Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Acheni Ndiyo Yenu Imaanishe Ndiyo

Acheni Ndiyo Yenu Imaanishe Ndiyo

“Acheni tu neno lenu Ndiyo limaanishe Ndiyo, Siyo yenu, Siyo.”​—MT. 5:37.

1. Yesu alisema nini kuhusu kuapa, na kwa nini?

KWA ujumla, si lazima Wakristo waape, kwa sababu wanamtii Yesu aliyesema hivi: “Acheni tu neno lenu Ndiyo limaanishe Ndiyo.” Alimaanisha kwamba mtu anapaswa kutimiza ahadi zake. Kabla ya kutaja amri hiyo, Yesu alisema hivi: “Msiape hata kidogo.” Alisema jambo hilo ili kushutumu zoea la watu wengi la kuapa mara nyingi kuhusu hili au lile, bila kuwa na nia ya kufanya mambo wanayosema. Watu wanaposema jambo “linalozidi” Ndiyo au Siyo inapohusu jambo wanalotaka kufanya, wanadhihirisha kwamba kwa kweli si washikamanifu na kwa hiyo wako chini ya uvutano wa “yule mwovu.”​—Soma Mathayo 5:33-37.

2. Eleza kwa nini si kosa kuapa katika pindi fulani.

2 Je, maneno ya Yesu yanamaanisha kwamba ni vibaya kuapa kwa njia yoyote? Ingewezekanaje? Kama tulivyojifunza katika makala iliyotangulia, Yehova Mungu na mtumishi wake mwadilifu Abrahamu walitoa ahadi zenye viapo katika pindi fulani muhimu. Pia, Sheria ya Mungu iliagiza kwamba watu waape ili kutatua mizozo fulani. (Kut. 22:10, 11; Hes. 5:21, 22) Kwa hiyo, huenda ikawa lazima kwa Mkristo kuapa kwamba atasema ukweli anapotoa ushahidi katika mahakama ya kisheria. Au, katika visa vichache, Mkristo anaweza kuona kwamba ni muhimu kuapa ili awahakikishie wengine kuhusu nia yake au ili asuluhishe suala fulani. Kwa kweli, Yesu mwenyewe alipowekwa chini ya kiapo na kuhani mkuu, hakupinga bali alisema ukweli mbele ya Sanhedrini ya Kiyahudi. (Mt. 26:63, 64) Hata hivyo, haikuwa lazima kwa Yesu kuapa kwa mtu yeyote yule. Ingawa hivyo, ili awahakikishie wasikilizaji wake kwamba ujumbe wake ulikuwa wenye kutegemeka, mara nyingi alianza ujumbe wake kwa njia hii ya pekee: “Kwa kweli kabisa [kihalisi, “Kweli, kweli”] ninawaambia ninyi.” (Yoh. 1:51; 13:16, 20, 21, 38) Acheni tuone mambo mengine tunayoweza kujifunza kutokana na mfano wa Yesu, Paulo, na wengine ambao Ndiyo yao ilimaanisha Ndiyo.

YESU NI MFANO BORA ZAIDI

3. Katika sala, Yesu alimwahidi Mungu nini, na Baba yake wa mbinguni aliitikiaje?

3 “Tazama! Nimekuja . . . ili kufanya mapenzi yako, Ee Mungu.” (Ebr. 10:7) Kwa maneno hayo yenye maana, Yesu alijitoa mwenyewe kwa Mungu ili atimize mambo yote yaliyotabiriwa kuhusu ule Uzao ulioahidiwa, kutia ndani yeye mwenyewe ‘kutiwa jeraha kwenye kisigino’ na Shetani. (Mwa. 3:15) Hakuna mwanadamu mwingine yeyote ambaye amewahi kujitolea kubeba daraka zito kama hilo. Yehova alisema kutoka mbinguni kwamba anamtumaini kabisa Mwana wake, hata ingawa haikuwa lazima kwa Yesu kuapa kwamba angeishi kupatana na wakfu wake.​—Luka 3:21, 22.

