Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kudumisha Msimamo Wetu Tukiwa “Wakaaji wa Muda”

Kudumisha Msimamo Wetu Tukiwa “Wakaaji wa Muda”

“Nawahimiza ninyi kama wageni na wakaaji wa muda kwamba mwendelee kujiepusha na tamaa za kimwili.”—1 PET. 2:11.

1, 2. Petro alikuwa akiwarejelea nani alipotumia maneno “wale waliochaguliwa,” na kwa nini aliwaita “wakaaji wa muda”?

MIAKA 30 hivi baada ya Yesu kwenda mbinguni, mtume Petro aliwaandikia barua “wakaaji wa muda waliotawanyika huku na huku katika Ponto, Galatia, Kapadokia, Asia, na Bithinia, kwa wale waliochaguliwa.” (1 Pet. 1:1) Ni wazi kwamba Petro alitumia maneno “wale waliochaguliwa,” kuwarejelea Wakristo waliotiwa mafuta kwa roho takatifu na ‘kuzaliwa upya kwenye tumaini lililo hai’ kama yeye ili watawale pamoja na Kristo mbinguni. (Soma 1 Petro 1:3, 4.) Lakini kwa nini baadaye alisema kwamba watu hao waliochaguliwa ni “wageni na wakaaji wa muda”? (1 Pet. 2:11) Na maneno hayo yana maana gani kwetu leo ilhali Mashahidi watendaji wanaodai kuwa watiwa-mafuta waliochaguliwa ni wachache sana, yaani, uwiano wao ni karibu tu mtiwa-mafuta 1 kwa kila Mashahidi 650?

2 Maneno “wakaaji wa muda” yaliwafaa watiwa-mafuta katika karne ya kwanza. Wakristo hao hawakuwa wakaaji wa kudumu duniani sawa na Wakristo watiwa-mafuta walio duniani leo. Mtume Paulo, aliyekuwa mshiriki wa “kundi dogo” lililotiwa mafuta alieleza hivi: “Lakini sisi, uraia wetu uko mbinguni, ambako kutoka huko pia tunamngojea mwokozi kwa hamu, Bwana Yesu Kristo.” (Luka 12:32; Flp. 3:20) Kwa kuwa ‘uraia wao uko mbinguni,’ watiwa-mafuta wanapokufa wanaondoka duniani na kupata kitu bora zaidi, uhai usioweza kufa mbinguni. (Soma Wafilipi 1:21-23.) Kwa hiyo, kihalisi wanaweza kuitwa “wakaaji wa muda” katika dunia iliyo chini ya utawala wa Shetani.

3. Ni swali gani linalozuka kuhusu “kondoo wengine”?

3 Lakini namna gani “kondoo wengine”? (Yoh. 10:16) Je, si ni kweli kwamba wana tumaini thabiti linalotegemea Maandiko la kuwa wakaaji wa kudumu duniani? Bila shaka, wataishi humo milele! Hata hivyo, kwa sasa tunaweza kusema kwamba kwa njia fulani wao ni wakaaji wa muda. Kwa njia gani?

“UUMBAJI WOTE UNAENDELEA KUUGUA”

4. Viongozi wa ulimwengu hawawezi kuzuia nini?

4 Maadamu Yehova anauruhusu mfumo mwovu wa Shetani uendelee kuwapo, kila mtu, kutia ndani Wakristo, wataendelea kuteseka kwa sababu ya uasi wa Shetani dhidi ya Yehova. Tunasoma hivi katika Waroma 8:22: “Tunajua kwamba uumbaji wote unaendelea kuugua pamoja na kuwa katika maumivu pamoja mpaka sasa.” Viongozi wa ulimwengu, wanasayansi, na watetezi wa haki za kibinadamu hawawezi kuzuia jambo hilo hata kama wana nia nzuri kadiri gani.

5. Tangu mwaka wa 1914, mamilioni ya watu wamechukua hatua gani, na kwa nini?

5 Kwa hiyo, tangu mwaka wa 1914, mamilioni ya watu wamechagua kwa hiari kuwa raia wa Kristo Yesu, Mfalme aliyetawazwa na Mungu. Hawatamani kuwa sehemu ya mfumo wa ulimwengu wa Shetani. Wanakataa kuunga mkono ulimwengu wa Shetani. Badala yake, wanatumia maisha yao na mali zao kuunga mkono Ufalme wa Mungu, na kuendeleza masilahi yake.—Rom. 14:7, 8.

