Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Unakumbuka?

Je, Unakumbuka?

Je, Unakumbuka?

Je, umesoma kwa makini makala hizi za hivi karibuni za Mnara wa Mlinzi? Ona ikiwa unaweza kujibu maswali yafuatayo:

Je, nguvu za Samsoni zilitokana na nywele zake?

Nguvu za Samsoni hazikutokana na nywele zake. Nywele zake ziliwakilisha uhusiano wake wa pekee pamoja na Mungu akiwa Mnadhiri. Uhusiano huo uliathiriwa wakati Delila alipopanga ili nywele za Samsoni zinyolewe.​—4/15, ukurasa wa 9.

Sawa na moyo wetu halisi, ni mambo gani matatu yanayoathiri moyo wetu wa mfano?

(1) Chakula Bora. Moyo wetu halisi unahitaji chakula bora, vivyo hivyo, tunahitaji chakula cha kutosha cha kiroho kilicho bora. (2) Mazoezi. Kushiriki kwa bidii katika huduma, kunafanya moyo wetu wa kiroho uendelee kuwa katika hali nzuri. (3) Mazingira. Tunaweza kupunguza mkazo kwa kushirikiana na waamini wenzetu, ambao wanatujali.​—4/15, ukurasa wa 16.

Baada ya mwenzi mmoja wa ndoa kukosa uaminifu, wenzi hao wanawezaje kuanza tena kuaminiana?

Wanapaswa (1) kuwa wanyoofu kwa mwenzi wao; (2) kushirikiana; (3) kuacha tabia za zamani; na (4) kujua wakati wa kuachilia mbali kinyongo, na kujitahidi kusamehe.​—5/1, ukurasa wa 12-15.

Kwa nini mtu anayetoa hotuba ya mazishi hapaswi kutumia Zaburi 116:15 kumhusu Mkristo aliyekufa?

Andiko hilo linasema hivi: “Ni chenye thamani machoni pa Yehova kifo cha washikamanifu wake.” Hilo linamaanisha kwamba Mungu anaona kifo cha washikamanifu wake wote kuwa cha gharama kubwa sana kwake hivi kwamba hawezi kuwaruhusu waangamizwe wote wakiwa kikundi kutoka duniani.​—5/15, ukurasa wa 22.

Makolpota walikuwa nani?

Kabla ya mwaka wa 1931, neno “makolpota” lilitumiwa kuwarejelea wale ambao leo wanaitwa mapainia.​—5/15, ukurasa wa 31.

Ni mambo gani yanayoonyesha kwamba Biblia si kitabu tu kilichoandikwa na wanadamu?

Biblia ina unabii mwingi uliotimizwa. Inasimulia mambo sahihi ya kihistoria, na wala si ngano. Biblia ni sahihi kisayansi, na vitabu vyake vinapatana. Inatufaa leo.​—6/1, ukurasa wa 4-8.

“Falme hizi zote” zinazotajwa katika Danieli 2:44 ni falme gani?

Maneno hayo yanarejelea falme, au serikali, zinazofananishwa na sehemu mbalimbali za ile sanamu yenye madini mbalimbali iliyofafanuliwa na Danieli.​—6/15, ukurasa wa 17.

Serikali Kuu ya Ulimwengu ya Uingereza na Marekani ilianza lini kuwa mfalme wa saba kulingana na unabii wa Biblia?

Serikali hiyo kuu ya muungano ilianza wakati Uingereza na Marekani zilipotenda pamoja kwa njia ya pekee katika Vita vya Kwanza vya Ulimwengu.​—6/15, ukurasa wa 19.

Mungu anasamehe na kusahau jinsi gani dhambi za watu wanaotubu?

Yehova anasema hivi kuhusu wale anaowaonyesha kibali: “Dhambi yao sitaikumbuka tena.” (Yer. 31:34) Anaweza kusamehe dhambi kwa msingi wa fidia. Anaposamehe, Mungu husahau katika maana ya kwamba hatamwadhibu tena mkosaji kwa sababu ya dhambi alizotubu.​—7/1, ukurasa wa 18.

Kwa nini tunaweza kuamini miujiza inayotajwa katika Biblia?

Mara nyingi miujiza hiyo ilifanywa hadharani, haikufanywa kwa siri. Ilifanywa kwa njia rahisi bila kutumia vifaa vya pekee. Miujiza hiyo ilifanywa ili kumletea Mungu utukufu, bali si wanadamu. Miujiza mingi mbalimbali ilifanywa, na wapinzani hawakupinga kwamba ilitokea. Sababu hizo zinatusaidia kuamini miujiza inayotajwa katika Biblia.​—8/1, ukurasa wa 7-8.