Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jinsi Unavyoweza Kupata Mafanikio ya Kweli Maishani

Jinsi Unavyoweza Kupata Mafanikio ya Kweli Maishani

‘Utaifanikisha njia yako na kutenda kwa hekima.’—YOS. 1:8.

1, 2. (a) Watu wengi wana maoni gani kuhusu kufanikiwa? (b) Unawezaje kutambua maoni yako kuhusu kufanikiwa?

KUFANIKIWA maishani kunamaanisha nini? Ukiwauliza watu swali hilo, utapata majibu tofauti-tofauti. Kwa mfano, wengi wanafikiri kwamba mtu aliyefanikiwa ni yule aliye na pesa nyingi, kazi nzuri, au elimu kubwa. Wengine hufikiri kwamba mafanikio yanahusisha kuwa na uhusiano mzuri pamoja na watu wa familia, marafiki, au wafanyakazi wenzao. Mtu anayemtumikia Mungu huenda hata akafikiri kwamba kufanikiwa ni kupata pendeleo fulani kutanikoni au matokeo mazuri katika utumishi.

2 Ili ujue maoni yako kuhusu mafanikio, unaweza kuandika majina ya watu wachache ambao unaona kwamba wamefanikiwa, hasa wale unaowaheshimu na kuwapenda sana. Wote hao wana sifa gani ya pekee? Je, ni matajiri au ni watu maarufu? Je, wao ni mashuhuri? Majibu yako kwa maswali hayo yanaweza kufunua kilicho moyoni mwako, na jambo hilo linaweza kuwa na uvutano mkubwa sana kuelekea maamuzi unayofanya na miradi unayofuatilia.—Luka 6:45.

3. (a) Yoshua alipaswa kufanya nini ili aifanikishe njia yake? (b) Tutachunguza nini?

3 Jambo muhimu zaidi ni ikiwa Yehova anaona kwamba tumefanikiwa, kwa sababu maisha yetu yanategemea kupata kibali chake. Alipokuwa akimpa Yoshua mgawo mzito wa kuwaongoza Waisraeli kuingia katika Nchi ya Ahadi, Yehova alimwambia asome Sheria ya Musa “usiku na mchana” na awe mwangalifu kutii mambo yaliyoandikwa humo. Mungu alimhakikishia hivi: “Ndipo utakapoifanikisha njia yako, kisha utatenda kwa hekima.” (Yos. 1:7, 8) Bila shaka, unajua kwamba Yoshua alifanikiwa. Namna gani sisi? Tunawezaje kujua ikiwa tuna maoni kama ya Mungu kuhusu mafanikio? Ili upate jibu la swali hilo, fikiria maisha ya wanaume wawili wanaotajwa katika Biblia.

JE, SULEMANI ALIFANIKIWA MAISHANI?

4. Kwa nini tunaweza kusema kwamba Sulemani alifanikiwa?

4 Sulemani alifanikiwa kwa njia ya pekee katika mambo mengi. Kwa nini? Kwa sababu alimwogopa na kumtii Yehova kwa miaka mingi, na Yehova akambariki sana. Kumbuka kwamba Yehova alipomwambia Sulemani aombe chochote anachotaka, mfalme huyo aliomba hekima ya kuwaongoza watu. Ndipo Mungu alipombariki kwa kumpa hekima na utajiri. (Soma 1 Wafalme 3:10-14.) Hekima yake ilikuwa “pana zaidi kuliko hekima ya watu wengine wote wa Mashariki na kuliko hekima yote ya Misri.” Umashuhuri wa Sulemani ulijulikana “katika mataifa yote yanayozunguka pande zote.” (1 Fal. 4:30, 31) Kuhusu utajiri wake, kila mwaka alipata dhahabu yenye uzito wa tani 25 hivi bila kuhesabu mapato mengine. (2 Nya. 9:13) Alikuwa na uwezo mkubwa sana katika kuwapatanisha watu, katika masuala ya ujenzi, na biashara. Naam, Sulemani alifanikiwa sana alipokuwa na uhusiano mzuri pamoja na Mungu.—2 Nya. 9:22-24.

