Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Tazama! Mimi Nipo Pamoja Nanyi Siku Zote”

“Tazama! Mimi Nipo Pamoja Nanyi Siku Zote”

“Tazama! Mimi nipo pamoja nanyi siku zote mpaka umalizio wa mfumo wa mambo.”—MT. 28:20.

1. (a) Eleza kwa ufupi mfano wa ngano na magugu. (b) Yesu alielezaje maana ya mfano huo?

MFANO mmoja aliotumia Yesu kueleza kuhusu Ufalme ni wa mkulima anayepanda mbegu nzuri ya ngano na adui anayepanda magugu katikati ya mbegu hiyo nzuri. Magugu yanakua na kufunika ngano, lakini mkulima anawaamuru watumwa wake ‘waache magugu na ngano zikue pamoja mpaka wakati wa mavuno.’ Katika majira ya mavuno, magugu yanaharibiwa na ngano inakusanywa. Yesu mwenyewe alieleza maana ya mfano huo. (Soma Mathayo 13:24-30, 37-43.) Mfano huo unafunua nini? (Tazama chati yenye kichwa “Ngano na Magugu.”)

2. (a) Mambo yanayotukia katika shamba la mkulima yanafananisha nini? (b) Tutachunguza sehemu gani ya mfano huo?

2 Mambo yanayotukia katika shamba la mkulima huyo yanaonyesha jinsi na wakati ambapo Yesu angekusanya jamii yote ya ngano kutoka miongoni mwa wanadamu, yaani, Wakristo watiwa-mafuta watakaotawala pamoja naye katika Ufalme wake. Kazi ya kupanda ilianza Pentekoste ya 33 W.K. Kazi hiyo ya kuwakusanya itakwisha watiwa-mafuta watakaokuwa hai mwishoni mwa mfumo huu wa mambo watakapotiwa muhuri wa mwisho na kisha kuchukuliwa kwenda mbinguni. (Mt. 24:31; Ufu. 7:1-4) Kama vile tu mtu anavyoweza kuona vizuri mazingira yanayomzunguka akipanda juu ya mlima, ndivyo mfano huo unavyotusaidia kuona kikamili mambo ambayo yangetukia kwa kipindi cha miaka 2,000 hivi. Kuelewa mambo hayo kumetusaidia kutambua matukio gani yanayohusiana na Ufalme? Mfano huo unaeleza kuhusu wakati wa kupanda, wa kukua, na wa mavuno. Makala hii itazungumzia hasa wakati wa mavuno. *

CHINI YA UTUNZAJI MZURI WA YESU

3. (a) Ni hali gani iliyotokea baada ya karne ya kwanza? (b) Kulingana na Mathayo 13:28, ni swali gani lililoulizwa, na ni nani waliouliza swali hilo? (Tazama pia maelezo ya chini.)

3 Mwanzoni mwa karne ya pili W.K., “magugu yalionekana” wakati Wakristo wa uwongo walipoanza  kuonekana katika shamba la ulimwengu. (Mt. 13:26) Kufikia karne ya nne, Wakristo walio mfano wa magugu walikuwa wengi sana kuliko Wakristo watiwa-mafuta. Kumbuka kwamba katika mfano huo, watumwa walimwomba bwana wao ruhusa ya kung’oa magugu. * (Mt. 13:28) Bwana wao aliwaambia nini?

4. (a) Jibu la Yesu, yule Bwana, linaonyesha nini? (b) Wakristo walio kama ngano walianza kutambuliwa wakati gani?

4 Akiongea kuhusu ngano na magugu hayo, Yesu alisema hivi: “Acheni zikue pamoja mpaka wakati wa mavuno.” Amri hiyo inaonyesha kwamba tangu karne ya kwanza hadi leo, sikuzote kumekuwa na Wakristo fulani watiwa-mafuta walio kama ngano duniani. Mkataa huo unathibitishwa na jambo hili ambalo Yesu aliwaambia wanafunzi wake baadaye: “Mimi nipo pamoja nanyi siku zote mpaka umalizio wa mfumo wa mambo.” (Mt. 28:20) Kwa hiyo, Yesu angewalinda Wakristo watiwa-mafuta siku zote mpaka mwisho ufike. Hata hivyo, kwa kuwa Wakristo walio kama magugu wangeongezeka na kuwafunika watiwa-mafuta, hatujui kwa hakika ni nani waliokuwa wa jamii ya ngano katika kipindi hicho kirefu. Hata hivyo, makumi kadhaa ya miaka kabla ya kuanza kwa majira ya mavuno, jamii ya ngano ilianza kutambuliwa. Hilo lilitokea jinsi gani?

