Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Shule za Kitheokrasi Zinathibitisha Upendo wa Yehova

Shule za Kitheokrasi Zinathibitisha Upendo wa Yehova

YEHOVA ni ‘Mfundishaji wetu Mkuu.’ (Isa. 30:20) Upendo unamchochea kuwaelimisha na kuwazoeza wengine. Kwa mfano, akichochewa na upendo mwingi sana, Yehova anamwonyesha Yesu “mambo yote anayofanya yeye mwenyewe.” (Yoh. 5:20) Kwa sababu ya upendo wake kutuelekea tukiwa Mashahidi wake, Yehova anatupatia “ulimi wa waliofundishwa,” tunapojitahidi kabisa kumheshimu na kuwasaidia wengine.​—Isa. 50:4.

Kwa kuiga mfano wa Yehova katika kuonyesha upendo, Halmashauri ya Ufundishaji ya Baraza Linaloongoza inatumia shule kumi za kitheokrasi ili kuwazoeza wale walio na tamaa na hali zinazowaruhusu kujiunga na shule hizo. Je, unaziona shule hizo kuwa uthibitisho wa upendo wa Yehova?

Furahia maelezo kuhusu shule zilizopo za kitheokrasi na maelezo kutoka kwa baadhi ya wale waliohudhuria shule hizo. Kisha jiulize, ‘Ninawezaje kufaidika na elimu hii ya kimungu?’

FAIDIKA KUTOKANA NA MAZOEZI YA KITHEOKRASI

Akiwa “Mungu wa upendo,” Yehova anatupatia mazoezi yanayofanya maisha yetu yawe yenye kusudi zaidi, yanayotutayarisha kushinda magumu, na kutusaidia kupata shangwe nyingi katika huduma yetu. (2 Kor. 13:11) Sawa na wanafunzi wa karne ya kwanza, tunatayarishwa kikamili ili kuwasaidia wengine, na ‘kuwafundisha kushika mambo yote’ tuliyoamriwa.​—Mt. 28:20.

Huenda tusiweze kuhudhuria shule hizi zote, hata hivyo, tunaweza kufaidika kutokana na shule moja au kadhaa. Nasi tunaweza kuyatumia mafundisho hayo yanayotegemea Biblia. Tunaweza pia kuongeza ustadi wetu katika huduma kwa kuhubiri pamoja na watumishi wa Yehova waliozoezwa vizuri.

Jiulize hivi: ‘Je hali zangu zinaniruhusu kuhudhuria mojawapo ya shule hizo?’

Waabudu wa Yehova wanaona kuwa ni pendeleo kuunga mkono na kujifunza katika shule hizo zenye thamani. Acha mazoezi unayopata yakusaidie kumkaribia zaidi Mungu na kukusaidia kutimiza majukumu yote aliyokupa, hasa kazi yenye uharaka ya kuhubiri habari njema.