Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jiendesheni Kama Raia Wa Ufalme!

Jiendesheni Kama Raia Wa Ufalme!

Jiendesheni Kama Raia Wa Ufalme!

“Jiendesheni kwa namna inayostahili habari njema.”​—FLP. 1:27.

UNGEJIBUJE?

Ni nani wanaoweza kuwa raia wa Ufalme?

Tunahitaji kufanya nini kuhusu lugha, historia, na sheria za Ufalme?

Raia wa Ufalme wanaonyeshaje kwamba wanapenda viwango vya Mungu?

1, 2. Kwa nini shauri la Paulo kwa kutaniko la Filipi lilikuwa na maana ya pekee?

MTUME Paulo alilitia moyo kutaniko la Filipi ‘lijiendeshe kwa namna inayostahili habari njema.’ (Soma Wafilipi 1:27.) Neno la Kigiriki ambalo Paulo alitumia linalotafsiriwa “jiendesheni” linaweza pia kutafsiriwa “jiendesheni kama raia.” Maneno hayo yalikuwa na maana ya pekee kwa kutaniko la Filipi. Kwa nini? Kwa sababu inaonekana kwamba Filipi lilikuwa moja kati ya majiji machache ambayo wenyeji wake walipewa haki fulani za uraia wa Roma. Raia wa Roma walioishi Filipi na kotekote katika Milki ya Roma walijivunia uraia wao na walifurahia ulinzi wa pekee chini ya sheria ya Roma.

2 Washiriki wa kutaniko la Filipi walikuwa na sababu nyingine kubwa zaidi ya kujivunia. Paulo aliwakumbusha kwamba wakiwa Wakristo watiwa-mafuta, uraia wao uko “mbinguni.” (Flp. 3:20) Walikuwa raia, si wa milki ya wanadamu, bali raia wa Ufalme wa Mungu. Kwa hiyo, walifurahia baraka na ulinzi usio na kifani.​—Efe. 2:19-22.

3. (a) Ni nani walio na fursa ya kuwa raia wa Ufalme? (b) Tutachunguza nini katika makala hii?

3 Himizo la Paulo la ‘kujiendesha kama raia’ linawahusu hasa wale ambao watatawala pamoja na Kristo huko mbinguni. (Flp. 3:20) Lakini linaweza pia kutumiwa kuwahusu wale ambao watakuwa raia wa Ufalme wa Mungu hapa duniani. Kwa nini? Kwa sababu Wakristo wote waliojiweka wakfu wanamtumikia Mfalme yuleyule, Yehova, na ni lazima waishi kulingana na viwango vilevile. (Efe. 4:4-6) Leo, watu wanafanya juu chini ili wastahili kuwa raia wa nchi tajiri. Je, hatupaswi kuthamini hata zaidi fursa tuliyo nayo ya kuwa raia wa Ufalme? Ili tuthamini hata zaidi pendeleo hilo, acheni tuchunguze ulinganifu fulani uliopo kati ya matakwa ya kuwa raia wa serikali ya wanadamu na matakwa ya kuwa raia wa Ufalme wa Mungu. Kisha tutachunguza mambo matatu ambayo ni lazima tufanye ili tuendelee kuwa na pendeleo la kuwa raia wa Ufalme.