MJUMBE ‘ANAFUNGUA NJIA’

5. Unabii wa Malaki ulitimizwa jinsi gani katika karne ya kwanza?

 5 Karne nyingi kabla Yesu hajatoa mfano wa ngano na magugu, Yehova alitumia roho takatifu kumwongoza Malaki, nabii wake kutabiri matukio yanayotajwa katika mfano wa Yesu. (Soma Malaki 3:1-4.) Yohana Mbatizaji ndiye ‘mjumbe aliyefungua njia.’ (Mt. 11:10, 11) Alipokuja katika mwaka wa 29 W.K.,  wakati wa kuhukumu taifa la Israeli ulikuwa umekaribia. Yesu alikuwa mjumbe wa pili. Alilitakasa hekalu la Yerusalemu mara mbili—mara ya kwanza mwanzoni mwa huduma yake na mara ya pili karibu mwisho wa huduma yake. (Mt. 21:12, 13; Yoh. 2:14-17) Kwa hiyo, Yesu alitumia kipindi fulani cha wakati kufanya kazi ya kulitakasa hekalu.

6. (a) Unabii wa Malaki ulitimizwaje kwa njia kubwa zaidi? (b) Yesu alikagua hekalu la kiroho katika kipindi gani cha wakati? (Tazama pia maelezo ya chini.)

 6 Unabii wa Malaki unatimizwaje kwa njia kubwa zaidi? Kwa makumi ya miaka kabla ya 1914, C. T. Russell pamoja na washiriki wake wa karibu walifanya kazi kama ya Yohana Mbatizaji. Kazi hiyo muhimu ilitia ndani kurudisha kweli za Biblia. Wanafunzi hao wa Biblia walifundisha maana sahihi ya dhabihu ya fidia ya Kristo, wakafunua fundisho la uwongo kuhusu moto wa mateso, na kutangaza kwamba Nyakati za Mataifa zinakaribia mwisho wake. Hata hivyo, bado kulikuwa na vikundi vingi vya kidini vilivyodai kumfuata Kristo. Kwa hiyo, swali muhimu sana lilihitaji kujibiwa: Ni kikundi gani kati ya hivyo kilichokuwa ngano? Ili kujibu swali hilo, Yesu alianza kukagua hekalu la kiroho katika mwaka wa 1914. Kazi hiyo ya kukagua na kutakasa ilitukia kwa kipindi fulani cha wakati, yaani, kuanzia mwaka wa 1914 hadi mwanzoni mwa mwaka wa 1919. *

MIAKA YA KUKAGUA NA KUTAKASA

7. Yesu alipata nini alipoanza ukaguzi wake mwaka wa 1914?

7 Yesu alipoanza ukaguzi wake, alipata nini? Alipata kikundi kidogo cha Wanafunzi wa Biblia wenye bidii ambao kwa miaka zaidi ya 30, walikuwa wametumia nguvu na mali zao ili kufanya kampeni kubwa ya kuhubiri. * Ni wazi kwamba Yesu na malaika  walikuwa na shangwe sana walipopata kwamba watu hao wachache waliokuwa kama mabua ya ngano yaliyo thabiti hawakusongwa na magugu ya Shetani. Hata hivyo, bado kulikuwa na uhitaji wa ‘kuwatakasa wana wa Lawi,’ yaani, watiwa-mafuta. (Mal. 3:2, 3; 1 Pet. 4:17) Kwa nini?

