Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wakaaji wa Muda” Waungana Katika Ibada ya Kweli

Wakaaji wa Muda” Waungana Katika Ibada ya Kweli

“Watu wa nchi nyingine watakuwa wakulima wenu na watunza-mizabibu wenu. Nanyi mtaitwa makuhani wa Yehova.”—ISA. 61:5, 6.

1. Baadhi ya watu wana maoni gani kuhusu watu wa nchi nyingine, lakini kwa nini maoni hayo hayafai?

KAMA makala iliyotangulia ilivyoonyesha, watu hutumia maneno “mtu wa nchi nyingine” au mgeni ili kumdharau mtu, kumdhihaki, au hata kuonyesha waziwazi kwamba wanamchukia. Si jambo la heshima kuwadharau watu wa taifa lingine. Isitoshe, mtazamo kama huo unaonyesha kwamba hatukubali ukweli wa mambo. Kitabu kimoja (The Races of Mankind) kinasema hivi: “Wanadamu wa jamii zote ni ndugu, kama Biblia inavyosema.” Kwa kawaida, ndugu wanakuwa tofauti sana, lakini vyovyote vile, wao ni ndugu.

2, 3. Yehova ana maoni gani kuhusu watu wa nchi nyingine?

2 Bila shaka, watu wa nchi nyingine wanaishi miongoni mwetu popote tulipo. Ndivyo ilivyokuwa pia kwa Waisraeli wa kale, ambao walikuwa na uhusiano wa pekee pamoja na Yehova Mungu kwa msingi wa agano la Sheria. Watu hao ambao hawakuwa Waisraeli walikuwa na haki kwa kiasi fulani, hata hivyo, Waisraeli walipaswa kuwatendea kwa heshima na bila ubaguzi. Huo ni mfano mzuri kama nini wa kuiga! Wakristo wa kweli hawapaswi kamwe kuwa na ubaguzi au upendeleo. Kwa nini? Mtume Petro alisema hivi: “Kwa hakika ninaona kwamba Mungu hana ubaguzi, bali katika kila taifa mtu ambaye anamwogopa na kutenda uadilifu anakubalika kwake.”—Mdo. 10:34, 35.

3 Wageni walioishi katika taifa la kale la Israeli walinufaika kwa kushirikiana kwa ukaribu na Waisraeli. Hilo lilionyesha maoni ya Yehova kuhusu jambo hilo, maoni ambayo yaliandikwa miaka mingi baadaye na mtume Paulo alipouliza hivi kumhusu Yehova: “Je, yeye ni Mungu wa Wayahudi peke yao? Je, yeye si wa watu wa mataifa pia? Ndiyo, wa watu wa mataifa pia.”—Rom. 3:29; Yoe. 2:32.

4. Kwa nini tunaweza kusema kwamba hakuna wageni katika taifa la “Israeli wa Mungu”?

4 Kwa msingi wa agano jipya, kutaniko la Wakristo watiwa-mafuta lilichukua mahali pa taifa la asili la Israeli na kuwa na uhusiano wa pekee na Mungu. Kwa hiyo, kutaniko hilo linaitwa “Israeli wa Mungu.” (Gal. 6:16) Na kama Paulo alivyoeleza, katika taifa hilo jipya, “hakuna Mgiriki wala Myahudi, tohara wala kutotahiriwa, mgeni, Msikithe, mtumwa, mtu huru, bali Kristo ni kila kitu na katika vitu vyote.” (Kol. 3:11) Basi, ni katika maana hiyo kwamba hakungekuwa na wageni katika kutaniko la Kikristo.

5, 6. (a) Andiko la Isaya 61:5, 6 linaweza kutokeza swali gani? (b) “Makuhani wa Yehova” na “wageni” wanaotajwa na Isaya ni nani? (c) Vikundi hivyo viwili vinashirikiana kufanya kazi gani?

5 Kwa upande mwingine, huenda mtu akarejelea sura ya 61 ya kitabu cha Isaya, ambayo ina unabii unaotimizwa katika kutaniko la Kikristo. Mstari wa 6 wa sura hiyo unawataja wale ambao watatumikia wakiwa “makuhani wa Yehova.” Hata hivyo, mstari wa 5 unawataja “wageni” ambao watashirikiana na kufanya kazi na “makuhani” hao. Tunapaswa kuuelewaje unabii huo?

