Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Mimi Nipo Pamoja Nanyi”

“Mimi Nipo Pamoja Nanyi”

“Mimi Nipo Pamoja Nanyi”

“Wengi watakwenda huku na huku, na ujuzi wa kweli utakuwa mwingi.”​—DAN. 12:4.

UNGEJIBUJE?

Katika nyakati za kisasa, “ujuzi wa kweli” umeenea kadiri gani?

Wale wanaoikubali kweli wamekuwaje “wengi”?

Ujuzi sahihi umekuwa “mwingi” katika njia zipi?

1, 2. (a) Tunajuaje kwamba Yesu yupo pamoja na raia wake sasa na atakuwa pamoja nao wakati ujao? (b) Kulingana na andiko la Danieli 12:4, kujifunza Maandiko kwa makini kungekuwa na matokeo gani?

JIWAZIE ukiwa katika Paradiso. Kila asubuhi, unaamka ukihisi kwamba umepumzika vya kutosha na una hamu ya kuanza siku mpya. Huna maumivu wala uchungu. Magonjwa yoyote uliyokuwa nayo yametoweka. Hisi zako zote zinafanya kazi kikamilifu, yaani, uwezo wa kuona, kusikia, kunusa, kugusa, na kuonja. Una nguvu nyingi sana, unafurahia kazi yako, una marafiki wengi, na huna wasiwasi wowote tena. Hizo ndizo baraka ambazo utaweza kufurahia chini ya Ufalme wa Mungu. Kristo Yesu, Mfalme aliyewekwa rasmi, atawabariki raia wake na kuwafundisha kumjua Yehova.

2 Yehova atakuwa pamoja na watumishi wake washikamanifu watakaposhiriki katika kazi hiyo ya kuwaelimisha wanadamu duniani pote. Kwa karne nyingi, Mungu pamoja na Mwana wake wamekuwa na watumishi waaminifu. Kabla ya kupanda mbinguni, Yesu aliwahakikishia wanafunzi wake washikamanifu kwamba angekuwa pamoja nao. (Soma Mathayo 28:19, 20.) Ili kuimarisha imani yetu katika ahadi hiyo, acheni tuchunguze sentensi moja tu ya unabii fulani ulioongozwa na roho ya Mungu ambao uliandikwa katika milki ya kale ya Babiloni miaka zaidi ya 2,500 iliyopita. Kuhusu “wakati wa mwisho” tunamoishi sasa, nabii Danieli aliandika hivi: “Wengi watakwenda huku na huku, na ujuzi wa kweli utakuwa mwingi.” (Dan. 12:4) Kwa njia ya mfano na kupatana na mambo hakika yanayotukia leo, kitenzi cha Kiebrania ambacho kinatafsiriwa, ‘kwenda huku na huku’ katika mstari huo, kinatoa wazo la kuchunguza kwa makini. Kwenda huku na huku kwa njia ya mfano kungetokeza baraka nzuri kama nini! Wale ambao wangejifunza Maandiko kwa makini wangebarikiwa kwa kupata ujuzi wa kweli, au sahihi, wa Neno la Mungu. Unabii huo unasema pia kwamba watu wengi wangepata “ujuzi wa kweli.” Isitoshe, ujuzi huo ungekuwa mwingi. Ungesambazwa kila mahali na kupatikana kwa urahisi. Tunapochunguza jinsi ambavyo unabii huo umetimizwa, tunaona kwamba Yesu yupo pamoja na wanafunzi wake leo na kwamba Yehova ana uwezo kamili wa kutimiza mambo yote ambayo ameahidi.

WAKRISTO WANYOOFU WAPATA “UJUZI WA KWELI”

3. Ilikuwaje kuhusiana na “ujuzi wa kweli” baada ya mitume kufa?

3 Kama ilivyotabiriwa, baada ya mitume kufa, waasi-imani walijitenga na Ukristo wa kweli, wakasitawi na kuenea kama moto. (Mdo. 20:28-30; 2 The. 2:1-3) Kwa karne nyingi, wale ambao hawakujua lolote kuhusu Biblia hawakuwa kamwe na “ujuzi wa kweli,” na hata wale waliodai kuwa Wakristo. Ingawa walidai kwamba wanaamini Maandiko, viongozi wa dini zinazodai kuwa za Kikristo walifundisha uwongo wa kidini, yaani, “mafundisho ya roho waovu” ambayo yalimvunjia Mungu heshima. (1 Tim. 4:1) Watu kwa ujumla walikuwa katika giza la kiroho. Mafundisho ya waasi-imani yalitia ndani fundisho la uwongo la kwamba Mungu ni Utatu, nafsi haifi, na kwamba nafsi fulani zinateswa milele motoni.