4. Yesu aliacha Ndiyo yake iwe Ndiyo kwa kadiri gani?

4 Daima, Yesu aliishi kupatana na mambo aliyohubiri, akiacha Ndiyo yake imaanishe Ndiyo. Yesu hakuruhusu jambo lolote limkengeushe asitimize kazi aliyopewa na Baba yake ya kuhubiri habari njema ya Ufalme wa Mungu na kuwafanya wanafunzi wale wote ambao Mungu aliwavuta kwake. (Yoh. 6:44) Kupitia maneno haya yanayojulikana sana, Biblia inaonyesha jinsi Yesu alivyojitahidi kabisa kusema kweli: “Hata ahadi za Mungu ziwe nyingi kadiri gani, zimekuwa Ndiyo kwa njia yake.” (2 Kor. 1:20) Kwa hakika, Yesu aliweka mfano bora zaidi katika kutimiza mambo aliyomwahidi Baba yake. Sasa, mfikirie mtu ambaye alijitahidi kabisa kumwiga Yesu.

PAULO​—MWANAMUME ALIYEFANYA MAMBO ALIYOSEMA

5. Mtume Paulo alituwekea mfano gani mzuri?

5 “Nitafanya nini, Bwana?” (Mdo. 22:10) Kwa maneno hayo ya unyoofu, Paulo, aliyeitwa Sauli wakati huo, alikubali mwelekezo wa Bwana Yesu aliyetukuzwa, ambaye alimtokea katika maono na kumzuia asiendelee kuwatesa wanafunzi wa Kristo. Kwa sababu ya tukio hilo, Sauli alitubu kwa unyenyekevu mwenendo wake wa zamani, akabatizwa, na kukubali mgawo wa pekee aliopewa wa kuwatolea mataifa ushahidi kumhusu Yesu. Kuanzia wakati huo na kuendelea, Paulo aliendelea kumwita Yesu “Bwana” wake, huku akiishi kupatana na maneno hayo hadi alipofikia mwisho wa maisha yake hapa duniani. (Mdo. 22:6-16; 2 Kor. 4:5; 2 Tim. 4:8) Paulo hakuwa kama wengine ambao Yesu alisema hivi kuwahusu: “Kwa nini, basi, mnaniita ‘Bwana! Bwana!’ lakini hamfanyi mambo ninayosema?” (Luka 6:46) Naam, Yesu anatarajia wote wanaomkubali kuwa Bwana wao wafanye mambo wanayosema, kama mtume Paulo alivyofanya.

6, 7. (a) Kwa nini Paulo alibadili mpango wake wa kutembelea tena Korintho, na kwa nini watu waliomchambua-chambua hawakuwa na sababu nzuri ya kusema kwamba hategemeki? (b) Tunapaswa kuwaonaje wale ambao wamewekwa rasmi ili kuongoza miongoni mwetu?

6 Paulo alieneza kwa bidii ujumbe wa Ufalme kotekote katika Asia Ndogo na Ulaya, akianzisha makutaniko mengi na kuyatembelea tena. Pindi fulani, aliona uhitaji wa kuapa kwamba maneno aliyoandika yalikuwa ya kweli. (Gal. 1:20) Watu fulani huko Korintho walipodai kwamba Paulo hategemeki, aliandika hivi ili kujitetea: “Mungu anaweza kutegemewa ili neno letu kwenu lisiwe ni Ndiyo na pia Siyo.” (2 Kor. 1:18) Alipoandika maneno hayo, Paulo alikuwa ameondoka Efeso na alipitia Makedonia akielekea Korintho. Mwanzoni, alikuwa amepanga kurudi Korintho kabla ya kwenda Makedonia. (2 Kor. 1:15, 16) Lakini, kama tu ilivyo na waangalizi wanaosafiri leo, nyakati nyingine inabidi ratiba ibadilike. Mabadiliko kama hayo hayafanywi kwa sababu za kichoyo au mambo madogo-madogo, bali kwa sababu ya hali za dharura. Katika kisa cha Paulo, alikawia kuzuru kutaniko la Korintho kama alivyopanga kwa faida ya kutaniko hilo. Jinsi gani?

