Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Tuambie, Mambo Haya Yatakuwa Wakati Gani?”

“Tuambie, Mambo Haya Yatakuwa Wakati Gani?”

“Ni nini itakayokuwa ishara ya kuwapo kwako na ya umalizio wa mfumo wa mambo?”—MT. 24:3.

1. Kama mitume, tuna hamu ya kujua nini?

YESU alikuwa anakaribia kumaliza huduma yake duniani, na wanafunzi wake walikuwa na hamu ya kujua kuhusu wakati wao ujao. Kwa hiyo, siku chache tu kabla ya kifo chake, mitume wake wanne walimuuliza hivi: “Mambo haya yatakuwa wakati gani, na ni nini itakayokuwa ishara ya kuwapo kwako na ya umalizio wa mfumo wa mambo?” (Mt. 24:3; Marko 13:3) Yesu alijibu kwa kutaja unabii wenye mambo mengi ulio katika Mathayo sura ya 24 na 25. Katika unabii huo, Yesu alitabiri matukio mengi muhimu. Maneno yake yana maana sana kwetu kwa sababu sisi pia tunapendezwa sana kujua kuhusu wakati ujao.

2. (a) Kwa miaka mingi, tumejitahidi kuelewa nini vizuri zaidi? (b) Ni maswali gani matatu tutakayochunguza?

2 Kwa miaka mingi, watumishi wa Yehova wamesali na kujifunza unabii wa Yesu kuhusu siku za mwisho. Wamejitahidi kuelewa vizuri zaidi wakati ambapo maneno ya Yesu yangetimia. Ili kuonyesha jinsi ambavyo uelewaji wetu umerekebishwa, acheni tufikirie maswali matatu kuhusu “wakati.” “Dhiki kuu” inaanza wakati gani? Yesu anahukumu “kondoo” na “mbuzi” wakati gani? Yesu ‘anafika’ au kuja wakati gani?—Mt. 24:21; 25:31-33.

DHIKI KUU INAANZA WAKATI GANI?

3. Tulielewa nini zamani kuhusu wakati wa kuanza kwa dhiki kuu?

3 Kwa miaka kadhaa, tulifikiri kwamba dhiki kuu ilianza mwaka wa 1914, wakati wa Vita vya Kwanza vya Ulimwengu, na kwamba Yehova ‘alifupisha siku hizo’ vita hivyo vilipoisha katika mwaka wa 1918 ili mabaki wapate nafasi ya kuhubiria mataifa yote habari njema. (Mt. 24:21, 22) Baada ya wao kumaliza kazi hiyo ya kuhubiri, milki ya Shetani ingeharibiwa. Hivyo, ilidhaniwa kwamba dhiki kuu ingetukia katika hatua tatu: Kungekuwa  na mwanzo (1914-1918), dhiki hiyo ingekatizwa (kuanzia 1918 na kuendelea), na ingemalizikia katika Har–Magedoni.

4. Ni ufahamu gani uliotusaidia kuelewa vizuri zaidi unabii wa Yesu kuhusu siku za mwisho?

4 Hata hivyo, baada ya kuchunguza zaidi unabii wa Yesu, tulitambua kwamba sehemu ya unabii wa Yesu kuhusu siku za mwisho inatimizwa kwa njia mbili. (Mt. 24:4-22) Ulitimizwa kwanza huko Yudea katika karne ya kwanza W.K., na ungetimizwa ulimwenguni pote katika siku zetu. Ufahamu huo ulitusaidia kufanya marekebisho kadhaa. *

5. (a) Ni kipindi gani kigumu kilichoanza mwaka wa 1914? (b) Kipindi hicho cha taabu ni kama kipindi gani cha wakati katika karne ya kwanza W.K.?

5 Tulitambua pia kwamba sehemu ya kwanza ya dhiki kuu haikuanza mwaka wa 1914. Kwa nini? Kwa sababu unabii wa Biblia unafunua kwamba dhiki kuu haitaanza na vita kati ya mataifa, badala yake itaanza wakati dini ya uwongo itakaposhambuliwa. Hivyo, matukio yaliyoanza mwaka wa 1914 hayakuwa mwanzo wa dhiki kuu, bali “mwanzo wa maumivu ya taabu.” (Mt. 24:8) Hayo “maumivu ya taabu” ni kama yale yaliyotokea Yerusalemu na Yudea kuanzia mwaka wa 33 W.K. mpaka 66 W.K.