MATAKWA YA KUWA RAIA

4. Lugha safi ni nini, na “tunaizungumza” jinsi gani?

4 Jifunze lugha. Baadhi ya serikali za wanadamu huwataka wale wanaoomba uraia wazungumze lugha kuu ya nchi hiyo. Hata baada ya kupata uraia, huenda watu wakaendelea kujitahidi kwa miaka mingi kuijua vizuri zaidi lugha hiyo mpya. Wanaweza kujifunza haraka sheria za lugha hiyo ingawa huenda ikawachukua muda mrefu kutamka maneno kwa njia inayofaa. Vivyo hivyo, Ufalme wa Mungu unawataka raia wake wajifunze ile inayoitwa katika Biblia “lugha safi.” (Soma Sefania 3:9.) Ni lugha gani hiyo? Ni ukweli kumhusu Mungu na makusudi yake ambayo yameandikwa katika Biblia. “Tunazungumza” lugha safi tunapojiendesha kupatana na sheria na kanuni za Mungu. Huenda raia wa Ufalme wa Mungu wakajifunza haraka mafundisho ya msingi ya Biblia na kubatizwa. Lakini, hata baada ya kubatizwa, ni lazima wajitahidi “kuizungumza” vizuri zaidi hiyo lugha safi. Kwa njia gani? Kila mmoja wetu anahitaji kuendelea kujitahidi hata zaidi kutenda kupatana na kanuni za Biblia alizojifunza.

5. Kwa nini tunapaswa kujifunza yote tunayoweza kuhusu historia ya tengenezo la Yehova?

5 Jifunze historia. Mtu anayetaka kuwa raia wa serikali ya wanadamu huenda akalazimika kujifunza mambo fulani kuhusu historia ya serikali hiyo. Vivyo hivyo, wale wanaotaka kuwa raia wa Ufalme wanapaswa kujifunza yote wanayoweza kuhusu Ufalme wa Mungu. Fikiria mfano uliowekwa na wana wa Kora waliotumikia katika taifa la kale la Israeli. Waliupenda sana mji wa Yerusalemu na mahali pa ibada nao walifurahia sana kusimulia historia yake. Kilichowavutia zaidi si majengo yake bali ni kile ambacho kiliwakilishwa na mji huo na mahali hapo pa ibada. Yerusalemu ulikuwa “mji wa Mfalme Mkuu,” Yehova, kwa kuwa ulikuwa kitovu cha ibada safi. Huko ndiko Sheria ya Yehova ilikofundishwa. Yehova aliwaonyesha fadhili zenye upendo watu waliotawaliwa na Mfalme wa Yerusalemu. (Soma Zaburi 48:1, 2, 9, 12, 13.) Je, sisi pia tuna tamaa kama yao ya kujifunza na kusimulia historia ya sehemu ya kidunia ya tengenezo la Yehova? Kadiri unavyojifunza mengi zaidi kuhusu tengenezo la Mungu na jinsi Yehova anavyowategemeza watu wake, ndivyo Ufalme wa Mungu utakavyokuwa halisi zaidi kwako. Na bila shaka hilo litakuchochea kuwa na tamaa zaidi ya kuhubiri habari njema ya Ufalme.​—Yer. 9:24; Luka 4:43.

6. Kwa nini ni jambo linalopatana na akili kwa Yehova kututarajia tujifunze na kutii sheria na kanuni za Ufalme?

6 Zijue sheria. Serikali za wanadamu zinawataka raia wake wajifunze na kutii sheria za nchi. Basi inaonekana kwamba ni jambo linalopatana na akili kwa Yehova kututarajia tujifunze na kutii sheria na kanuni ambazo zinawaongoza raia wote wa Ufalme. (Isa. 2:3; Yoh. 15:10; 1 Yoh. 5:3) Mara nyingi sheria za wanadamu zina kasoro na huenda zisiwe za haki. Kinyume na hilo, “sheria ya Yehova ni kamilifu.” (Zab. 19:7) Je, tunapendezwa na sheria ya Mungu na kulisoma Neno lake kila siku? (Zab. 1:1, 2) Njia pekee ya kuijua sheria ya Mungu ni kujifunza sheria hiyo sisi wenyewe. Hakuna mtu mwingine yeyote anayeweza kufanya hivyo kwa ajili yetu.

