Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Je, Waisraeli waliwaua wahalifu kwa kuwatundika juu ya miti?

Mataifa mengi katika nyakati za kale yaliwaua wahalifu fulani kwa kuwatundika juu ya mti au nguzo. Waroma walimfunga mhalifu kwa kamba au kumpigilia misumari juu ya mti, na huenda mhalifu huyo angekufa baada ya siku kadhaa kwa sababu ya maumivu, kiu, njaa, na hali mbaya ya hewa. Waroma waliona kumtundika mhalifu juu ya mti kuwa adhabu yenye aibu wanayostahili wahalifu wasiofaa chochote.

Vipi taifa la kale la Israeli? Je, Waisraeli waliwaua wahalifu kwa kuwatundika juu ya mti? Sheria ya Musa ilisema hivi: “Ikiwa mtu atakuwa na dhambi inayostahili hukumu ya kifo, naye ameuawa, nawe umemtundika juu ya mti, maiti yake isibaki usiku kucha juu ya mti; bali kwa vyovyote utamzika siku hiyo.” (Kum. 21:22, 23) Hivyo, ni wazi kwamba mtu aliyestahili kufa, katika Maandiko ya Kiebrania, aliuawa kwanza na kisha kutundikwa juu ya nguzo au mti.

Kuhusiana na hilo, andiko la Mambo ya Walawi 20:2 linasema hivi: “Mtu yeyote wa wana wa Israeli, na mkaaji mgeni yeyote anayekaa akiwa mgeni katika Israeli, anayempa Moleki yeyote kati ya uzao wake, lazima auawe. Watu wa nchi watampiga kwa mawe mpaka afe.” Wote waliokuwa na “roho ya kuwasiliana na pepo au roho ya kubashiri” walipaswa kuuawa pia. Kwa njia gani? Kwa ‘kupigwa kwa mawe.’—Law. 20:27.

Katika andiko la Kumbukumbu la Torati 22:23, 24, tunasoma hivi: “Ikiwa kulikuwa na msichana bikira aliyechumbiwa na mwanamume, na mwanamume fulani akamkuta jijini na kulala naye, mtawatoa wote wawili mpaka kwenye lango la jiji na kuwapiga kwa mawe, nao lazima wafe, yule msichana kwa sababu hakupiga mayowe jijini, na yule mwanamume kwa sababu alimfedhehesha mke wa mwenzake. Kwa hiyo lazima utaondolea mbali lililo ovu kutoka katikati yako.” Hivyo, Waisraeli wa kale waliona kuwapiga mawe wahalifu kuwa njia kuu ya kuwaua wale waliokuwa na hatia kwa sababu ya kufanya uhalifu mbaya sana. *

Ni wazi kwamba mtu aliyestahili kufa, katika Maandiko ya Kiebrania, aliuawa kwanza na kisha kutundikwa juu ya nguzo au mti

Andiko la Kumbukumbu la Torati 21:23 linasema kwamba “mtu aliyetundikwa ni kitu kilicholaaniwa na Mungu.” Bila shaka, Waisraeli waliathiriwa walipoona maiti ya mtu mwovu ‘aliyelaaniwa na Mungu’ ikiwa imetundikwa hadharani. Kwa kweli, kuutundika mwili wa mhalifu juu ya mti au nguzo kulitoa onyo kwa wengine.

^ fu. 6 Wasomi wengi wanakubali kwamba chini ya Sheria, mhalifu aliuawa kabla ya mwili wake kutundikwa juu ya mti. Hata hivyo, kuna ushahidi unaoonyesha kwamba katika karne ya kwanza, Wayahudi waliwatundika wahalifu fulani juu ya mti wakiwa hai na baadaye wakafa.