupata mahali pengine pazuri zaidi isipokuwa jukwaa kuu la uwanja wa michezo. Tulificha masanduku yetu katika jukwaa hilo na kuendelea kuhubiri. Giza lilianza kuingia, lakini tuliamua kuhubiri nyumba chache zaidi ili tumalize barabara hiyo. Kwenye nyumba moja, mwanamume fulani alitupa mahali pa kulala katika nyumba ndogo yenye vyumba viwili nyuma ya nyumba yake!

KAZI YA MZUNGUKO NA GILEADI

Baada ya kuhubiri katika mgawo huo kwa miezi minane hivi, nilipokea mwaliko kutoka kwenye Ofisi ya Tawi ya Australia, mwaliko wa kuwa mwangalizi wa mzunguko. Mwaliko huo ulinishtua kwa sababu nilikuwa na umri wa miaka 20 tu. Baada ya kuzoezwa kwa majuma kadhaa, nilianza kutembelea makutaniko kwa ukawaida ili kuyatia moyo. Watu wenye umri mkubwa kuliko mimi, yaani, karibu kila mtu, hawakunidharau kwa sababu nilikuwa kijana lakini waliheshimu kazi niliyokuwa nikifanya.

Kila kutaniko nililotembelea lilitofautiana kama nini na lile lingine! Juma moja nilisafiri kwa basi, juma lingine kwa gari-moshi la umeme, kisha nilisafiri kwa gari au nilibebwa kwenye pikipiki, huku nikiwa nimebeba sanduku na mkoba wa mahubiri. Kukaa na Mashahidi wenzangu kuliniletea shangwe ya kweli. Mtumishi mmoja wa kampuni alikuwa na hamu ya kukaa pamoja nami hata ingawa nyumba yake haikuwa imemalizika kujengwa. Juma hilo nililala ndani ya beseni kubwa la kuogea, lakini sote tulifurahia kama nini mambo ya kiroho juma hilo!

Nilishangaa tena mwaka wa 1953 nilipopokea ombi la kuhudhuria darasa la 22 la Shule ya Gileadi. Nilishangilia lakini pia nilikuwa na wasiwasi. Unaona, baada ya dada yangu na mume wake kuhitimu Gileadi mnamo Julai 30, 1950, walipewa mgawo wa kwenda Pakistan. Katika muda usiozidi mwaka mmoja, Lesley alianza kuugua na akafia huko. Nilijiuliza, wazazi wangu wangehisije kuhusu mimi kwenda katika sehemu nyingine ya ulimwengu muda mfupi tu baadaye? Hata hivyo, walisema hivi: “Nenda umtumikie Yehova mahali popote anapokutuma.” Sikumwona Baba tena. Alikufa mwishoni mwa miaka ya 1950.

Baada ya muda mfupi, nilipanda meli pamoja na Waaustralia wengine watano ili kusafiri kwa majuma sita kwenda New York City. Tukiwa safarini, tulisoma Biblia, tulijifunza, na kuwahubiria abiria wenzetu. Kabla ya kwenda kaskazini kuhudhuria Shule ya Gileadi huko South Lansing, New York, tulihudhuria kusanyiko la kimataifa katika uwanja wa Yankee Stadium mnamo Julai 1953. Hudhurio lilikuwa kilele cha watu 165,829!

Darasa letu la Gileadi lilikuwa na wanafunzi 120 kutoka kila pembe ya dunia. Hatukuambiwa kuhusu migawo yetu mpaka siku ya kuhitimu ilipofika. Tulienda haraka katika maktaba ya Gileadi ili kujifunza kuhusu nchi ambako tulitumwa. Niligundua kwamba nchi ya Paraguai, ambako nilitumwa, ilikuwa na historia ya mapinduzi ya kisiasa. Muda mfupi baada ya kufika huko, niliwauliza asubuhi moja wamishonari wengine kulikuwa na “sherehe” gani wakati wa usiku. Walitabasamu na kusema: “Umeshuhudia mapinduzi yako ya kwanza. Tazama nje upande wa mbele.” Wanajeshi walikuwa kila mahali!

KUKABILI HALI YA HATARI

Pindi moja, nilienda pamoja na mwangalizi wa mzunguko alipotembelea kutaniko la mashambani ili kuonyesha sinema ya The New World Society in Action. Tulisafiri kwa saa nane au tisa, kwanza kwa gari-moshi, kisha kwa farasi na gari la kukokotwa na farasi, na hatimaye gari linalokokotwa na ng’ombe. Tulibeba jenereta na mashini ya kuonyesha sinema. Mwishowe, baada ya kufika mahali tulipokuwa tukienda, siku iliyofuata tulitembelea eneo lenye mashamba na kuwaalika wote waje kuona sinema hiyo usiku huo. Watu 15 walihudhuria.

Baada ya kuonyesha sinema hiyo kwa dakika 20, tuliambiwa tuingie ndani ya nyumba haraka iwezekanavyo. Tulichukua haraka mashini ya kuonyesha sinema na tukatii. Huo ndio wakati ambapo wanaume fulani walianza kupiga kelele, kufyatua risasi, na kupaaza sauti hivi: “Mungu wetu ni mungu mwenye kiu ya damu, naye anataka damu ya gringos.” Kulikuwa tu na gringos au wageni wawili hapo, na mimi nilikuwa mmoja wao! Wale waliokuja kuona sinema hiyo waliuzuia umati huo uliojaribu kuvunja nyumba na kuingia ndani. Lakini wapinzani hao walirudi karibu saa tisa usiku, wakifyatua risasi na kuapa kwamba wangeturudisha mjini siku hiyo.