6 Tunaelewa kwamba hao “makuhani wa Yehova” ni Wakristo watiwa-mafuta walio na sehemu “katika ufufuo wa kwanza” na ambao ‘watakuwa makuhani wa Mungu na wa Kristo, na kutawala wakiwa wafalme pamoja naye ile miaka elfu.’ (Ufu. 20:6) Kwa kuongezea, kuna Wakristo wengi washikamanifu wenye tumaini la kuishi duniani. Wakristo hao ni wageni kwa njia ya mfano, ingawa wanafanya kazi na kushirikiana kwa ukaribu na wale watakaotumika mbinguni. Wanafurahia kuwaunga mkono na kufanya kazi pamoja na “makuhani wa Yehova,” wakitumikia kama “wakulima” na “watunza-mizabibu” wao kwa njia ya mfano. Naam, wanawasaidia watu kusitawisha matunda ya kiroho na kumletea Mungu utukufu, wakiwatunza na kuwavuna watu kwa njia ya mfano. Kwa kweli, watiwa-mafuta na “kondoo-wengine” wanawatafuta na kuwachunga kwa upendo watu wanyoofu wanaotamani kumtumikia Mungu milele.—Yoh. 10:16.

“WAKAAJI WA MUDA” KAMA ABRAHAMU

7. Wakristo leo wako kama Abrahamu na wanaume wengine waaminifu wa kale katika njia gani?

7 Kama ilivyotajwa katika makala iliyotangulia, Wakristo wa kweli ni kama wageni, au wakaaji wa muda, katika ulimwengu mwovu wa Shetani. Kwa hiyo, wanaweza kulinganishwa na wanaume waaminifu wa kale, kama Abrahamu, ambao Biblia inasema kwamba walikuwa “wageni na wakaaji wa muda katika nchi.” (Ebr. 11:13) Hata iwe tuna tumaini gani la wakati ujao, tuna pendeleo la kufurahia uhusiano kama ule ambao Abrahamu alikuwa nao pamoja na Yehova. Yakobo anasema kwamba “‘Abrahamu alikuwa na imani katika Yehova, na ikahesabiwa kwake kuwa ni uadilifu,’ naye akaitwa ‘rafiki ya Yehova.’”—Yak. 2:23.

8. Abrahamu alipewa ahadi gani, naye alihisije kuhusu kutimizwa kwa ahadi hiyo?

8 Mungu aliahidi kwamba familia zote duniani—si taifa moja tu—zingebarikiwa kupitia Abrahamu na wazao wake. (Soma Mwanzo 22:15-18.) Ingawa ahadi hiyo ya Mungu ingetimizwa wakati ujao, Abrahamu aliendelea kuwa na hakika kwamba ingetimizwa. Abrahamu alihama-hama pamoja na familia yake kwa zaidi ya miaka tisini. Kwa muda huo wote, Abrahamu alidumisha urafiki wake pamoja na Yehova.

9, 10. (a) Tunaweza kuiga mfano wa Abrahamu katika njia zipi? (b) Tunaweza kuwapa wengine mwaliko gani?

9 Ingawa hakujua angengoja kwa muda mrefu kadiri gani ili aone tumaini lake likitimia, Abrahamu hakuyumbayumba kamwe katika upendo na ujitoaji wake kwa Yehova. Alikazia macho tumaini lake, hakuishi maisha ya kawaida na kuwa mkaaji wa kudumu katika taifa fulani. (Ebr. 11:14, 15) Ni jambo la hekima kama nini kwetu kuiga mfano wa Abrahamu kwa kuishi maisha rahisi na kutohangaikia kupita kiasi vitu vya kimwili, vyeo katika jamii, au kutafuta kazi zenye mshahara mnono! Kwa nini tung’ang’ane kuwa na yale yanayoitwa eti maisha ya kawaida katika mfumo ambao utaangamia hivi karibuni? Kwa nini ushikamane sana na kitu ambacho ni cha muda mfupi tu? Kama Abrahamu, tunatazamia kupata kitu bora zaidi. Tuko tayari kuonyesha mtazamo wa kungojea kwa subira hadi tumaini letu litimie.—Soma Waroma 8:25.

10 Yehova bado anawaalika watu wa mataifa yote ili wapate baraka kupitia uzao wa Abrahamu. Na “makuhani wa Yehova” waliotiwa mafuta, na vilevile “wageni,” yaani, kondoo wengine, wanawatolea watu ulimwenguni pote mwaliko huo katika lugha zaidi ya 600.