4. Kikundi fulani cha Wakristo kilianza jinsi gani kutafuta “ujuzi wa kweli” katika miaka ya 1870?

4 Hata hivyo, katika miaka ya 1870, miongo minne hivi kabla ya “siku za mwisho” kuanza, kikundi kidogo cha Wakristo wanyoofu huko Pennsylvania, Marekani, kilikutana ili kujifunza Biblia kwa bidii na kutafuta “ujuzi wa kweli.” (2 Tim. 3:1) Walijiita Wanafunzi wa Biblia. Wanafunzi hao hawakuwa watu “wenye hekima na wenye akili” ambao Yesu alisema kwamba wangefichwa ujuzi huo. (Mt. 11:25) Walikuwa watu wanyenyekevu ambao walitamani kwa unyoofu kufanya mapenzi ya Mungu. Walisali, wakasoma kwa makini, wakazungumzia, na kutafakari kuhusu Maandiko. Walilinganisha pia maandiko mbalimbali ya Biblia na kuchunguza maandishi ya watu wengine waliokuwa wamefanya utafiti kama huo. Wanafunzi hao wa Biblia walielewa hatua kwa hatua kweli ambazo zilikuwa zimefichwa kwa karne nyingi.

5. Trakti mbalimbali zenye kichwa The Old Theology zilichapishwa kwa kusudi gani?

5 Ingawa Wanafunzi hao wa Biblia walisisimuka kwa sababu ya mambo waliyokuwa wakijifunza, hawakuruhusu ujuzi ambao walikuwa wamepata uwafanye wajivune kwa kiburi; wala hawakujigamba kwamba walikuwa wamepata jambo jipya. (1 Kor. 8:1) Badala yake, walichapisha trakti mbalimbali zenye kichwa The Old Theology. Kusudi lao lilikuwa kuwasaidia wasomaji wajifunze kweli za Kimaandiko zilizoandikwa katika Biblia. Trakti ya kwanza kati ya hizo ilikuwa na “habari zaidi za kusoma za kumsaidia mtu ajifunze Biblia na kukataa kabisa mapokeo yote ya uwongo ya wanadamu na kufuata tena mafundisho ya awali ya Bwana wetu na ya mitume.”​—The Old Theology, Na. 1, Aprili 1889, uku. 32.

6, 7. (a) Ni kweli gani ambazo tumesaidiwa kuelewa kuanzia miaka ya 1870? (b) Ni kweli gani hasa ambazo umethamini kujifunza?

6 Tumejifunza kweli nzuri kama nini tangu mwanzo huo mdogo miaka zaidi ya 100 iliyopita! * Kweli hizo si masuala ya kielimu tu na yenye kuchosha ambayo wanatheolojia wanabishania. Ni kweli zenye kusisimua sana zinazotuweka huru na kufanya maisha yetu yawe na kusudi, yajae shangwe na tumaini. Zinatusaidia kumjua Yehova, yaani, kujua utu wake wenye upendo na makusudi yake. Zinafafanua pia daraka la Yesu, na zinaeleza kwa nini aliishi na kufa, na mambo anayofanya sasa. Kweli hizo zenye thamani zinafunua kwa nini Mungu anaruhusu uovu, kwa nini tunakufa, jinsi tunavyopaswa kusali, na jinsi tunavyoweza kupata furaha ya kweli.

