Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wewe Ni Msimamizi-nyumba Mwenye Kutegemeka!

Wewe Ni Msimamizi-nyumba Mwenye Kutegemeka!

“Ninyi si mali yenu wenyewe.”—1 KOR. 6:19.

1. Kwa ujumla, ulimwengu una maoni gani kuhusu uhuru?

MIAKA 2,500 hivi iliyopita, mwandishi wa michezo ya kuigiza Mgiriki aliandika hivi: “Hakuna anayekubali kwa hiari kuvaa nira ya utumwa.” Watu wengi leo watakubaliana na maneno hayo. Watu wanaposikia neno “utumwa” wanafikiria kuhusu watu wanaoonewa na walio kifungoni, wanaofanya kazi na kuteseka ili kuwafaidi wale wanaowamiliki, lakini wao wenyewe hawanufaiki.

2, 3. (a) Watumwa au watumishi wa Kristo waliojitolea kwa hiari wanafurahia cheo gani? (b) Tutazungumzia maswali gani kuhusu usimamizi-nyumba?

2 Hata hivyo, Yesu alionyesha kwamba wanafunzi wake wangekuwa watumishi wanyenyekevu, au watumwa. Lakini wakiwa watumwa, Wakristo wa kweli hawadharauliwi au kuonewa. Watumwa hao wanafurahia cheo cha heshima, staha, nao wanaaminiwa. Kwa mfano, muda mfupi kabla ya kifo Chake, fikiria yale ambayo Yesu alisema kuhusu “mtumwa” fulani. Kristo alitabiri kwamba angempa majukumu “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.”—Mt. 24:45-47.

3 Tunapaswa kuzingatia kwamba katika simulizi la Luka, mtumwa huyo anaitwa “msimamizi-nyumba.” (Soma Luka 12:42-44.) Wakristo wengi waaminifu walio hai sasa si sehemu ya jamii ya msimamizi-nyumba mwaminifu. Hata hivyo, Maandiko yanaonyesha kwamba wote wanaomtumikia Mungu wana majukumu ya usimamizi-nyumba. Ni majukumu gani hayo? Wanapaswa kuyaonaje? Ili kupata majibu, acheni tuchunguze jukumu la wasimamizi-nyumba katika nyakati za kale.

JUKUMU LA WASIMAMIZI-NYUMBA

4, 5. Ni majukumu gani waliyokuwa nayo wasimamizi-nyumba katika nyakati za kale? Toa mifano.

4 Katika nyakati za kale, mara nyingi msimamizi-nyumba alikuwa mtumwa aliyeaminiwa na kupewa mgawo wa kusimamia nyumba au biashara za bwana wake. Kwa kawaida, wasimamizi-nyumba walikuwa na mamlaka kubwa nao walikabidhiwa jukumu la kusimamia mali, pesa, na watumishi wengine nyumbani. Tunaweza kuona jambo hilo katika kisa cha Eliezeri, aliyekabidhiwa jukumu la kutunza mali nyingi za Abrahamu. Huenda Abrahamu alimtuma Eliezeri huko Mesopotamia ili amtafutie mke Isaka, mwana wake. Huo ulikuwa mgawo mkubwa na muhimu kama nini!—Mwa. 13:2; 15:2; 24:2-4.

5 Yosefu, mwana wa mjukuu wa Abrahamu aliisimamia nyumba ya Potifa. (Mwa. 39:1, 2) Baadaye, Yosefu akawa na msimamizi-nyumba wake mwenyewe, aliyewekwa “juu ya nyumba ya Yosefu.” Msimamizi-nyumba huyo aliwakaribisha ndugu kumi wa Yosefu. Na kwa amri ya Yosefu, alipanga mambo kuhusiana na kikombe cha fedha “kilichoibwa.” Ni wazi kwamba wasimamizi-nyumba waliaminiwa na kukabidhiwa majukumu makubwa.—Mwa. 43:19-25; 44:1-12.