7 Muda fulani baada ya kupanga ziara yake, Paulo alipata habari zenye kushtua kwamba migawanyiko na upotovu wa maadili uliachiliwa katika kutaniko la Korintho. (1 Kor. 1:11; 5:1) Ili kurekebisha hali hiyo, aliandika shauri kali katika barua yake ya kwanza kwa Wakorintho. Kisha, badala ya kusafiri kwa meli moja kwa moja kutoka Efeso hadi Korintho, Paulo aliamua kuwapa ndugu zake muda ili wafuate shauri lake hivi kwamba wakati ambapo angewatembelea, ziara yake ingekuwa ya kuwatia moyo zaidi. Akiwasadikishia kwamba alikuwa na sababu nzuri za kubadili mipango ya kuwatembelea, Paulo aliandika hivi katika barua yake ya pili: “Namwita Mungu awe shahidi juu ya nafsi yangu mwenyewe ya kuwa ni kwa kuwahurumia ninyi kwamba bado sijaja Korintho.” (2 Kor. 1:23) Tusiwe kamwe kama watu waliomchambua-chambua Paulo; badala yake, acheni tuwaheshimu sana wale ambao wamewekwa rasmi ili kuongoza miongoni mwetu. Ukweli ni kwamba tunafanya vyema kumwiga Paulo, kama alivyomwiga Kristo.​—1 Kor. 11:1; Ebr. 13:7.

MIFANO MINGINE BORA

8. Rebeka alituwekea mfano gani mzuri?

8 “Mimi niko tayari kwenda.” (Mwa. 24:58) Kwa maneno hayo rahisi, Rebeka alimwambia mama yake na ndugu yake kwamba yuko tayari kuondoka nyumbani siku hiyohiyo na kusafiri umbali wa kilomita zaidi ya 800 pamoja na mtu asiyemfahamu ili awe mke wa Isaka, mwana wa Abrahamu. (Mwa. 24:50-58) Ndiyo ya Rebeka ilimaanisha Ndiyo, naye alithibitika kuwa mke mwaminifu kwa Isaka, mke ambaye alimhofu Mungu. Muda wote wa maisha yake, aliishi katika mahema akiwa mkaaji mgeni katika Nchi ya Ahadi. Alithawabishwa kwa sababu ya ushikamanifu wake kwa kuwa nyanya ya ule Uzao ulioahidiwa, Yesu Kristo.​—Ebr. 11:9, 13.

9. Ruthu alitimiza ahadi yake jinsi gani?

9 “Hapana, bali tutarudi pamoja nawe kwa watu wako.” (Rut. 1:10) Wale wajane Wamoabu, Ruthu na Orpa walimwambia tena na tena maneno hayo Naomi, mama-mkwe wao aliyekuwa mjane, alipokuwa akirudi Bethlehemu kutoka Moabu. Hatimaye, Orpa alirudi katika nchi yao baada ya Naomi kumsihi sana. Lakini Siyo ya Ruthu ilimaanisha Siyo. (Soma Ruthu 1:16, 17.) Alishikamana na Naomi, akaiacha kabisa familia yake na dini ya uwongo ya Moabu. Alivumilia akiwa mwabudu mwaminifu wa Yehova na alithawabishwa kwa kuwa miongoni mwa wanawake watano pekee waliotajwa na Mathayo katika nasaba ya Kristo.​—Mt. 1:1, 3, 5, 6, 16.

10. Kwa nini Isaya alikuwa mfano mzuri kwetu?

10 “Mimi hapa! Nitume mimi.” (Isa. 6:8) Kabla hajasema maneno hayo, Isaya alimwona Yehova katika maono yenye utukufu akiwa ameketi kwenye kiti Chake cha ufalme juu ya hekalu la Israeli. Alipokuwa akiona maono hayo yenye utukufu, Isaya alimsikia Yehova akisema: “Nitamtuma nani, na ni nani atakayeenda kwa ajili yetu?” Huo ulikuwa mwaliko wa kuwa msemaji wa Yehova ili apeleke ujumbe wa Mungu kwa watu Wake wasiotii. Isaya alitimiza ahadi yake—Ndiyo yake ilimaanisha Ndiyo. Kwa miaka zaidi ya 46, alitumikia kwa uaminifu akiwa nabii, akitangaza ujumbe mkali wa hukumu na vilevile ahadi nzuri ajabu kuhusu kurudishwa upya kwa ibada ya kweli.