8. Ni mambo gani yaliyotukia baada ya mwaka wa 1914?

8 Mwishoni mwa mwaka wa 1914, baadhi ya Wanafunzi wa Biblia walivunjika moyo kwa sababu hawakuwa wameenda mbinguni. Katika mwaka wa 1915 na 1916, upinzani kutoka nje ya tengenezo ulipunguza bidii yao katika kazi ya kuhubiri. Jambo baya zaidi ni kwamba baada ya kifo cha Ndugu Russell mnamo Oktoba 1916, upinzani ulitokea ndani ya tengenezo. Wanne kati ya wasimamizi saba wa shirika la Watch Tower Bible and Tract Society walipinga uamuzi wa kumchagua Ndugu Rutherford kuongoza. Walijaribu kusababisha migawanyiko miongoni mwa akina ndugu, lakini mnamo Agosti 1917, waliondoka Betheli—huo ulikuwa utakasaji mkubwa kama nini! Pia, baadhi ya Wanafunzi wa Biblia waliwaogopa wanadamu. Hata hivyo, kwa ujumla walikubali kwa hiari kutakaswa na Yesu na kufanya mabadiliko yaliyohitajika. Kwa hiyo, Yesu aliwahukumu kuwa ngano ya kweli ya Kikristo, lakini akawakataa Wakristo wote wa uwongo, kutia ndani wote waliokuwa katika makanisa yanayodai kuwa ya Kikristo. (Mal. 3:5; 2 Tim. 2:19) Ni nini kilichotokea baadaye? Ili tujue, acheni tuendelee kuchunguza mfano wa ngano na magugu.

NI NINI KINACHOTUKIA BAADA YA MAJIRA YA MAVUNO KUANZA?

9, 10. (a) Tutachunguza jambo gani kuhusu majira ya mavuno? (b) Ni nini kilichotukia kwanza katika majira ya mavuno?

9 Yesu alisema hivi: “Yale mavuno ni umalizio wa mfumo wa mambo.” (Mt. 13:39) Majira hayo ya mavuno yalianza mwaka wa 1914. Tutachunguza mambo matano ambayo Yesu alitabiri kwamba yangetukia katika kipindi hicho.

10 Kwanza, kuyakusanya magugu. Yesu anasema hivi: “Katika majira ya mavuno nitawaambia wavunaji, Kwanza kusanyeni magugu na kuyafunga matita-matita.” Baada ya mwaka wa 1914, malaika walianza ‘kuwakusanya’ Wakristo walio kama magugu kwa kuwatenganisha na “wana wa ufalme” waliotiwa mafuta.—Mt. 13:30, 38, 41.

11. Ni jambo gani linalowatofautisha Wakristo wa kweli na Wakristo wa uwongo hadi leo?

11 Kadiri kazi ya kukusanya ilivyoendelea, tofauti kati ya vikundi hivyo viwili ilionekana wazi zaidi. (Ufu. 18:1, 4) Kufikia mwaka wa 1919, ikawa wazi kwamba Babiloni Mkubwa alikuwa ameanguka. Ni jambo gani hasa lililowatofautisha Wakristo wa kweli na wa uwongo? Ni kazi ya kuhubiri. Wale walioongoza miongoni mwa Wanafunzi wa Biblia walianza kusisitiza kwamba ni muhimu kila mtu ashiriki katika kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme. Kwa mfano, kijitabu Kwa Wale Waliokabidhiwa Kazi (cha Kiingereza) kilichochapishwa mwaka wa 1919, kilihimiza Wakristo wote watiwa-mafuta wahubiri nyumba kwa nyumba. Kilisema hivi: “Kazi inaonekana kuwa nyingi sana, lakini ni kazi ya Bwana, na kwa nguvu zake tutaifanya. Mna pendeleo la kushiriki katika kazi hiyo.” Watu waliitikiaje? Gazeti la Mnara wa Mlinzi liliripoti katika mwaka wa 1922 kwamba tangu wakati huo na kuendelea, Wanafunzi wa Biblia walishiriki kwa bidii zaidi katika kazi ya kuhubiri. Punde si punde, kazi ya kuhubiri nyumba kwa nyumba ikawa alama muhimu inayowatambulisha Wakristo hao waaminifu, kama ilivyo leo.

12. Jamii ya ngano imekuwa ikikusanywa kuanzia wakati gani?

12 Pili, kukusanya ngano. Yesu anawaamuru malaika zake hivi: “Nendeni mkusanye ngano ghalani mwangu.” (Mt. 13:30)  Tangu mwaka wa 1919, watiwa-mafuta wamekuwa wakikusanywa katika kutaniko la Kikristo lililopangwa upya. Wakristo watiwa-mafuta watakaokuwa hai mwishoni mwa mfumo huu wa mambo, watakusanywa mara ya mwisho watakapopokea thawabu yao ya kimbingu.—Dan. 7:18, 22, 27.

13. Andiko la Ufunuo 18:7 linaonyesha nini kuhusu mtazamo wa sasa wa yule kahaba, au Babiloni Mkubwa, pamoja na dini zinazodai kuwa za Kikristo?

