Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jihadhari Usiitumie Biblia Kishirikina

Jihadhari Usiitumie Biblia Kishirikina

“NENO la Mungu liko hai nalo lina nguvu.” (Ebr. 4:12) Kwa maneno hayo, mtume Paulo alikazia jinsi ambavyo neno la Mungu lina nguvu za kugusa mioyo na kubadili maisha ya watu.

Hata hivyo, maoni hayo kuhusu nguvu za ujumbe wa Biblia yalivurugwa wakati uasi-imani uliotabiriwa ulipotia mizizi baada ya mitume kufa. (2 Pet. 2:1-3) Baada ya muda, viongozi wa makanisa walianza kudai kwamba Neno la Mungu lina nguvu za kichawi. Profesa Harry Y. Gamble aliandika kuhusu “kutumia maandiko ya Kikristo kwa njia ya kichawi.” Alisema kwamba katika karne ya tatu, Origen, Baba wa Kanisa, alidai kwamba “kusikia tu maneno matakatifu kuna manufaa fulani: ikiwa maneno yana nguvu katika mizungu ya kipagani, basi maneno ya maandiko yaliyotoka kwa Mungu yana nguvu nyingi hata zaidi.” John Chrysostom aliyeishi mwishoni mwa karne ya nne aliandika kwamba “ibilisi hawezi kudhubutu kuikaribia nyumba yenye vitabu vya Injili.” Alisema pia kwamba watu fulani walining’iniza sehemu za maandiko ya Injili shingoni mwao kama hirizi yenye nguvu. Profesa Gamble aliendelea kusema kwamba Agostino, aliyekuwa mwanatheolojia Mkatoliki “aliona si makosa kuweka nakala ya Injili ya Yohana chini ya mto unaolalia ikiwa unaumwa na kichwa”! Kwa hiyo, maandiko ya Biblia yalitumiwa katika mambo ya uchawi. Je, unaiona Biblia kuwa hirizi ya bahati njema, inayoweza kukulinda ili usipatwe na maovu?

Labda njia moja ambayo watu wamezoea kuitumia Biblia isivyofaa ni ile inayoitwa katika lugha ya Kiingereza, bibliomancy. Neno hilo linamaanisha nini? Linamaanisha kufungua kitabu fulani bila kufikiri, hasa Biblia, na kusoma andiko ambalo mtu analiona kwanza, akiamini kwamba maneno hayo yatampa mwongozo anaohitaji. Kwa mfano, kulingana na Profesa Gamble, wakati mmoja Agostino alipomsikia mtoto kutoka katika nyumba ya jirani akisema: “Chukua usome, chukua usome,” Agostino aliamini kwamba ni Mungu aliyekuwa akimwagiza afungue Biblia na kusoma andiko atakaloona kwanza.

Je, umewahi kusikia kuhusu watu ambao walipokabili hali ngumu, walisali kwa Mungu, kisha wakafungua ukurasa wowote wa Biblia bila kufikiri, wakiamini kwamba mstari wa kwanza waliouona ungewasaidia kukabiliana na tatizo lao? Ingawa huenda watu hao walikuwa na nia nzuri, Wakristo hawapaswi kutafuta mwongozo kutoka katika Maandiko kwa njia hiyo.

Yesu aliwahakikishia wanafunzi wake kwamba angewatumia “msaidizi, roho takatifu.” Aliendelea kuwaambia hivi: “Hiyo itawafundisha ninyi mambo yote na kuwakumbusha mambo yote niliyowaambia.” (Yoh. 14:26) Kinyume na hilo, zoea la kufungua Biblia bila kufikiri halihitaji mtu awe na ujuzi wowote wa Maandiko.

Zoea hilo na mazoea mengine ya kuitumia Biblia kwa njia ya kishirikina yameenea sana. Hata hivyo, Neno la Mungu linashutumu mazoea ya kutafuta ishara za bahati. (Law. 19:26; Kum. 18:9-12; Mdo. 19:19) “Neno la Mungu liko hai nalo lina nguvu,” hata hivyo ni lazima tuwe na ustadi wa kulitumia. Ujuzi sahihi wa Biblia ndio unaoboresha maisha ya watu wala si matumizi ya kishirikina ya kitabu hicho. Kupata ujuzi huo kumewasaidia watu wengi kuwa na maadili mazuri, kuacha maisha yanayoweza kuwadhuru, kuimarisha maisha ya familia, na kujenga uhusiano mzuri pamoja na Mtungaji wa Biblia.