Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Huu Ni Urithi Wetu wa Kiroho

Huu Ni Urithi Wetu wa Kiroho

“Huu ndio urithi wa watumishi wa Yehova.”—ISA. 54:17, Byington.

1. Kwa upendo Yehova amehifadhi nini kwa faida ya wanadamu?

YEHOVA, “Mungu aliye hai na anayedumu,” amehifadhi ujumbe wake unaookoa uhai kwa faida ya wanadamu. Bila shaka utadumu kwa sababu “neno la Yehova linadumu milele.” (1 Pet. 1:23-25) Tunashukuru kama nini kwamba kwa upendo Yehova amehifadhi ujumbe huo muhimu katika Neno lake lililoandikwa, Biblia!

2. Mungu amehifadhi nini katika Neno lake lililoandikwa kwa ajili ya watu wake?

2 Mungu amehifadhi katika Neno lake jina ambalo yeye mwenyewe alijichagulia ili watu wake walitumie. Maandiko yanamtaja “Yehova Mungu” kwa mara ya kwanza wakati wa “historia ya mbingu na dunia.” (Mwa. 2:4) Jina la Mungu lilichongwa kimuujiza mara kadhaa kwenye yale mabamba ya mawe yenye Amri Kumi. Kwa mfano, amri ya kwanza ilianza kwa kusema: “Mimi ni Yehova Mungu wako.” (Kut. 20:1-17) Jina la Mungu limedumu kwa sababu Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova amelihifadhi Neno lake na jina lake licha ya jitihada zote za Shetani za kuliondolea mbali.—Zab. 73:28.

3. Mungu amehifadhi nini licha ya kwamba uwongo wa kidini umeenea sana?

3 Yehova amehifadhi pia kweli katika Neno lake. Ingawa uwongo wa kidini umeenea sana ulimwenguni pote, tunashukuru kama nini kwamba Mungu ametupatia kweli na nuru ya kiroho! (Soma Zaburi 43:3, 4.) Wanadamu wengi wanatembea katika giza, lakini sisi tunaendelea kutembea kwa shangwe katika nuru tuliyopewa na Mungu.—1 Yoh. 1:6, 7.

TUNA URITHI TUNAOPASWA KUTHAMINI

4, 5. Tumekuwa na pendeleo gani la pekee tangu mwaka wa 1931?

4 Tukiwa Wakristo, tuna urithi wenye thamani. Kamusi moja (Collins Cobuild English Dictionary) inasema hivi: “Urithi wa nchi ni desturi zote, tamaduni, au mitindo ya maisha ya nchi hiyo ambayo imekuwapo kwa miaka  mingi na kupitishwa kutoka kizazi kimoja hadi kingine.” Urithi wetu wa kiroho unatia ndani baraka ya kuwa na ujuzi sahihi wa Neno la Mungu na kuelewa kwa usahihi ukweli kumhusu Mungu na makusudi yake. Pia, unatia ndani pendeleo fulani la pekee sana.

Tulisisimka kulikubali jina Mashahidi wa Yehova kwenye kusanyiko letu la wilaya la mwaka wa 1931

5 Pendeleo hilo lilikuja kuwa sehemu ya urithi wetu wa kiroho mwaka wa 1931 kwenye kusanyiko letu la wilaya huko Columbus, Ohio, Marekani. Programu ya kusanyiko hilo ilikuwa na herufi “JW.” Dada mmoja alisema hivi: “Tulikisia-kisia kuhusu maana ya herufi JW, tukifikiri zinamaanisha, Ngoja tu (Just Wait), Kesha tu (Just Watch), na wengine wakakisia maana sahihi.” Tulikuwa tukiitwa Wanafunzi wa Biblia, lakini Jumapili, Julai 26, 1931, tulipitisha azimio la kuitwa Mashahidi wa Yehova. Tulisisimka sana kuitwa kwa jina hilo la Kimaandiko. (Soma Isaya 43:12.) Ndugu mmoja alikumbuka hivi: “Sitasahau kamwe shangwe na makofi mengi yaliyopigwa katika kusanyiko hilo.” Hakuna kikundi kingine chochote ulimwenguni kilichotaka kuitwa kwa jina hilo, lakini Mungu ametubariki kwa kuturuhusu tulitumie kwa miaka zaidi ya themanini. Ni pendeleo la pekee kama nini kuwa Mashahidi wa Yehova!

