Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 SIMULIZI LA MAISHA

Kinachofanya Maisha Yetu Yawe na Kusudi la Kweli

Kinachofanya Maisha Yetu Yawe na Kusudi la Kweli

MUDA mfupi baada ya kumzaa mwana wangu, Gary, mwaka wa 1958, nilitambua kwamba hakuwa sawa. Hata hivyo, iliwachukua madaktari miezi kumi kugundua ugonjwa aliokuwa nao na miaka mitano zaidi kwa wataalamu wa afya katika jiji la London kuthibitisha jambo hilo. Nilihuzunika sana binti yangu Louise, aliyezaliwa miaka tisa baada ya Gary, alipoanza kuwa na dalili mbaya hata zaidi za ugonjwa kuliko zile za Gary.

Kwa fadhili, madaktari waliniambia hivi: “Watoto wako wana ugonjwa unaoitwa LMBB syndrome, * nao hauna tiba.” Wakati huo, mengi hayakuwa yamejulikana kuhusu ugonjwa huo wa chembe za urithi usiowapata watu wengi. Dalili za kawaida za ugonjwa huo zinatia ndani tatizo la kutoona vizuri linalosababisha upofu, kunenepa kupita kiasi, kuwa na vidole vya ziada, kukua polepole, tatizo la misuli, ugonjwa wa kisukari, yabisi-kavu aina ya osteoarthritis, na matatizo ya figo. Kwa hiyo, ilikuwa vigumu sana kuwatunza watoto wangu. Utafiti wa hivi karibuni ulikadiria kwamba mtu 1 kati ya watu 125,000 nchini Uingereza anaugua ugonjwa huo, ijapokuwa huenda hauwasumbui sana wengi wao.

YEHOVA NI ‘KILELE CHETU SALAMA’

Baada tu ya kuolewa, niliongea na Shahidi wa Yehova, na mara moja nikagundua kwamba nimepata kweli. Lakini mume wangu hakupendezwa hata kidogo. Sikuzote tulihamahama kwa sababu ya kazi yake na hivyo sikuhudhuria mikutano yoyote ya kutaniko. Hata hivyo, niliendelea kusoma Biblia na kusali kwa Yehova. Nilifarijika sana kusoma kwamba “Yehova atakuwa kilele salama kwa ajili ya mtu yeyote aliyekandamizwa, kilele salama wakati wa taabu” na kwamba ‘kwa hakika hatawaacha wale wanaomtafuta’!—Zab. 9:9, 10.

Gary alikuwa na tatizo la kutoona vizuri, kwa hiyo alipokuwa na umri wa miaka sita, alipelekwa shule ya bweni ya watoto wenye mahitaji ya pekee, iliyo katika pwani ya kusini nchini Uingereza. Kwa kawaida alinipigia simu akinieleza mambo yaliyomhangaisha, na kupitia simu nilimsaidia kuelewa kanuni za msingi za Biblia. Miaka michache baada ya kumzaa Louise, nilianza kuugua ugonjwa wa misuli na wa mfumo wa neva. Gary alirudi nyumbani kutoka shule ya bweni alipokuwa na umri wa miaka 16. Hata hivyo, uwezo wake wa kuona ulizidi kupungua, naye akawa kipofu kabisa mwaka wa 1975. Katika mwaka wa 1977, mume wangu alituacha.

Muda mfupi baada ya Gary kurudi nyumbani, tulishirikiana sana na kutaniko lililotuonyesha upendo, nami nikabatizwa mwaka wa 1974. Nilithamini sana mzee wa kutaniko alipomsaidia Gary kukabiliana na mabadiliko ya kubalehe. Mashahidi wengine walinisaidia kufanya kazi za nyumbani, na baadaye, shirika la kijamii liliwaweka rasmi dada watano kati yao ili watusaidie nyumbani. Mpango huo umekuwa baraka kama nini!

Gary aliendelea kufanya maendeleo katika kweli naye akabatizwa mwaka wa 1982. Alitamani sana kufanya upainia msaidizi. Kwa hiyo, niliamua kumuunga mkono na niliendelea kufanya hivyo kwa miaka kadhaa. Muda fulani baadaye, mwana wangu alifurahi sana mwangalizi wetu wa mzunguko alipomuuliza hivi: “Gary, kwa nini usiwe painia wa kawaida?” Gary alihitaji sana kitia-moyo hicho, na mwaka 1990 aliwekwa rasmi kuwa painia wa kawaida.

