Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Yehova Mmoja” Anaikusanya Familia Yake

“Yehova Mmoja” Anaikusanya Familia Yake

“Yehova Mmoja” Anaikusanya Familia Yake

‘Ninawasihi muushike umoja wa roho.’​—EFE. 4:1, 3.

UNGEELEZAJE?

Ni nini kusudi la usimamizi wa mambo wa Mungu?

‘Tunaushikaje umoja wa roho’?

Ni nini kitakachotusaidia ‘kuwa wenye fadhili sisi kwa sisi’?

1, 2. Yehova ana kusudi gani kwa ajili ya dunia na wanadamu?

FAMILIA. Neno hilo linakukumbusha nini? Uchangamfu? Furaha? Kufanya kazi pamoja ili kutimiza lengo au mradi fulani? Mahali salama ambapo watu hukua, hujifunza mambo, na kubadilishana mawazo? Inaelekea kwamba unahisi hivyo ikiwa familia yenu ni yenye upendo. Yehova mwenyewe ndiye Mwanzilishi wa familia. (Efe. 3:14, 15) Yehova alikusudia kwamba viumbe wake wote mbinguni na duniani wafurahie hali ya usalama, waaminiane, na kuwa na umoja wa kweli.

2 Baada ya Adamu na Hawa kutenda dhambi, wanadamu hawakuwa tena sehemu ya familia ya Mungu ya ulimwenguni pote, lakini kusudi la Yehova halikuvurugwa. Atahakikisha kwamba dunia Paradiso inajaa wazao wa Adamu na Hawa. (Mwa. 1:28; Isa. 45:18) Amefanya matayarisho kamili ili kutimiza kusudi hilo. Tunaelezwa kuhusu baadhi ya mipango hiyo katika kitabu cha Biblia cha Waefeso, ambacho kinakazia umoja. Acheni tuchunguze mistari michache katika kitabu hicho ili tuone jinsi tunavyoweza kuunga mkono kusudi la Yehova la kuunganisha uumbaji wake.

USIMAMIZI WA MAMBO NA KAZI YAKE

3. Usimamizi wa mambo wa Mungu unaozungumziwa katika Waefeso 1:10 ni nini, na hatua ya kwanza ya usimamizi huo ilianza lini?

3 Musa aliwaambia Waisraeli hivi: “Yehova Mungu wetu ni Yehova mmoja.” (Kum. 6:4) Matendo ya Yehova na kusudi lake yanapatana. Kwa hiyo, “kwenye kikomo kamili cha nyakati zilizowekwa rasmi,” Mungu alianzisha “usimamizi wa mambo,” yaani, mpango wa kuunganisha viumbe wake wote wenye akili. (Soma Waefeso 1:8-10.) Usimamizi huo utatimiza kusudi lake katika hatua mbili. Hatua ya kwanza ni kulitayarisha kutaniko la watiwa-mafuta kwa ajili ya uhai mbinguni chini ya uongozi wa Yesu Kristo akiwa Kichwa cha kiroho cha watiwa-mafuta. Hatua hiyo ilianza katika Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K. Yehova alipoanza kuwakusanya wale watakaotawala pamoja na Kristo mbinguni. (Mdo. 2:1-4) Kwa kuwa watiwa-mafuta wametangazwa kuwa waadilifu kwa ajili ya uhai kwa msingi wa dhabihu ya fidia ya Kristo, wanatambua waziwazi kwamba wamefanywa kuwa “watoto wa Mungu.”​—Rom. 3:23, 24; 5:1; 8:15-17.

4, 5. Hatua ya pili ya usimamizi wa mambo ni ipi?

