Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Simama Imara Na Uepuke Mitego Ya Shetani!

Simama Imara Na Uepuke Mitego Ya Shetani!

Simama Imara Na Uepuke Mitego Ya Shetani!

‘Simama imara na kupinga hila za Ibilisi.’​—EFE. 6:11.

UNGEJIBUJE?

Mtumishi wa Yehova anawezaje kuepuka kunaswa na mtego wa kupenda vitu vya kimwili?

Ni nini kinachoweza kumsaidia Mkristo aliyefunga ndoa kutoanguka katika shimo la uzinzi?

Kwa nini unaamini kwamba kuna faida za kusimama imara dhidi ya kupenda vitu vya kimwili na mwenendo mpotovu wa kingono?

1, 2. (a) Kwa nini Shetani hana huruma kuelekea watiwa-mafuta na “kondoo wengine”? (b) Ni mitego gani ya Shetani itakayozungumziwa katika makala hii?

SHETANI IBILISI hana huruma kuwaelekea wanadamu, hasa wale wanaomtumikia Yehova. Kwa kweli, Shetani anapigana vita na watiwa-mafuta wanaobaki duniani. (Ufu. 12:17) Leo, Wakristo hao jasiri wameongoza kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme na wamewaonyesha watu kwamba Shetani ndiye mtawala wa ulimwengu huu. Pia, Ibilisi hawapendi hata kidogo “kondoo wengine” ambao wanawaunga mkono watiwa-mafuta na ambao wana tumaini la kuishi milele, tumaini ambalo Shetani hana tena. (Yoh. 10:16) Haishangazi kwamba ana hasira kali sana! Iwe tuna tumaini la kuishi mbinguni au la kuishi duniani, bila shaka Shetani hapendezwi na hali yetu njema. Lengo lake ni kutunasa.​—1 Pet. 5:8.

2 Ili kutimiza lengo lake, Shetani ametega mitego ya aina mbalimbali. Kwa kuwa “amezipofusha akili” za watu wasioamini, hawakubali habari njema na hawawezi kuiona mitego hiyo. Hata hivyo, Ibilisi anawatega pia baadhi ya wale ambao wamekubali ujumbe wa Ufalme. (2 Kor. 4:3, 4) Makala iliyotangulia ilionyesha jinsi tunavyoweza kuepuka mitego mitatu ya Shetani: (1) usemi usiodhibitiwa, (2) woga na msongo wa watu, na (3) kujihisi kuwa na hatia kupita kiasi. Acheni sasa tuchunguze jinsi tunavyoweza kusimama imara dhidi ya mitego mingine miwili ya Shetani, yaani, kupenda vitu vya kimwili na kishawishi cha kufanya uzinzi.

KUPENDA VITU VYA KIMWILI—MTEGO UNAOSONGA

3, 4. Mahangaiko ya mfumo huu wa mambo yanawezaje kumfanya mtu apende vitu vya kimwili?

3 Katika mojawapo ya mifano yake, Yesu alisema kuhusu mbegu iliyopandwa katikati ya miiba. Alisema kwamba mtu anaweza kusikia neno, “lakini mahangaiko ya mfumo huu wa mambo na nguvu za udanganyifu wa utajiri hulisonga neno, naye huwa asiyezaa matunda.” (Mt. 13:22) Naam, kupenda vitu vya kimwili ni mtego unaotumiwa na adui yetu Shetani.

4 Kuna mambo mawili ambayo yakiwa pamoja yanaweza kulisonga lile neno. Jambo moja ni “mahangaiko ya mfumo huu wa mambo.” Katika ‘nyakati hizi za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo,’ kuna mambo mengi yanayoweza kukufanya uwe na mahangaiko. (2 Tim. 3:1) Kwa sababu ya kupanda sana kwa gharama ya maisha na ukosefu mkubwa wa kazi, inaweza kuwa vigumu kupata riziki. Huenda pia ukawa na mahangaiko kuhusu wakati ujao na kujiuliza, ‘Je, nitakuwa na pesa za kutosha baada ya kustaafu?’ Kwa sababu ya mahangaiko hayo, watu wengine wamejaribu kufuatia utajiri, wakifikiri kwamba pesa zitawahakikishia usalama.