7 Sasa tunaweza kuelewa maana ya unabii mbalimbali ambao ulibaki kuwa “siri” kwa maelfu ya miaka lakini unatimia wakati huu wa mwisho. (Dan. 12:9) Unabii huo unatia ndani ule ulio katika Maandiko, hasa katika vitabu vya Injili na kitabu cha Ufunuo. Yehova hata ametusaidia kuelewa matukio ambayo hatungeweza kuona kwa macho yetu, kama vile kutawazwa kwa Yesu kuwa mfalme, vita vilivyotokea mbinguni, na kutupwa kwa Shetani duniani. (Ufu. 12:7-12) Mungu pia ametusaidia kuelewa maana ya mambo tunayoona kama vile vita, matetemeko ya nchi, tauni au magonjwa ya kuambukiza, upungufu wa chakula, na pia watu wasiomwogopa Mungu ambao wanafanya hali iwe mbaya zaidi katika ‘nyakati hizi za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.’​—2 Tim. 3:1-5; Luka 21:10, 11.

8. Tunamtukuza nani kwa sababu ya mambo ambayo tumeona na kusikia?

8 Ni rahisi kwetu kuelewa maana ya maneno haya ambayo Yesu aliwaambia wanafunzi wake: “Yenye furaha ni macho yanayoona mambo ambayo ninyi mnayaona. Kwa maana ninawaambia ninyi, Manabii na wafalme wengi walitamani kuyaona mambo ambayo ninyi mnayaona lakini hawakuyaona, na kuyasikia mambo ambayo ninyi mnayasikia lakini hawakuyasikia.” (Luka 10:23, 24) Tunamtukuza Yehova Mungu kwa kutuwezesha kuona na kusikia mambo hayo. Na tunathamini kama nini kwamba “msaidizi,” yaani, roho takatifu ya Mungu, ametumwa ili kuwaongoza wafuasi wa Yesu “ndani ya kweli yote”! (Soma Yohana 16:7, 13.) Sikuzote na tuthamini kabisa “ujuzi wa kweli” na kuwafundisha wengine bila ubinafsi.

“WENGI” WANAKUBALI “UJUZI WA KWELI”

9. Ni mwito gani uliotolewa katika toleo la Aprili 1881 la gazeti hili?

9 Mnamo Aprili 1881, miaka isiyozidi miwili baada ya kuchapishwa kwa toleo la kwanza la Mnara wa Mlinzi, gazeti hili lilitoa mwito wa kutafuta wahubiri 1,000. Makala hiyo ilisema hivi: “Wale ambao wanaweza kutumia nusu au kiasi kikubwa zaidi cha wakati wao kwa ajili tu ya kazi ya Bwana, tunapendekeza . . . , kwamba: Mwende katika miji mikubwa au midogo, kulingana na uwezo wenu, mkiwa Makolpota au Waeneza-Injili, ili kutafuta kila mahali Wakristo wanyoofu, na wengi wao mtaona kwamba wana bidii kwa ajili ya Mungu, lakini si kulingana na ujuzi; waambieni watu hao kuhusu wema mwingi sana wa Baba Yetu, na mambo yenye kuvutia yaliyo katika neno Lake.”

10. Watu waliitikiaje mwito wa kutafuta wahubiri wa wakati wote?

10 Mwito huo ulionyesha kwamba Wanafunzi wa Biblia walitambua kuwa kazi muhimu ya Wakristo wa kweli ni kuhubiri habari njema. Lakini mwito wa kutafuta wahubiri 1,000 wa wakati wote ulionekana unawezekana, ingawa ni mamia kadhaa tu ya watu waliohudhuria mikutano ya Wanafunzi wa Biblia wakati huo. Hata hivyo, baada ya kusoma trakti au gazeti, watu wengi walitambua kwamba ujumbe huo ulikuwa wa kweli nao wakaukubali mwito huo kwa utayari. Kwa mfano, baada ya kusoma gazeti la Mnara wa Mlinzi na kijitabu kilichochapishwa na Wanafunzi wa Biblia, katika mwaka wa 1882, msomaji mmoja huko London, Uingereza, aliandika hivi: “Tafadhali nifundisheni jambo la kuhubiri na namna ya kuhubiri ili nitimize kazi iliyobarikiwa ambayo Mungu anataka ifanywe.”

11, 12. (a) Kama makolpota, tuna lengo gani? (b) Makolpota walianzishaje “madarasa,” au makutaniko?