6. Ni usimamizi-nyumba wa aina gani walio nao wazee tofauti-tofauti Wakristo?

6 Karne nyingi baadaye, mtume Paulo aliandika kwamba waangalizi Wakristo wangekuwa ‘wasimamizi-nyumba wa Mungu.’ (Tito 1:7) Wakiwa wamewekwa rasmi kulichunga “kundi la Mungu,” waangalizi hutoa mwelekezo na kuongoza katika makutaniko. (1 Pet. 5:1, 2) Bila shaka, majukumu yao yanatofautiana. Kwa mfano, waangalizi wengi Wakristo leo hutumika katika kutaniko moja. Waangalizi wanaosafiri hutumikia makutaniko mengi. Nao washiriki wa Halmashauri za Tawi wanashughulikia makutaniko katika nchi nzima-nzima. Lakini wote wanatazamiwa kutimiza majukumu yao kwa uaminifu; ni lazima wote ‘watoe hesabu’ kwa Mungu.—Ebr. 13:17.

7. Tunajuaje kwamba kwa njia fulani Wakristo wote ni wasimamizi-nyumba?

7 Lakini vipi Wakristo wengi washikamanifu ambao si waangalizi? Mtume Petro aliwaandikia barua Wakristo kwa ujumla, akisema hivi: “Kwa kadiri ambayo kila mmoja amepokea zawadi, itumieni katika kuhudumiana kama wasimamizi-nyumba wazuri wa fadhili zisizostahiliwa za Mungu zinazoonyeshwa kwa njia mbalimbali.” (1 Pet. 1:1; 4:10) Kwa fadhili zake zisizostahiliwa, Mungu amempa kila mmoja wetu zawadi, mali, uwezo, au vipawa tunavyoweza kutumia ili kuwanufaisha waamini wenzetu. Kwa hiyo, wote wanaomtumikia Mungu ni wasimamizi-nyumba, na kwa sababu ya usimamizi-nyumba huo, wanaheshimiwa, wanaaminiwa, na kukabidhiwa majukumu.

SISI NI MALI YA MUNGU

8. Ni kanuni gani moja muhimu tunayopaswa kukumbuka?

8 Tutazungumzia sasa kanuni tatu ambazo tunahitaji kufikiria tukiwa wasimamizi-nyumba. Kwanza: Sisi sote ni mali ya Mungu na tunawajibika kwake. Paulo aliandika hivi: “Ninyi si mali yenu wenyewe, kwa maana mlinunuliwa kwa bei,” yaani, kwa damu ya Kristo iliyotolewa dhabihu. (1 Kor. 6:19, 20) Kwa kuwa sisi ni mali ya Yehova, tuna wajibu wa kutii amri zake, ambazo si mzigo mzito. (Rom. 14:8; 1 Yoh. 5:3) Tunakuwa pia watumwa wa Kristo. Kama wasimamizi-nyumba wa zamani, tunapewa uhuru mwingi—lakini uhuru wetu una mipaka. Ni lazima tutimize majukumu yetu kama tulivyoagizwa. Hata iwe tuna mapendeleo gani ya utumishi, bado sisi ni watumishi wa Mungu na wa Kristo.

9. Yesu alitumia mfano gani kuonyesha uhusiano uliopo kati ya bwana na mtumwa?

9 Yesu anatusaidia kuelewa uhusiano uliopo kati ya bwana na mtumwa. Wakati mmoja aliwaambia wanafunzi wake kuhusu mtumwa aliyerudi nyumbani baada ya kufanya kazi siku nzima. Je, bwana wake anasema: “Njoo hapa mara moja uketi mezani”? Hapana. Anasema: “Nitayarishie kitu ili nipate mlo wangu wa jioni, nawe jifunge unihudumie mpaka niwe nimemaliza kula na kunywa, kisha unaweza kula na kunywa.” Yesu aliutumiaje mfano huo? “Ndivyo na ninyi, pia, wakati mmefanya mambo yote mliyoagizwa, semeni, ‘Sisi ni watumwa wasiofaa kitu. Jambo ambalo tumefanya ndilo tulilopaswa kufanya.’”—Luka 17:7-10.

