Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jihadhari Na Mitego Ya Ibilisi!

Jihadhari Na Mitego Ya Ibilisi!

Jihadhari Na Mitego Ya Ibilisi!

‘Toka katika mtego wa Ibilisi.’​—2 TIM. 2:26.

UNGEJIBUJE?

Unahitaji kujichunguza jinsi gani ikiwa una mwelekeo wa kuwachambua-chambua wengine isivyofaa?

Kutokana na mifano ya Pilato na Petro, unaweza kujifunza nini kuhusu kutoshindwa na woga na misongo ya watu?

Unawezaje kuepuka kujihisi kuwa na hatia kupita kiasi?

1, 2. Katika makala hii tutachunguza mitego ipi ya Ibilisi?

IBILISI anawawinda watumishi wa Yehova. Lengo lake hasa si kuwaangamiza, kama mwindaji wa wanyama anavyofanya. Badala yake, lengo kuu la Ibilisi ni kunasa windo au mtu akiwa hai na kumtumia mtu huyo kama atakavyo.​—Soma 2 Timotheo 2:24-26.

2 Ili kunasa windo likiwa hai, huenda mtegaji akatumia mtego wa aina fulani. Huenda akajaribu kumfanya mnyama atoke nje mahali ambapo anaweza kumnasa kwa kitanzi. Au mtegaji anaweza kutumia mtego uliofichwa unaofyatuka ili kumnasa mnyama kwa ghafla. Ibilisi anatumia mitego kama hiyo ili kuwanasa watumishi wa Mungu wakiwa hai. Ikiwa tunataka kuepuka kunaswa, ni lazima tuwe macho na kutii ishara zinazotuonya kwamba kuna mtego au mitego ya Shetani karibu. Makala hii itachunguza jinsi tunavyoweza kujilinda dhidi ya mitego mitatu ambayo Ibilisi ametumia na kufanikiwa kwa kiasi fulani. Mitego hiyo ni (1) usemi usiodhibitiwa, (2) woga na msongo wa watu, na (3) kujihisi kuwa na hatia kupita kiasi. Makala inayofuata itachunguza mitego mingine miwili ya Shetani.

ZIMA MOTO WA USEMI USIODHIBITIWA

3, 4. Kushindwa kuudhibiti ulimi wetu kunaweza kuwa na matokeo gani? Toa mfano.

3 Ili kuwatimua wanyama mahali wanapojificha, huenda mwindaji akawasha moto sehemu fulani ya pori na kuwanasa wanyama wanapojaribu kukimbia. Kwa njia ya mfano, Ibilisi angependa kuwasha moto katika kutaniko la Kikristo. Ibilisi akifaulu kufanya hivyo, anaweza kufanya ndugu na dada walikimbie kutaniko, mahali penye usalama, na kuanguka mikononi mwake. Tunawezaje kushirikiana na Shetani bila kujua na hivyo kunaswa na mtego wake?

4 Mwanafunzi Yakobo aliufananisha ulimi na moto. (Soma Yakobo 3:6-8.) Tukishindwa kuudhibiti ulimi wetu, tunaweza kuwasha moto wa mfano unaoenea kwa kasi kutanikoni. Hali hiyo inaweza kutokeaje? Fikiria mfano ufuatao: Kwenye mkutano mmoja wa kutaniko, tangazo linatolewa kwamba dada fulani amewekwa rasmi kuwa painia wa kawaida. Baada ya mkutano huo, dada wawili wahubiri wanazungumza kuhusu tangazo hilo. Mmoja wao anashangilia na kusema kwamba anamtakia painia huyo mpya mafanikio. Yule dada mwingine anatilia shaka nia ya painia huyo na kudai kwamba painia huyo anatafuta tu umaarufu kutanikoni. Ni yupi kati ya wahubiri hao wawili ambaye ungependa awe rafiki yako? Si vigumu kutambua ni dada yupi anayeweza kuwasha moto kutanikoni kupitia usemi wake.

