Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Unifundishe Kufanya Mapenzi Yako”

“Unifundishe Kufanya Mapenzi Yako”

“Unifundishe kufanya mapenzi yako, kwa maana wewe ni Mungu wangu.”​—ZAB. 143:10.

1, 2. Tutanufaikaje tukitilia maanani mapenzi ya Mungu, na tutajifunza nini kutokana na Mfalme Daudi kuhusu jambo hilo?

TUSEME unatembea kwenye eneo lenye milima-milima. Unafika mahali penye njia mbili. Utafuata njia ipi? Huenda ukapanda mahali palipoinuka ili uone kila njia inaelekea upande gani, kisha unaweza kuchagua njia bora zaidi ya kufuata. Kutumia kanuni hiyohiyo kunaweza kutusaidia tunapofanya maamuzi muhimu. Kuona mambo kulingana na maoni ya Muumba yaliyo juu kutatuwezesha ‘kutembea katika njia’ ambayo Yehova anakubali.​—Isa. 30:21.

2 Mara nyingi katika maisha yake, Mfalme Daudi wa taifa la kale la Israeli aliweka mfano bora wa kutilia maanani mapenzi ya Mungu. Acheni tuchunguze matukio fulani katika maisha ya Daudi ili tujifunze kutokana na mwenendo wa mwanamume huyo aliyekuwa na moyo mkamilifu mbele za Yehova Mungu.​—1 Fal. 11:4.

DAUDI ALILIHESHIMU SANA JINA LA YEHOVA

3, 4. (a) Ni nini kilichomchochea Daudi kupambana na Goliathi? (b) Daudi alilionaje jina la Mungu?

3 Fikiria wakati ambapo Daudi alikabiliana na bingwa Mfilisti aliyeitwa Goliathi. Ni nini kilichomchochea kijana Daudi kupambana na jitu hilo lenye urefu wa mita 2.9, lililokuwa limejihami kikamili? (1 Sam. 17:4) Je, ni ujasiri wa Daudi? Je, ni imani yake katika Mungu? Sifa hizo mbili zilimsaidia sana kutenda kwa ushujaa. Hata hivyo, kilichomchochea Daudi hasa kupambana na jitu hilo refu ni heshima yake kuelekea Yehova na jina Lake kuu. Kwa hasira, Daudi aliuliza hivi: “Huyu Mfilisti asiyetahiriwa ni nani hata avitukane vikosi vya Mungu aliye hai?”​—1 Sam. 17:26.

4 Alipokuwa akimkabili Goliathi, kijana Daudi alitangaza hivi: “Unakuja kwangu ukiwa na upanga na mkuki na fumo, lakini mimi naja kwako nikiwa na jina la Yehova wa majeshi, Mungu wa vikosi vya Israeli, ambaye umemtukana.” (1 Sam. 17:45) Akimtegemea Mungu wa kweli, Daudi alimwangusha chini bingwa huyo wa Wafilisti kwa jiwe moja tu alilorusha kwa kombeo. Daudi alimtegemea Yehova na kuliheshimu sana jina Lake si katika pindi hiyo tu bali pia katika maisha yake yote. Kwa kweli, Daudi aliwahimiza Waisraeli wenzake ‘wajisifu katika jina takatifu la Yehova.’​—Soma 1 Mambo ya Nyakati 16:8-10.

5. Unaweza kukabili hali gani inayoweza kufananishwa na dhihaka za Goliathi?

5 Je, unajivunia uhakika wa kwamba Yehova ni Mungu wako? (Yer. 9:24) Unatendaje wakati ambapo majirani, wafanyakazi wenzako, wanafunzi wenzako, au watu wako wa ukoo wanaposema mabaya kumhusu Yehova na kuwadhihaki Mashahidi wake? Je, unalitetea jina la Yehova linapotukanwa, huku ukitumaini kwamba atakusaidia? Ni kweli kwamba kuna “wakati wa kukaa kimya,” hata hivyo, hatupaswi kuonea aibu kuwa Mashahidi wa Yehova na wafuasi wa Yesu. (Mhu. 3:1, 7; Marko 8:38) Ingawa tunapaswa kuwa wenye busara na adabu tunaposhughulika na watu wenye mwelekeo usiofaa, acheni tusiwe kama wale Waisraeli ‘walioingiwa na hofu na kuogopa sana’ waliposikia maneno ya dhihaka ya Goliathi. (1 Sam. 17:11) Badala yake, acheni tuchukue hatua mara moja ili tulitakase jina la Yehova Mungu. Tamaa yetu ni kuwasaidia watu wamjue Yehova Mungu kikweli. Hivyo, tunatumia Neno lake lililoandikwa tunapojitahidi kuwasaidia wengine kuona umuhimu wa kumkaribia Mungu.​—Yak. 4:8.