4 Hatua ya pili inawatayarisha wale watakaoishi katika Paradiso duniani chini ya uongozi wa Ufalme wa Kimasihi wa Kristo. “Umati mkubwa” ndiyo sehemu ya kwanza ya kikundi hicho. (Ufu. 7:9, 13-17; 21:1-5) Wakati wa Utawala wa ile Miaka Elfu Moja, mabilioni ya watu watakaofufuliwa watajiunga na wale wa umati mkubwa. (Ufu. 20:12, 13) Fikiria jinsi ufufuo utakavyoonyesha wazi zaidi umoja wetu! Mwishoni mwa ile miaka elfu moja, “vitu vilivyo duniani” vitapitia jaribu la mwisho. Wale watakaobaki waaminifu watafanywa kuwa “watoto wa Mungu” duniani.​—Rom. 8:21; Ufu. 20:7, 8.

5 Hatua hizo mbili za usimamizi wa mambo wa Mungu zinaenda sambamba leo, yaani, kuwatayarisha wale watakaoishi mbinguni na wale watakaoishi duniani. Lakini tukiwa mtu mmoja-mmoja, tunaungaje mkono sasa usimamizi wa mambo wa Mungu?

‘USHIKE UMOJA WA ROHO’

6. Maandiko yanaonyeshaje kwamba Wakristo wanapaswa kushirikiana?

6 Maandiko yanaonyesha kwamba ni lazima Wakristo wakusanyike pamoja kihalisi. (1 Kor. 14:23; Ebr. 10:24, 25) Ili tuwe na umoja huo, ni lazima tufanye mengi zaidi ya kukusanyika tu mahali pamoja, kama wanavyofanya watu wanaoenda sokoni au kwenye uwanja wa michezo. Umoja wa kweli ni zaidi ya hilo. Tunafikia umoja huo tunapofuata mafundisho ya Yehova na kujiruhusu tufinyangwe na roho takatifu ya Mungu.

7. Inamaanisha nini “kuushika umoja wa roho”?

7 Ingawa Yehova amewatangaza watiwa-mafuta kuwa waadilifu wakiwa wana na kondoo wengine kuwa waadilifu wakiwa marafiki kwa msingi wa dhabihu ya fidia ya Kristo, kutoelewana kutatokea kati yetu maadamu tunaishi katika mfumo huu wa mambo. (Rom. 5:9; Yak. 2:23) Kama sivyo hatungehitaji shauri lililoongozwa na roho ya Mungu linalotuhimiza tuendelee ‘kuvumiliana.’ Lakini, tunawezaje kuwa na umoja na waamini wenzetu? Tunahitaji kusitawisha “unyenyekevu kamili wa akili na upole.” Zaidi ya hayo, Paulo anatuhimiza tujitahidi sana “kuushika umoja wa roho katika kifungo chenye kuunganisha cha amani.” (Soma Waefeso 4:1-3.) Kufuata shauri hilo kunatia ndani kukubali kuongozwa na roho ya Mungu na kuiruhusu itokeze tunda lake ndani yetu. Tunda hilo la roho linawasaidia watu kusuluhisha matatizo kati yao, tofauti na matendo ya mwili, ambayo sikuzote yanawatenganisha watu.

8. Matendo ya mwili yanaharibu umoja kwa njia gani?

8 Ona jinsi “matendo ya mwili” yanavyoharibu umoja. (Soma Wagalatia 5:19-21.) Uasherati unamtenganisha mtu na Yehova na pia na kutaniko, na uzinzi unaweza kuwatenganisha kikatili watoto na wazazi wao na pia unawatenganisha wenzi wa ndoa wasio na hatia na wenzi wao. Uchafu unaathiri umoja ambao mtu anao pamoja na Mungu na pamoja na wale wanaompenda. Mtu ambaye amejaribu kuunganisha vitu viwili kwa gundi anajua kwamba sehemu zote mbili zinapaswa kuwa safi ili vitu hivyo vishikane vizuri. Kujiingiza katika mwenendo mpotovu bila aibu kunaonyesha kwamba mtu anapuuza kabisa sheria za Mungu za uadilifu. Matendo mengine ya mwili yanafanya watu watengane na pia yanawatenganisha watu na Mungu. Mwenendo kama huo haupatani kabisa na utu wa Yehova.