6. Urithi wetu wa kiroho unatia ndani habari gani sahihi?

6 Urithi wetu wa kiroho unatia ndani habari nyingi sana zenye thamani na zilizo sahihi kuhusu watumishi wa kale wa Mungu. Kwa mfano, mfikirie Abrahamu, Isaka, na Yakobo. Bila shaka, wazee hao wa ukoo walizungumza na familia zao kuhusu jinsi ya kumpendeza Yehova. Basi haishangazi kwamba Yosefu aliyekuwa mwadilifu alikataa kufanya uasherati ili ‘asimtendee Mungu dhambi.’ (Mwa. 39:7-9) Mapokeo ya Kikristo yalipitishwa pia kwa matendo au mafundisho. Mambo hayo yalitia ndani miongozo kuhusu Mlo wa Jioni wa Bwana ambayo mtume Paulo aliyapatia makutaniko ya Kikristo. (1 Kor. 11:2, 23) Leo, Neno la Mungu lililoandikwa linatia ndani miongozo ya kutusaidia kumwabudu Mungu “kwa roho na kweli.” (Soma Yohana 4:23, 24.) Biblia imekusudiwa kuwaelimisha wanadamu wote, lakini sisi tukiwa watumishi wa Yehova tunaithamini sana.

7. Urithi wetu unatia ndani ahadi gani inayotia moyo?

7 Kwa sehemu, urithi wetu wa kiroho unatia ndani masimulizi yaliyochapishwa hivi karibuni yanayothibitisha kwamba ‘Yehova yuko upande wetu.’ (Zab. 118:7) Urithi huo unatufanya tuhisi tukiwa salama, hata tunapoteswa. Urithi wetu wa kiroho unaozidi kuongezeka unatia ndani ahadi hii yenye kutia moyo: “‘Silaha yoyote itakayofanywa juu yako haitafanikiwa, na ulimi wowote utakaoinuka juu yako katika hukumu wewe utauhukumu. Hilo ndilo fungu la urithi [au, “urithi,” By] la watumishi wa Yehova, na uadilifu wao ni kutoka kwangu,’ asema Yehova.” (Isa. 54:17) Shetani hana silaha  yoyote inayoweza kutuletea madhara ya kudumu.

8. Tutachunguza nini katika makala hii na inayofuata?

8 Shetani amejaribu kuliangamiza Neno la Mungu, kuliondolea mbali jina la Yehova, na kuificha kweli. Lakini bila shaka hawezi kamwe kulinganishwa na Yehova ambaye amekomesha kabisa jitihada hizo zote. Katika makala hii na inayofuata, tutaona (1) jinsi ambavyo Mungu amelihifadhi Neno lake; (2) jinsi ambavyo Yehova amelilinda jina lake; na (3) jinsi Baba yetu wa mbinguni alivyo Chanzo na Mhifadhi wa kweli tunayofurahia.

YEHOVA AMELIHIFADHI NENO LAKE

9-11. Ni mifano gani inayoonyesha kwamba Biblia imehifadhiwa licha ya jitihada zote za kuiangamiza?

9 Yehova amelihifadhi Neno lake licha ya jitihada zote za kuliangamiza. Kitabu kimoja (Catholic Encyclopedia) kinasema hivi: ‘Katika mwaka wa 1229, Baraza la Toulouse liliwapiga marufuku watu wa kawaida wasitumie Biblia za lugha za kienyeji katika jitihada za kanisa za kupambana na Waalbigene na Wawaldo. Mkutano uliofanywa mwaka wa 1234 huko Tarragona, Hispania, chini ya usimamizi wa James wa Kwanza ulitoa amri kama hiyo. Baraza Kuu la Maaskofu Wakatoliki lilizungumzia jambo hilo kwa mara ya kwanza mwaka wa 1559, wakati Orodha ya Paulo wa Nne ilipopiga marufuku uchapishaji na umiliki wa Biblia za lugha za kienyeji bila ruhusa ya Ofisi Takatifu.’