13 Tatu, kulia na kusaga meno. Baada ya malaika kuyafunga magugu matita-matita, ni nini kinachotokea? Akiongea kuhusu hali ya jamii ya magugu, Yesu anasema: “Humo ndimo watalia na kusaga meno yao.” (Mt. 13:42) Je, jambo hilo linatukia sasa? Hapana. Leo, dini zinazodai kuwa za Kikristo, ambazo ni sehemu ya yule kahaba, bado zinasema hivi: “Ninaketi nikiwa malkia, nami si mjane, nami sitaona maombolezo kamwe.” (Ufu. 18:7) Kwa kweli, dini zinazodai kuwa za Kikristo zinahisi kuwa zina uvutano mkubwa sana, na hata zinadai kwamba ‘zinaketi kama malkia’ juu ya jamii ya viongozi wa kisiasa. Wakati huu, wale wanaofananishwa na magugu wanajigamba badala ya kulia. Lakini hali hiyo itabadilika hivi karibuni.

Uhusiano wa karibu wa dini zinazodai kuwa za Kikristo na viongozi wa kisiasa utaisha hivi karibuni (Tazama fungu la 13)

14. (a) Ni wakati gani na kwa nini Wakristo wa uwongo ‘watasaga meno yao’? (b) Uelewaji wetu uliorekebishwa wa andiko la Mathayo 13:42 unapatana jinsi gani na wazo lililo katika Zaburi 112:10? (Tazama maelezo ya chini.)

14 Wakati wa dhiki kuu, baada ya dini yote ya uwongo kuharibiwa, wafuasi wa dini watakimbia ili wajifiche lakini hawatapata mahali salama pa kujificha. (Luka 23:30; Ufu. 6:15-17) Kisha, watakapotambua kwamba hawawezi kuepuka uharibifu, watalia kwa sababu ya kukata tamaa na ‘kusaga meno yao’ kwa hasira. Kama Yesu anavyotabiri katika unabii wake kuhusu ile dhiki kuu, katika kipindi hicho kigumu, ‘watajipiga-piga wenyewe kwa kuomboleza.’ *Mt. 24:30; Ufu. 1:7.

15. Magugu yatafanywa nini, na jambo hilo litatukia wakati gani?

15 Nne, kutupwa ndani ya tanuru. Matita ya magugu yatafanywa nini? Malaika ‘watayatupa ndani ya tanuru ya moto.’ (Mt. 13:42) Hilo linamaanisha uharibifu wa milele. Kwa hiyo, wafuasi hao wa mashirika ya dini za uwongo wataharibiwa katika sehemu ya mwisho ya ile dhiki kuu, yaani, wakati wa Har–Magedoni.—Mal. 4:1.

16, 17. (a) Ni tukio gani la mwisho analotaja Yesu katika mfano wake? (b) Kwa nini tunafikia mkataa kwamba jambo hilo litatukia wakati ujao?

16 Tano, kung’aa kwa uangavu. Yesu anamalizia unabii wake kwa kusema hivi: “Wakati huo waadilifu watang’aa kwa uangavu kama jua katika ufalme wa Baba yao.” (Mt. 13:43) Jambo hilo litatukia wakati gani na wapi? Maneno hayo yatatimia wakati ujao. Yesu alitabiri jambo  litakalotukia mbinguni wakati ujao, bali si jambo linalotukia sasa duniani. * Fikiria sababu mbili zinazofanya tufikie mkataa huo.

17 Kwanza, acheni tuone jambo hilo litatukia “wakati gani.” Yesu alisema: “Wakati huo waadilifu watang’aa.” Ni wazi kwamba maneno “wakati huo” yanarejelea tukio ambalo Yesu alikuwa ametangulia kutaja, yaani, ‘kutupwa kwa magugu ndani ya tanuru ya moto.’ Hilo linatukia katika sehemu ya mwisho ya ile dhiki kuu. Hivyo, kule ‘kung’aa kwa uangavu’ kwa watiwa-mafuta lazima kutukie pia wakati huo ujao. Pili, acheni tufikirie jambo hilo litatukia “wapi.” Yesu alisema kwamba waadilifu ‘watang’aa katika ufalme.’ Hilo linamaanisha nini? Watiwa-mafuta wote waaminifu ambao bado watakuwa duniani baada ya sehemu ya kwanza ya dhiki kuu kupita watakuwa tayari wametiwa muhuri wa mwisho. Kisha, watakusanywa kwenda mbinguni kama unabii wa Yesu kuhusu dhiki kuu unavyoonyesha. (Mt. 24:31) Huko, watang’aa “katika ufalme wa Baba yao,” na muda mfupi baada ya vita vya Har–Magedoni, watashangilia kuwa bibi arusi wa Yesu katika ile “ndoa ya Mwana-Kondoo.”—Ufu. 19:6-9.