6. Ni nini itakayokuwa ishara ya kuanza kwa dhiki kuu?

6 Ni nini itakayokuwa ishara ya kuanza kwa dhiki kuu? Yesu alitabiri hivi: “Mtakapoona lile chukizo linalosababisha ukiwa, kama vile lilivyosemwa kupitia nabii Danieli, likiwa limesimama katika mahali patakatifu, (msomaji na atumie utambuzi,) ndipo wale walio katika Yudea waanze kukimbilia milimani.” (Mt. 24:15, 16) Katika utimizo wa kwanza, ‘kusimama katika mahali patakatifu’ kulitokea mwaka wa 66 W.K, jeshi la Waroma (“lile chukizo”) liliposhambulia Yerusalemu na hekalu lake (mahali ambapo Wayahudi walipaona kuwa patakatifu). Katika utimizo mkubwa zaidi, ‘kusimama’ kutatokea wakati Umoja wa Mataifa (“lile  chukizo” katika wakati wetu) litakaposhambulia dini zinazodai kuwa za Kikristo (zinazoonwa kuwa takatifu na wale wanaodai kuwa Wakristo) na pia sehemu inayobaki ya Babiloni Mkubwa. Shambulizi hilo linatajwa kwenye Ufunuo 17:16-18. Tukio hilo litakuwa mwanzo wa ile dhiki kuu.

7. (a) ‘Mwili uliokolewa’ kwa njia gani katika karne ya kwanza? (b) Tutarajie nini wakati ujao?

7 Yesu alitabiri hivi pia: “Siku hizo zitafupishwa.” Jambo hilo lilitimizwa kwanza katika mwaka wa 66 W.K. wakati jeshi la Waroma ‘lilipofupisha’ shambulizi lake. Kisha, Wakristo watiwa-mafuta katika Yerusalemu na Yudea wakakimbia na hivyo ‘mwili, au uhai wao, ukaokolewa.’ (Soma Mathayo 24:22; Mal. 3:17) Kwa hiyo, tutarajie nini wakati wa dhiki kuu inayokuja? Yehova ‘atafupisha’ shambulizi la Umoja wa Mataifa dhidi ya dini ya uwongo, na hivyo kuzuia dini ya kweli isiangamizwe pamoja na dini ya uwongo. Hilo litahakikisha kwamba watu wa Mungu wataokolewa.

8. (a) Ni mambo gani yatakayotukia baada ya sehemu ya kwanza ya dhiki kuu kupita? (b) Inaonekana kwamba mshiriki wa mwisho wa wale 144,000 atapokea thawabu yake ya kimbingu wakati gani? (Tazama maelezo ya chini.)

 8 Ni nini kinachotokea baada ya sehemu ya kwanza ya dhiki kuu kupita? Maneno ya Yesu yanaonyesha kwamba kutakuwa na kipindi cha wakati kitakachoendelea mpaka kuanza kwa Har–Magedoni. Ni mambo gani yatakayotukia katika kipindi hicho? Jibu linapatikana katika Ezekieli 38:14-16 na Mathayo 24:29-31. (Soma.) * Baada ya mambo hayo, tutashuhudia Har–Magedoni, yaani, upeo wa dhiki kuu, unaofanana na uharibifu wa Yerusalemu katika mwaka wa 70 W.K. (Mal. 4:1) Vita vya Har–Magedoni vikiwa vimefikia upeo, dhiki kuu inayokuja itakuwa ya pekee sana, litakuwa tukio ‘la namna ambayo haijapata kutukia tangu mwanzo wa ulimwengu.’ (Mt. 24:21) Vita hivyo vitakapokwisha, Utawala wa Miaka Elfu wa Kristo utaanza.

9. Unabii wa Yesu kuhusu dhiki kuu una matokeo gani kwa watu wa Yehova?

 9 Unabii huo kuhusu dhiki kuu unatuimarisha. Kwa nini? Kwa sababu unatuhakikishia kwamba hata tukabili hali ngumu kadiri gani, watu wa Yehova wataokoka ile dhiki kuu wakiwa kikundi. (Ufu. 7:9, 14) Zaidi ya yote, tunafurahi kwa sababu katika Har–Magedoni Yehova atatetea enzi yake kuu na kulitakasa jina lake takatifu.—Zab. 83:18; Eze. 38:23.