10 Biblia imehifadhiwa licha ya jitihada zote za kutaka kuiangamiza. Yapata mwaka wa 1382, John Wycliffe na wenzake walitafsiri Biblia ya kwanza katika Kiingereza. William Tyndale aliyekuwa pia mtafsiri wa Biblia aliuawa mwaka wa 1536. Inasemekana kwamba alipaaza sauti hivi huku akiwa amefungwa mtini: “Bwana, yafungue macho ya mfalme wa Uingereza.” Kisha akanyongwa na kuchomwa moto.

11 Biblia imedumu licha ya upinzani. Kwa mfano, mwaka wa 1535, Miles Coverdale alitafsiri Biblia ya Kiingereza. Coverdale alitumia tafsiri ya Tyndale ya “Agano Jipya” na “Agano la Kale,” kuanzia kitabu cha Mwanzo hadi kitabu cha Mambo ya Nyakati. Alitafsiri sehemu nyingine za Maandiko kutoka katika Biblia ya Kilatini na Biblia ya Kijerumani ya Martin Luther. Leo, Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya inathaminiwa kwa sababu ni tafsiri sahihi, inayoeleweka kwa urahisi, na inayotusaidia sana katika huduma yetu. Tunafurahi kwamba hakuna roho yeyote mwovu au mwanadamu yeyote mwenye mamlaka anayeweza kumzuia Yehova asilihifadhi Neno lake.

YEHOVA AMELIHIFADHI JINA LAKE

Watu kama vile Tyndale walitoa uhai wao kwa ajili ya Neno la Mungu

12. Tafsiri ya Ulimwengu Mpya imetimiza sehemu gani katika kulihifadhi jina la Mungu?

12 Yehova Mungu amehakikisha kwamba  jina lake limehifadhiwa katika Neno lake. Tafsiri ya Ulimwengu Mpya inatimiza kusudi hilo kwa njia muhimu sana. Katika utangulizi wa tafsiri hiyo, halmashauri ya watafsiri waliojitolea kwa moyo wote waliandika hivi: “Jambo linalotokeza zaidi katika tafsiri hii ni kule kulirudisha jina la Mungu mahali pake panapofaa katika maandishi ya Biblia. Jambo hilo limefanywa kwa kutumia jina ‘Yehova’ ambalo linakubalika na wengi katika Kiswahili, mara 6,973 katika Maandiko ya Kiebrania na mara 237 katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo.” Tafsiri ya Ulimwengu Mpya inapatikana sasa ikiwa nzima au sehemu, katika lugha zaidi ya 116, na nakala zaidi ya 178,545,862 zimechapishwa.

13. Kwa nini tunaweza kusema kwamba wanadamu wamelijua jina la Mungu tangu walipoumbwa?

13 Wanadamu wamelijua jina la Mungu tangu walipoumbwa. Adamu na Hawa walijua jina hilo, na hata walijua jinsi ya kulitamka. Hamu alipomkosea heshima baba yake baada ya Gharika, Noa alisema hivi: “Abarikiwe Yehova, Mungu wa Shemu, Kanaani [mwana wa Hamu] na awe mtumwa wake.” (Mwa. 4:1; 9:26) Mungu mwenyewe alitangaza hivi: “Mimi ni Yehova. Hilo ni jina langu; nami sitampa mwingine yeyote utukufu wangu mwenyewe.” Mungu alisema hivi pia: “Mimi ni Yehova, na hakuna mwingine yeyote. Zaidi ya mimi hakuna Mungu.” (Isa. 42:8; 45:5) Yehova amehakikisha kwamba jina lake limehifadhiwa na watu duniani pote wamejulishwa jina hilo. Tuna pendeleo kubwa kama nini la kutumia jina Yehova na kumtumikia tukiwa Mashahidi wake! Ni kana kwamba tunapaaza sauti hivi: “Tutainua bendera zetu katika jina la Mungu wetu.”—Zab. 20:5.