6. Daudi alitaka kutimiza nini kwa kupambana na Goliathi, na hangaiko letu kuu linapaswa kuwa nini?

6 Pambano la Daudi na Goliathi linatufundisha somo lingine muhimu. Daudi alipokuja mbio katika uwanja wa mapigano, aliuliza hivi: “Atafanyiwa nini mtu atakayempiga yule Mfilisti pale na kuondolea mbali shutuma kutoka juu ya Israeli?” Watu wakamjibu kwa kurudia maneno waliyokuwa wamesema mwanzoni: “Mtu yule atakayempiga [Goliathi], mfalme atamtajirisha kwa utajiri mwingi sana, naye atampa binti yake.” (1 Sam. 17:25-27) Hangaiko kuu la Daudi halikuwa kupata ufanisi wa kimwili. Alikuwa na lengo lingine kubwa zaidi. Daudi alitaka kumtukuza Mungu wa kweli. (Soma 1 Samweli 17:46, 47.) Namna gani sisi? Je, hangaiko letu kuu ni kujifanyia jina letu wenyewe kwa kujikusanyia utajiri na kuwa maarufu katika ulimwengu? Bila shaka tunataka kuwa kama Daudi aliyeimba hivi: “Mtukuzeni Yehova pamoja nami, na tulikweze jina lake pamoja.” (Zab. 34:3) Basi, na tumtegemee Mungu, tukitanguliza jina lake badala ya jina letu.​—Mt. 6:9.

7. Tunawezaje kusitawisha imani yenye nguvu inayohitajika tunapokutana na watu wenye mwelekeo usiofaa?

7 Ili akabiliane kwa ujasiri na Goliathi, Daudi alihitaji kumtegemea kabisa Yehova. Kijana Daudi alikuwa na imani yenye nguvu. Njia moja aliyotumia kujenga imani yake ni kumtegemea Mungu alipokuwa akifanya kazi ya uchungaji. (1 Sam. 17:34-37) Sisi pia tunahitaji imani yenye nguvu ili tuendelee kuitimiza huduma, hasa tunapokutana na watu wenye mwelekeo usiofaa. Tunaweza kusitawisha imani ya aina hiyo kwa kumtegemea Mungu katika shughuli zetu za kila siku. Kwa mfano, tunapotumia usafiri wa umma, tunaweza kuanzisha mazungumzo na abiria wenzetu kuhusu kweli za Biblia. Na kwa nini tusitesite kuzungumza na watu tunaokutana nao barabarani tunapohubiri nyumba kwa nyumba?​—Mdo. 20:20, 21.

DAUDI ALIMNGOJEA YEHOVA

8, 9. Daudi alionyeshaje kwamba alitilia maanani mapenzi ya Yehova aliposhughulika na Mfalme Sauli?

8 Mfano mwingine unaoonyesha utayari wa Daudi wa kumtegemea Yehova ni maoni yake kumhusu Sauli, mfalme wa kwanza wa Israeli. Sauli mwenye wivu alijaribu kumpigilia Daudi ukutani mara tatu kwa kutumia mkuki, lakini kila mara Daudi alikwepa naye alikataa kulipiza kisasi. Hatimaye, alimkimbia Sauli. (1 Sam. 18:7-11; 19:10) Kisha, Sauli akachukua wanaume 3,000 waliochaguliwa kutoka katika Israeli yote na kwenda kumtafuta Daudi nyikani. (1 Sam. 24:2) Mwishowe, bila kujua, Sauli akaingia ndani ya pango lilelile ambamo Daudi na watu wake walikuwa. Daudi angeweza kutumia nafasi hiyo kumwangamiza mfalme huyo aliyetaka kumuua. Isitoshe, yalikuwa mapenzi ya Mungu kwamba Daudi awe mfalme wa Israeli badala ya Sauli. (1 Sam. 16:1, 13) Kwa kweli, ikiwa Daudi angesikiliza ushauri wa watu wake, mfalme angeuawa. Lakini Daudi alisema hivi: “Ni jambo lisilowaziwa kwangu, kwa maoni ya Yehova, kwamba nimfanyie bwana wangu jambo hili, mtiwa-mafuta wa Yehova.” (Soma 1 Samweli 24:4-7.) Bado Sauli alikuwa mfalme mtiwa-mafuta wa Mungu. Daudi hakutaka kumnyang’anya Sauli ufalme kwa sababu Yehova alikuwa bado hajamwondoa. Kwa kukata tu upinde wa koti lisilo na mikono la Sauli, Daudi alionyesha kwamba hakuwa na nia ya kumdhuru Sauli.​—1 Sam. 24:11.