11 Kufikia mwaka wa 1885, Wanafunzi 300 hivi wa Biblia walikuwa wakishiriki katika utumishi wa ukolpota. Wahudumu hao wa wakati wote walikuwa na lengo kama letu leo, yaani, kufanya wanafunzi wa Yesu Kristo. Hata hivyo, njia walizotumia zilikuwa tofauti na zetu. Leo, kwa kawaida tunajifunza Biblia na mtu binafsi, na kumwelimisha akiwa peke yake. Kisha tunamwalika mwanafunzi huyo wa Biblia ili ashirikiane na kutaniko ambalo tayari lipo. Zamani, makolpota waliwaachia watu vitabu kisha waliwakusanya pamoja wanaopendezwa ili wajifunze Maandiko wakiwa kikundi. Badala ya kujifunza na mtu binafsi, walianzisha “madarasa,” au makutaniko.

12 Kwa mfano, katika mwaka wa 1907, kikundi kimoja cha makolpota kilienda katika jiji fulani kutafuta watu ambao tayari walikuwa na vitabu Millennial Dawn (ambavyo pia viliitwa Studies in the Scriptures). Gazeti la Mnara wa Mlinzi liliripoti hivi: “Watu hao [wanaopendezwa] walikusanyika ili kufanya mkutano mdogo katika mojawapo ya nyumba zao. Kwa kawaida kolpota alizungumza nao kuhusu kitabu Divine Plan of the Ages Jumapili nzima, na Jumapili iliyofuata aliwahimiza wafanye mikutano kwa ukawaida.” Mwaka wa 1911, akina ndugu walirekebisha utaratibu huo. Wahudumu wa pekee hamsini na wanane wanaosafiri walitoa hotuba za watu wote kotekote nchini Marekani na Kanada. Ndugu hao waliandika majina na anwani za watu waliopendezwa ambao walihudhuria hotuba hizo na kufanya mipango ya kukutana pamoja katika nyumba za watu binafsi ili kuanzisha “madarasa” mapya. Kufikia mwaka wa 1914, kulikuwa na makutaniko 1,200 ya Wanafunzi wa Biblia ulimwenguni pote.

13. Ni nini kinachokupendeza kuhusu kuenea kwa “ujuzi wa kweli” leo?

13 Leo, kuna makutaniko yapatayo 109,400 ulimwenguni pote, na ndugu na dada 895,800 wanatumikia wakiwa mapainia. Watu karibu milioni nane sasa wanakubali “ujuzi wa kweli,” na kuutumia katika maisha yao. (Soma Isaya 60:22.) * Jambo hilo ni la pekee hasa kwa sababu Yesu alitabiri kwamba wanafunzi wake ‘wangechukiwa na watu wote’ kwa sababu ya jina lake. Aliongeza kwamba wafuasi wake wangeteswa, wangefungwa gerezani, na hata kuuawa. (Luka 21:12-17) Waabudu wa Yehova wamepata mafanikio makubwa sana katika kazi yao ya kufanya wanafunzi licha ya kwamba wamepingwa na Shetani, roho wake waovu, na watu fulani. Leo, wanahubiri katika “dunia yote inayokaliwa,” kuanzia kwenye misitu mikubwa, nyanda tambarare zenye baridi kali, milimani, jangwani, katika miji, mpaka kwenye maeneo ya mbali sana ya mashambani. (Mt. 24:14) Kazi hiyo haingeweza kamwe kutimizwa bila utegemezo wa Mungu.

“UJUZI WA KWELI” UMEKUWA “MWINGI”

14. “Ujuzi wa kweli” umeenezwaje kotekote kupitia machapisho?