9. Tunawezaje kujichunguza wenyewe ili kuona ikiwa ‘tunajitahidi sana kuushika umoja wa roho’?

9 Kwa hiyo, kila mmoja wetu anahitaji kujiuliza hivi: ‘Ninajitahidi kadiri gani “kuushika umoja wa roho katika kifungo chenye kuunganisha cha amani”? Ninafanya nini ninapokosana na mwingine? Je, ninawaeleza marafiki wangu wengi kuhusu matatizo hayo nikitazamia waniunge mkono? Je, ninatarajia wazee waingilie kati kwa niaba yangu badala ya mimi mwenyewe kujitahidi sana kurudisha uhusiano wenye amani pamoja na mtu huyo? Je, ninawaepuka watu tuliokosana nao ili tusizungumzie matatizo yetu, labda kwa kuhakikisha kwamba ninajitenga nao kadiri iwezekanavyo?’ Je, matendo kama hayo yanaonyesha kwamba tunatenda kupatana na kusudi la Yehova la kukusanya pamoja tena vitu vyote katika Kristo?

10, 11. (a) Kuna umuhimu gani wa kuwa na amani pamoja na ndugu zetu? (b) Tunaweza kufanya nini ili kusitawisha amani na hivyo kupata baraka za kiroho?

10 Yesu alisema hivi: “Basi, ikiwa unaleta zawadi yako kwenye madhabahu na hapo ukumbuke kwamba ndugu yako ana jambo fulani juu yako, acha zawadi yako hapo mbele ya madhabahu, na uende zako; kwanza fanya amani yako pamoja na ndugu yako, na ndipo, ukiisha kurudi, itoe zawadi yako. Uwe tayari kusuluhisha mambo upesi.” (Mt. 5:23-25) Yakobo aliandika kwamba “mbegu ya tunda la uadilifu hupandwa chini ya hali zenye amani kwa wale wanaofanya amani.” (Yak. 3:17, 18) Kwa hiyo, hatuwezi kudumisha mwenendo wa uadilifu katika mazingira yasiyokuwa na amani.

11 Kwa mfano, katika nchi fulani ambazo zimeharibiwa na vita, inakadiriwa kwamba zaidi ya asilimia 35 ya ardhi ingelimwa ikiwa raia hawangekuwa na wasiwasi kuhusu mabomu ya ardhini. Bomu la ardhini likilipuka, wakulima hawalimi tena, na inakuwa vigumu kwa watu kulima vijijini, na hivyo miji inakosa chakula. Vivyo hivyo, inakuwa vigumu kwetu kukua kiroho ikiwa tuna tabia ambazo zinaweza kuvuruga amani kati yetu na ndugu zetu. Lakini ikiwa tunawasamehe wengine kwa wepesi na kuwatendea mambo mema, tunasitawisha hali ambazo zinaleta baraka kwelikweli.

12. Wazee wanawezaje kutusaidia kuwa na umoja?

12 Zaidi ya hayo, wale ambao ni “zawadi katika wanadamu” wanaweza kusaidia sana kudumisha umoja. Wamewekwa rasmi ili kutusaidia ‘kuufikia umoja katika imani.’ (Efe. 4:8, 13) Wazee wanapofanya kazi pamoja nasi katika utumishi mtakatifu na kutoa mashauri yanayotegemea Neno la Mungu, wanatusaidia kufanya maendeleo katika kuvaa utu mpya. (Efe. 4:22-24) Je, unaona mashauri yao kuwa jitihada za Yehova za kukutayarisha kupata uzima katika ulimwengu mpya chini ya utawala wa Mwana wake? Enyi wazee, je, mnajitahidi kuwarekebisha wengine mkiwa na kusudi hilo?​—Gal. 6:1.