5. Ili kuzima moto unaosababishwa na usemi usiodhibitiwa, ni vizuri tujichunguze jinsi gani?

5 Tunawezaje kuzima moto unaosababishwa na usemi usiodhibitiwa? Yesu alisema hivi: “Kinywa kinasema kutokana na mambo yaliyojaa katika moyo.” (Mt. 12:34) Hivyo, hatua ya kwanza ni kuuchunguza moyo wetu. Je, tunaepuka hisia mbaya zinazochochea usemi wenye kuharibu? Kwa mfano, tunaposikia kwamba ndugu mmoja anajitahidi kufikia pendeleo fulani la utumishi, je, tunaamini mara moja kwamba ana nia nzuri, au tunahisi kwamba anachochewa na faida za kichoyo? Ikiwa tuna mwelekeo wa kufikiri kwamba ndugu zetu wanamtumikia Mungu kwa sababu za kichoyo, ni vizuri tukumbuke kwamba Ibilisi alitilia shaka nia ya Ayubu, mtumishi mwaminifu wa Mungu. (Ayu. 1:9-11) Badala ya kumshuku ndugu yetu, ingekuwa vizuri tuchunguze kwa nini tunamchambua-chambua ndugu huyo. Je, kweli tuna sababu nzuri ya kuwa na mawazo kama hayo? Au je, moyo wetu umetiwa sumu na roho isiyo ya upendo iliyoenea katika siku hizi za mwisho?​—2 Tim. 3:1-4.

6, 7. (a) Taja baadhi ya sababu zinazoweza kutufanya tuwachambue-chambue wengine. (b) Tunapaswa kutendaje tunapotukanwa?

6 Ona sababu nyingine ambazo huenda zikafanya tuwachambue-chambue wengine. Sababu moja inaweza kuwa kwamba tunatamani mambo tunayofanya yajulikane zaidi. Kwa kweli, huenda tunajaribu kuonyesha kwamba sisi ni bora kwa kuwadharau wengine. Au huenda tunajaribu kutoa visingizio kwa kutofanya jambo lililo sawa. Iwe tunawachambua-chambua wengine kwa sababu tunaongozwa na kiburi, wivu, au kutojiamini, matokeo ni mabaya.

7 Huenda tukahisi kwamba tuna sababu ya kumchambua mtu fulani. Labda mtu huyo amewahi kutuumiza kwa kusema nasi bila kujidhibiti. Ikiwa ndivyo mambo yalivyo, kulipiza kisasi hakutasuluhisha tatizo hilo. Kutenda kwa njia hiyo kunafanya tu hali iwe mbaya zaidi na kunatimiza mapenzi ya Ibilisi, bali si mapenzi ya Mungu. (2 Tim. 2:26) Ni vizuri tumwige Yesu. Alipokuwa akitukanwa, “hakujibu kwa matukano.” Badala yake, “aliendelea kujiweka mkononi mwa yule ambaye anahukumu kwa uadilifu.” (1 Pet. 2:21-23) Yesu alikuwa na hakika kwamba Yehova angeshughulikia mambo hayo kwa njia Yake na kwa wakati Wake mwenyewe. Tunapaswa kumtegemea Mungu kwa njia hiyohiyo. Tunaposema mambo mazuri yanayoponya, tunasaidia kudumisha “kifungo chenye kuunganisha cha amani” katika kutaniko letu.​—Soma Waefeso 4:1-3.

EPUKA MTEGO WA WOGA NA MSONGO WA WATU

8, 9. Kwa nini Pilato alimhukumu Yesu?

8 Mnyama anayenaswa katika mtego hana uhuru wa kwenda popote anapotaka. Vivyo hivyo, mtu anayeshindwa na woga na msongo wa watu hupoteza kwa kiasi fulani uhuru wa kudhibiti maisha yake. (Soma Methali 29:25.) Acheni tuchunguze mifano ya wanaume wawili tofauti kabisa walioshindwa na misongo na kuwaogopa wengine ili tuone yale tunayoweza kujifunza kutokana na mambo yaliyowapata maishani.