RAIA WA UFALME WANAVIPENDA VIWANGO VYA MUNGU

7. Raia wa Ufalme wanaishi kulingana na viwango gani vya juu zaidi?

7 Ili kuendelea kuwa raia wa Ufalme, hatuhitaji tu kujua viwango vya Mungu bali pia kuvipenda. Raia wengi wa serikali za wanadamu husema kwamba wanakubali sheria na viwango vya nchi ambamo wanaishi. Hata hivyo, wanapoona kwamba takwa fulani haliwapendezi na wanapohisi kwamba hakuna mtu anayewaona, wao huvunja sheria. Mara nyingi, watu hao ‘wanawapendeza wanadamu.’ (Kol. 3:22) Raia wa Ufalme wanaishi kulingana na viwango vya juu zaidi. Tunafurahia kutii sheria za Mungu, hata wakati ambapo hakuna mwanadamu anayetuona. Kwa nini? Kwa sababu tunampenda Mpaji-sheria wetu.​—Isa. 33:22; soma Luka 10:27.

8, 9. Utajuaje ikiwa unapenda kikweli sheria za Mungu?

8 Utajuaje ikiwa unapenda kikweli sheria za Mungu? Chunguza jinsi unavyoitikia unaposhauriwa kuhusu mambo fulani unayopenda, kama vile mavazi na kujipamba. Kabla ya kuwa raia wa Ufalme, huenda ulipenda kuvaa ovyoovyo au kwa njia iliyowaudhi wengine. Kadiri upendo wako kwa Mungu ulivyoongezeka, ndivyo ulivyojifunza kuvaa kwa njia inayomletea heshima. (1 Tim. 2:9, 10; 1 Pet. 3:3, 4) Huenda ukahisi kwamba sasa unavaa mavazi yenye kiasi. Lakini namna gani mzee wa kutaniko akikwambia kwamba mavazi yako yanawaudhi wahubiri wengi katika kutaniko? Utaitikiaje? Je, utaanza kujitetea, kukasirika, au kuwa mkaidi? Sheria ya msingi ya Ufalme wa Mungu ni kwamba raia wote wanapaswa kumwiga Kristo. (1 Pet. 2:21) Mtume Paulo aliandika hivi kuhusu mfano wa Yesu: “Kila mmoja wetu na ampendeze jirani yake katika yaliyo mema kwa ajili ya kujengwa kwake. Kwa maana hata Kristo hakujipendeza mwenyewe.” (Rom. 15:2, 3) Ili kudumisha amani kutanikoni, Mkristo mkomavu yuko tayari kutii bila kinyongo na kuepuka kuumiza dhamiri za wengine.​—Rom. 14:19-21.

9 Fikiria mambo mengine mawili yaliyo muhimu: mtazamo wetu kuhusu ngono na maoni yetu kuhusu ndoa. Wale ambao hawajawa raia wa Ufalme wa Mungu huenda wakakubali ngono kati ya watu wa jinsia moja, kuiona ponografia kuwa burudani tu isiyo na madhara, na kufikiri kwamba uzinzi na talaka ni mambo ya kibinafsi. Raia wa Ufalme wameacha kabisa mitazamo hiyo ya kichoyo isiyozingatia madhara. Ingawa mwanzoni Wakristo wengi waliishi maisha mapotovu kimaadili, sasa wanaona ngono na ndoa kuwa zawadi kutoka kwa Mungu. Wanathamini sana viwango vya juu vya Yehova na kukubali kwa moyo wote kwamba wale wanaoendelea kutenda mambo mapotovu ya kingono hawastahili kuwa raia wa Ufalme. (1 Kor. 6:9-11) Hata hivyo, wanatambua pia kwamba moyo ni wenye hila. (Yer. 17:9) Kwa hiyo, wanathamini kupokea maonyo hususa ambayo yanawasaidia kudumisha viwango vya juu vya maadili.

RAIA WA UFALME WANATHAMINI MAONYO

10, 11. Ni maonyo gani ya wakati unaofaa yanayotolewa na Ufalme wa Mungu, na unahisije kuhusu maonyo hayo?