6. Mashahidi wa Yehova wanaweza kuitwa wakaaji wageni katika maana gani?

6 Naam, Mashahidi wa Yehova ni raia wanaotii sheria katika nchi zaidi ya 200, lakini wao ni kama wakaaji wageni popote wanapoishi. Wanadumisha msimamo wa kutounga mkono kamwe upande wowote ule katika mambo ya kisiasa na ya kijamii. Hata sasa wanajiona kuwa raia wa ulimwengu mpya wa Mungu. Wanashangilia kuona siku zao za kuwa wakaaji wa muda katika mfumo huu wa mambo wa ulimwengu usio mkamilifu zikikaribia haraka kwisha.

7. Watumishi wa Mungu watakuwaje wakaaji wa kudumu, na wataishi wapi?

7 Hivi karibuni Kristo atatumia mamlaka yake kuuharibu mfumo mwovu wa Shetani. Serikali kamilifu ya Kristo itaondoa dhambi na huzuni duniani. Itaondoa kabisa madhara yote yanayoonekana na yasiyoonekana ya uasi dhidi ya enzi kuu halali ya Yehova. Watumishi washikamanifu wa Mungu watapata fursa ya kuwa wakaaji wa kudumu katika Paradiso duniani. (Soma Ufunuo 21:1-5.) Wakati huo, uumbaji utakuwa ‘umewekwa huru kikamili kutoka katika utumwa wa uharibifu na kuwa na uhuru wenye utukufu wa watoto wa Mungu.’—Rom. 8:21.

WAKRISTO WA KWELI WANATARAJIWA KUTIMIZA MATAKWA GANI?

8, 9. Eleza alichomaanisha Petro alipotumia maneno “kujiepusha na tamaa za kimwili.”

Petro anaeleza matakwa ambayo Wakristo wanatarajiwa kutimiza anaposema hivi: “Wapendwa, nawahimiza ninyi kama wageni na wakaaji wa muda kwamba mwendelee kujiepusha na tamaa za kimwili, ambazo ndizo huendelea kupambana na nafsi.” (1 Pet. 2:11) Shauri hilo lilielekezwa kwanza kwa Wakristo watiwa-mafuta, lakini linawahusu pia kondoo wengine wa Yesu.

9 Tamaa fulani si mbaya ikiwa zinatoshelezwa kulingana na maagizo ya Muumba. Kwa kweli, zinaongeza furaha maishani. Kwa mfano, kuna tamaa za kawaida kama vile tamaa ya kufurahia kinywaji na chakula kizuri, kushiriki katika tafrija yenye kuburudisha, na kufurahia urafiki mzuri. Hata tamaa ya kufurahia ngono na mwenzi wa ndoa inafaa na ina wakati wake. (1 Kor. 7:3-5) Hata hivyo, kwa kufaa Petro alizungumzia hasa “tamaa za kimwili” ambazo “huendelea kupambana na nafsi.” Tafsiri fulani za Biblia zinaonyesha waziwazi ni tamaa gani hizo zinapotaja “uchu wa kimwili” (King James Version) au “tamaa zenye dhambi” (New International Version). Kwa wazi, ni lazima mtu adhibiti tamaa yoyote ya kibinadamu inayopingana na kusudi la Yehova lililofunuliwa na inayoweza kuathiri uhusiano wake mzuri pamoja na Mungu. Mkristo asipofanya hivyo anaweza kuhatarisha kabisa tumaini lake la kuendelea kuwa hai.

10. Ni baadhi ya njia gani anazotumia Shetani kuwafanya Wakristo wawe sehemu ya ulimwengu wake?

10 Lengo la Shetani ni kudhoofisha azimio la Wakristo wa kweli la kuwa “wakaaji wa muda” katika mfumo wa sasa. Ni lazima tutambue kwamba Shetani anatumia mitego kama vile fahari ya kuwa na vitu vya kimwili, maadili mapotovu yenye kushawishi, tamaa yenye nguvu ya kuwa maarufu, roho inayovutia ya “mimi kwanza,” na roho ya utaifa yenye uvutano mkubwa. Tukiazimia kabisa kuepuka tamaa hizo za kimwili zisizofaa, tunaonyesha waziwazi kwamba hatutaki kuwa sehemu ya ulimwengu mwovu wa Shetani. Tunathibitisha kwamba sisi ni wakaaji wa muda tu katika ulimwengu huu. Kwa kweli tunachotaka na tunachojitahidi kabisa kupata ni fursa ya kuwa wakaaji wa kudumu katika ulimwengu mpya wa Mungu wenye uadilifu.

MWENENDO MZURI

11, 12. Nyakati nyingine wageni wanaonwaje, na tunaweza kusema nini kuhusu Mashahidi wa Yehova?