9 Gavana Mroma Pontio Pilato alijua kwamba Yesu hakuwa na hatia na inaonekana kwamba hakutaka kumdhuru. Kwa kweli, Pilato alisema kwamba Yesu hakufanya “jambo lolote linalostahili kifo.” Hata hivyo, Pilato aliamua Yesu auawe. Kwa nini? Kwa sababu Pilato alishindwa na msongo wa umati. (Luka 23:15, 21-25) Wapinzani hao walipiga kelele hivi wakimsonga Pilato afanye walichotaka: “Ukimfungua mtu huyu, wewe si rafiki ya Kaisari.” (Yoh. 19:12) Huenda Pilato aliogopa kwamba angepoteza cheo chake au labda uhai wake ikiwa angemtetea Kristo. Kwa hiyo, alijiruhusu kushawishiwa kutenda mapenzi ya Ibilisi.

10. Ni nini kilichomfanya Petro amkane Kristo?

10 Mtume Petro alikuwa kati ya marafiki wa karibu zaidi wa Yesu. Alitangaza hadharani kwamba Yesu alikuwa ndiye Masihi. (Mt. 16:16) Petro alibaki mshikamanifu wakati wanafunzi wengine walipokosa kuelewa maana ya yale ambayo Yesu alisema na hivyo wakamwacha. (Yoh. 6:66-69) Na maadui walipokuja kumkamata Yesu, Petro aliutumia upanga kumlinda Bwana wake. (Yoh. 18:10, 11) Hata hivyo, baadaye Petro alishindwa na woga na kukana kwamba hata hamjui Yesu Kristo. Kwa kipindi fulani, mtume huyo alinaswa katika mtego wa kuogopa wanadamu na akaruhusu woga huo umzuie kuwa jasiri.​—Mt. 26:74, 75.

11. Huenda tukalazimika kupambana na uvutano gani mbaya?

11 Tukiwa Wakristo tunahitaji kushinda misongo ya kufanya mambo yasiyompendeza Mungu. Waajiri au watu wengine wanaweza kujaribu kutulazimisha kufanya mambo ya udanganyifu au wanaweza kutushawishi tujihusishe katika mwenendo mpotovu kingono. Huenda wanafunzi wakashawishiwa na wanafunzi wenzao kuiba mitihani, kutazama ponografia, kuvuta sigara, kutumia madawa ya kulevya, kunywa pombe, au kujihusisha katika mwenendo mpotovu kingono. Kwa hiyo, ni nini kinachoweza kutusaidia kuepuka mtego wa woga na wa msongo wa kufanya mambo yasiyompendeza Yehova?

12. Ni mambo gani tunayoweza kujifunza kutokana na mifano ya Pilato na Petro?

12 Acheni tuone mambo tunayoweza kujifunza kutokana na mifano ya Pilato na Petro. Pilato alijua mambo machache kumhusu Kristo. Hata hivyo, alijua kwamba Yesu hakuwa na hatia na kwamba hakuwa mtu wa kawaida. Lakini Pilato alikosa unyenyekevu na upendo kumwelekea Mungu wa kweli. Ibilisi alimnasa kwa urahisi akiwa hai. Petro alikuwa na ujuzi sahihi na pia alimpenda Mungu. Hata hivyo, nyakati nyingine alikosa sifa ya kiasi, akawa mwoga, na akashindwa na msongo wa watu. Kabla ya Yesu kukamatwa, Petro alijigamba hivi: “Hata ikiwa wengine wote watakwazika, hata hivyo mimi sitakwazika.” (Marko 14:29) Mtume huyo angejitayarisha vizuri zaidi kukabiliana na majaribu yaliyokuwa mbele yake ikiwa angekuwa na msimamo kama ule wa mtunga-zaburi aliyemtegemea Mungu na kuimba hivi: “Yehova yuko upande wangu; sitaogopa. Mtu wa udongo anaweza kunitenda nini?” (Zab. 118:6) Usiku wa mwisho wa maisha Yake duniani, Yesu alimchukua Petro na mitume wengine wawili na kuingia ndani kabisa ya bustani ya Gethsemane. Hata hivyo, badala ya kukaa macho, Petro na wenzake walilala usingizi. Yesu aliwaamsha na kusema: “Endeleeni kukesha na kusali, ili msiingie katika jaribu.” (Marko 14:38) Lakini Petro alilala tena na baadaye akashindwa na woga na pia msongo wa watu.