5. ‘Nguvu za utajiri’ zinaweza kwa njia gani kuwa za udanganyifu?

5 Yesu alizungumza kuhusu jambo lingine, yaani, “nguvu za udanganyifu wa utajiri.” Jambo hilo likiwa pamoja na mahangaiko linaweza kulisonga neno. Biblia inakiri kwamba “pesa ni ulinzi.” (Mhu. 7:12) Hata hivyo, si jambo la hekima kufuatia utajiri. Watu wengi wametambua kwamba kadiri wanavyojitahidi kupata utajiri, ndivyo wanavyotumbukia katika mtego wa kupenda vitu vya kimwili. Wengine hata wamekuwa watumwa wa utajiri.​—Mt. 6:24.

6, 7. (a) Kupenda vitu vya kimwili kunawezaje kumhatarisha mtu kazini? (b) Mkristo anapaswa kufikiria nini anapoombwa kufanya kazi saa za ziada?

6 Tamaa ya kupata utajiri inaweza kuanza bila mtu kutambua. Kwa mfano, fikiria hali ifuatayo. Mwajiri wako anakufikia na kukwambia hivi: “Nina habari njema! Kampuni yetu imepewa kazi kubwa ya kufanya. Kwa hiyo, itakulazimu kufanya kazi kwa saa nyingi zaidi miezi michache ijayo. Lakini ninakuhakikishia kwamba si kazi ya bure kwa sababu utalipwa pesa nyingi.” Utaitikiaje ukipata fursa kama hiyo? Bila shaka, ni daraka zito kuiandalia familia yako mahitaji ya kimwili, lakini hilo si daraka pekee ulilo nalo. (1 Tim. 5:8) Unapaswa kushughulikia madaraka mengine mengi. Utafanya kazi kwa saa ngapi za ziada? Je, kazi yako ya kimwili itavuruga utendaji wako wa kiroho, kutia ndani mikutano ya kutaniko na jioni yenu ya Ibada ya Familia?

7 Fikiria kwa uzito uamuzi wako, ni jambo gani unaloona kuwa muhimu, je, ni kiasi cha pesa utakachopata baada ya kufanya kazi saa za ziada au ni jinsi uamuzi huo utakavyoathiri hali yako ya kiroho? Je, tamaa ya kupata pesa zaidi itakufanya uache kutanguliza masilahi ya Ufalme maishani mwako? Je, unaweza kuona jinsi kupenda vitu vya kimwili kutakavyokuathiri ikiwa utapuuza afya yako ya kiroho na ya familia yako? Ikiwa unakabili hali hiyo sasa, unawezaje kusimama imara na kuepuka kusongwa na upendo wa vitu vya kimwili?​—Soma 1 Timotheo 6:9, 10.

8. Ni mifano gani ya Kimaandiko inayoweza kutusaidia kuchunguza mtindo wetu wa maisha?

8 Ili kuepuka kusongwa na tamaa ya vitu vya kimwili, ni vizuri kuchunguza pindi kwa pindi mtindo wako wa maisha. Usiwe kamwe kama Esau, ambaye alionyesha kwa matendo yake kwamba alidharau mambo ya kiroho! (Mwa. 25:34; Ebr. 12:16) Na bila shaka hupaswi kuwa kama yule mwanamume tajiri aliyeombwa auze vitu vyake, awape maskini, na kumfuata Yesu. Badala ya kufanya hivyo, mwanamume huyo ‘alienda zake akiwa amehuzunika, kwa maana alikuwa na mali nyingi.’ (Mt. 19:21, 22) Akiwa amenaswa na mtego wa utajiri, mwanamume huyo alipoteza pendeleo kubwa kama nini la kumfuata yule mtu mkuu zaidi aliyepata kuishi! Uwe makini ili usipoteze pendeleo la kuwa mwanafunzi wa Yesu Kristo.

9, 10. Maandiko yanasema nini kuhusu vitu vya kimwili?