14. Mbali na Biblia, jina la Mungu linaweza kupatikana wapi pengine?

14 Jina la Mungu halipatikani katika Biblia tu. Fikiria Jiwe la Moabu, lililopatikana huko Dhiban (Dibon), kilomita 21 upande wa mashariki wa Bahari ya Chumvi. Jiwe hilo linamtaja Mfalme Omri wa Israeli na lina masimulizi ya Mfalme Mesha wa Moabu kuhusu uasi wake dhidi ya Israeli. (1 Fal. 16:28; 2 Fal. 1:1; 3:4, 5) Lakini Jiwe la Moabu ni la pekee kwa sababu jina la Mungu limeandikwa juu yake kwa herufi za Tetragramatoni. Herufi hizo zinaonekana mara kadhaa katika Barua za Lakishi, yaani, vigae vya udongo vilivyopatikana katika nchi ya Israel.

15. Septuajinti ni nini, na kwa nini ilitafsiriwa?

15 Watafsiri wa awali wa Biblia walisaidia sana kulihifadhi jina la Mungu. Baada ya Wayahudi kukaa uhamishoni huko Babiloni kuanzia mwaka wa 607 K.W.K. hadi 537 K.W.K., wengi wao hawakurudi Yuda na Israeli. Kufikia karne ya tatu K.W.K., jiji la Alexandria, huko Misri, lilikuwa na Wayahudi wengi waliotaka Maandiko ya Kiebrania yatafsiriwe katika Kigiriki, iliyokuwa lugha ya kimataifa. Tafsiri hiyo iliyokamilishwa katika karne ya pili K.W.K., inaitwa Septuajinti. Nakala fulani za tafsiri hiyo zina jina Yehova katika Kiebrania.

16. Toa mfano unaoonyesha matumizi ya jina la Mungu katika kitabu kilichochapishwa kwa mara ya kwanza mwaka wa 1640.

16 Jina la Mungu linapatikana katika kitabu kinachoitwa Bay Psalm, kitabu cha kwanza katika koloni za Uingereza huko Amerika. Kitabu cha kwanza (kilichochapishwa mwaka wa 1640) kina Zaburi zilizoandikwa katika Kiebrania na kutafsiriwa katika Kiingereza cha wakati huo. Kinatumia jina la Mungu katika maandiko kama vile Zaburi 1:1, 2, inayosema kwamba “mtu aliyebarikiwa” hatembei katika shauri la waovu, “lakini anapendezwa sana na sheria ya Iehovah.” Unaweza kupata habari zaidi kuhusu jina la Mungu katika broshua yenye kichwa Jina la Mungu Litakaloendelea Milele.

YEHOVA AHIFADHI KWELI YA KIROHO

17, 18. (a) “Kweli” ni nini? (b) “Kweli ya habari njema” inatia ndani nini?

17 Tunamtumikia kwa furaha “Yehova  Mungu wa ukweli.” (Zab. 31:5) Kamusi moja inasema “ukweli kuhusu kitu fulani ni mambo yote ya hakika kuhusu kitu hicho, wala si mambo ya kubuniwa au ya kuwaziwa.” Katika Kiebrania cha Biblia, neno ambalo mara nyingine limetafsiriwa kuwa “ukweli” linahusu kitu ambacho ni hakika, chenye kuaminika, au kinachotegemeka. Neno la Kigiriki linalotafsiriwa kuwa “ukweli” linarejelea jambo ambalo linapatana na mambo ya hakika au yanayofaa na yaliyo sawa.