JINSI TUNAVYONUFAIKA

18, 19. Kuelewa mfano wa Yesu wa ngano na magugu kunatunufaisha kibinafsi katika njia zipi?

18 Sisi binafsi tunanufaikaje kwa kuelewa kikamili zaidi maana ya mfano huo? Fikiria njia tatu. Kwanza, mfano huo unaongeza kina cha ufahamu wetu. Unafunua sababu muhimu inayomfanya Yehova aruhusu uovu. “Alivumilia . . . vyombo vya ghadhabu” ili atayarishe “vyombo vya rehema,” yaani, jamii ya ngano. * (Rom. 9:22-24) Pili, mfano huo unaimarisha uhakika wetu. Kadiri mwisho unavyokaribia, adui zetu watazidi kupigana nasi, ‘lakini hawatashinda.’ (Soma Yeremia 1:19.) Yehova ameilinda jamii ya ngano kwa miaka mingi, vivyo hivyo akiwa Baba yetu wa mbinguni atakuwa pamoja nasi “siku zote,” kupitia Yesu na malaika.—Mt. 28:20.

19 Tatu, mfano huo unatuwezesha kuitambua ile jamii ya ngano. Kwa nini jambo hilo ni muhimu sana? Ili kupata jibu la swali ambalo Yesu aliuliza katika unabii wenye mambo mengi kuhusu siku za mwisho, ni muhimu kwetu kuwajua Wakristo hao walio kama ngano. Aliuliza hivi: “Ni nani kwa kweli mtumwa mwaminifu na mwenye busara?” (Mt. 24:45) Makala mbili zinazofuata zitajibu swali hilo kwa njia yenye kuridhisha.

 

^ fu. 2 Fungu la 2: Ili ujikumbushe maana ya mambo mengine katika mfano huo, tunakutia moyo usome makala yenye kichwa “Waadilifu Watang’aa kwa Uangavu Kama Jua” katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Machi 15, 2010.

^ fu. 3 Fungu la 3: Kwa kuwa mitume wa Yesu walikuwa wamekufa na watiwa-mafuta waliobaki duniani walifananishwa na ngano wala si watumwa, kwa kufaa watumwa hao wanafananisha malaika. Baadaye katika mfano huo, wale wanaokusanya magugu wanatambulishwa kuwa malaika.—Mt. 13:39.

^ fu. 6 Fungu la 6: Huu ni uelewaji uliorekebishwa. Awali, tulifikiri kwamba Yesu alifanya ukaguzi katika mwaka wa 1918.

^ fu. 7 Fungu la 7: Kuanzia mwaka wa 1910 hadi 1914, Wanafunzi wa Biblia waligawanya karibu vitabu 4,000,000 na vijitabu na trakti zaidi ya 200,000,000.

^ fu. 14 Fungu la 14: Huu ni uelewaji uliorekebishwa wa andiko la Mathayo 13:42. Awali, machapisho yetu yalisema kwamba Wakristo wa uwongo wamekuwa ‘wakilia na kusaga meno yao’ kwa makumi ya miaka wakiomboleza kwamba “wana wa ufalme” wanafunua wazi kuwa wao ni “wana wa yule mwovu.” (Mt. 13:38) Hata hivyo, tunapaswa kuzingatia kwamba wazo la kulia na kusaga meno linahusiana na uharibifu.—Zab. 112:10.

^ fu. 16 Fungu la 16: Andiko la Danieli 12:3 linasema kwamba “wale walio na ufahamu [Wakristo watiwa-mafuta] watang’aa kama mwangaza wa anga.” Wakiwa wangali duniani, wanang’aa kwa kushiriki katika kazi ya kuhubiri. Hata hivyo, Mathayo 13:43 linataja wakati ambapo watang’aa kwa uangavu katika Ufalme wa mbinguni. Awali, tulifikiri kwamba maandiko hayo mawili yalirejelea utendaji uleule, yaani, kazi ya kuhubiri.

^ fu. 18 Fungu la 18: Tazama kitabu Mkaribie Yehova, ukurasa wa 288-289.