9 Ili kushinda mahangaiko yasiyo ya lazima kuhusu vitu vya kimwili, tii himizo hili la Yesu: “Msihangaike kamwe na kusema, ‘Tutakula nini?’ au, ‘Tutakunywa nini?’ au, ‘Tutavaa nini?’ Kwa maana vyote hivi ndivyo vitu ambavyo mataifa yanafuatilia kwa tamaa. Kwa maana Baba yenu wa mbinguni anajua mnahitaji vitu hivi vyote.”​—Mt. 6:31, 32; Luka 21:34, 35.

10 Badala ya kushindwa na nguvu za udanganyifu wa utajiri, jitahidi kuwa na maoni ya mwandikaji wa Biblia Aguri, aliyesema hivi: “Usiniache niwe maskini sana au tajiri sana. Nipe tu kile ninachohitaji.” (Met. 30:8, Contemporary English Version) Ni wazi kwamba Aguri alielewa kuwa pesa zina uwezo wa kulinda na alielewa pia kuhusu nguvu za udanganyifu wa utajiri. Tambua kwamba mahangaiko ya mfumo huu na nguvu za udanganyifu wa utajiri zinaweza kuharibu hali yetu ya kiroho. Mahangaiko yasiyo ya lazima kuhusu vitu vya kimwili yanaweza kupoteza wakati wako, kukuchosha, na kukufanya ukose hamu ya kufuatia masilahi ya Ufalme. Kwa hiyo, azimia kutonaswa na mtego wa Shetani wa kupenda vitu vya kimwili!​—Soma Waebrania 13:5.

UZINZI​—SHIMO LILILOFUNIKWA KWA UJANJA

11, 12. Mkristo anawezaje kufanya uzinzi kazini?

11 Wawindaji wanaotaka kumnasa mnyama mwenye nguvu huenda wakachimba shimo katika njia ambayo mnyama huyo hupitia mara kwa mara. Mara nyingi shimo hilo hufunikwa na kifuniko chembamba kilichotengenezwa kwa vijiti na udongo. Kishawishi kimoja ambacho Shetani anatumia kwa mafanikio zaidi kinafanana na mtego huo. Ni dhambi ya upotovu wa maadili. (Met. 22:14; 23:27) Baadhi ya Wakristo wameanguka katika shimo hilo kwa kujiruhusu kuingia katika hali zilizowashawishi kwa urahisi kutenda dhambi. Wakristo fulani ambao wamefunga ndoa wameanguka katika uzinzi baada ya kusitawisha uhusiano usiofaa wa kimahaba.

12 Uhusiano usiofaa wa kimahaba unaweza kusitawi kati yako na mfanyakazi mwenzako. Utafiti mmoja ulionyesha kwamba zaidi ya nusu ya wanawake waliofanya uzinzi na pia wanaume 3 kati ya 4 waliofanya uzinzi walifanya hivyo na mfanyakazi mwenzao. Je, kazi yako ya kimwili inakulazimu kushirikiana na watu wa jinsia tofauti? Ikiwa ndivyo, basi una uhusiano gani pamoja nao? Je, unaweka mipaka ili uhusiano wako pamoja nao usigeuke na kuwa wa kimahaba? Kwa mfano, baada ya mazungumzo ya kawaida tu ya mara kwa mara na mfanyakazi mwenzake mwanamume, dada Mkristo anaweza kumfanya mwanamume huyo kuwa rafiki yake wa karibu, na hata kumweleza matatizo yake ya ndoa. Kwa upande mwingine, baada ya kuwa na urafiki na mfanyakazi mwenzake mwanamke, mwanamume Mkristo huenda akafikiri hivi: “Anajali maoni yangu na kunisikiliza kwa makini ninapozungumza naye. Na hata ananithamini. Laiti ningetendewa hivi nyumbani!” Je, unaweza kuona jinsi Wakristo wanaojiingiza katika hali kama hizo walivyo katika hatari ya kufanya uzinzi?

