Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutoka Katika Hifadhi ya Vitu Vyetu vya Kale

Kusafiri Pamoja na Mapilgrimu

Kusafiri Pamoja na Mapilgrimu

“KWA kweli siwezi kuhubiri nyumba kwa nyumba!” Wanafunzi wengi wapya wa Biblia wamehisi hivyo kuhusu kuwahubiria watu wasiowajua! Hata hivyo, maneno hayo yalisemwa na msemaji mwenye uzoefu na mwalimu wa Biblia aliyeitwa pilgrimu.

Wasomaji wengi wa Zion’s Watch Tower walioacha kushirikiana na makanisa yao, walitamani kushirikiana na wale waliokuwa na kiu kama yao ya kujua kweli za Biblia. Gazeti hilo liliwahimiza wasomaji wake kuwatafuta watu wengine wenye imani yenye thamani kama yao na kukusanyika kwa ukawaida ili kujifunza Biblia. Kuanzia mwaka wa 1894, shirika la Watch Tower Society liliwatuma wawakilishi wake wanaosafiri kukutana na vikundi vilivyoomba kutembelewa. Wanaume hao waliokuja kuitwa mapilgrimu, walikuwa wenye uzoefu na wenye bidii, nao walichaguliwa kwa sababu ya sifa zao nzuri kama vile upole, ujuzi wa Biblia, ustadi wao wa kufundisha na kusema, na kuonyesha uaminifu kuelekea dhabihu ya Kristo. Kwa kawaida, waliwatembelea kwa siku moja au mbili tu zenye shughuli nyingi. Wanafunzi wengi wa Biblia walianza kushiriki utumishi wa shambani kwa kugawanya mialiko ya kuwakaribisha wengine kusikiliza hotuba ya watu wote ambayo ingetolewa na pilgrimu. Jioni moja baada ya kumaliza kutoa hotuba katika shule fulani, Hugo Riemer, ambaye baadaye alikuja kuwa mshiriki wa Baraza Linaloongoza, alijibu maswali ya Biblia ya wasikilizaji mpaka usiku wa manane. Ijapokuwa alikuwa amechoka alikuwa mwenye furaha, naye alisema kwamba mkutano “ulipendeza sana.”

Gazeti la Mnara wa Mlinzi lilitaja kwamba “lengo kuu” la ziara za mapilgrimu ni kuijenga “nyumba ya imani” kupitia mikutano iliyofanywa katika nyumba za waamini. Wanafunzi wa Biblia kutoka maeneo jirani walikuja kusikiliza hotuba na kushiriki katika vipindi vya maswali na majibu. Kisha ukafika wakati wa kuonyesha ukarimu wa Kikristo. Alipokuwa msichana, Maude Abbott alihudhuria hotuba asubuhi, na baadaye wote wakakusanyika kwenye meza moja ndefu nje ya nyumba. “Kulikuwa na vyakula vingi vizuri—nyama ya paja la nguruwe, kuku wa kukaangwa, mikate ya kila aina, maandazi, na keki! Kila mtu alikula kadiri alivyoweza, na ilipofika saa nane hivi mchana, tukakusanyika tena ili kusikiliza hotuba nyingine.” Lakini anakiri hivi, “Kufikia wakati huo karibu kila mtu alikuwa anasinzia.” Pindi moja, Benjamin Barton, pilgrimu wa muda mrefu alisema, ‘Ikiwa ningekula vyakula vyote vinono ambavyo nilipewa, ningeiacha kazi yangu ya upilgrimu siku nyingi zilizopita.’ Hatimaye barua kutoka makao makuu huko Brooklyn, iliwashauri akina dada wenye nia nzuri. Ilisema kwamba itakuwa vyema zaidi ikiwa watawaandalia mapilgrimu “vyakula vya kawaida, ambavyo ni rahisi kupika” na “vitakavyowawezesha kupata usingizi mzuri.”

Mapilgrimu walikuwa stadi katika kufundisha wakitumia michoro, vielelezo, au kitu chochote ambacho kingesaidia kufanya wazo kuu liwe wazi zaidi. Hotuba zilizotolewa na R. H. Barber “siku zote zilikuwa tamu sana kiroho.” Akiwa kama Baba, W. J. Thorn alizungumza “kama mmoja wa wazee wa ukoo wa zamani.” Siku moja alipokuwa akisafiri kwa gari aina ya Model A Ford, Shield Toutjian kwa ghafla alipaaza sauti, “Simama!” Kisha akatoka katika gari, akachuma maua fulani na kuwapa wale aliokuwa anasafiri pamoja nao, akawafundisha somo ambalo hawakutarajia kuhusiana na uumbaji wa Yehova.