YESU ANAHUKUMU KONDOO NA MBUZI WAKATI GANI?

10. Tulielewa nini zamani kuhusu wakati wa kuhukumiwa kwa kondoo na mbuzi?

10 Sasa fikiria wakati wa kutimizwa kwa sehemu nyingine ya unabii wa Yesu, yaani, mfano unaohusu kuhukumiwa kwa kondoo na mbuzi. (Mt. 25:31-46) Zamani, tulifikiri kwamba watu wangehukumiwa kuwa kondoo au mbuzi katika kipindi chote cha siku za mwisho kuanzia mwaka wa 1914 na kuendelea. Tulifikia mkataa kwamba wale waliokataa ujumbe wa Ufalme na kufa kabla ya dhiki kuu kuanza wangekuwa mbuzi, yaani, hawangekuwa na tumaini la ufufuo.

11. Kwa nini Yesu hakuanza kuwahukumu watu kuwa kondoo au mbuzi katika mwaka wa 1914?

11 Katikati ya miaka ya 1990, gazeti la Mnara wa Mlinzi lilizungumzia tena andiko la Mathayo 25:31 linalosema hivi: “Wakati Mwana wa binadamu atakapofika katika utukufu wake, na malaika wote pamoja naye, ndipo atakapoketi juu ya kiti chake cha ufalme chenye utukufu.” Gazeti hilo lilisema kwamba Yesu aliwekwa kuwa Mfalme wa Ufalme wa Mungu katika mwaka wa 1914, hata hivyo ‘hakuketi juu ya kiti chake cha ufalme chenye utukufu’ akiwa Hakimu wa “mataifa yote.” (Mt. 25:32; linganisha na Danieli 7:13.) Hata hivyo, katika mfano wa kondoo na mbuzi Yesu anaonekana hasa akiwa Hakimu. (Soma Mathayo 25:31-34, 41, 46.) Kwa kuwa Yesu hakuwa ameanza kutenda akiwa Hakimu wa mataifa yote katika mwaka wa 1914, ni wazi kwamba hakuanza mwaka huo kuhukumu watu kuwa kondoo au mbuzi. * Basi, Yesu ataanza kuhukumu wakati gani?

12. (a) Ni wakati gani Yesu atakapotenda kwa mara ya kwanza akiwa Hakimu wa mataifa yote? (b) Ni matukio gani yanayotajwa katika Mathayo 24:30, 31 na Mathayo 25:31-33, 46?

 12 Unabii wa Yesu kuhusu siku za mwisho unafunua kwamba atatenda kwa mara ya kwanza kabisa akiwa Hakimu wa mataifa yote baada ya uharibifu wa dini ya uwongo. Kama ilivyotajwa katika  fungu la 8, baadhi ya mambo yatakayotukia wakati huo yameandikwa katika Mathayo 24:30 na 31. Unapochunguza mistari hiyo, utaona kwamba Yesu anatabiri matukio yanayofanana na yale anayotaja katika mfano wa kondoo na mbuzi. Kwa mfano, Mwana wa binadamu anafika akiwa na utukufu na akiwa pamoja na malaika; makabila na mataifa yote yanakusanyika; wale wanaohukumiwa kuwa kondoo ‘wanainua vichwa vyao’ kwa sababu watapata “uzima wa milele.” * Wale wanaohukumiwa kuwa mbuzi ‘wanajipiga-piga wenyewe kwa kuomboleza,’ wakijua kwamba ‘watakatiliwa mbali milele.’—Mt. 25:31-33, 46.

13. (a) Ni wakati gani Yesu atahukumu watu kuwa kondoo au mbuzi? (b) Uelewaji huo unapaswa kutusaidia kuwa na mtazamo gani kuelekea huduma yetu?