18 Yehova amehifadhi kweli ya kiroho na kuhakikisha kwamba tunaendelea kupata ujuzi huo kwa wingi zaidi. (2 Yoh. 1, 2) Uelewaji wetu wa kweli unazidi kuwa wazi zaidi, kwa kuwa “njia ya waadilifu ni kama nuru inayong’aa, inayozidi kuongezeka mpaka mchana mkamilifu”! (Met. 4:18) Bila shaka, tunakubaliana kabisa na Yesu aliyesema hivi aliposali kwa Mungu: “Neno lako ni kweli.” (Yoh. 17:17) Neno la Mungu lililoandikwa lina “kweli ya habari njema,” ambayo ni mafundisho yote ya Kikristo kwa ujumla. (Gal. 2:14) Kweli hiyo inatia ndani mambo ya hakika kuhusu jina la Yehova, enzi yake kuu, dhabihu ya fidia ya Yesu, ufufuo, na Ufalme. Acheni sasa tuchunguze jinsi ambavyo Mungu amehifadhi kweli hiyo licha ya jitihada za Shetani za kuificha.

YEHOVA AZUIA JITIHADA ZA KUIFICHA KWELI

19, 20. Nimrodi alikuwa nani, naye alipanga njama gani katika siku zake ambayo haikufaulu?

19 Baada ya Gharika, kulikuwa na msemo huu: “Kama tu Nimrodi, mwindaji mwenye nguvu kwa kumpinga Yehova.” (Mwa. 10:9) Kwa sababu alimpinga Yehova Mungu, Nimrodi alimwabudu Shetani, na alikuwa kama wapinzani ambao Yesu aliwaambia hivi: “Ninyi mmetoka kwa baba yenu Ibilisi, nanyi mnataka kufanya tamaa za baba yenu. Huyo . . . hakusimama imara katika kweli.”—Yoh. 8:44.

20 Utawala wa Nimrodi ulitia ndani Babeli na majiji mengine kati ya Mto Tigri na Mto Efrati. (Mwa. 10:10) Inawezekana kwamba yeye ndiye aliyeamuru jiji na mnara wa Babeli ujengwe kuanzia mwaka wa 2269 K.W.K. hivi. Kinyume kabisa na mapenzi ya Yehova kwamba wanadamu watawanyike duniani kote, wajenzi hao walisema hivi: “Haya! Na tujijengee jiji na pia mnara na kilele chake kiwe mbinguni, na tujifanyie jina maarufu, tusije tukatawanyika juu ya uso wote wa dunia.” Lakini mpango huo ulikatishwa Mungu ‘alipovuruga lugha ya dunia yote’ na kuwatawanya watu waliotaka kujenga mnara huo. (Mwa. 11:1-4, 8, 9) Ikiwa huo ulikuwa mpango wa Shetani wa kuanzisha dini moja ili kila mtu amwabudu yeye, njama yake haikufaulu kamwe. Katika historia yote ya wanadamu, ibada ya Yehova imesitawi na inaendelea kuenea siku baada ya siku.

21, 22. (a) Kwa nini dini ya uwongo haijawahi kamwe kuwa tisho kubwa kwa ibada ya kweli? (b) Tutachunguza nini katika makala inayofuata?

21 Dini ya uwongo haijawahi kamwe kuwa tisho kubwa kwa ibada ya kweli. Kwa nini? Kwa sababu Mfundishaji wetu Mkuu amehakikisha kwamba Neno lake lililoandikwa limehifadhiwa, amewajulisha wanadamu jina lake, na amekuwa Chanzo kisicho na mwisho cha kweli ya kiroho. (Isa. 30:20, 21) Kumwabudu Mungu kupatana na kweli hutuletea shangwe, hata hivyo, ni lazima tuendelee kukesha kiroho huku tukimtegemea kabisa Yehova na kufuata mwongozo wa roho yake takatifu.

22 Katika makala inayofuata, tutachunguza jinsi baadhi ya mafundisho ya uwongo yalivyoanza. Tutaona kwamba mafundisho hayo hayapatani kamwe na Maandiko. Zaidi ya hayo, tutaona jinsi ambavyo Yehova, yule Mhifadhi asiye na kifani wa ile kweli, ametubariki kwa kutupatia mafundisho ya kweli tunayothamini sana na ambayo ni sehemu ya urithi wetu wa kiroho.