USIWABAGUE WATU WA MATAIFA MENGINE

11. Sulemani alisema jambo gani ambalo liliwahusu watu wengine wasio Waisraeli?

11 Wakati wa uzinduzi wa hekalu mwaka wa 1026 K.W.K., na kupatana na ahadi ambayo Yehova alimpa Abrahamu, Sulemani alisema kwamba watu wa mataifa yote wangeshiriki katika kumsifu Yehova. Alisali hivi kutoka moyoni: “Pia kwa mgeni, ambaye si sehemu ya watu wako Israeli na ambaye anatoka katika nchi ya mbali kwa sababu ya jina lako (kwa maana watasikia habari za jina lako kuu na za mkono wako wenye nguvu na za mkono wako ulionyooshwa), naye kwa kweli aje na kusali kuelekea nyumba hii, basi na usikilize ukiwa mbinguni, makao yako yaliyofanywa imara, nawe ufanye kulingana na yote ambayo mgeni huyo anakuomba; kusudi watu wote wa dunia wajue jina lako ili wakuogope kama vile watu wako Israeli wanavyokuogopa.”—1 Fal. 8:41-43.

12. Kwa nini huenda watu fulani wanawaona Mashahidi wa Yehova kuwa watu wa ajabu au kama “wageni”?

12 Mgeni ni mtu anayeishi katika nchi ya kigeni au mtu anayejiunga na jamii au kikundi fulani. Hivyo ndivyo Mashahidi wa Yehova walivyo. Wanawajibika kwanza kwa serikali ya kimbingu, yaani, Ufalme wa Mungu ulio mikononi mwa Kristo. Hivyo, hawajihusishi kamwe na mambo ya kisiasa, hata ikiwa wengine wanawaona kuwa watu wa ajabu wasiofaa katika jamii ya leo.

13. (a) Kwa nini mara nyingi maana ya neno “mgeni” inategemea maoni ya mtu binafsi? (b) Je, kusudi la Yehova la mwanzoni lilitia ndani wazo la wageni? Eleza.

13 Kwa kawaida wageni wanatambuliwa kwa sababu ya mambo fulani yanayowafanya waonekane kuwa tofauti na wengine. Wanaweza kutambuliwa kwa lugha yao, desturi zao, mwonekano au sura yao, au mavazi yao. Hata hivyo, mambo yanayowatofautisha na wengine ni machache yakilinganishwa na mambo yanayofanya wafanane na wanadamu wengine wote bila kujali ni wa taifa gani. Basi, kwa kweli mtu huonwa kuwa mgeni kwa sababu yuko tofauti katika njia fulani. Tunapojifunza kutokazia fikira mambo hayo yanayofanya mtu aonekane kuwa tofauti, inaelekea kwamba hatutamwona yeyote kuwa “mgeni” katika maana hiyo. Ikiwa watu wote duniani wangeishi chini ya serikali au chama kimoja cha kisiasa, hakungekuwa na mgeni katika maana ya kisiasa. Kwa kweli, Yehova alikusudia mwanzoni wanadamu wote waungane wakiwa familia moja chini ya utawala mmoja—utawala wake. Je, watu wa mataifa yote duniani wanaweza kuwa kama familia moja chini ya utawala mmoja leo?

14, 15. Mashahidi wa Yehova wamethamini nini wakiwa kikundi?

14 Katika ulimwengu wenye roho ya uchoyo na utaifa, inaburudisha kuona watu wasiowabagua watu wa mataifa mengine. Kwa kweli, si rahisi kuishinda roho ya ubaguzi. Mwanzilishi wa kituo cha televisheni cha CNN, Ted Turner, anaeleza jinsi alivyohisi alipofanya kazi na watu wenye vipawa kutoka katika mataifa mbalimbali: “Nilifurahi sana kukutana na watu hao. Nilijifunza kuwaona watu kutoka nchi nyingine kuwa raia wenzangu badala ya kuwaona kuwa ‘wageni.’ Nilianza kuona neno ‘mgeni’ kuwa neno la dharau na nikaweka sheria katika kituo cha CNN ya kwamba neno hilo lisitumiwe katika vipindi vya televisheni au katika mazungumzo ofisini. Badala yake, niliwaamuru watumie neno ‘kimataifa.’”

15 Katika nchi zote duniani, ni Mashahidi wa Yehova peke yao wakiwa kikundi wanaoiga njia ya Mungu ya kufikiri. Kwa sababu wamejifunza kuona mambo kama Yehova anavyoyaona, wamefanikiwa kushinda mawazo na hisia za ubaguzi kuelekea watu wa mataifa mengine. Badala ya kuwatilia shaka, kutowaamini, au hata kuwachukia watu wa mataifa mengine, wamejifunza kuthamini uwezo na sifa mbalimbali za watu hao nao wanaziona kuwa zenye kuvutia. Je, umetafakari kuhusu jambo hilo la pekee na kuona jinsi ambavyo limekunufaisha unaposhughulika na wengine?