13. Uhusiano usiofaa wa kimahaba unaweza kuanza jinsi gani kutanikoni?

13 Uhusiano usiofaa wa kimahaba unaweza kuanza pia kutanikoni. Fikiria kisa hiki cha kweli. Daniel na mke wake, Sarah, * walikuwa mapainia wa kawaida. Daniel anasema kwamba alikubali mgawo wowote aliopewa kutanikoni. Alikuwa tayari kukubali kila pendeleo alilopata. Danieli aliwafunza Biblia vijana watano wanaume, na watatu kati yao wakabatizwa. Ndugu hao wapya waliobatizwa walihitaji sana msaada. Daniel alipokuwa akishughulikia migawo mbalimbali ya kitheokrasi, mara nyingi Sarah aliwasaidia ndugu hao. Punde si punde, hali hii ikatokea: Ndugu hao waliokuwa wanafunzi wa Biblia wa Daniel walihitaji msaada wa kihisia, na waliupata kutoka kwa Sarah. Naye Sarah alihitaji mtu anayemjali na kumsikiliza, na wanafunzi wa Biblia wa Daniel walifanya hivyo. Mtego hatari ulikuwa umetegwa. Daniel anasema hivi: “Mke wangu alidhoofika kiroho na kuumia kihisia kwa sababu ya kuwasaidia wale wanafunzi kwa miezi mingi. Jambo hilo, pamoja na kwamba nilikuwa nikimpuuza, lilisababisha madhara makubwa sana. Mke wangu alifanya uzinzi na mmoja wa ndugu hao waliokuwa wanafunzi wangu wa Biblia. Alidhoofika kiroho bila mimi kutambua kwa sababu nilijishughulisha sana na migawo yangu ya kutaniko.” Unawezaje kuepuka msiba kama huo?

14, 15. Ni mambo gani yanayoweza kuwasaidia Wakristo waliofunga ndoa kuepuka shimo la uzinzi?

14 Ili kuepuka kuanguka ndani ya shimo la uzinzi, tafakari kuhusu maana ya kuwa mshikamanifu kwa mwenzi wako wa ndoa. Yesu alisema hivi: “Kile ambacho Mungu ameunganisha mtu yeyote asikitenganishe.” (Mt. 19:6) Usifikiri kamwe kwamba mapendeleo yako ya kitheokrasi ni muhimu zaidi kuliko mwenzi wako wa ndoa. Isitoshe, tambua kwamba kumwacha mara kwa mara mwenzi wako wa ndoa ili kufanya kazi zisizo za lazima huenda kukaonyesha kwamba ndoa yako ni dhaifu na kunaweza kukuongoza katika kishawishi na labda hata dhambi nzito.

15 Ikiwa wewe ni mzee kutanikoni, unapaswa kulitunza kundi. Mtume Petro aliandika hivi: “Lichungeni kundi la Mungu lililo chini ya uangalizi wenu, si kwa kulazimishwa, bali kwa kupenda; wala si kwa kupenda pato lisilo la haki, bali kwa hamu.” (1 Pet. 5:2) Bila shaka, hupaswi kuwapuuza washiriki wa kutaniko walio chini ya uangalizi wako. Hata hivyo, hupaswi kutimiza jukumu lako ukiwa mchungaji na kupuuza jukumu lako ukiwa mume. Lingekuwa jambo lisilo na maana, na hatari, kujitahidi kabisa kulilisha kutaniko huku mwenzi wako wa ndoa “akifa njaa” kiroho nyumbani. Daniel anasema, “Hupaswi kamwe kung’ang’ana kupita kiasi kutimiza mapendeleo yako huku familia yako mwenyewe ikidhoofika kiroho.”

16, 17. (a) Wakristo waliofunga ndoa wanaweza kuchukua hatua gani zinazofaa kazini ili kuonyesha wazi kwamba hawako tayari kuwa na uhusiano wa kimahaba? (b) Ni habari gani zilizochapishwa zinazoweza kuwasaidia Wakristo kuepuka uzinzi?