14 “Ujuzi wa kweli” umekuwa mwingi kwa sababu ya wahubiri wengi wanaotangaza habari njema. Pia, umekuwa mwingi kwa sababu ya machapisho yanayotolewa. Mnamo Julai 1879, Wanafunzi wa Biblia walichapisha toleo la kwanza la gazeti hili, ambalo liliitwa Zion’s Watch Tower and Herald of Christ’s Presence. Toleo hilo lilichapishwa na kampuni fulani iliyochapa nakala 6,000 za Kiingereza tu. Charles Taze Russell ambaye alikuwa na umri wa miaka ishirini na saba alichaguliwa kuwa mhariri wa gazeti hilo, na Wanafunzi wengine wa Biblia watano walio wakomavu wakawa waandishi wa kawaida wa gazeti hilo. Sasa gazeti Mnara wa Mlinzi linachapishwa katika lugha 195. Ndilo gazeti linalosambazwa kwa wingi zaidi duniani, kwa kuwa nakala 42,182,000 za kila toleo zinachapishwa. Gazeti la pili ambalo linasambazwa kwa wingi zaidi ni gazeti Amkeni! Nakala 41,042,000 za gazeti hilo zinachapishwa katika lugha 84. Kwa kuongezea, nakala milioni 100 hivi za vitabu na Biblia zinachapishwa kila mwaka.

15. Kazi yetu ya uchapishaji inagharimiwaje?

15 Kazi hiyo kubwa sana inagharimiwa na michango ya hiari. (Soma Mathayo 10:8.) Jambo hilo peke yake linawashangaza sana wenye viwanda vya uchapishaji kwa sababu wanajua kwamba mashini za kuchapa, karatasi, wino, na vifaa vingine vinagharimu pesa nyingi sana. Ndugu mmoja anayenunua vifaa kwa ajili ya ofisi za tawi za Mashahidi wa Yehova anasema hivi: “Wafanyabiashara wanaotembelea viwanda vyetu vya uchapishaji wanashangaa kujua kwamba viwanda hivyo vyenye mashini zinazotumia teknolojia ya kisasa na ambazo zinatokeza machapisho mengi sana, vinagharimiwa na michango ya hiari. Wanavutiwa pia kuona kwamba wengi wa wale wanaofanya kazi Betheli ni vijana wenye furaha.”

UJUZI KUMHUSU MUNGU UTAIJAZA DUNIA

16. Yehova amefunua “ujuzi wa kweli” kwa kusudi gani?

16 “Ujuzi wa kweli” umekuwa mwingi kwa kusudi zuri. Mapenzi ya Mungu ni kwamba “watu wa namna zote waokolewe na kupata ujuzi sahihi wa kweli.” (1 Tim. 2:3, 4) Yehova anataka watu wajue kweli ili waweze kumwabudu kwa njia inayofaa na kupata baraka zake. Kwa kufunua “ujuzi wa kweli,” Yehova amekusanya Wakristo watiwa-mafuta waaminifu duniani. Anakusanya pia “umati mkubwa” kutoka “mataifa yote na makabila na vikundi vya watu na lugha.” Umati huo una tumaini la kuishi milele duniani.​—Ufu. 7:9.

17. Kuenea kwa ibada ya kweli kunaonyesha nini?

17 Kuenea kwa ibada ya kweli katika miaka zaidi ya 130 ambayo imepita kunaonyesha waziwazi kwamba Mungu na Mfalme wake aliyewekwa rasmi, Yesu Kristo, wamekuwa pamoja na watumishi wa Yehova duniani, wakiwaongoza, wakiwalinda, wakiwapanga kitengenezo, na kuwaelimisha. Ukuzi wao pia unaonyesha kwa hakika kwamba ahadi za Yehova za wakati ujao zitatimizwa. “Dunia hakika itajawa na kumjua Yehova kama vile maji yanavyoifunika bahari.” (Isa. 11:9) Wanadamu watafurahia baraka nyingi kama nini wakati huo!

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 6 Utafaidika ukitazama DVD zenye kichwa, Mashahidi wa Yehova​—Imani Yenye Matendo, Sehemu ya 1: Kutoka Gizani na Mashahidi wa Yehova—​Imani Yenye Matendo, Sehemu ya 2: Nuru na Iangaze.

^ fu. 13 Tazama kitabu cha Unabii wa Isaya​—Nuru kwa Wanadamu Wote II, ukurasa wa 320.

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 6]

Wanafunzi wa mapema wa Biblia walikuwa watu wanyenyekevu ambao walitamani kwa unyoofu kufanya mapenzi ya Mungu

[Picha katika ukurasa wa 7]

Yehova anathamini jitihada zako katika kueneza “ujuzi wa kweli” wa Mungu