Kazi ya upilgrimu, ilitokeza magumu mengi hasa kwa mapilgrimu waliokuwa na umri wa makamo au umri mkubwa zaidi. Hata hivyo, jaribio kubwa zaidi kwa wengine lilikuwa ni badiliko kuhusu kazi yao ya upilgrimu. Sasa walitazamiwa kuongoza katika kazi ya kuhubiri nyumba kwa nyumba. Gazeti la Mnara wa Mlinzi la Machi 15, 1924 lilitaja kwamba “moja kati ya majukumu makuu” waliyopewa Wakristo wa kweli “ni kutoa ushahidi kuhusu ufalme. Mapilgrimu wanatumwa kwa kusudi hilo.”

Hata hivyo, mapilgrimu fulani walichukizwa na badiliko hilo nao wakaacha kazi ya kusafiri, hata wengine wao wakaanzisha vikundi vyao. Robie D. Adkins anamkumbuka pilgrimu mmoja aliyekuwa mtoaji mzuri sana wa hotuba ambaye alilalamika hivi kwa uchungu: “Kile ninachojua ni kuhubiri nikiwa jukwaani. Siwezi kwenda nyumba kwa nyumba!” Ndugu Adkins alikumbuka hivi: “Nilimwona tena ndugu huyo katika kusanyiko la mwaka 1924 huko Columbus, Ohio. Akiwa amesimama peke yake chini ya mti, alionekana kuwa mtu mwenye taabu nyingi sana, asiye na furaha kati ya maelfu ya ndugu wenye shangwe nyingi. Sikumwona tena kamwe ndugu huyo. Muda mfupi baadaye aliacha kushirikiana na tengenezo.” Kwa upande mwingine, “ndugu wengi walibeba vitabu na kuvipeleka ndani ya magari yao wakiwa na shangwe,” huku wakiwa na hamu ya kuhubiri nyumba kwa nyumba.​—Mdo. 20:20, 21.

Ijapokuwa mapilgrimu wengi walikuwa na wasiwasi sana kuhusu kazi ya kuhubiri nyumba kwa nyumba sawa tu na ndugu wapya ambao walipaswa kuwazoeza, bado walihubiri kwa bidii. Kuhusiana na kazi ya kutoa ushahidi nyumba kwa nyumba, pilgrimu mmoja mwenye kuzungumza Kijerumani anayeitwa Maxwell G. Friend (Freschel) aliandika hivi: “Sehemu hii ya kazi ya upilgrimu inafanya safari iwe na baraka nyingi zaidi.” Pilgrimu John A. Bohnet aliripoti kwamba ndugu kwa ujumla walikubali kwa moyo wote himizo la kuhubiri kuhusu Ufalme. Kulingana na maelezo ya ndugu huyo, wengi wao walikuwa “na bidii ya kuwa mbele katika pambano.”

Kwa miaka mingi, waangalizi waaminifu wanaosafiri wamekuwa na uvutano mzuri sana juu ya ndugu na dada. Norman Larson, Shahidi wa muda mrefu alisema hivi: “Tangu nilipokuwa mvulana, nilitambua kwamba thamani na faida ya mapilgrimu si ya kutiliwa shaka. Walijitahidi kunifinyanga katika njia inayofaa.” Mpaka leo, waangalizi kama hao wanaosafiri walio washikamanifu na wenye kujidhabihu, wanawasaidia waamini wenzao kusema, “Tunaweza kuhubiri nyumba kwa nyumba!”

[Blabu katika ukurasa wa 32]

Ilikuwa siku yenye shangwe sana pilgrimu alipotutembelea!

[Picha katika ukurasa wa 31]

Ratiba ya Benjamin Barton ya mwaka 1905 inaonyesha kwamba alitembelea vituo 170

[Picha katika ukurasa wa 32]

Walter J. Thorn alikuwa pilgrimu, naye aliitwa na rafiki zake Baba kwa sababu alikuwa na mwelekeo kama wa Kristo

[Picha katika ukurasa wa 32]

J. A. Browne alitumwa Jamaika kama pilgrimu katika mwaka 1902 ili kuimarisha na kutia moyo vikundi 14 vidogo

[Picha katika ukurasa wa 32]

Kazi ya upilgrimu ilijenga imani, ikaimarisha umoja wa Kikristo, na kuwaleta akina ndugu karibu na tengenezo