Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Wajua?

Je, Wajua?

Je, hekalu la Yerusalemu liliwahi kujengwa upya baada ya mwaka wa 70 W.K.?

YESU alisema kwamba hakuna jiwe hata moja ambalo lingeachwa juu ya jiwe lingine katika hekalu la Yehova. Unabii huo ulitimia wakati jeshi la Waroma chini ya Tito lilipoharibu Yerusalemu mwaka wa 70 W.K. (Mt. 24:2) Baadaye, Maliki Juliano alifanya mipango ya kujenga upya hekalu hilo.

Inasemekana kwamba Juliano ndiye aliyekuwa maliki wa mwisho wa Roma aliyekuwa mpagani. Inadaiwa kwamba mpwa huyo wa Konstantino Mkuu alipata ile inayoitwa elimu ya Kikristo. Lakini alipotangazwa kuwa maliki mwaka wa 361 W.K., alikataa waziwazi elimu hiyo na Ukristo bandia katika siku zake, na kuamua kuwa mpagani. Vitabu vya historia vinamwita “yule Mwasi-Imani.”

Juliano alichukia sana Ukristo. Huenda sababu moja iliyomfanya auchukie ni kwamba alipokuwa na umri wa miaka sita, aliwaona wawakilishi wa Ukristo wakimuua baba yake na watu wa jamaa yake. Kulingana na wanahistoria wa kanisa, Juliano aliwatia moyo Wayahudi kujenga upya hekalu lao, akiamini kwamba kufanya hivyo kungethibitisha kwamba Yesu alikuwa nabii wa uwongo. *

Hatuna shaka yoyote kwamba Juliano alifanya mipango ya kujenga upya hekalu hilo. Wanahistoria wanabishana ikiwa ni kweli kwamba Juliano alianza kazi hiyo ya kujenga upya, na kama ndivyo, ni kwa nini kazi hiyo haikumalizwa. Hata hivyo, tuna uhakika kuhusu jambo moja. Juliano aliuawa kabla hajamaliza miaka miwili tangu alipowekwa kuwa maliki, na mradi wake haukuendelea alipokufa.

Huenda hekalu lilikuwa hivi katika siku za Yesu likiwekwa katika eneo hilo leo

^ fu. 5 Yesu hakusema kwamba hekalu hilo halingejengwa kamwe upya bali alisema lingeharibiwa, na ndivyo ilivyotukia mwaka wa 70 W.K.