11. (a) Kwa nini ni muhimu sana tutimize ahadi zetu? (b) Kuna mifano gani yenye kuonya ya watu ambao hawakusema ukweli?

11 Kwa nini Yehova alihakikisha kwamba mifano hiyo inaandikwa katika Neno lake kwa ajili yetu? Kuacha Ndiyo yetu iwe Ndiyo ni jambo zito kadiri gani? Biblia inaonya waziwazi kwamba mtu ambaye ni ‘mwongo kwa mapatano’ yuko kati ya wale ambao “wanastahili kifo.” (Rom. 1:31, 32) Farao wa Misri, Mfalme Sedekia wa Yudea, na Anania na Safira ni miongoni mwa mifano mibaya inayotajwa waziwazi katika Biblia ya watu ambao Ndiyo yao haikumaanisha Ndiyo. Wote hao waliangamia na ni mifano yenye kutuonya.​—Kut. 9:27, 28, 34, 35; Eze. 17:13-15, 19, 20; Mdo. 5:1-10.

12. Ni nini kitakachotusaidia kutimiza ahadi zetu?

12 Kwa kuwa tunaishi “katika siku za mwisho,” tunazungukwa na watu “wasio washikamanifu,” ambao ‘wana namna ya ujitoaji-kimungu lakini wanazikana nguvu zake.’ (2 Tim. 3:1-5) Kwa kadiri inavyowezekana, ni lazima tuepuke mashirika mabaya kama hayo. Badala yake, tunapaswa kukusanyika kwa ukawaida na wale ambao wanajitahidi nyakati zote kuhakikisha kwamba Ndiyo yao inamaanisha Ndiyo.​—Ebr. 10:24, 25.

NDIYO MUHIMU ZAIDI MAISHANI MWAKO

13. Ni Ndiyo gani iliyo muhimu zaidi inayosemwa na mfuasi wa Yesu Kristo?

13 Ahadi muhimu zaidi ambayo mtu anaweza kutoa ni ile inayohusu wakfu wake kwa Mungu. Katika pindi tatu hususa, wale wanaotaka kujikana wenyewe ili wawe wanafunzi wa Yesu wanapata fursa ya kujibu Ndiyo wanapoulizwa kuhusu nia yao. (Mt. 16:24) Wazee wawili wanapozungumza na mtu anayetaka kuwa mhubiri ambaye hajabatizwa, mtu huyo huulizwa hivi: “Je, kwa kweli unataka kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova?” Baadaye, mtu huyo anapofanya maendeleo zaidi ya kiroho na kutaka kubatizwa, wazee wanakutana naye na kumuuliza, “Je, umejiweka wakfu kwa Yehova katika sala?” Hatimaye, siku ya kubatizwa, kila anayestahili kubatizwa huulizwa hivi: “Kwa msingi wa dhabihu ya Yesu Kristo, je, umetubu dhambi zako na kujiweka wakfu kwa Yehova ili kufanya mapenzi yake?” Hivyo basi, mbele ya mashahidi, wapya hao wanasema Ndiyo wanapotoa ahadi ya kumtumikia Mungu milele.

14. Mara kwa mara, tunapaswa kujichunguza jinsi gani?

14 Iwe umebatizwa karibuni au umekuwa ukimtumikia Mungu kwa makumi ya miaka, unahitaji kujichunguza mara kwa mara na kujiuliza maswali kama haya: ‘Kwa kumwiga Yesu Kristo, je, ninaendelea kuishi kupatana na Ndiyo yangu iliyo muhimu zaidi? Je, ninaendelea kumtii Yesu kwa kuifanya kazi ya kuhubiri na kufanya wanafunzi kuwa jambo muhimu zaidi maishani mwangu?’​—Soma 2 Wakorintho 13:5.