 Gary amefanyiwa upasuaji mara mbili na kuwekwa nyonga bandia, upasuaji wa kwanza ulifanywa katika mwaka wa 1999 na wa pili mwaka 2008, lakini afya ya Louise ilizidi kuzorota. Alizaliwa akiwa kipofu kabisa, na nilipoona kidole cha ziada katika mguu wake, niligundua kwamba yeye pia ana ugonjwa wa LMBB. Uchunguzi ulionyesha pia kwamba viungo vyake vingi vya ndani vilikuwa na kasoro kubwa. Katika miaka iliyopita, amefanyiwa upasuaji mkubwa mara nyingi, kutia ndani kufanyiwa upasuaji wa figo mara tano. Pia, Louise ana ugonjwa wa kisukari kama Gary.

Kwa kuwa anajua kwamba hali za dharura zinaweza kutokea wakati wa upasuaji, Louise huongea mapema na madaktari wanaofanya upasuaji, madaktari wa unusukaputi, na wasimamizi wa hospitali ili kuwaeleza msimamo wake kuhusu matibabu yasiyohusisha damu. Kwa hiyo, yeye hufurahia uhusiano mzuri na wote wanaomtibu ipasavyo.

TUNA KUSUDI MAISHANI

Tunafanya mambo mengi katika nyumba yetu yanayohusu ibada ya Yehova. Kabla ya kupata vifaa vya kisasa vya kielektroniki, nilitumia saa nyingi kuwasomea machapisho Gary na Louise. Sasa CD, DVD, na rekodi katika www.pr418.com zinatusaidia sote kufurahia ratiba ya kila juma ya funzo la Biblia katika pindi tofauti-tofauti na hilo linatuwezesha kushiriki kutoa maelezo yenye kujenga katika mikutano ya Kikristo.

Tunathamini kama nini kweli zenye thamani zinazopatikana katika Neno la Yehova lililoongozwa na roho yake!

Mara nyingine, Gary hukariri maelezo atakayotoa katika mikutano, na ikiwa ana hotuba katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi yeye huitoa kwa maneno yake. Aliwekwa rasmi kuwa mtumishi wa huduma mwaka wa 1995, na mara nyingi amekuwa akifanya mengi katika Jumba la Ufalme kama vile kuwakaribisha ndugu na dada na kusaidia katika idara ya sauti.

Mashahidi wenzetu huhubiri pamoja na Gary, mara nyingi wakifanya hivyo kwa kusukuma kiti chake cha magurudumu anachotumia kwa sababu anaugua ugonjwa wa yabisi-kavu. Shahidi mmoja amekuwa akimsaidia Gary kuongoza funzo la Biblia la mtu anayependezwa. Pia, Gary amemtia moyo Mkristo aliyekuwa asiyetenda kwa miaka 25. Sasa, wote wawili wanahudhuria mikutano ya Kikristo.

Alipokuwa na miaka tisa, Louise alifundishwa na nyanya yake kushona, mimi na mmoja kati ya waliomtunza tulimfundisha jinsi ya kudarizi au kutia nakshi kwenye nguo. Kwa kuwa anafurahia sana kazi hiyo, yeye hushona blanketi za watoto zenye rangi mbalimbali na za washiriki wa kutaniko waliozeeka. Anatengeneza pia kadi akitumia picha ndogo zenye gundi. Kadi hizo zinathaminiwa sana. Mwanzoni mwa miaka yake ya utineja, Louise alijifunza kupiga chapa kwa kompyuta. Sasa, kwa msaada wa kompyuta maalumu inayoongea, Louise huwasiliana kwa ukawaida na marafiki zake kupitia barua-pepe. Louise alibatizwa alipokuwa na miaka 17. Katika kipindi cha kampeni maalumu za kuhubiri, sisi hufurahia kufanya upainia msaidizi pamoja. Kama Gary, Louise hukariri maandiko ili kufafanua imani yake katika ahadi za Mungu kuhusu dunia ambamo “macho ya vipofu yatafunguliwa” na “hakuna mkaaji atakayesema: ‘Mimi ni mgonjwa.’”—Isa. 33:24; 35:5.

Tunathamini kama nini kweli zenye thamani zinazopatikana katika Neno la Yehova lililoongozwa na roho yake! Mioyo yetu imejaa shukrani kwa sababu ya msaada wenye upendo wa kutaniko letu, kwa sababu bila msaada huo tusingeweza kutimiza mengi. Tunashukuru hasa kwa sababu ya msaada wa Yehova, kwa kuwa maisha yetu yana kusudi la kweli.

^ fu. 5 Ugonjwa wa Laurence-Moon-Bardet-Biedl syndrome uliitwa hivyo kutokana na majina ya madaktari wanne waliogundua ugonjwa huo unaosababishwa na kurithi chembe zenye kasoro kutoka kwa wazazi wote wawili. Leo, ugonjwa huo unaitwa Bardet-Biedl syndrome. Ugonjwa huo hauna tiba.