11 Petro anaendelea kueleza matakwa ambayo Wakristo wanatarajiwa kutimiza wakiwa “wakaaji wa muda.” Anasema hivi katika mstari wa 12: “Dumisheni mwenendo wenu ukiwa mzuri katikati ya mataifa, ili, katika jambo ambalo wanasema juu yenu ya kuwa ninyi ni watenda-maovu, waweze, likiwa tokeo la matendo yenu mazuri ambayo wameshuhudia kwa macho, kumtukuza Mungu katika siku ya ukaguzi wake.” Nyakati nyingine, wageni, yaani, wakaaji wa muda katika nchi ya kigeni hushutumiwa. Huenda hata wakaonwa kama watenda-maovu kwa sababu tu ya kuwa tofauti na wenyeji. Usemi wao, matendo yao, na mavazi yao yako tofauti, na labda hata wanaonekana kuwa tofauti kwa njia fulani. Lakini wanapotenda mema, yaani, wanapojiendesha kwa njia nzuri, mambo mabaya ambayo watu wanawasingizia eti kwa sababu wako tofauti, yanathibitika kuwa yasiyo na msingi.

12 Vivyo hivyo, Wakristo wa kweli wako tofauti na jirani zao wengi katika mambo fulani, kama vile usemi wao au burudani wanayochagua. Mara nyingi, mavazi na mapambo yao yanawatofautisha na watu wengi katika jamii. Nyakati nyingine tofauti hizo zimewafanya watu waliopotoshwa wadai kwamba Wakristo wa kweli ni watenda-maovu. Hata hivyo, huenda watu wengine wakawasifu kwa sababu ya mtindo wao wa maisha.

13, 14. Hekima ‘huonyeshwaje kuwa yenye uadilifu kwa matendo yake’? Toa mfano.

13 Naam, mwenendo mzuri unaweza kuonyesha kwamba madai ya uwongo hayana msingi. Hata Yesu, mwanadamu pekee aliyewahi kuishi na kudumisha uaminifu mkamilifu kwa Mungu, alishtakiwa kwa uwongo. Watu fulani walimwita “mtu mlafi na mwenye mazoea ya kunywa divai, rafiki ya wakusanya-kodi na watenda-dhambi.” Hata hivyo, ukweli ni kwamba mwenendo wake wa hekima katika utumishi wa Mungu ulithibitisha kwamba madai hayo yalikuwa ya uwongo. Yesu alisema hivi: “Hekima huonyeshwa kuwa yenye uadilifu kwa matendo yake.” (Mt. 11:19) Ndivyo ilivyo leo pia. Kwa mfano, baadhi ya watu wanaoishi karibu na Betheli ya Selters, Ujerumani, wanaona kwamba ndugu na dada wanaotumika katika Betheli hiyo ni watu wa ajabu. Hata hivyo, meya wa mji huo aliwatetea Wakristo hao kwa kusema hivi: “Ni kweli kwamba Mashahidi wanaotumikia katika majengo hayo wana njia yao ya maisha, lakini hawawasumbui kamwe watu wengine katika jamii.”

14 Maoni kama hayo yalitolewa hivi karibuni kuhusu Mashahidi wa Yehova wanaoishi Moscow, Urusi. Walikuwa wameshtakiwa kwa uwongo kwamba walitenda mambo fulani mabaya. Kisha mnamo Juni 2010, Mahakama ya Ulaya ya Haki za Kibinadamu huko Strasbourg, Ufaransa, ikatoa uamuzi huu: “Mahakama hii imeona kwamba wenye mamlaka jijini [Moscow] waliingilia bila sababu halali haki ya washtakiwa ya kuwa na uhuru wa kidini na ushirika. Mahakama za Urusi hazikutoa sababu ‘za kutosha na zinazofaa’ kuthibitisha kwamba walalamishi” walikuwa na hatia ya kufanya mambo kama vile kuvunja familia, kuwachochea watu wajiue, au kukataa matibabu. Kwa hiyo, “vizuizi vilivyotangazwa na mahakama za nchi hiyo vilipita mipaka kwa sababu sheria za nchi hazikuzingatia kila jambo na hivyo zilikiuka lengo la kisheria ambalo zilipaswa kutimiza.”

KUJITIISHA IFAAVYO

15. Wakristo wa kweli ulimwenguni pote wanafuata kanuni gani ya Biblia?

15 Mashahidi wa Yehova jijini Moscow, na hata ulimwenguni pote, wanatimiza takwa lingine ambalo Petro anasema linapaswa kutimizwa na Wakristo. Aliandika hivi: “Kwa ajili ya Bwana jitiisheni wenyewe kwa kila kitu kilichofanywa na binadamu: iwe ni kwa mfalme akiwa mkubwa au ni kwa magavana.” (1 Pet. 2:13, 14) Ingawa Wakristo wa kweli si sehemu ya ulimwengu huu mwovu, wanajitiisha kwa hiari kwa wenye mamlaka za kiserikali walio “katika vyeo vyao vya kadiri,” kama Paulo alivyowaagiza.—Soma Waroma 13:1, 5-7.