15. Ni muhimu kuacha Ndiyo yetu imaanishe Ndiyo katika mambo gani maishani?

15 Kutimiza nadhiri yetu ya kujiweka wakfu kunamaanisha kwamba ni lazima pia tuwe waaminifu katika mambo mengine muhimu. Kwa mfano: Je, umefunga ndoa? Basi, endelea kutimiza nadhiri muhimu uliyoweka ya kumpenda na kumthamini mwenzi wako wa ndoa. Je, umetia sahihi mkataba wa kibiashara au kujaza fomu ya ombi la mapendeleo fulani ya kitheokrasi? Basi, timiza wajibu wako kwa kufanya ulichoahidi. Je, umekubali mwaliko wa kushiriki mlo na mtu asiye na uwezo mkubwa wa kifedha? Basi, usikatae mwaliko huo kwa sababu tu umepata mwaliko mwingine kutoka kwa mtu mwenye uwezo zaidi. Au je, umeahidi kumrudia mtu fulani uliyekutana naye katika huduma ya nyumba kwa nyumba ili umpe msaada zaidi wa kiroho? Basi, kwa vyovyote vile, acha Ndiyo yako imaanishe Ndiyo, na Yehova ataibariki huduma yako.​—Soma Luka 16:10.

KUNUFAISHWA NA KUHANI WETU MKUU NA MFALME

16. Tufanye nini ikiwa hatujatimiza ahadi yetu?

16 Biblia inasema kwamba tukiwa wanadamu wasio wakamilifu, “sisi sote hujikwaa mara nyingi,” hasa tunapotumia ulimi wetu. (Yak. 3:2) Tunapaswa kufanya nini tukitambua kwamba hatukutimiza ahadi yetu? Katika Sheria ambayo Mungu aliwapa Waisraeli, kulikuwa na uandalizi wa kumwonyesha rehema mtu aliyekuwa na hatia ya “kusema kwa midomo yake bila kufikiri.” (Law. 5:4-7, 11) Vivyo hivyo, kuna uandalizi wa upendo kwa Wakristo wanaofanya dhambi ya aina hiyo. Tukiungama dhambi hiyo hususa kwa Yehova, atatusamehe kwa rehema kupitia ofisi ya Kuhani wetu Mkuu, Yesu Kristo. (1 Yoh. 2:1, 2) Hata hivyo, ili tuendelee kupata kibali cha Mungu, ni lazima tudhihirishe matunda yanayoonyesha toba kwa kutozoea kutenda dhambi za namna hiyo na kujitahidi kabisa kusuluhisha matatizo yoyote tuliyosababisha kwa kusema bila kufikiri. (Met. 6:2, 3) Bila shaka, ni afadhali zaidi kufikiria kwa makini ili tusitoe ahadi ambazo hatuwezi kutimiza.​—Soma Mhubiri 5:2.

17, 18. Ni wakati gani mzuri ajabu unaowangojea wale wote wanaojitahidi sana kuacha Ndiyo yao imaanishe Ndiyo?

17 Wakati mzuri ajabu unawangojea waabudu wote wa Yehova wanaoendelea kujitahidi sana kuiacha Ndiyo yao imaanishe Ndiyo! Wale watiwa-mafuta 144,000 watapata uhai usioweza kufa mbinguni, ambako watashiriki na Yesu ‘kutawala wakiwa wafalme pamoja naye ile miaka elfu’ katika Ufalme wake. (Ufu. 20:6) Na mamilioni ya wanadamu wengine, watanufaishwa na utawala wa Ufalme wa Kristo katika paradiso duniani. Wakiwa humo, watasaidiwa kuwa wakamilifu kimwili na kiakili.​—Ufu. 21:3-5.

18 Tukithibitika kuwa waaminifu katika mtihani wa mwisho ambao utatukia mwishoni mwa Utawala wa Miaka Elfu Moja wa Yesu, hatutakuwa tena kamwe na sababu ya kutilia shaka ahadi ya mtu yeyote. (Ufu. 20:7-10) Kila Ndiyo itamaanisha Ndiyo, na kila Siyo, itamaanisha Siyo. Kila mtu atakayeishi wakati huo atakuwa akimwiga kikamili Baba yetu wa mbinguni mwenye upendo, Yehova, yule “Mungu wa ukweli.”​—Zab. 31:5.