5. Sulemani alifikia mkataa gani kuhusu wale ambao wamefanikiwa kwa maoni ya Mungu?

5 Mambo ambayo Sulemani aliandika katika kitabu cha Mhubiri yanaonyesha kwamba hakupotoshwa afikirie kwamba watu wenye utajiri au walio maarufu peke yao ndio wenye shangwe na waliofanikiwa. Sivyo hata kidogo. Aliandika hivi: “Nimekuja kujua kwamba hakuna jambo lingine bora kwao kuliko mtu kufurahi na kufanya mema maishani mwake; na pia kwamba kila mtu ale, naam, anywe na kuona mema kwa ajili ya kazi yake yote iliyo ngumu. Hiyo ndiyo zawadi ya Mungu.” (Mhu. 3:12, 13) Pia, alitambua kwamba mambo hayo yenye kufurahisha ni yenye thamani kwelikweli kwa mtu mwenye kibali cha Mungu, na aliye na uhusiano mzuri pamoja naye. Kwa kufaa, Sulemani alisema hivi: “Huu ndio mwisho wa mambo, kila jambo limekwisha sikiwa: Mwogope Mungu wa kweli na kushika amri zake. Kwa maana huo ndio wajibu wote wa mwanadamu.”—Mhu. 12:13.

6. Mfano wa Sulemani unatusaidiaje kupima mafanikio ya kweli?

6 Kwa miaka mingi, Sulemani alitembea kwa kumwogopa Mungu. Tunasoma kwamba ‘aliendelea kumpenda Yehova kwa kutembea katika sheria za Daudi baba yake.’ (1 Fal. 3:3) Je, huoni kwamba alifanikiwa kikweli? Akiongozwa na Mungu, Sulemani alijenga hekalu lenye utukufu kwa ajili ya ibada ya kweli na kuandika vitabu vitatu vya Biblia. Ingawa huenda tusifanye mambo hayo aliyofanya Sulemani, mfano alioweka alipokuwa mwaminifu kwa Mungu unaweza kutusaidia kuelewa kufanikiwa kikweli kunamaanisha nini, na tunachohitaji kufanya ili tufanikiwe. Kuhusiana na hilo, kumbuka kwamba roho ya Mungu ilimwongoza Sulemani kuandika kwamba mambo ambayo watu wengi leo huona kuwa kipimo cha mafanikio, yaani, utajiri, hekima, umashuhuri, na mamlaka, yote ni ubatili. Kwa kweli, mambo hayo hayana faida yoyote, ni “kufuatilia upepo.” Je, hujaona kwamba watu wengi wanaopenda utajiri wanatamani kupata mali zaidi? Na mara nyingi wana wasiwasi kuhusu vitu walivyo navyo. Isitoshe, siku moja mali zao zitachukuliwa na watu wengine.—Soma Mhubiri 2:8-11, 17; 5:10-12.

7, 8. Sulemani alikosa uaminifu jinsi gani, na matokeo yalikuwa nini?

7 Pia, unajua kwamba hatimaye Sulemani hakuendelea kuwa mwaminifu na mtiifu. Neno la Mungu linasema: “Ikawa kwamba wakati Sulemani alipokuwa mzee, wake zake wakawa wameugeuza moyo wake ukaifuata miungu mingine; na moyo wake haukuwa mkamilifu kwa Yehova Mungu wake, kama moyo wa Daudi baba yake. . . . Sulemani akaanza kufanya yaliyokuwa mabaya machoni pa Yehova.”—1 Fal. 11:4-6.

8 Akiwa na sababu ya kuudhika, Yehova alimwambia hivi Sulemani: “Kwa sababu . . . hukushika agano langu na sheria zangu nilizokuamuru, hakika nitaurarua ufalme kutoka kwako, nami nitampa mtumishi wako.” (1 Fal. 11:11) Ulikuwa msiba mkubwa kama nini! Ingawa Sulemani alikuwa amefanikiwa katika njia nyingi, baadaye alimhuzunisha Yehova. Sulemani alishindwa kufanya jambo muhimu zaidi maishani, yaani, kubaki mwaminifu kwa Mungu. Kila mmoja wetu anaweza kujiuliza hivi: ‘Je, mimi nimeazimia kuhakikisha kwamba somo ambalo nimejifunza kutokana na maisha ya Sulemani litanisaidia kufanikiwa?’