ULIMWENGU USIO NA WAGENI

16, 17. Utimizo wa Ufunuo 16:16 na Danieli 2:44 utamaanisha nini kwako?

16 Hivi karibuni mataifa yote yatakabiliana na Yesu Kristo na majeshi yake ya kimbingu katika vita vya mwisho dhidi ya utawala wa Mungu, vita ambavyo ‘vinaitwa katika Kiebrania Har–Magedoni.’ (Ufu. 16:14, 16; 19:11-16) Miaka zaidi ya 2,500 iliyopita, nabii Danieli aliongozwa na roho ya Mungu kutabiri mambo yatakayozipata serikali za wanadamu zinazopinga kusudi la Mungu. Aliandika hivi: “Katika siku za wafalme hao, Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme ambao hautaharibiwa kamwe. Na ufalme huo hautapewa watu wengine wowote. Utazivunja na kuzikomesha falme hizi zote, nao utasimama mpaka wakati usio na kipimo.”—Dan. 2:44.

17 Je, waweza kuwazia manufaa utakayopata wakati unabii huo utakapotimizwa? Hakutakuwa tena na mipaka ya kitaifa iliyowekwa na wanadamu inayomfanya kila mtu awe mgeni kwa njia fulani leo. Tofauti zozote zilizopo za kimaumbile au sifa nyingine za kawaida za kimwili zitaonyesha tu kwamba Mungu aliumba vitu vingi vya aina mbalimbali vyenye kustaajabisha. Tumaini hilo lenye kusisimua linapaswa kutuchochea sote tuendelee kadiri tunavyoweza kumsifu na kumheshimu Muumba wetu, Yehova Mungu.

Je, unatazamia wakati ambapo hakutakuwa tena na mipaka ya kitaifa iliyowekwa na wanadamu, wala hakutakuwa na “mgeni”?

18. Ni matukio gani ya hivi karibuni yanayoonyesha kwamba Mashahidi wa Yehova hawawaoni wengine kuwa “wageni”?

18 Je, ni ndoto tu kuamini kwamba kutakuwa na mabadiliko hayo duniani? Hapana, kwa kweli si ndoto. Kinyume chake, ni jambo linalopatana kabisa na akili kuamini kwamba dunia itabadilika. Hata sasa, Mashahidi wa Yehova hawawaoni wengine kuwa “wageni” kwa sababu hawatilii maanani mataifa ya wale wanaoshirikiana nao. Kwa mfano, hivi karibuni ofisi kadhaa ndogo za Mashahidi wa Yehova ziliunganishwa ili kurahisisha usimamizi katika maeneo hayo na kuwasaidia kutimiza kazi ya kuhubiri habari njema ya Ufalme kwa njia bora zaidi. (Mt. 24:14) Kwa kadiri ambavyo matakwa ya kisheria yaliruhusu, hawakuzingatia mipaka ya kitaifa walipounganisha ofisi hizo. Huo pia ni uthibitisho unaoonyesha wazi kwamba Yesu Kristo, Mtawala aliyetawazwa kihalali na Yehova, anavunja mipaka iliyowekwa na wanadamu, na hivi karibuni ‘atakamilisha ushindi wake’!—Ufu. 6:2.

19. Lugha safi ya kweli imewawezesha watu wa Yehova kuwa na hali gani?

19 Mashahidi wa Yehova wanatoka katika mataifa mengi nao wanazungumza lugha nyingi mbalimbali, lakini wanajitahidi kudumisha lugha safi ya kweli. Lugha hiyo inawawezesha kuwa na kifungo cha umoja ambacho hakiwezi kuvunjwa. (Soma Sefania 3:9.) Mashahidi wa Yehova si sehemu ya mfumo huu mwovu licha ya kwamba wanaishi ndani yake, badala yake wao ni familia moja ya kimataifa. Familia hiyo yenye umoja inaonyesha kwa kadiri ndogo tu jinsi mambo yatakavyokuwa katika ulimwengu utakaokuja ambao hautakuwa na wageni. Kila mtu atakayeishi wakati huo atafurahi kuona ukweli wa maneno haya yaliyosemwa na kitabu kilichonukuliwa awali: “Wanadamu wa jamii zote ni ndugu, kama Biblia inavyosema.”—The Races of Mankind.