10. Ni nini kinachoonyesha kwamba Yehova anathamini jitihada zetu za kumtumikia?

10 Bila shaka, Yehova anathamini jitihada zetu za kumtumikia. Biblia inatuhakikishia hivi: “Mungu hakosi kuwa mwadilifu hivi kwamba asahau kazi yenu na upendo mlioonyesha kwa ajili ya jina lake.” (Ebr. 6:10) Yehova hatarajii tufanye mambo tusiyoweza. Isitoshe, mambo yote anayotuambia tufanye ni kwa faida yetu na si yenye kulemea kamwe. Hata hivyo, kulingana na mfano wa Yesu, mtumwa hajipendezi mwenyewe na kutanguliza mapendezi yake. Somo ni kwamba tunapojiweka wenyewe wakfu kwa Mungu, tunachagua kutanguliza mapenzi yake maishani mwetu. Je, hukubaliani na hilo?

MAMBO AMBAYO YEHOVA ANATAKA SOTE TUTIMIZE

11, 12. Tukiwa wasimamizi-nyumba, ni lazima tuonyeshe sifa gani, na tunapaswa kuepuka nini?

11 Kanuni ya pili ni hii: Tukiwa wasimamizi-nyumba, sote tunafuata viwango vilevile vya msingi. Ni kweli kwamba ni watu wachache wanaopewa majukumu fulani katika kutaniko la Kikristo. Hata hivyo, majukumu mengi yanatimizwa na Wakristo wote. Kwa mfano, tukiwa wanafunzi wa Kristo na Mashahidi wa Yehova tunaamriwa tupendane. Yesu alisema upendo ndio unaowatambulisha Wakristo wa kweli. (Yoh. 13:35) Hata hivyo, tunawapenda pia watu ambao si ndugu zetu. Tunajitahidi kuwaonyesha upendo wale ambao si waamini wenzetu. Hilo ni jambo ambalo sote tunaweza na tunapaswa kufanya.

12 Tunapaswa pia kuwa na mwenendo mzuri. Tunapaswa kuepuka mwenendo na mtindo wa maisha unaoshutumiwa katika Neno la Mungu. Paulo aliandika hivi: “Wala waasherati, wala waabudu-sanamu, wala wazinzi, wala wanaume wanaowekwa kwa ajili ya makusudi yasiyo ya asili, wala wanaume wanaolala na wanaume, wala wezi, wala watu wenye pupa, wala walevi, wala watukanaji, wala wanyang’anyi hawataurithi ufalme wa Mungu.” (1 Kor. 6:9, 10) Ni kweli kwamba jitihada zinahitajiwa ili kuishi kupatana na viwango vya uadilifu vya Mungu. Hata hivyo, jitihada hizo si za bure, zinatunufaisha sana, kwa mfano, tunakuwa na mtindo wa maisha unaotusaidia kuwa na afya nzuri, uhusiano mzuri na wengine, na msimamo mzuri mbele za Mungu.—Soma Isaya 48:17, 18.

13, 14. Wakristo wote wamepewa jukumu gani, nasi tunapaswa kulionaje?

13 Kumbuka pia kwamba msimamizi-nyumba alikuwa na kazi ya kufanya. Sisi pia tunayo. Tumepewa zawadi yenye thamani ya ujuzi wa kweli. Mungu anatarajia tuwafundishe wengine ujuzi huo. (Mt. 28:19, 20) Paulo aliandika hivi: “Acheni mtu atukadirie sisi hivyo kuwa tuko chini ya Kristo nasi ni wasimamizi-nyumba wa siri takatifu za Mungu.” (1 Kor. 4:1) Paulo alitambua kuwa usimamizi-nyumba wake ulimaanisha kwamba alipaswa kutunza kwa uangalifu sana “siri takatifu” na kuwafundisha wengine kwa uaminifu siri hizo kulingana na mwongozo wa Bwana-Mkubwa, Yesu Kristo.—1 Kor. 9:16.