ALIFANIKIWA KIKWELI MAISHANI

9. Je, Paulo alifanikiwa maishani kulingana na viwango vya ulimwengu? Eleza.

9 Maisha ya mtume Paulo yalikuwa tofauti kabisa na ya Mfalme Sulemani. Mtume Paulo hakuwa na kiti cha kifalme kilichotengenezwa kwa pembe za tembo wala hakuwa na fursa za kula pamoja na wafalme. Badala yake, nyakati nyingine alikumbwa na njaa, kiu, baridi, na kuwa uchi. (2 Kor. 11:24-27) Mara tu alipokubali kwamba Yesu ndiye Masihi, Paulo alikataa cheo chochote cha heshima katika dini ya Kiyahudi. Kwa hiyo, viongozi wa dini ya Kiyahudi walimchukia. Alifungwa gerezani, akapigwa mijeledi, akapigwa kwa fimbo, na mawe. Paulo alikiri kwamba yeye na Wakristo wenzake walitukanwa, wakateswa, na kudharauliwa. Aliandika hivi: “Tumekuwa kama takataka ya ulimwengu, uchafu wa vitu vyote, mpaka sasa.”—1 Kor. 4:11-13.

10. Kwa nini huenda watu walifikiri kwamba Paulo alipoteza fursa za kufanikiwa?

10 Akiwa kijana, alipokuwa akiitwa Sauli, mtume Paulo alikuwa na fursa nyingi za kufanikiwa maishani. Alizaliwa katika familia ambayo huenda ilikuwa maarufu, na alifundishwa na Gamalieli, mwalimu aliyeheshimiwa. Baadaye, mtume Paulo aliandika hivi: “Nilikuwa nikifanya maendeleo makubwa zaidi katika dini ya Kiyahudi kuliko watu wengi wa umri wangu.” (Gal. 1:14) Sauli alizungumza Kiebrania na Kigiriki kwa ufasaha na alikuwa na uraia wa Roma, jambo lililomwezesha kupata mapendeleo na haki za raia wa Roma ambazo wengi walitamani sana. Kama angeamua kufuatilia ufanisi huo wa kilimwengu, inaelekea kwamba angepata umaarufu na kuwa salama kifedha. Badala yake, aliamua kufuatilia maisha ambayo yalionekana kwa wengine, labda hata kwa baadhi ya watu wake wa ukoo, kuwa upuuzi mtupu. Kwa nini?

11. Paulo alithamini sana mambo gani, naye alikuwa na mradi gani, na kwa nini?

11 Paulo alimpenda Yehova na alitamani kupata kibali chake kuliko kupata utajiri na umaarufu miongoni mwa wanadamu. Alipopata ujuzi sahihi wa ile kweli, Paulo aliithamini sana fidia, huduma ya Kikristo, na tumaini la kuishi mbinguni, mambo ambayo watu wengi ulimwenguni wanayapuuza. Paulo alitambua kwamba kuna suala linalohitaji kutatuliwa. Shetani alidai kuwa angeweza kuwageuza wanadamu ili wasimtumikie Mungu. (Ayu. 1:9-11; 2:3-5) Haidhuru Paulo alikabili majaribu gani, aliazimia kuwa mwaminifu kwa Mungu na kudumu katika ibada ya kweli licha ya hali ngumu. Huo ndio mradi ambao watu wa ulimwengu hawaufikirii wanapozungumza kuhusu mafanikio.