Akina ndugu walimjulisha mkuu wa polisi, ambaye alikuja alasiri na farasi wawili ili aturudishe mjini. Tulipokuwa njiani, kila mara tulipofika mahali penye vichaka au miti, mkuu huyo wa polisi alitoa bunduki yake na kwenda mbele ili akague eneo hilo. Niliona kwamba farasi walikuwa njia muhimu ya usafiri, kwa hiyo baadaye nilinunua farasi mmoja.

WAMISHONARI ZAIDI WANAFIKA

Kazi ya kuhubiri iliendelea kufanikiwa licha ya upinzani wa mara kwa mara wa makasisi. Katika mwaka wa 1955, wamishonari wapya watano walifika, kutia ndani dada kijana kutoka Kanada aliyeitwa Elsie Swanson, ambaye alihitimu katika darasa la 25 la Gileadi. Tulikuwa pamoja kwa kipindi fulani kwenye ofisi ya tawi kabla hajapewa mgawo katika mji mwingine. Alikuwa ametumia maisha yake yote katika utumishi wa Yehova kwa msaada mdogo kutoka kwa wazazi wake, ambao hawakuwahi kamwe kukubali kweli. Mnamo Desemba 31, 1957, mimi na Elsie tulifunga ndoa, na tuliishi peke yetu katika nyumba ya wamishonari kusini mwa Paraguai.

Nyumba yetu haikuwa na maji ya bomba; badala yake, tulikuwa na kisima nyuma ya nyumba. Kwa hiyo, hakukuwa na bafu au choo ndani ya nyumba, wala mashini ya kufua, au hata friji. Tulinunua vyakula vya kupika kila siku. Lakini kuwa na maisha rahisi na mahusiano yenye upendo pamoja na ndugu na dada zetu kutanikoni kulifanya kipindi hicho kiwe kipindi chenye furaha sana katika maisha yetu ya ndoa.

Mwaka wa 1963, muda mfupi baada ya kurudi Australia kumtembelea mama yangu, mama alipatwa na mshtuko wa moyo, ambao inaonekana ulisababishwa na msisimuko wa kumwona tena mwana wake baada ya miaka kumi. Wakati ulipofika wa kurudi kwenye mgawo wetu huko Paraguai, tulihitaji kufanya mojawapo ya maamuzi magumu zaidi katika maisha yetu. Je, tumwache mama yangu hospitalini, tukitumaini kwamba mtu fulani angemtunza, na sisi turudi katika mgawo wetu ambao tulipenda huko Paraguai? Baada ya kusali sana, mimi na Elsie tuliamua kubaki na kumtunza Mama. Tuliweza kufanya hivyo na kuendelea na huduma ya wakati wote hadi mama alipokufa mwaka wa 1966.

Lilikuwa pendeleo kutumiwa katika kazi ya mzunguko na wilaya nchini Australia kwa miaka mingi na kufundisha katika Shule ya Huduma ya Ufalme ya wazee. Kisha badiliko lingine likatokea katika maisha yetu. Nilipewa mgawo wa kutumika nikiwa mshiriki wa Halmashauri ya kwanza ya Tawi ya Australia. Halafu, tulipohitaji kujenga ofisi mpya ya tawi, niliwekwa rasmi kuwa mwenyekiti wa halmashauri ya ujenzi. Kwa msaada wa wafanyakazi wengi wenye uzoefu na ushirikiano wao, tulijenga ofisi maridadi.

Kisha nilipewa mgawo katika Idara ya Utumishi, ambayo inasimamia kazi ya kuhubiri katika nchi. Pia, nilipata pendeleo la kutembelea ofisi nyingine za tawi ulimwenguni pote nikiwa mwangalizi wa eneo la dunia ili kutoa msaada na kitia-moyo. Imani yangu iliimarishwa hasa nilipotembelea nchi fulani na kukutana na watu ambao walifungwa kwa miaka mingi, hata makumi ya miaka, katika magereza na kambi za mateso kwa sababu ya kumtii Yehova kwa uaminifu.

MGAWO WETU WA SASA

Baada ya kurudi kutoka kwenye ziara ya eneo la dunia yenye kuchosha mwaka wa 2001, nilipata barua ya kunialika kuja Brooklyn, New York, ili kutumikia nikiwa mshiriki wa Halmashauri mpya ya Tawi ya Marekani. Mimi na Elsie tulisali na kuzungumzia mwaliko huo, na kwa furaha tukakubali mgawo huo. Baada ya miaka zaidi ya 11, bado tungali Brooklyn.

Ninafurahi sana kwamba nina mke ambaye anafurahia kufanya chochote kile ambacho Yehova anataka tufanye. Mimi na Elsie sasa tuna umri wa miaka 80 na kitu na bado tuna afya nzuri ya kadiri. Tunatazamia kufurahia mafundisho ya Yehova kwa umilele wote na pia baraka nyingi ambazo zitafurahiwa na wale wanaoendelea kufanya mapenzi yake.

[Blabu katika ukurasa wa 19]

Juma moja nilisafiri kwa basi, juma lingine kwa gari-moshi la umeme, kisha nilisafiri kwa gari au nilibebwa kwenye pikipiki, huku nikiwa nimebeba sanduku na mkoba wa mahubiri

[Blabu katika ukurasa wa 21]

Tunatazamia kufurahia mafundisho ya Yehova kwa umilele wote

[Picha katika ukurasa wa 18]

Kushoto: Nikiwa katika kazi ya mzunguko huko Australia

Kulia: Nikiwa na wazazi wangu

[Picha katika ukurasa wa 20]

Siku yetu ya arusi, Desemba 31, 1957