13 Kwa hiyo, tufikie mkataa gani? Yesu atawahukumu watu wa mataifa yote kuwa kondoo au mbuzi atakapokuja wakati wa ile dhiki kuu. Kisha, katika Har–Magedoni, upeo wa ile dhiki kuu, watu walio mfano wa mbuzi ‘watakatiliwa mbali’ milele. Uelewaji huo unapaswa kutusaidia kuwa na mtazamo gani kuelekea huduma yetu? Unatusaidia kuona jinsi kazi yetu ya kuhubiri ilivyo muhimu. Kabla ya dhiki kuu kuanza, watu bado wana wakati wa kubadili maoni yao na kuanza kutembea katika barabara yenye nafasi ndogo “inayoongoza kwenye uzima.”  (Mt. 7:13, 14) Ni kweli kwamba huenda leo watu wakaonyesha mwelekeo wa kondoo au mbuzi. Hata hivyo, tunapaswa kukumbuka kwamba hukumu ya mwisho ya walio kondoo au mbuzi itakuwa wakati wa ile dhiki kuu. Kwa hiyo, tuna sababu nzuri ya kuendelea kuwapa watu wengi iwezekanavyo fursa ya kusikiliza na kukubali ujumbe wa Ufalme.

YESU ANAFIKA AU KUJA WAKATI GANI?

14, 15. Ni maandiko gani manne yanayohusu kuja kwa Kristo wakati ujao akiwa Hakimu?

 14 Je, uchunguzi zaidi wa unabii wa Yesu unafunua kwamba tunahitaji kurekebisha uelewaji wetu kuhusu wakati wa kutimia kwa matukio mengine muhimu? Unabii wenyewe unajibu swali hilo. Acheni tuone ni kwa njia gani.

15 Katika sehemu ya unabii wake iliyo katika Mathayo 24:29–25:46, Yesu anakazia hasa mambo yatakayotukia katika siku hizi za mwisho na wakati wa dhiki kuu inayokuja. Katika unabii huo, Yesu anataja mara nane kuhusu ‘kuja’ au kufika kwake. * Anasema hivi kuhusu dhiki kuu: “Yatamwona Mwana wa binadamu akija juu ya mawingu.” “Hamjui ni siku gani Bwana yenu atakuja.” “Mwana wa binadamu atakuja katika saa msiyofikiria.” Na katika mfano wake wa kondoo na mbuzi, Yesu anasema hivi: ‘Mwana wa binadamu atafika katika utukufu wake.’ (Mt. 24:30, 42, 44; 25:31) Marejeo yote manne yanahusu kuja kwa Kristo wakati ujao akiwa Hakimu. Marejeo manne yanayobaki yanapatikana wapi katika unabii wa Yesu?

16. Kuja kwa Yesu kunatajwa katika maandiko gani mengine?

16 Kuhusu mtumwa mwaminifu na mwenye busara, Yesu alisema hivi: “Mtumwa huyo atakuwa mwenye furaha ikiwa bwana wake atakapofika atamkuta akifanya hivyo.” Katika mfano wake wa mabikira, Yesu alisema hivi: “Walipokuwa wakienda zao kununua, bwana-arusi akafika [“akaja,” Kingdom Interlinear].” Katika mfano wa talanta, Yesu anasimulia hivi: “Baada ya muda mrefu bwana wa watumwa hao alikuja.” Katika mfano huohuo, bwana anasema hivi: “Wakati wa kufika kwangu [“kuja,” Int] ningekuwa nikipokea kilicho changu.” (Mt. 24:46; 25:10, 19, 27) Kuja kwa Yesu katika pindi hizo nne kunatukia wakati gani?

17. Tulisema nini kuhusu kufika kunakotajwa katika Mathayo 24:46?

 17 Zamani, tulitaja katika machapisho yetu kwamba marejeo hayo manne ya mwisho yanahusu kufika, au kuja, kwa Yesu katika mwaka wa 1918. Kwa mfano, fikiria maneno ya Yesu kuhusu “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” (Soma Mathayo 24:45-47.) Tulielewa kwamba ‘kufika’ kunakotajwa katika mstari wa 46 kulihusiana na wakati ambapo Yesu alikuja kukagua hali ya kiroho ya watiwa-mafuta katika mwaka wa 1918 na mtumwa aliwekwa rasmi juu ya mali zote za Bwana katika mwaka wa 1919. (Mal. 3:1) Hata hivyo, uchunguzi zaidi wa unabii wa Yesu unaonyesha kwamba tunahitaji kurekebisha uelewaji wetu kuhusu wakati wa kutimia kwa mambo fulani yaliyo katika unabii huo wa Yesu. Kwa nini?