12. Kwa nini uliamua kumtumaini Mungu?

12 Je, una azimio kama la Paulo? Ingawa sikuzote si rahisi kuishi maisha ya uaminifu, tunajua kwamba kuishi kwa uaminifu huleta baraka na kibali cha Yehova, na hilo ndilo humfanya mtu afanikiwe kikweli. (Met. 10:22) Tunafaidika sasa, na bila shaka tunaweza kutarajia baraka wakati ujao. (Soma Marko 10:29, 30.) Kwa hiyo, tuna kila sababu ya kuweka tumaini letu, “si katika utajiri usio hakika, bali katika Mungu, ambaye hutupa sisi vitu vyote kwa wingi ili tuvifurahie.” ‘Tunajiwekea wenyewe kwa usalama hazina ya msingi mzuri kwa ajili ya wakati ujao, ili tuushike imara uzima ulio wa kweli.’ (1 Tim. 6:17-19) Naam, tunaweza kuwa na uhakika kabisa kwamba miaka mia moja kutoka sasa, hata miaka elfu au zaidi inayokuja, tutakumbuka azimio letu na kusema hivi: “Kwa hakika nilichagua njia ya maisha yenye mafanikio ya kweli!”

MAHALI ILIPO HAZINA YAKO

13. Yesu alitoa shauri gani kuhusu kujiwekea hazina?

13 Yesu alisema hivi kuhusu hazina: “Acheni kujiwekea hazina duniani, ambako nondo na kutu hula, na ambako wezi huvunja na kuiba. Badala yake, jiwekeeni hazina mbinguni, ambako nondo na kutu havili, na ambako wezi hawavunji na kuiba. Kwa maana mahali ilipo hazina yako, ndipo moyo wako utakapokuwa pia.”—Mt. 6:19-21.

14. Kwa nini si hekima kutafuta hazina za ulimwengu?

14 Hazina ambazo mtu anaweza kujiwekea duniani zinaweza kuwa zaidi ya pesa tu. Kwa njia fulani, zinaweza kutia ndani chochote kati ya vitu ambavyo Sulemani aliandika kuvihusu vinavyoonwa na watu kuwa kipimo cha mafanikio, yaani, sifa, umashuhuri, au mamlaka. Yesu alikazia jambo lilelile ambalo Sulemani alikazia katika kitabu cha Mhubiri—hazina za ulimwengu hazidumu. Kama vile tu ambavyo huenda umejionea katika ulimwengu unaokuzunguka, hazina hizo zote zinaweza kuharibika na kupotea kwa urahisi. Profesa F. Dale Bruner aliandika hivi kuhusu hazina za aina hiyo: “Inajulikana wazi kwamba umashuhuri haudumu. Mtu aliye mashuhuri leo anasahauliwa kesho. Mtu aliye na pesa nyingi mwaka huu huenda akafilisika mwaka ujao. . . . [Yesu] anawapenda wanadamu. Anawasaidia kuepuka kutamauka ambako bila shaka kunasababishwa na utukufu ambao haudumu, unaotoweka upesi. Yesu hataki wanafunzi [wake] watamauke. ‘Kila siku, ulimwengu humgeuzia kisogo mtu fulani ambaye alikuwa maarufu sana.’” Ingawa watu wengi huenda wakakubali maneno hayo, ni wangapi wanaoruhusu maneno hayo ya hakika yabadili njia yao ya maisha? Je, utafanya hivyo?

15. Tunapaswa kujitahidi kutafuta mafanikio ya aina gani?

15 Viongozi fulani wa kidini wamehubiri kwamba ni makosa kujitahidi kufanikiwa na kwamba jitihada zote za kutafuta mafanikio zinapaswa kukomeshwa. Hata hivyo, kumbuka kwamba Yesu hakuwa akishutumu jitihada zote za aina hiyo. Badala yake, alikuwa akiwashauri wanafunzi wake wajitahidi kutafuta mafanikio yanayofaa, akiwahimiza kuweka “hazina [zisizoharibika] mbinguni.” Tamaa yetu kuu inapaswa kuwa kujitahidi kufanikiwa kulingana na maoni ya Yehova. Naam, maneno ya Yesu yanatukumbusha kwamba tuna hiari ya kuchagua mambo tutakayofuatilia. Hata hivyo, ukweli ni kwamba tutafuatilia mambo yaliyo moyoni mwetu, yale tunayothamini.