10 Huenda serikali za wanadamu zikatoa maonyo kuhusu vyakula na dawa ambazo zinaweza kudhuru afya ya raia. Bila shaka, si vyakula na dawa zote zilizo mbaya. Lakini ikiwa chakula au dawa fulani ni hatari, serikali inaweza kutoa maonyo yaliyosawazika ili kuwalinda raia wake. Ikiwa serikali haifanyi hivyo, itakuwa na hatia kwa sababu ya kutojali afya ya raia wake. Vivyo hivyo, Ufalme wa Mungu unatoa maonyo ya wakati unaofaa kuhusu hatari fulani hususa za kimaadili na kiroho. Kwa mfano, Intaneti imekuwa njia muhimu ya mawasiliano, burudani, na ya kuwaelimisha watu. Tengenezo la Mungu linatumia Intaneti kutimiza mambo mengi mazuri. Hata hivyo, vituo vingi vya Intaneti ni hatari kwa hali yetu ya kiroho na ya kimaadili. Ni wazi kwamba vituo vya Intaneti vinavyoeneza ponografia ni hatari kwa afya ya kiroho ya raia wa Ufalme. Kwa makumi ya miaka, jamii ya mtumwa mwaminifu imetuonya kuhusu vituo vya aina hiyo. Tunathamini sana maonyo hayo yanayolinda afya yetu ya kiroho.

11 Katika miaka ya hivi karibuni, vituo fulani vya Intaneti vimependwa na watu wengi sana. Vituo hivyo vinaweza kuwa vyenye faida ikiwa vinatumiwa kwa uangalifu mkubwa. Lakini vituo hivyo, ambavyo vinaitwa vituo vya mawasiliano, vinaweza pia kumharibu mtu. Vinaweza kumwingiza mtu katika mashirika mabaya. (1 Kor. 15:33) Basi, haishangazi kwamba tengenezo la Mungu limetoa maonyo yaliyosawazika kuhusu kutumia vituo vya aina hiyo. Je, umesoma habari zote ambazo zimechapishwa hivi karibuni na mtumwa mwaminifu kuhusu kutumia vituo vya mawasiliano? Ni jambo lisilo la hekima kama nini kutumia vituo hivyo bila kusoma habari hizo! * Kufanya hivyo ni kama kumeza dawa yenye nguvu bila kusoma kibandiko chenye onyo kilicho juu ya chupa ya dawa hiyo.

12. Kwa nini ni jambo la upumbavu kupuuza maonyo?

12 Wale wanaopuuza maonyo yanayotolewa na mtumwa mwaminifu bila shaka wanajiletea wenyewe na wapendwa wao madhara. Wengine wamekuwa na mazoea ya kutazama ponografia au wamefanya uasherati kisha wanajidanganya wenyewe kwa kufikiri kwamba Yehova hawezi kuona mambo wanayofanya. Ni upumbavu kama nini kuamini kwamba tunaweza kuficha mwenendo wetu machoni pa Yehova! (Met. 15:3; soma Waebrania 4:13.) Mungu anataka kuwasaidia watu hao naye anawaongoza wawakilishi wake duniani ili wajaribu kuwasaidia. (Gal. 6:1) Hata hivyo, kama vile tu ambavyo serikali za wanadamu zinavyoweza kumnyang’anya uraia mtu anayetenda mambo fulani, vivyo hivyo, Yehova atawanyang’anya uraia wale ambao wanavunja viwango vyake bila kutubu. * (1 Kor. 5:11-13) Hata hivyo, yeye ni mwenye rehema. Wale wanaotubu na kubadili mwenendo wao wanaweza kuwa tena na msimamo mzuri machoni pa Yehova na kuendelea kuwa raia wa Ufalme. (2 Kor. 2:5-8) Ni heshima kubwa kama nini kumtumikia Mfalme huyo mwenye upendo!