13. Tunawezaje kushinda misongo ya kufanya jambo fulani baya?

13 Mifano ya Pilato na Petro inaweza kutufundisha somo lingine muhimu: Ili kufaulu kushinda misongo tunahitaji sifa kama vile ujuzi sahihi, unyenyekevu, kiasi, kumpenda na kumwogopa Yehova Mungu, wala si wanadamu. Ikiwa imani yetu inajengwa juu ya msingi wa ujuzi sahihi, tutasema kwa ujasiri na usadikisho kuhusu imani yetu. Hilo litatusaidia kushinda msongo na woga wa wanadamu. Bila shaka, hatupaswi kamwe kujiamini kupita kiasi. Badala yake, tunapaswa kutambua kwa unyenyekevu kwamba tunahitaji nguvu za Mungu ili kushinda misongo ya watu. Tunahitaji kumwomba Yehova roho yake na pia ni lazima tuache upendo kumwelekea utuchochee kutetea jina na viwango vyake. Zaidi ya hayo, tunahitaji kujitayarisha kukabiliana na misongo kabla jaribu halijatokea. Kwa mfano, kujitayarisha mapema pamoja na kusali kunaweza kuwasaidia watoto wetu kujua vizuri jambo la kufanya watoto wenzao wanapojaribu kuwashawishi wafanye jambo fulani baya.​—2 Kor. 13:7. *

EPUKA MTEGO UNAOPONDA​—KUJIHISI KUWA NA HATIA KUPITA KIASI

14. Ibilisi angetaka tukate kauli gani kuhusu makosa tuliyotenda wakati uliopita?

14 Nyakati nyingine mtego wa wanyama unakuwa ni gogo au jiwe zito linaloning’inizwa juu ya njia ambayo wanyama wanapitia kwa ukawaida. Mnyama asiyekuwa mwangalifu anakanyaga waya, na hivyo kusababisha gogo hilo au jiwe kuanguka na kumponda. Kujihisi kuwa na hatia kupita kiasi kunaweza kulinganishwa na mzigo mzito wenye kuponda. Tunapofikiria makosa tuliyotenda wakati uliopita, huenda tukahisi ‘tumepondwa kupita kiasi.’ (Soma Zaburi 38:3-5, 8.) Shetani angetaka tukate kauli kwamba hatustahili rehema za Yehova na hatuwezi kutimiza viwango Vyake.

15, 16. Unawezaje kuepuka kunaswa na mtego wa kujihisi kuwa na hatia kupita kiasi?

15 Unawezaje kuepuka mtego huo unaoponda? Ikiwa umefanya dhambi nzito, chukua hatua sasa ili urudishe uhusiano wako pamoja na Yehova. Waone wazee, na uwaombe msaada. (Yak. 5:14-16) Fanya yote uwezayo ili kurekebisha kosa hilo. (2 Kor. 7:11) Ukitiwa nidhamu, usivunjike moyo. Nidhamu inaonyesha kwa hakika kwamba Yehova anakupenda. (Ebr. 12:6) Azimia kutofuata tena hatua zilizokuongoza kwenye dhambi, na utende kulingana na azimio lako. Baada ya kutubu na kugeuka, uwe na imani kwamba dhabihu ya fidia ya Yesu Kristo inaweza kwa kweli kufunika makosa yako.​—1 Yoh. 4:9, 14.

16 Baadhi ya watu wanaendelea kujihisi kuwa na hatia kuhusu dhambi ambazo kwa kweli wamesamehewa. Ikiwa unahisi hivyo, kumbuka kwamba Yehova alimsamehe Petro na mitume wengine waliomwacha Mwana Wake mpendwa Yesu wakati ambapo aliwahitaji zaidi. Yehova alimsamehe mwanamume aliyetengwa na kutaniko la Korintho kwa sababu ya upotovu mbaya sana wa maadili lakini baadaye akatubu. (1 Kor. 5:1-5; 2 Kor. 2:6-8) Neno la Mungu linasema kuhusu watu waliotenda dhambi nzito ambao walitubu na kusamehewa na Mungu.​—2 Nya. 33:2, 10-13; 1 Kor. 6:9-11.