14 Kwa kweli, tunaonyesha upendo tunapowafundisha wengine kweli. Bila shaka, kila Mkristo ana hali tofauti. Wote hawawezi kutimiza mambo yaleyale katika huduma. Yehova anaelewa hilo. Jambo muhimu ni kufanya kibinafsi yote tuwezayo. Tunapofanya hivyo tunaonyesha upendo usio wa kichoyo kuelekea Mungu na jirani yetu.

UMUHIMU WA KUWA MWAMINIFU

15-17. (a) Kwa nini ni jambo muhimu kwa msimamizi-nyumba kuwa mwaminifu? (b) Yesu alitoa mfano gani kuonyesha matokeo ya kukosa uaminifu?

15 Kanuni ya tatu inayohusiana sana na kanuni mbili tulizozungumzia ni hii: Ni lazima tuwe waaminifu, wenye kutegemeka. Msimamizi-nyumba anaweza kuwa na uwezo na sifa nyingi nzuri, hata hivyo, sifa zote hizo hazina maana ikiwa hatimizi jukumu lake au si mshikamanifu kwa bwana wake. Uaminifu ni muhimu ili kuwa msimamizi-nyumba mzuri na mwenye mafanikio. Kumbuka kwamba Paulo aliandika hivi: “Kinachoangaliwa katika wasimamizi-nyumba ni mtu kupatwa akiwa mwaminifu.”—1 Kor. 4:2.

16 Tukiwa waaminifu, bila shaka tutathawabishwa. Ikiwa sisi si waaminifu, tutapoteza kila kitu. Tunaona kanuni hiyo katika mfano wa Yesu wa talanta. Watumwa waliotumia pesa za bwana wao ‘kufanya biashara’ kwa uaminifu walipongezwa na kubarikiwa sana. Mtumwa ambaye hakujali mali aliyokabidhiwa na bwana wake alihukumiwa kuwa “mwovu,” “goigoi,” na “asiyefaa kitu.” Ile talanta aliyopewa ilichukuliwa, naye akatupwa nje.—Soma Mathayo 25:14-18, 23, 26, 28-30.

17 Pindi nyingine, Yesu alionyesha matokeo ya kutokuwa mwaminifu. Alisema hivi: “Mtu fulani alikuwa tajiri naye alikuwa na msimamizi-nyumba, na huyo akashtakiwa kwake kuwa anapoteza mali zake. Kwa hiyo akamwita na kumwambia, ‘Ni nini hili ninalosikia juu yako? Toa hesabu ya usimamizi wako, kwa maana huwezi tena kuisimamia nyumba.’” (Luka 16:1, 2) Kwa kuwa msimamizi-nyumba huyo alitumia vibaya mali ya bwana wake, bwana huyo alimfukuza. Ni somo muhimu kama nini kwetu! Bila shaka, hatutaki kamwe kukosa uaminifu katika majukumu tunayopewa.

JE, NI JAMBO LA HEKIMA KUJILINGANISHA NA WENGINE?