“IWENI WENYE FADHILI NINYI KWA NINYI”

13. Matokeo yatakuwa nini tusipotii mashauri yaliyo katika andiko la Waefeso 4:25-32?

13 Andiko la Waefeso 4:25-29 linataja mwenendo ambao tunapaswa hasa kuepuka. Mwenendo huo unatia ndani kusema uwongo, kuwa mwenye hasira kali, kuwa mvivu, na kusema maneno yaliyooza badala ya maneno mema na yenye kujenga. Mtu akishindwa kutii mashauri hayo, ataihuzunisha roho ya Mungu, kwa kuwa roho takatifu ni nguvu inayowasaidia watu wawe na umoja. (Efe. 4:30) Ili kudumisha amani na umoja, ni muhimu pia kufuata maneno yafuatayo ambayo Paulo aliandika: “Uchungu wote wenye uovu na hasira na ghadhabu na kupiga kelele na matukano na viondolewe mbali kutoka kwenu pamoja na ubaya wote. Bali iweni wenye fadhili ninyi kwa ninyi, wenye huruma nyororo, mkisameheana kwa hiari kama vile Mungu pia kupitia Kristo alivyowasamehe ninyi kwa hiari.”​—Efe. 4: 31, 32.

14. (a) Maneno “iweni wenye fadhili” yanadokeza nini? (b) Ni nini kitakachotusaidia kuwa wenye fadhili?

14 Maneno “iweni wenye fadhili” yanadokeza kwamba huenda kwa kadiri fulani hatujawa wenye fadhili na hivyo huenda tunahitaji kufanya maendeleo. Inafaa kama nini kwamba tujizoeze kujali na kutanguliza hisia za wengine badala ya hisia zetu! (Flp. 2:4) Labda jambo tunalofikiria kusema litachekesha au litafanya tuonekane kuwa wenye akili, lakini je, ni lenye fadhili? Kufikiria kimbele jambo hilo kutatusaidia ‘kuwa wenye fadhili.’

KUJIFUNZA UPENDO NA HESHIMA KATIKA FAMILIA

15. Katika andiko la Waefeso 5:28, Paulo alikuwa akizungumzia sifa gani ambayo Kristo alionyesha aliposhughulika na kutaniko?

15 Biblia inalinganisha uhusiano wa Kristo na kutaniko na ule wa mume na mke wake. Mfano wa Kristo unapaswa kumsaidia mume kuelewa jinsi ambavyo anapaswa kumwongoza, kumpenda, na kumtunza mke wake, na unamsaidia pia mke kuelewa jinsi anavyopaswa kujitiisha katika ndoa. (Efe. 5:22-33) Paulo alipoandika: “Vivyo hivyo waume wanapaswa kuwa wakiwapenda wake zao kama miili yao wenyewe,” alikuwa akizungumzia nini? (Efe. 5:28) Maneno yake yanayotangulia yanaonyesha jinsi “Kristo pia alivyolipenda kutaniko na kujitoa mwenyewe kwa ajili yake, . . . akilisafisha na kuliosha kwa maji kwa njia ya neno.” Kwa kweli, ili mume afanye kazi kupatana na kusudi la Yehova la kukusanya tena vitu vyote pamoja katika Kristo, ni lazima awe makini katika kuilisha familia yake kiroho.