17. Fidia inaweza kutusaidiaje?

17 Yehova atayasamehe na kuyasahau makosa yetu ya wakati uliopita tukitubu kikweli na kukubali rehema yake. Usihisi kamwe kwamba dhabihu ya fidia ya Yesu haiwezi kufunika dhambi zako. Tukihisi hivyo, tutakuwa tumenaswa na mojawapo ya mitego ya Shetani. Licha ya yale ambayo Ibilisi anataka uamini, ukweli ni kwamba fidia inaweza kufunika dhambi za wote ambao wametenda dhambi na kutubu. (Met. 24:16) Imani katika fidia inaweza kukuondolea mzigo unaokulemea wa kujihisi ukiwa na hatia kupita kiasi na inaweza kukupa nguvu za kumtumikia Mungu kwa moyo, akili, na nafsi yako yote.—Mt. 22:37.

HATUKOSI KUZIJUA MBINU ZA SHETANI

18. Tunaweza kuepukaje mitego ya Ibilisi?

18 Shetani hajali ni mtego upi anaotumia ili kutunasa, mradi tu atunase. Kwa kuwa hatukosi kuzijua mbinu za Shetani, tunaweza kuepuka kushindwa akili na Ibilisi. (2 Kor. 2:10, 11) Hatutanaswa na mitego yake ikiwa tunasali tupewe hekima ya kuvumilia majaribu. Yakobo aliandika hivi: “Ikiwa yeyote kati yenu anakosa hekima, na aendelee kumwomba Mungu, kwa maana yeye huwapa wote kwa ukarimu na bila kushutumu; naye atapewa hiyo.” (Yak. 1:5) Tunahitaji kutenda kulingana na sala zetu kwa kuwa na funzo la kibinafsi la kawaida na kufuata Neno la Mungu. Machapisho yanayotegemea Biblia yanayotolewa na jamii ya mtumwa mwaminifu na mwenye busara yanaonyesha mitego inayotumiwa na Ibilisi na yanatusaidia kuiepuka.

19, 20. Kwa nini tunapaswa kuchukia mambo mabaya?

19 Kusali na kujifunza Biblia kunatusaidia kupenda mambo mema. Lakini pia ni jambo muhimu kujifunza kuchukia mambo mabaya. (Zab. 97:10) Kutafakari matokeo mabaya ya kufuatia tamaa za kichoyo kunaweza kutusaidia kuepuka tamaa hizo. (Yak. 1:14, 15) Tunapojifunza kuchukia mambo mabaya na kupenda kikweli yale yaliyo mazuri, tunachukia kabisa mambo ambayo Shetani anatumia kama chambo ili kutunasa; nayo hayawezi kamwe kutuvutia.

20 Tunashukuru kama nini kwamba Mungu anatusaidia ili Shetani asitushinde akili! Kupitia roho, Neno, na tengenezo Lake, Yehova anatukomboa “kutokana na yule mwovu.” (Mt. 6:13) Katika makala inayofuata, tutajifunza jinsi ya kuepuka mitego mingine miwili ambayo Ibilisi ametumia kwa mafanikio kuwanasa watumishi wa Mungu wakiwa hai.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 13 Ni vizuri wazazi wazungumze na watoto wao sehemu yenye kichwa “Kukabiliana na Mkazo” katika kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza​—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2, ukurasa wa 132-133. Habari hizo zinaweza kutumiwa katika jioni ya Ibada ya Familia.

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 21]

Usemi usiodhibitiwa unaweza kuwasha moto wa matatizo kutanikoni

[Picha katika ukurasa wa 24]

Unaweza kuondoa mzigo wa kujihisi kuwa na hatia kupita kiasi