18. Kwa nini hatupaswi kujilinganisha na wengine?

18 Kila mmoja wetu anaweza kujiuliza hivi: ‘Ninauonaje usimamizi-nyumba wangu?’ Matatizo yanaweza kutokea tukijilinganisha na wengine. Biblia inatushauri hivi: “Kila mmoja na athibitishe kazi yake mwenyewe ni nini, kisha atakuwa na sababu ya kufurahi kwa habari yake mwenyewe peke yake, na si kwa kujilinganisha na mtu yule mwingine.” (Gal. 6:4) Badala ya kulinganisha yale tunayofanya na yale ambayo wengine wanafanya, tunapaswa kukazia fikira yale ambayo sisi binafsi tunaweza kufanya. Hilo litatulinda ili tusijitutumue kwa kiburi na pia tusivunjike moyo. Tunapojichunguza, tunapaswa kutambua kwamba hali hubadilika. Huenda kwa sababu ya umri, afya mbaya, au majukumu mbalimbali, hatuwezi kufanya mambo yote tuliyofanya zamani. Kwa upande mwingine, huenda tukafanya mengi zaidi kuliko yale tunayofanya sasa. Ikiwa ndivyo ilivyo, kwa nini tusijaribu kuongeza utendaji wetu?

19. Kwa nini hatupaswi kuvunjika moyo tusipopata pendeleo fulani?

19 Jambo lingine la kufikiria ni mapendeleo tuliyonayo au tunayotamani sana kuwa nayo. Kwa mfano, huenda ndugu akatamani kutumikia akiwa mzee katika kutaniko au kupewa hotuba katika makusanyiko. Ni jambo linalofaa kujitahidi sana kustahili kupata mapendeleo kama hayo, hata hivyo, hatupaswi kuvunjika moyo ikiwa hatupati mapendeleo tuliyotumaini kupata. Kwa sababu ambazo huenda tusielewe kwa sasa, huenda tukapata mapendeleo fulani baada ya muda mrefu kuliko tulivyotarajia. Kumbuka kwamba Musa alionekana kuwa tayari kuwaongoza Waisraeli kutoka Misri, lakini alihitaji kusubiri kwa miaka 40 kabla ya kufanya hivyo. Jambo hilo lilimpa wakati wa kutosha kusitawisha sifa alizohitaji ili kuwaongoza watu hao waasi na wenye shingo ngumu.—Mdo. 7:22-25, 30-34.

20. Tunajifunza nini kutokana na simulizi la Yonathani?

20 Wakati mwingine huenda tusipate kabisa pendeleo fulani. Mambo yalikuwa hivyo kwa Yonathani. Alikuwa mwana wa Sauli na kwa hiyo angekuwa mfalme wa taifa lote la Israeli. Hata hivyo, Mungu alimchagua Daudi, mwanamume mwenye umri mdogo zaidi, awe mfalme. Yonathani aliuonaje uamuzi huo? Aliukubali uamuzi huo na kumuunga mkono Daudi hata uhai wake ulipokuwa hatarini. Alimwambia hivi Daudi: “Wewe utakuwa mfalme juu ya Israeli, na mimi nitakuwa wa pili kwako.” (1 Sam. 23:17) Je, umeona wazo kuu? Yonathani aliikubali hali yake, na tofauti na baba yake, hakumwonea wivu Daudi. Badala ya kuwaonea wengine wivu kwa sababu ya migawo waliyopewa, sisi sote tunaweza kujitahidi kutimiza majukumu tuliyonayo. Tunaweza kuwa na hakika kwamba katika ulimwengu mpya, Yehova atahakikisha kwamba tamaa nzuri za watumishi wake wote zinatoshelezwa.

21. Tunapaswa kuuonaje usimamizi-nyumba wetu?

21 Acheni tukumbuke kwamba tukiwa wasimamizi-nyumba wenye kutegemeka, hatuko chini ya utumwa mbaya unaokandamiza na kutufanya tutoe machozi. Sivyo mambo yalivyo. Tunafurahia pendeleo lenye heshima kubwa kwa kuwa tumekabidhiwa kazi ambayo haitarudiwa tena ya kutangaza habari njema katika siku za mwisho za mfumo huu wa mambo. Tunapofanya kazi hiyo, tunafurahia uhuru mkubwa katika kutimiza majukumu yetu. Acheni basi, tuwe wasimamizi-nyumba waaminifu. Na tuthamini pendeleo tulilonalo la kumtumikia Yehova ambaye ni Mkuu zaidi katika ulimwengu wote.