9 Daudi alionyesha tena heshima kwa mtiwa-mafuta wa Mungu alipomwona mfalme huyo kwa mara ya mwisho. Wakati huo, Daudi na Abishai walifika mahali ambapo Sauli alikuwa amepiga kambi na kumkuta akiwa amelala. Ijapokuwa Abishai alikata kauli kwamba Mungu alikuwa amewaweka adui za Daudi mikononi mwake, na hivyo akajitolea kumpigilia chini Sauli kwa mkuki, Daudi hakumruhusu afanye hivyo. (1 Sam. 26:8-11) Kwa kuwa Daudi aliendelea kutafuta mwongozo wa Mungu, hakuyumbayumba katika azimio lake la kutenda kupatana na mapenzi ya Yehova licha ya ushauri aliopewa na Abishai.

10. Sisi binafsi tunaweza kukabili hali gani ngumu, na ni nini kitakachotusaidia kusimama imara?

10 Sisi pia tunaweza kukabili hali ngumu marafiki wetu wanapojaribu kutushinikiza tufuate maoni yao ya kibinadamu badala ya kutuunga mkono katika kufanya mapenzi ya Yehova. Kama Abishai, huenda hata baadhi yao wakatutia moyo tufanye jambo fulani bila kufikiria mapenzi ya Mungu. Ili tusimame imara, tunahitaji kujua vizuri maoni ya Yehova kuhusu jambo hilo na kuazimia kushikamana na njia zake.

11. Umejifunza nini kutokana na Daudi kuhusu kutilia maanani kwanza mapenzi ya Mungu?

11 Daudi alisali hivi kwa Yehova Mungu: “Unifundishe kufanya mapenzi yako.” (Soma Zaburi 143:5, 8, 10.) Badala ya kutegemea mawazo yake mwenyewe au kukubali tu ushauri wa mtu mwingine, Daudi alitaka sana kufundishwa na Mungu. ‘Alitafakari juu ya utendaji wote wa Yehova na kwa kupenda aliendelea kuhangaikia kazi ya mikono ya Mungu mwenyewe.’ Sisi pia tunaweza kutambua mapenzi ya Mungu kwa kuchunguza Maandiko kwa makini na kutafakari kuhusu masimulizi mengi ya Biblia yanayoonyesha jinsi Yehova alivyoshughulika na wanadamu.

DAUDI ALITHAMINI KANUNI ZILIZOTEGEMEZA SHERIA

12, 13. Kwa nini Daudi aliyamwaga chini maji yaliyoletwa na wanaume wake watatu?

12 Tunapaswa pia kumwiga Daudi katika kuthamini kanuni zinazotegemeza Sheria na kuiga tamaa yake ya kuishi kupatana na kanuni hizo. Fikiria jambo lililotukia Daudi alipotamani sana “maji kutoka katika tangi la Bethlehemu.” Wanaume watatu wa Daudi waliingia kwa nguvu katika jiji lililokaliwa na Wafilisti na kuleta maji hayo. Hata hivyo, ‘Daudi hakukubali kuyanywa, bali aliyamwaga mbele za Yehova.’ Kwa nini? Daudi alisema hivi: “Ni jambo lisiloweza kuwaziwa kwangu, kwa habari ya Mungu wangu, nifanye hivi! Je, ninywe damu ya watu hawa kwa kuhatarisha nafsi zao? Kwa maana waliyaleta kwa kuhatarisha nafsi zao.”​—1 Nya. 11:15-19.

13 Daudi alijua kulingana na Sheria kwamba damu ilipaswa kumwagwa mbele za Yehova wala si kuliwa. Alielewa pia kwa nini jambo hilo lilipasa kufanywa. Daudi alijua kwamba “nafsi ya mwili iko katika damu.” Hata hivyo, hayo yalikuwa maji, si damu. Kwa nini Daudi alikataa kuyanywa? Alithamini kanuni iliyotegemeza takwa hilo la kisheria. Kwa maoni ya Daudi, maji hayo yalikuwa yenye thamani sawa na damu ya wanaume hao watatu. Kwa hiyo, lilikuwa jambo lisilowaziwa kwake kunywa maji hayo. Badala ya kuyanywa, aliamua kuyamwaga chini.​—Law. 17:11; Kum. 12:23, 24.

