Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Mnara wa Mlinzi

Kwa Nini Mnara wa Mlinzi

KWA miaka mingi, wanaume na wanawake ulimwenguni pote wamethamini na kunufaika na habari za Biblia zinazochapishwa katika Mnara wa Mlinzi. Mnamo Julai 2011, toleo la kwanza la funzo la Mnara wa Mlinzi lilichapishwa katika lugha ya Kiingereza iliyorahisishwa. Toleo hilo lilieleza hivi: “Toleo hili jipya litajaribiwa kwa mwaka mmoja, na ikiwa litasaidia, litaendelea kuchapishwa.”

Kwa hiyo, tunafurahi kutangaza kwamba tumeamua kuendelea kuchapisha gazeti hilo. Isitoshe, baada ya muda matoleo yaliyorahisishwa katika lugha ya Kifaransa, Kihispania, na Kireno yatachapishwa.

KWA NINI LINATHAMINIWA?

Baada ya kupokea toleo lililorahisishwa, watu wengi huko Pasifiki ya Kusini waliripoti hivi: “Sasa akina ndugu wanaweza kuelewa vizuri zaidi Mnara wa Mlinzi.” Barua nyingine ilisema hivi: “Muda tuliotumia kutafuta maana ya maneno na misemo tunautumia sasa kuelewa maandiko ambayo hayajanukuliwa na kuelewa jinsi yanavyohusiana na jambo kuu.”

Mhitimu mmoja wa chuo nchini Marekani alisema hivi: “Kwa miaka 18 nilizoea kuongea na kuandika lugha ngumu inayotumiwa katika elimu ya juu. Nilizoea kufikiri na kuongea kwa njia iliyo ngumu isivyo lazima. Niligundua kwamba nilihitaji kubadili kabisa njia yangu ya kufikiri na kusema.” Sasa akiwa mweneza-injili mwenye matokeo, dada huyo anaandika hivi: “Mnara wa Mlinzi uliorahisishwa umenisaidia sana. Lugha yake inanisaidia sana kuelewa jinsi ya kueleza mambo kwa njia rahisi.”

Dada mmoja nchini Uingereza aliyebatizwa mwaka 1972 aliandika hivi kuhusu Mnara wa Mlinzi uliorahisishwa: “Niliposoma toleo la kwanza kabisa, nilihisi ni kana kwamba Yehova ameketi kando yangu, akiwa ameuweka mkono wake kwenye mabega yangu na tulikuwa tukiisoma nakala hiyo pamoja. Ilikuwa ni kama baba akimsomea hadithi mtoto wake kabla ya kulala.”

Dada aliye Mwanabetheli nchini Marekani ambaye alibatizwa zaidi ya miaka 40 iliyopita alisema kwamba mara kwa mara toleo lililorahisishwa linamsaidia kuelewa mambo mapya. Kwa mfano, sanduku lenye kichwa, “Ufafanuzi wa Baadhi ya Maneno” katika toleo la Septemba 15, 2011, lilifafanua hivi maneno “wingu la mashahidi” yaliyo katika Waebrania 12:1: “Walikuwa wengi sana hivi kwamba hawangeweza kuhesabiwa.” Dada huyo alisema hivi: “Ufafanuzi huo ulinisaidia kuelewa vizuri maneno hayo.” Kuhusu funzo la kila juma, anaongeza hivi: “Hata mtoto akijibu moja kwa moja kutoka katika toleo lililorahisishwa, hatumii maneno yaleyale yanayopatikana katika toleo la kawaida la Mnara wa Mlinzi ambalo wengi wanatumia. Kwa hiyo maelezo yake ni mapya kwa wasikilizaji.”

Dada mwingine Mwanabetheli aliandika hivi: “Ninatazamia kwa hamu kusikia maelezo ya watoto wadogo kutanikoni. Toleo lililorahisishwa la Mnara wa Mlinzi limewasaidia kujieleza kwa usadikisho. Maelezo yao yamenitia moyo.”

Dada aliyebatizwa mwaka wa 1984 alionyesha uthamini wake kuelekea toleo lililorahisishwa kwa kusema hivi: “Ninahisi kwamba liliandikwa kwa ajili yangu. Linanisaidia kuelewa kwa urahisi mambo ninayosoma. Sasa nina uhakika kwamba ninaweza kujibu wakati wa Funzo la Mnara wa Mlinzi.

KIFAA AMBACHO WAZAZI WANATHAMINI

Mama aliye na mvulana wa miaka saba alisema hivi: “Lilikuwa jambo lenye kuchosha na linalochukua muda mrefu kumfafanulia sentensi nyingi tulipokuwa tukitayarisha Funzo la Mnara wa Mlinzi.Toleo lililorahisishwa lilimsaidiaje? Dada huyo anaandika hivi: “Ninashangaa kuona kwamba anaweza kusoma mafungu na kuelewa vizuri maana yake. Kwa kuwa maneno si magumu na sentensi ni fupi zaidi, haogopi kutoa maelezo. Ameanza kutayarisha maelezo ya kutoa mikutanoni bila msaada wangu, naye hukazia uangalifu gazeti wakati wote wa funzo.”

Mama aliye na binti mwenye umri wa miaka tisa aliandika hivi: “Kabla ya kupata gazeti hili, tulihitaji kumsaidia kutayarisha maelezo yake. Sasa anatayarisha mwenyewe. Ni mara chache tu tunapohitaji kutumia wakati kumfafanulia habari. Kwa kuwa anaelewa makala ya funzo, sasa anafurahia kushiriki katika Funzo la Mnara wa Mlinzi.

WATOTO WANAHISIJE?

Watoto wengi wanahisi kwamba Mnara wa Mlinzi uliorahisishwa umetolewa hasa kwa ajili yao. Rebecca mwenye umri wa miaka kumi na miwili alitoa ombi hili: “Tafadhali endeleeni kuchapisha toleo hili jipya!” Aliongezea hivi: “Ninaipenda sehemu yenye kichwa ‘Ufafanuzi wa Baadhi ya Maneno.’ Ni rahisi sana kwa watoto.”

Nicolette mwenye umri wa miaka saba anahisi vivyo hivyo: “Ilikuwa vigumu kwangu kuelewa Mnara wa Mlinzi. Sasa ninaweza kutoa maelezo yangu mwenyewe.” Emma mwenye umri wa miaka tisa aliandika hivi: “Gazeti hilo limenisaidia sana mimi na kaka yangu mwenye umri wa miaka sita. Tunalielewa vizuri zaidi! Asanteni!”

Ni wazi kwamba wengi wanafaidika kutokana na toleo lililorahisishwa la Mnara wa Mlinzi linalotumia sentensi fupi zenye maneo rahisi. Linawasaidia sana watu na litaendelea kuchapishwa pamoja na toleo la kawaida ambalo limekuwa uandalizi wenye thamani tangu 1879.