RAIA WA UFALME WANATHAMINI ELIMU

13. Raia wa Ufalme wanaonyeshaje kwamba wanathamini elimu?

13 Serikali nyingi za wanadamu zinajitahidi sana kuwaelimisha raia wake. Zinaanzisha shule za kuwafundisha watu kusoma na kuandika na pia ustadi unaofaa wa kazi. Raia wa Ufalme wanathamini shule hizo za kilimwengu na wanajifunza kwa bidii kusoma, kuandika, na wanajitegemeza wenyewe kifedha. Wanathamini hata zaidi elimu ambayo wanapata wakiwa raia wa Ufalme wa Mungu. Kupitia kutaniko la Kikristo, Yehova anawafundisha kusoma na kuandika. Wazazi wanatiwa moyo kuwasomea vitabu watoto wao wachanga. Kila mwezi, mtumwa mwaminifu anachapisha kurasa kadhaa zinazotegemea Biblia katika gazeti la Mnara wa Mlinzi na Amkeni! Ukisoma kurasa chache kila siku ya mwezi, utamaliza kusoma habari hizo zote zinazoandaliwa kupitia machapisho hayo muhimu yanayotumiwa kutoa elimu ya Ufalme.

14. (a) Tunapata mazoezi gani? (b) Ni mapendekezo gani kuhusu jioni ya Ibada ya Familia ambayo umefurahia kufuata?

14 Kila juma, raia wa Ufalme wanazoezwa katika mikutano yao ya kutaniko. Kwa mfano, kwa miaka zaidi ya sitini, Shule ya Huduma ya Kitheokrasi imekuwa ikiwasaidia wanafunzi kuwa walimu stadi wa Neno la Mungu. Je, umejiandikisha katika shule hiyo? Katika miaka ya hivi karibuni, mtumwa mwaminifu amekazia hasa umuhimu wa kuwa na jioni ya Ibada ya Familia kila juma. Mpango huo unaimarisha familia. Je, unafuata mapendekezo yanayochapishwa katika machapisho yetu kuhusu jioni ya Ibada ya Familia? *

15. Taja pendeleo moja kubwa zaidi tulilonalo.

15 Raia wa serikali za wanadamu huwatafuta hadharani wafuasi wa kuunga mkono chama chao cha kisiasa, hata wanaenda nyumba kwa nyumba kuwatafuta. Kwa kiwango kikubwa hata zaidi, raia wa Ufalme wanautetea kwa bidii Ufalme wa Mungu barabarani na nyumba kwa nyumba. Kwa kweli, kama ilivyotajwa katika makala iliyotangulia ya funzo, gazeti Mnara wa Mlinzi, ambalo linatangaza Ufalme wa Yehova, ndilo gazeti linalosambazwa kwa wingi zaidi duniani leo! Pendeleo moja kubwa zaidi tulilonalo ni kuwaambia wengine kuhusu Ufalme wa Mungu. Je, unashiriki kwa bidii katika kazi ya kuhubiri?​—Mt. 28:19, 20.

16. Unaweza kuthibitishaje kwamba wewe ni raia mzuri wa Ufalme wa Mungu?

16 Hivi karibuni Ufalme wa Mungu utakuwa ndio serikali pekee inayotawala dunia. Ufalme huo utasimamia mambo yote yanayohusu maisha ya kila siku, si mambo ya kiroho tu bali pia mambo yanayohusu maisha ya raia. Je, utakuwa raia mzuri wa Ufalme wa Mungu wakati huo? Huu ndio wakati wa kuthibitisha hivyo. Katika maamuzi yote unayofanya kila siku, fanya mambo yote kwa utukufu wa Yehova ili kuthibitisha kwamba unajiendesha kama raia mzuri wa Ufalme wa Mungu.​—1 Kor. 10:31.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 14 Tazama gazeti Mnara wa Mlinzi la Agosti 15, 2011, ukurasa wa 6-7 na Huduma Yetu ya Ufalme, Januari 2011, ukurasa wa 3-6.

[Maswali ya Funzo]

[Blabu katika ukurasa wa 14]

Je, unatii maonyo yanayotegemea Biblia kuhusu Intaneti?

[Picha katika ukurasa wa 12]

Kama wana wa Kora, je, unapendezwa na ibada safi na historia yake?

[Picha katika ukurasa wa 15]

Jioni yenu ya Ibada ya Familia inaweza kukusaidia sana wewe na wapendwa wako kuwa raia wazuri wa Ufalme