16. Matokeo yanakuwa nini wazazi wanapotimiza majukumu yao ya Kimaandiko nyumbani?

16 Ni vizuri wazazi wakumbuke kwamba wanatimiza mgawo ambao wamepewa na Yehova. Inasikitisha kwamba katika ulimwengu wa leo, watu wengi ‘hawana upendo wa asili.’ (2 Tim. 3:1, 3) Akina baba wengi wanapuuza majukumu yao na jambo hilo linawaathiri watoto wao na kuwahuzunisha. Lakini Paulo aliwashauri hivi baba Wakristo: “Msiwe mkiwakasirisha watoto wenu, bali endeleeni kuwalea katika nidhamu na mwongozo wa akilini wa Yehova.” (Efe. 6:4) Ni wapi pengine ambapo watoto wanajifunza kwa mara ya kwanza kuhusu upendo na kuheshimu mamlaka isipokuwa katika familia? Wazazi ambao wamefanikiwa kuwafundisha watoto wao masomo hayo wamefanya kazi kupatana na usimamizi wa mambo wa Yehova. Tunapohakikisha kwamba nyumba zetu ni mahali penye upendo ambapo tunaondolea mbali hasira na ghadhabu yote na matukano, tunawafundisha watoto wetu masomo muhimu kuhusu jinsi ya kuonyesha upendo na kuheshimu mamlaka. Hilo litawatayarisha kupata uzima katika ulimwengu mpya wa Mungu.

17. Tunahitaji kufanya nini ili kumpinga Ibilisi?

17 Tunahitaji kutambua kwamba Ibilisi, aliyekuwa wa kwanza kuvuruga amani ulimwenguni pote, atapinga vikali jitihada zetu za kufanya mapenzi ya Mungu. Bila shaka, watu wengi leo ulimwenguni wanafanya mambo yanayompendeza Shetani kwa kutalikiana, kuishi tu pamoja bila kufunga ndoa, na kukubali ndoa za watu wa jinsia moja. Sisi hatuigi tabia au mitazamo hiyo ambayo inaonekana ulimwenguni leo. Kristo ndiye kielelezo chetu. (Efe. 4:17-21) Kwa hiyo, tunahimizwa ‘tuvae mavazi kamili ya silaha kutoka kwa Mungu’ ili tufaulu kumpinga Ibilisi na roho wake waovu.​—Soma Waefeso 6:10-13.

“ENDELEENI KUTEMBEA KATIKA UPENDO”

18. Ni nini msingi wa umoja wetu wa Kikristo?

18 Upendo ndio msingi hasa wa umoja wetu wa Kikristo. Tukiwa na mioyo iliyojaa upendo kwa ‘Bwana wetu mmoja,’ kwa ‘Mungu wetu mmoja,’ na kati yetu wenyewe, tumeazimia “kuushika umoja wa roho katika kifungo chenye kuunganisha cha amani.” (Efe. 4:3-6) Yesu alisali hivi kuhusu upendo huo: “Ninawaombea, si hawa tu, bali pia wale wanaoniamini kupitia neno lao; ili wote wapate kuwa kitu kimoja, kama vile ambavyo wewe, Baba, umo katika muungano pamoja na mimi na mimi nimo katika muungano pamoja na wewe, ili wao pia wapate kuwa katika muungano pamoja na sisi . . . Nami nimewajulisha jina lako nami nitalijulisha, ili upendo ulionipenda nao upate kuwa ndani yao nami katika muungano pamoja nao.”​—Yoh. 17:20, 21, 26.

19. Umeazimia kufanya nini?

19 Ikiwa tuna udhaifu fulani kwa sababu ya hali yetu ya kutokamilika, basi upendo na utuchochee kusali hivi kama mtunga-zaburi: “Unganisha moyo wangu ili kuliogopa jina lako.” (Zab. 86:11) Basi na tuazimie kuzipinga jitihada za Ibilisi za kututenganisha na Baba yetu mwenye upendo na wale ambao anawakubali. Tujitahidi kabisa ‘kuwa waigaji wa Mungu, kama watoto wapendwa, na kuendelea kutembea katika upendo’ ndani ya familia, katika huduma yetu, na kutanikoni.​—Efe. 5:1, 2.

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 29]

Anaacha zawadi yake kwenye madhabahu, na kwenda kufanya amani na ndugu yake

[Picha katika ukurasa wa 31]

Wazazi, wafundisheni watoto wenu kuonyesha heshima