16, 17. (a) Ni nini kinachothibitisha kwamba hatupingi serikali? (b) Viongozi fulani wa kisiasa wamekiri nini?

16 Mashahidi wa Yehova wanapojiendesha kama “wakaaji wa muda” katika mfumo huu, hawafanyi hivyo kama njia ya kutetea haki zao kimya-kimya; wala hawapingi au kuingilia maamuzi ambayo wengine wanafanya katika masuala ya kisiasa au ya kijamii. Tofauti na vikundi vingine vya kidini, Mashahidi wa Yehova hawajihusishi na siasa. Hawajaribu kamwe kuwashurutisha wenye mamlaka ya kiserikali wafuate sera fulani. Wazo la kwamba wanaweza kuvuruga amani au kuchochea uasi dhidi ya serikali halina msingi kamwe!

17 Wakristo wanafuata shauri la Petro la ‘kumheshimu mfalme’ kwa kuwatii maofisa wa umma na kuwaonyesha heshima na staha wanayostahili kulingana na vyeo vyao. (1 Pet. 2:17) Nyakati nyingine, maofisa wa umma wamekiri kwamba hawana sababu halali ya kuwa na wasiwasi kuhusu Mashahidi wa Yehova. Kwa mfano, Steffen Reiche, mwanasiasa Mjerumani aliyekuwa waziri katika jimbo la Brandenburg na mbunge wa Ujerumani, alisema hivi: “Mwenendo wa Mashahidi wa Yehova walipokuwa kambini na gerezani unaonyesha sifa nzuri ambazo ni muhimu leo na ambazo zilikuwa muhimu zamani ili kuendeleza serikali ya kidemokrasia: hasa msimamo wao imara walipoteswa na askari wa SS na huruma waliyowaonyesha wafungwa wenzao. Tukifikiria jinsi matendo ya kinyama yanavyoongezeka dhidi ya wageni na dhidi ya watu wenye msimamo au maoni tofauti ya kisiasa, kila raia wa nchi yetu anapaswa kuwa na sifa hizo nzuri.”

KUONYESHA UPENDO

18. (a) Kwa nini tunafurahia kuupenda ushirika mzima wa akina ndugu? (b) Watu fulani ambao si Mashahidi wamesema nini kuwahusu?

18 Mtume Petro aliandika hivi: “Upendeni ushirika mzima wa akina ndugu, mwogopeni Mungu.” (1 Pet. 2:17) Mashahidi wa Yehova wana woga unaofaa wa kutompendeza Mungu, nao unawachochea zaidi kufanya mapenzi yake. Wanafurahia kumtumikia Yehova wakiwa sehemu ya ushirika wa ulimwenguni pote wa akina ndugu na dada wanaotamani kufanya vivyo hivyo. Kwa hiyo, wanafurahia ‘kuupenda ushirika mzima wa akina ndugu.’ Upendo huo wa kindugu, usiopatikana kwa urahisi katika ulimwengu wa leo wenye uchoyo, unawashangaza watu ambao si Mashahidi. Kwa mfano, mfanyakazi mmoja wa shirika la Marekani la kupanga safari za watalii alishangaa kuona jinsi Mashahidi walivyowasaidia na kuwaonyesha upendo wajumbe wa nchi nyingine waliohudhuria kusanyiko la kimataifa nchini Ujerumani mwaka wa 2009. Mwanamke huyo alisema kwamba katika miaka yote ambayo amekuwa akiwatembeza watalii, hajawahi kamwe kuona jambo kama hilo. Baadaye, Shahidi mmoja alisema hivi: “Kila jambo alilosema kutuhusu alilisema kwa mshangao na msisimko.” Je, umewahi kusikia watu wakisema vivyo hivyo walipowatazama Mashahidi katika kusanyiko ambalo ulihudhuria?

19. Tunapaswa kuazimia kufanya nini, na kwa nini?

19 Mashahidi wa Yehova wanaonyesha katika njia hizo zote na nyingine nyingi kwamba kwa kweli wao ni “wakaaji wa muda” katika mfumo huu wa Shetani. Na wameazimia kwa shangwe kuendelea kuwa wakaaji wa muda. Wana tumaini thabiti na lenye kutegemeka kwamba hivi karibuni watakuwa wakaaji wa kudumu katika ulimwengu mpya wa Mungu wenye uadilifu. Je, hutazamii kwa hamu wakati huo?