16 Mashauri mengi mazuri yamechapishwa katika gazeti la Mnara wa Mlinzi na Amkeni! ili kuwasaidia Wakristo waliofunga ndoa waepuke kuanguka katika mtego wa uzinzi. Kwa mfano, gazeti Mnara wa Mlinzi la Septemba 15, 2006, lilitoa shauri hili: “Unapokuwa kazini na kwingineko, jihadhari na hali zinazoweza kufanya uwe na uhusiano wa karibu pamoja na mtu wa jinsia tofauti. Kwa mfano, kufanya kazi kwa ukaribu pamoja na mtu wa jinsia tofauti baada ya saa za kazi kunaweza kutokeza kishawishi. Ikiwa wewe ni mwanamume au mwanamke aliyefunga ndoa, unapaswa kuonyesha waziwazi kwa maneno na matendo kwamba hutaki kuwa na uhusiano wa kimahaba isipokuwa na mwenzi wako. Kwa kuwa unafuatia ujitoaji-kimungu, bila shaka hungependa kuwavutia watu kwa kucheza-cheza nao kimapenzi au kwa kuvalia na kujipamba kwa njia isiyofaa. . . . Kuweka picha za mwenzi wako wa ndoa na za watoto wako mahali pa kazi kutakukumbusha na kuwakumbusha wengine kwamba unaipenda familia yako. Azimia kutochochea wala kuruhusu vishawishi vya uhusiano wa kimahaba.”

17 Makala yenye kichwa “Uaminifu Katika Ndoa Unamaanisha Nini Hasa?” katika gazeti Amkeni! la Aprili 2009 ilionya dhidi ya kuwazia-wazia ukifanya ngono na mtu mwingine ambaye si mwenzi wako wa ndoa. Makala hiyo ilionyesha kwamba kuwazia-wazia ukifanya ngono na mtu ambaye si mwenzi wako wa ndoa kutafanya iwe rahisi zaidi kwako kufanya uzinzi. (Yak. 1:14, 15) Ikiwa umefunga ndoa, lingekuwa jambo la hekima kupitia habari hizo mara kwa mara pamoja na mwenzi wako. Ndoa ni mpango mtakatifu ulioanzishwa na Yehova mwenyewe. Kutenga wakati wa kuzungumza na mwenzi wako wa ndoa kuhusu ndoa yenu ni njia nzuri ya kuonyesha kwamba unathamini mambo matakatifu.​—Mwa. 2:21-24.

18, 19. (a) Uzinzi unasababisha madhara gani? (b) Kuna faida gani za kuwa mwaminifu katika ndoa?

18 Ikiwa unashawishiwa kuanzisha uhusiano wa kimahaba usiofaa, tafakari kuhusu madhara ya uasherati na uzinzi. (Met. 7:22, 23; Gal. 6:7) Wale wanaofanya uzinzi wanamchukiza Yehova na kujiumiza wenyewe na pia kuwaumiza wenzi wao wa ndoa. (Soma Malaki 2:13, 14.) Tofauti na hilo, tafakari kuhusu faida wanazopata wale wanaodumisha mwenendo safi. Si kwamba tu wana tumaini la kuishi milele bali pia wanafurahia maisha bora sasa, kutia ndani kuwa na dhamiri safi.​—Soma Methali 3:1, 2.

19 Mtunga-zaburi aliimba hivi: “Wale wanaoipenda sheria [ya Mungu] wana amani nyingi, na hakuna kitu cha kuwakwaza.” (Zab. 119:165) Kwa hiyo, pendeni kweli, na ‘mwendelee kuangalia sana kwamba jinsi mnavyotembea si kama watu wasio na hekima bali kama watu wenye hekima’ katika nyakati hizi zenye uovu. (Efe. 5:15, 16) Njia tunazofuata zimejaa mitego iliyotegwa na Shetani ili kuwanasa waabudu wa kweli. Lakini tumetayarishwa vizuri ili kujilinda. Yehova ametupatia tunachohitaji ili “kusimama imara” na “kuizima mishale yote inayowaka moto ya yule mwovu”!​—Efe. 6:11, 16.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 13 Majina yamebadilishwa.

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 26]

Kupenda vitu vya kimwili kunaweza kumsonga mtu kiroho. Usiruhusu hilo likupate

[Picha katika ukurasa wa 29]

Kumchezea mtu mwingine kimahaba, au kukubali kuchezewa kimahaba, kunaweza kukuongoza kufanya uzinzi