14. Ni nini kilichomsaidia Daudi kuona mambo kama Yehova anavyoyaona?

14 Daudi alijitahidi kuielewa kwa undani zaidi sheria ya Mungu. Aliimba hivi: “Ee Mungu wangu, nimependezwa na kufanya mapenzi yako, na sheria yako imo ndani yangu.” (Zab. 40:8) Daudi alijifunza sheria ya Mungu na kutafakari kwa uzito kuihusu. Alitegemea hekima ya amri za Yehova. Matokeo ni kwamba Daudi akawa na hamu ya kufuata, si amri zilizoandikwa tu bali pia kanuni za Sheria ya Musa. Tunapojifunza Biblia, ni jambo la hekima kutafakari mambo tunayosoma na kuyaweka katika moyo wetu ili tuweze kujua kinachompendeza Yehova katika hali fulani hususa.

15. Sulemani hakuiheshimu Sheria ya Mungu kwa njia ipi?

15 Sulemani mwana wa Daudi, alipendwa sana na Yehova Mungu. Hata hivyo, baada ya muda Sulemani hakuheshimu Sheria ya Mungu. Hakutii amri ya Yehova ya kwamba mfalme wa Israeli “asizidishe wake kwa ajili yake.” (Kum. 17:17) Kwa kweli, Sulemani alioa wanawake wengi wageni. Alipozeeka, “wake zake wakawa wameugeuza moyo wake ukaifuata miungu mingine.” Hata awe alitoa visingizio gani, “Sulemani akaanza kufanya yaliyokuwa mabaya machoni pa Yehova, naye hakumfuata Yehova kikamilifu kama Daudi baba yake.” (1 Fal. 11:1-6) Ni muhimu kama nini kwamba tuishi kupatana na sheria na kanuni zilizo katika Neno la Mungu! Kwa mfano, ni muhimu sana kufanya hivyo tunapofikiria kufunga ndoa.

16. Kutambua kanuni ya amri ya kufunga ndoa “katika Bwana tu” kutawasaidiaje wale wanaotumaini kufunga ndoa?

16 Tunaposhawishiwa kimapenzi na watu wasio waamini, je, itikio letu linaonyesha maoni kama ya Daudi au kama ya Sulemani? Waabudu wa kweli wanaambiwa wafunge ndoa “katika Bwana tu.” (1 Kor. 7:39) Ikiwa Mkristo anaamua kufunga ndoa, anapaswa kufunga ndoa na mwamini mwenzake. Tukitambua kanuni ya takwa hilo la Kimaandiko, hatutaepuka tu kufunga ndoa na mtu asiye mwamini, bali pia hatutakubali ushawishi wowote wa kimapenzi kutoka kwa mtu huyo.

17. Ni nini kinachoweza kutusaidia kuepuka mtego wa ponografia?

17 Fikiria pia jinsi mfano wa Daudi wa kutafuta kwa bidii mwongozo wa Mungu unavyoweza kutusaidia kupinga kishawishi cha kutazama ponografia. Soma maandiko yafuatayo, fikiria kanuni zilizomo, na ujitahidi kujua mapenzi ya Yehova kuhusu jambo hilo. (Soma Zaburi 119:37; Mathayo 5:28, 29; Wakolosai 3:5.) Kutafakari kuhusu viwango vyake vya juu hutuwezesha kujiepusha na mtego wa ponografia.

FIKIRIA MAONI YA MUNGU NYAKATI ZOTE

18, 19. (a) Ni nini kilichomsaidia Daudi ampendeze Mungu licha ya kutokuwa mkamilifu? (b) Umeazimia kufanya nini?

18 Ingawa Daudi alikuwa mfano mzuri katika njia nyingi, alifanya dhambi kadhaa nzito. (2 Sam. 11:2-4, 14, 15, 22-27; 1 Nya. 21:1, 7) Hata hivyo, Daudi alitubu alipofanya dhambi. Alitembea mbele za Mungu “kwa utimilifu wa moyo.” (1 Fal. 9:4) Kwa nini tuseme hivyo? Kwa sababu Daudi alijitahidi kutenda kulingana na mapenzi ya Yehova.

19 Licha ya kutokamilika kwetu, tunaweza kuendelea kumpendeza Yehova. Tukiwa na lengo hilo akilini, acheni tujifunze Neno la Mungu kwa bidii, tutafakari kwa makini yale tunayojifunza kutokana nalo, na tutende haraka kulingana na yale tunayoweka moyoni. Tukifanya hivyo, ni kana kwamba tutakuwa tukisali kwa Yehova kama mtunga-zaburi aliyeomba hivi kwa unyenyekevu: “Unifundishe kufanya mapenzi yako.”