18. Kuchunguza unabii wote wa Yesu kunatufanya tufikie mkataa gani kuhusu kuja kwa Yesu?

18 Katika mistari inayotangulia Mathayo 24:46, neno “atakuja” linatumiwa kila mara kurejelea wakati ambapo Yesu atakuja kutangaza na kutekeleza hukumu wakati wa dhiki kuu. (Mt. 24:30, 42, 44) Pia, kama tulivyoona katika  fungu la 12, ‘kufika’ kwa Yesu kunakotajwa katika Mathayo 25:31 kunarejelea wakati huohuo ujao wa hukumu. Kwa hiyo, ni jambo linalopatana na akili kufikia mkataa kwamba kufika kwa Yesu ili kumweka rasmi mtumwa mwaminifu juu ya mali zake zote kunakotajwa katika Mathayo 24:46 na 47, kunahusu pia kuja kwake wakati ujao, wakati wa ile dhiki kuu. * Kwa kweli, kuchunguza unabii wote wa Yesu kunaonyesha wazi kwamba kila moja ya marejeo hayo manane kuhusu kuja kwake, yatatimia wakati ujao wa hukumu katika ile dhiki kuu.

19. Tumechunguza marekebisho gani kuhusu uelewaji wetu, na ni maswali gani yatakayojibiwa katika makala zinazofuata?

19 Kwa muhtasari, tumejifunza nini? Mwanzoni mwa makala hii tuliuliza maswali matatu kuhusu “wakati.” Kwanza, tumejifunza kwamba dhiki kuu haikuanza mwaka wa 1914, badala yake itaanza wakati Umoja wa Mataifa utakaposhambulia Babiloni Mkubwa. Kisha, tumeona ni kwa nini Yesu hakuanza kuhukumu kondoo na mbuzi mwaka wa 1914, badala yake atafanya hivyo wakati wa ile dhiki kuu. Mwishowe, tumechunguza kwa nini Yesu hakuja kumweka rasmi mtumwa mwaminifu juu ya mali zake zote mwaka wa 1919, lakini atafanya hivyo wakati wa ile dhiki kuu. Hivyo basi, semi zote tatu za “wakati,” zinatimia katika kipindi kimoja cha wakati ujao, yaani, ile dhiki kuu. Marekebisho hayo yanaathirije zaidi uelewaji wetu kuhusu mfano wa mtumwa mwaminifu? Pia, yanaathirije uelewaji wetu kuhusu vielezi au mifano mingine ya Yesu inayotimizwa katika siku hizi za mwisho? Maswali hayo muhimu yatazungumziwa katika makala zinazofuata.

 

^ fu. 4 Fungu la 4: Kwa habari zaidi, tazama gazeti la Mnara wa Mlinzi, Februari 15, 1994, ukurasa wa 8-21 na Mei 1, 1999, ukurasa wa 8-20.

^ fu. 8 Fungu la 8: Tukio moja linalotajwa katika mistari hiyo ni ‘kukusanywa kwa waliochaguliwa.’ (Mt. 24:31) Hivyo, inaonekana kwamba watiwa-mafuta wote ambao bado watakuwa duniani baada ya sehemu ya kwanza ya dhiki kuu kupita, watainuliwa kwenda mbinguni wakati fulani kabla ya kuanza kwa vita vya Har–Magedoni. Maelezo hayo yanarekebisha habari iliyotajwa katika “Maswali Kutoka kwa Wasomaji” katika gazeti la Mnara wa Mlinzi, Agosti 15, 1990, ukurasa wa 30.

^ fu. 11 Fungu la 11: Tazama gazeti la Mnara wa Mlinzi, Oktoba 15, 1995, ukurasa wa 18-28.

^ fu. 12 Fungu la 12: Tazama simulizi hilohilo katika Luka 21:28.

^ fu. 15 Fungu la 15: Maneno “atakuja” na “atafika” yametafsiriwa kutokana na kitenzi kilekile cha Kigiriki, er′kho·mai.

^ fu. 18 Fungu la 18: Kama ilivyoonyeshwa, neno la Kigiriki linalotafsiriwa “atakapofika” katika Mathayo 24:46 ni kitenzi kilekile cha Kigiriki kinachotafsiriwa “atakuja” katika Mathayo 24:30, 42, 44.