16. Tunaweza kuwa na uhakika kabisa katika jambo gani?

16 Ikiwa kwa kweli tumeazimia moyoni mwetu kumpendeza Yehova, tunaweza kuwa na hakika kwamba atahakikisha tunapata vitu tunavyohitaji. Huenda akaruhusu tupate njaa au kiu kwa muda, kama ilivyokuwa kwa mtume Paulo. (1 Kor. 4:11) Hata hivyo, tunaweza kuwa na uhakika kabisa katika shauri hili la Yesu lenye hekima: “Msihangaike kamwe na kusema, ‘Tutakula nini?’ au, ‘Tutakunywa nini?’ au, ‘Tutavaa nini?’ Kwa maana vyote hivi ndivyo vitu ambavyo mataifa yanafuatilia kwa tamaa. Kwa maana Baba yenu wa mbinguni anajua mnahitaji vitu hivi vyote. Basi, endeleeni kuutafuta kwanza ufalme na uadilifu wake, nanyi mtaongezewa hivi vitu vingine vyote.”—Mt. 6:31-33.

PATA MAFANIKIO MACHONI PA MUNGU

17, 18. (a) Mafanikio ya kweli yanategemea nini? (b) Mafanikio hayategemei nini?

17 Jambo kuu ni hili: Mafanikio ya kweli hayategemei kuwa na ufanisi au cheo machoni pa watu. Mbali na hilo, mafanikio ya kweli hayategemei kuwa na pendeleo fulani katika kutaniko la Kikristo. Ingawa hivyo, baraka kama hiyo inaweza kuhusianishwa na msingi halisi wa mafanikio, yaani, utii na uaminifu wetu kwa Mungu, ambaye anatuhakikishia hivi: “Kinachoangaliwa katika wasimamizi-nyumba ni mtu kupatwa akiwa mwaminifu.” (1 Kor. 4:2) Ni lazima pia tuvumilie ili tuendelee kuwa waaminifu. Yesu alisema hivi: “Yule atakayevumilia mpaka mwisho ndiye atakayeokolewa.” (Mt. 10:22) Je, hukubali kwamba kuokolewa ni uthibitisho ulio wazi kabisa wa mafanikio?

18 Ukitafakari mambo yaliyotajwa hapo juu, unaweza kuona kwamba uaminifu kwa Mungu hauhusiani na umaarufu, elimu, pesa, au cheo katika jamii; wala uaminifu hautegemei kuwa na akili nyingi, uwezo, au vipawa. Katika hali yoyote ile tunayokabili, tunaweza kuthibitika kuwa waaminifu kwa Mungu. Katika karne ya kwanza, baadhi ya watu wa Mungu walikuwa matajiri na wengine walikuwa maskini. Shauri hili la Paulo liliwafaa sana Wakristo matajiri: “Wafanye mema, wawe matajiri katika matendo mazuri, wawe wakarimu, tayari kushiriki.” Wakristo wote, matajiri na maskini, wangeweza ‘kuushika imara uzima ulio wa kweli.’ (1 Tim. 6:17-19) Ndivyo ilivyo leo pia. Sisi sote tuna fursa na daraka lilelile: Ni lazima tubaki waaminifu na kuwa “matajiri katika matendo mazuri.” Tukifanya hivyo, tutafanikiwa machoni pa Muumba wetu na tutakuwa na shangwe kwa sababu tunajua kwamba tunampendeza yeye.—Met. 27:11.

19. Kuhusu mafanikio, umeazimia nini?

19 Huenda usiweze kubadili kabisa hali zako, lakini unaweza kuamua jinsi utakavyozishughulikia. Jitahidi kabisa kuwa mwaminifu katika hali zozote unazokabili sasa. Utafaidika sana ukifanya hivyo. Uwe na hakika kwamba Yehova atakubariki sana, sasa na kwa umilele wote. Usisahau kamwe maneno haya ambayo Yesu aliwaambia Wakristo watiwa-mafuta: “Uwe mwaminifu hata kufikia kifo, nami nitakupa taji la uzima.” (Ufu. 2:10) Hayo ndiyo mafanikio ya kweli!